Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 87

Kijana Yesu Katika Hekalu

Kijana Yesu Katika Hekalu

TAZAMA mvulana anayezungumza na wazee hawa. Ni waalimu katika hekalu la Mungu Yerusalemu. Kijana huyo ni Yesu. Amekuwa mkubwa kidogo. Sasa ana miaka 12.

Waalimu wanashangaa sana kwa vile Yesu anajua mambo mengi juu ya Mungu na yale yaliyoandikwa katika Biblia. Lakini kwa nini Yusufu na Mariamu hawapo hapa pia? Wako wapi? Tuone.

Kila mwaka Yusufu anapeleka jamaa yake Yerusalemu kwenye sikukuu ya pekee inayoitwa Kupitwa. Ni safari ndefu kutoka Nazareti kufika Yerusalemu. Hakuna aliye na motokaa, wala hakuna magarimoshi. Hawakuwa nayo siku hizo. Watu wengi wanatembea kwa miguu, na inawachukua karibu siku tatu kufika Yerusalemu.

Wakati huu Yusufu ana jamaa kubwa. Sasa ana ndugu na dada wadogo wa Yesu wa kuangalia. Basi, mwaka huu Yusufu na Mariamu wameanza safari ndefu pamoja na watoto wao kurudi kwao Nazareti. Wanadhani Yesu anasafiri pamoja na wenzake. Lakini jioni wanaposimama, hawamwoni Yesu. Wanamtafuta kati ya watu wa ukoo na rafiki zao, wapi! Hivyo wanarudi Yerusalemu wakamtafute huko.

Mwishowe wanamkuta Yesu humu pamoja na waalimu. Anawasikiliza na kuuliza maulizo. Na watu wote wanastaajabia akili ya Yesu. Lakini Mariamu asema: ‘Wewe mtoto, kwa nini umetufanya hivi? Baba yako na mimi tumesumbuka sana tukikutafuta.’

‘Kwa nini mmenitafuta?’ Yesu ajibu. ‘Hamkujua ilinipasa kuwa katika nyumba ya Baba yangu?’

Ndiyo, Yesu anapenda kuwa mahali anapoweza kujifunza habari za Mungu. Si ndivyo sisi pia imetupasa kuona? Nyumbani Nazareti, Yesu alikuwa akihudhuria mikutano ya ibada kila juma. Alijifunza mengi katika Biblia kwa sababu alikuwa akisikiliza. Na tuwe kama Yesu, tufuate mfano wake.