Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 77

Walikataa Kuabudu

Walikataa Kuabudu

UNAKUMBUKA kama ulisikia habari ya vijana hawa watatu? Ndiyo, ni rafiki za Danieli waliokataa chakula kisichowafaa. Wababeli waliwaita Shadraka, Meshaki na Abedinego. Lakini watamaze sasa. Kwa nini hawaabudu sanamu hii kubwa mno kama wengine? Ebu tuone.

Unazikumbuka zile sheria ambazo Yehova mwenyewe aliandika zikaitwa Amri Kumi? Ya kwanza ni: ‘Usiabudu miungu yoyote ila mimi.’ Vijana nao hapa wanatii sheria hiyo, ijapo si rahisi.

Nebukdreza, mfalme wa Babeli, ameita watu wakubwa wengi waheshimu sanamu hii aliyosimamisha. Ndiyo amemaliza kuwaambia watu wote hivi: ‘Mkisikia sauti ya tarumbeta, vinubi na vinanda vingine, inawapasa mwabudu sanamu hii ya dhahabu. Mtu akikataa kuabudu atatupwa mara hiyo katika tanuru (jiko) inayowaka moto.’

Nebukadreza anapojua kwamba Shadraka, Meshaki na Abedinego wamekataa kuabudu, anakasirika sana. Anaagiza waletwe kwake. Anawapa nafasi nyingine waabudu. Lakini vijana hao wanamtumaini Yehova. ‘Mungu wetu tunayetumikia anaweza kutuokoa,’ wanamwambia Nebukadreza. ‘Lakini hata asipotuokoa, hatutaabudu sanamu yako ya dhahabu.’

Anaposikia hivyo, Nebukadreza anakasirika hata zaidi. Kuna tanuru ya moto karibu, naye aamuru hivi: ‘Ongezeni tanuru moto mara saba kuliko zamani!’ Ndipo anawaagiza wanaume wenye nguvu zaidi wa jeshi lake wafunge Shadraka, Meshaki na Abedinego na kuwatupa katika tanuru hiyo. Tanuru ina moto mwingi hata wanaume hao wenye nguvu wanauawa na miali yake. Lakini namna gani vijana hao watatu wanaoutupwa ndani?

Mfalme achungulia ndani ya tanuru, anaogopa sana. ‘Je! hatukufunga wanaume watatu na kuwatupa katika tanuru inayowaka moto?’ auliza.

‘Ndiyo,’ watumishi wake wanajibu.

‘Lakini naona wanaume wanne wakitembea katika moto,’ asema. ‘Na yule wa nne anaonekana kama mungu.’ Mfalme aukaribia zaidi mlango wa tanuru na kupaza sauti: ‘Shadraka! Meshaki! Abedinego! Tokeni, enyi watumishi wa Mungu Aliye Juu Zaidi!’

Wanapotoka, kila mtu anaona kwamba hawakuumizwa. Kisha mfalme anasema: ‘Mungu wa Shadraka, Meshaki na Abedinego asifiwe! Amemtuma malaika wake akawaokoa kwa sababu hawataki kuabudu mungu yeyote ila Mungu wao.’

Je! huo si mfano bora wa kufuata ili tuwe waaminifu kwa Yehova?