Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 97

Yesu Aja Kama Mfalme

Yesu Aja Kama Mfalme

MUDA mfupi akiisha kuwaponya vipofu wawili wenye kuomba-omba, Yesu anafikia kijiji karibu na Yerusalemu. Anawaambia wanafunzi wake wawili hivi: ‘Ingieni katika kijiji nanyi mtamwona mwana-punda. Mfungueni mmlete kwangu.’

Punda huyo anapopelekwa kwake, Yesu anamkalia. Kisha anapanda kwenda Yerusalemu, ulio karibu. Anapoukaribia mji huo, watu wengi sana wanakuja kumlaki. Wengi wao wanavua mavazi yao ya nje na kuyatandika njiani. Wengine wanakata matawi ya mitende. Wanayatandika pia barabarani, na kupaza sauti: ‘Mungu mbariki mfalme anayekuja katika jina la Yehova!’

Zamani katika Israeli wafalme wapya walikuwa wakipanda mwana-punda kuingia Yerusalemu wajionyeshe kwa watu. Ndivyo Yesu anafanya sasa. Watu hawa wanaonyesha kwamba wanataka Yesu awe mfalme wao. Lakini watu wote hawamtaki. Tunajua hivyo kwa matokeo wakati Yesu anaingia katika hekalu.

Yesu anaponya vipofu na vilema katika hekalu. Watoto wadogo wanapoona hayo, wanamsifu Yesu kwa sauti. Lakini makuhani wanakasirika, wakimwambia Yesu: ‘Unasikia watoto wanavyosema?’

‘Ndiyo,’ Yesu ajibu. ‘Ninyi hamjasoma katika Biblia hivi: “Katika vinywa vya watoto wadogo Mungu atatokeza sifa?”’ Basi wanazidi kumsifu mfalme aliyewekwa na Mungu.

Tunataka tuwe kama watoto hao, sivyo? Labda watu wengine watatuzuia tusiseme habari za ufalme wa Mungu. Lakini tutazidi kuwaambia wengine maajabu ambayo Yesu atafanyia watu.

Yesu alipokuwa duniani, haukuwa wakati wake kuanza kutawala. Itakuwa wakati gani? Wanafunzi wa Yesu wanataka kujua. Tutasoma hayo katika hadithi inayofuata.