Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 110

Timotheo—Msaidizi Mpya wa Paulo

Timotheo—Msaidizi Mpya wa Paulo

KIJANA unayeona hapa pamoja na mtume Paulo ni Timotheo. Timotheo anakaa pamoja na jamaa yake Listra. Jina la mama yake ni Eunike na nyanya yake Loisi.

Hii ndiyo mara ya tatu ya Paulo kutembelea Listra. Mwaka mmoja uliotangulia, Paulo na Barnaba walifika huku mara ya kwanza katika safari ya kuhubiri. Na sasa Paulo amerudi tena huko akiwa na rafiki yake Sila.

Unajua Paulo anamwambia Timotheo nini? ‘Ungependa kwenda pamoja na Sila na mimi?’ anauliza. ‘Ungeweza kutusaidia kuhubiri watu wa mbali.’

‘Ndiyo,’ Timotheo ajibu, ‘ningependa kwenda.’ Basi upesi baada ya hapo Timotheo aacha jamaa yake na kwenda pamoja na Paulo na Sila. Lakini kabla ya kujifunza juu ya safari yao, na tujifunze ambayo yamekuwa yakimpata Paulo. Imekuwa miaka 17 tangu Yesu alipomtokea akienda Damasko.

Adui fulani wanafanya mpango wa kumwua Paulo kwa sababu hawataki mafundisho juu ya Yesu. Lakini wanafunzi wanamsaidia Paulo aokoke. Wanamweka katika kikapu na kumtelemsha nje ya ukuta wa mji.

Baada ya hayo Paulo aenda Antiokia kuhubiri. Huko ndiko kwa mara ya kwanza, wafuasi wa Yesu wanaitwa Wakristo. Ndipo Paulo na Barnaba wanatumwa kutoka Antiokia waende katika safari ya kuhubiri nchi za mbali sana. Mji mmoja ambao wanatembelea ni Listra, nyumbani kwa Timotheo.

Baadaye, kama mwaka mmoja, Paulo anarudi Listra katika safari ya pili. Timotheo anapokwenda na Paulo na Sila, unajua wanakwenda wapi? Angalia ramani, tujifunze sehemu chache.

Kwanza, wanakwenda kwenye mji wa Ikonio, kisha mji wa pili wa Antiokia. Baada ya hapo wanasafiri kwenda Troʹa, kisha Filipi, Thesalonike na Beroya. Unaona Athene katika ramani? Paulo anahubiri huko. Kisha wanakaa mwaka mmoja na nusu wakihubiri Korintho. Mwishowe wanasimama kidogo katika Efeso. Kisha wanarudi Kaisaria kwa meli, na kusafiri kwenda juu Antiokia, ambako Paulo anakaa.

Hivyo Timotheo anasafiri mamia na mamia ya kilomita akimsaidia Paulo azihubiri “habari njema” na kuanza makundi mengi ya Kikristo. Utakapokuwa mkubwa, je! utakuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu kama Timotheo?