Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 96

Yesu Anaponya Wagonjwa

Yesu Anaponya Wagonjwa

YESU anaposafiri katika nchi yote, anaponya wagonjwa. Habari za miujiza hiyo zasimuliwa katika vijiji na miji yote. Watu wanamletea vilema na vipofu na viziwi, na wagonjwa wengine wengi. Yesu anaponya wote.

Zaidi ya miaka mitatu imepita sasa tangu Yesu abatizwe na Yohana. Yesu anawaambia mitume wake kwamba atakwenda Yerusalemu upesi, akauawe huko, kisha afufuliwe.

Siku moja Yesu anafundisha siku ya Sabato. Sabato ni siku ya Wayahudi kupumzika. Mwanamke unayeona hapa amekuwa mgonjwa sana. Alikunjamana kwa miaka 18 bila kunyoka. Basi Yesu anamwekea mikono yake, naye anaanza kunyoka. Ameponywa!

Kwa sababu hiyo, viongozi wa dini wanakasirika. Mmoja wao anapigia watu kelele akisema: ‘Kuna siku sita za kufanya kazi. Ndizo siku za kuponya wagonjwa, si siku ya Sabato!’

Lakini Yesu anajibu hivi: ‘Enyi watu wabaya. Yeyote kati yenu angemfungua punda wake amnyweshe maji siku ya Sabato. Je! mwanamke huyu maskini, mgonjwa wa miaka 18, asiponywe siku ya Sabato?’ Jibu la Yesu lawafanya watu hao wabaya waone haya.

Baadaye Yesu na mitume wake wanasafiri kuelekea Yerusalemu. Wakiwa nje ya mji wa Yeriko, vipofu wawili wenye kuombaomba wanajua kwamba Yesu anapita karibu nao. Basi wanapaza sauti hivi: ‘Yesu, tusaidie!’

Yesu anawaita kwake vipofu hao, na kuwauliza: ‘Mwataka niwafanyie nini?’ Wanasema: ‘Bwana, utufungue macho yetu.’ Yesu anagusa macho yao, mara hiyo wanaona! Unajua sababu Yesu anafanya miujiza yote hiyo? Kwa sababu anapenda watu na anataka wamwamini. Basi tunaweza kuwa na hakika kwamba atakapokuwa Mfalme juu ya dunia, hakuna atakayekuwa mgonjwa tena.