Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 70

Yona na Samaki Mkubwa

Yona na Samaki Mkubwa

TAZAMA mwanamume ndani ya maji. Ana taabu nyingi, sivyo? Samaki yuko karibu kummeza! Unamjua mtu huyu? Ni Yona. Na tuone alivyoingia katika taabu nyingi.

Yona ni nabii wa Yehova. Muda mfupi baada ya kufa nabii Elisha, Yehova amwambia Yona hivi: ‘Nenda kwenye mji wa Ninawi. Ubaya wa watu ni mkubwa sana, nataka ukawaambie hivyo.

Lakini Yona hataki kwenda. Basi anapanda meli ambayo haiendi Ninawi. Yehova hafurahi kwa sababu Yona anakimbia. Basi anatokeza upepo mkubwa. Upepo huo karibu kuzamisha meli. Wasafiri wa meli wanaogopa sana na kuililia miungu yao iwasaidie.

Mwishowe Yona anawaambia hivi: ‘Ninamwabudu Yehova, Mungu aliyeifanya mbingu na dunia. Ninakimbia kazi ya Yehova.’ Basi wasafiri wanamwuliza hivi: ‘Tukufanyie nini ili upepo utulie?’

‘Nitupeni baharini, na bahari itatulia,’ Yona asema. Wasafiri hao hawataki kufanya hivyo, lakini upepo unapozidi kuwa mbaya, wanamtupa Yona baharini. Mara upepo unatulia, na bahari inakuwa kimya tena.

Wakati Yona anapozama majini, samaki mkubwa anammeza. Lakini hafi. Anakuwa ndani ya tumbo la samaki huyo siku tatu mchana na usiku. Yona anasikitika sana kwa vile hakumtii Yehova aende Ninawi. Unajua analofanya sasa?

Yona anamwomba Yehova amsaidie. Ndipo Yehova anamwagiza samaki huyo amtapike Yona pwani. Baada ya hayo Yona aenda Ninawi. Je! hilo halitufundishi kutimiza agizo la Yehova?

Kitabu cha Biblia cha Yona.