Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 91

Yesu Anafundisha Juu ya Mlima

Yesu Anafundisha Juu ya Mlima

MWONE Yesu ameketi hapa. Anafundisha watu wote hawa mlimani katika Galilaya. Hao walioketi karibu naye ni wanafunzi wake. Amechagua 12 wawe mitume. Mitume ni wanafunzi wa pekee wa Yesu. Unajua majina yao?

Kuna Simoni Petro na nduguye Andrea. Halafu Yakobo na Yohana, nao pia ni ndugu. Mtume mwingine pia anaitwa Yakobo, na mwingine anaitwa pia Simoni. Mitume wawili wanaitwa Yuda. Mmoja ni Yuda Iskariote, na Yuda mwingine anaitwa pia Thadayo. Kisha kuna Filipo na Nathanaeli (pia aitwa Bartholomayo), na Mathayo na Tomaso.

Baada ya kurudi kutoka Samaria, Yesu alianza kuhubiri mara ya kwanza hivi: ‘Ufalme wa mbingu umekaribia.’ Je! unajua maana ya ufalme huo? Ni serikali halisi ya Mungu. Yesu ni mfalme wa huo. Atatawala kutoka mbinguni alete amani kwenye dunia hii. Dunia yote itafanywa na ufalme wa Mungu kuwa paradiso nzuri.

Hapa Yesu anafundisha watu habari za ufalme huo. ‘Msali hivi,’ anaeleza. ‘Baba yetu mbinguni, jina lako liheshimiwe. Ufalme wako uje. Mapenzi yako yafanywe duniani, kama mbinguni.’ Watu wengi wanaiita ‘Sala ya Bwana.’ Wengine wanaiita ‘Baba Yetu.’ Unaweza kutoa sala yote?

Yesu pia anafundisha watu namna ya kutendeana. ‘Watendee wengine unavyotaka wakutendee,’ asema. Unapenda wakati wengine wanakutendea vizuri, sivyo? Basi, Yesu anatuambia tuwatendee wengine vizuri. Je! haitakuwa vizuri sana wakati kila mtu atakapofanya hivyo katika dunia paradiso?