Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza

Enyi Mnaompenda Yehova:

Ilikuwa mwaka wa 1971. Mwaka huo, wale waliohudhuria Kusanyiko la Wilaya lenye kichwa: “Jina la Mungu” walifurahi kupokea machapisho kadhaa mapya. Wengi walisema machapisho hayo “yalipita matazamio yetu.” Ndugu mmoja alisema hivi kuhusu chapisho moja lililotolewa: “Ni kitabu chenye kusisimua zaidi ambacho tumewahi kuwa nacho kuhusu mambo yatakayokuja!” Alikuwa akizungumzia kitabu gani? Kilikuwa kitabu “The Nations Shall Know That I Am Jehovah”—How? (“Mataifa Yatalazimika Kujua Kwamba Mimi Ni Yehova”—Jinsi Gani?) Kwa nini kitabu hicho kiliwasisimua wengi? Kwa sababu kilikuwa na ufafanuzi uliorekebishwa kuhusu unabii ulio katika kitabu cha Ezekieli—unabii unaohusu wakati ujao wa wanadamu wote.

Miaka mingi imepita tangu kitabu ‘Watamjua Yehova’ kilipotolewa, na idadi ya watu wa Mungu imeongezeka haraka—kutoka watu milioni moja na nusu kufikia zaidi ya watu milioni nane. (Isa. 60:22) Mamilioni hayo ya watumishi wa Yehova wanazungumza zaidi ya lugha 900. (Zek. 8:23) Wengi hawajawahi kamwe kujifunza kitabu kinachofafanua kwa undani unabii wa Ezekieli ulioongozwa na roho.

Isitoshe, tangu 1971 uelewaji wetu kuhusu kweli nyingi za Biblia umeboreshwa sana kadiri ambavyo nuru imezidi kung’aa. (Met. 4:18) Mwaka wa 1985 tulianza kuelewa waziwazi jinsi “kondoo wengine” wanavyotangazwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Mungu. (Yoh. 10:16; Rom. 5:18; Yak. 2:23) Kisha mwaka wa 1995 tulielewa kwa mara ya kwanza kwamba hukumu ya mwisho ya “kondoo” na “mbuzi” ingefanyika wakati wa “dhiki kuu” inayokuja. (Mt. 24:21; 25:31, 32) Marekebisho hayo yote yamebadili sana uelewaji wetu wa kitabu cha Ezekieli.

“Mwana wa binadamu, tazama kwa uangalifu, sikiliza kwa makini, na ukazie fikira kila kitu ninachokuonyesha, kwa maana uliletwa hapa kwa sababu hiyo.”​—EZEKIELI 40:4

Miaka ya hivi karibuni, nuru imeendelea kung’aa hata zaidi. Fikiria masomo tunayojifunza kutokana na mifano ya Yesu. Sasa tunaelewa vizuri zaidi mengi kati ya masomo hayo. Mifano mingi inazungumzia matukio yatakayotokea hivi karibuni wakati wa dhiki kuu inayokaribia. Vilevile, uelewaji wetu wa unabii mbalimbali wa kitabu cha Ezekieli umerekebishwa. Marekebisho hayo yanatia ndani unabii kuhusu Gogu wa Magogu (sura ya 38 na 39), kazi ya mwanamume mwenye kidau cha wino cha mwandishi (sura ya 9), na bonde la mifupa mikavu na kuunganishwa kwa vijiti viwili (sura ya 37). Mabadiliko hayo yote yanarekebisha mambo yaliyoandikwa miaka mingi iliyopita katika kitabu ‘Watamjua Yehova.’

Basi haishangazi kwamba wengi kati ya watu wa Yehova wameuliza, “Tutapata lini kitabu kilicho na habari zilizorekebishwa kuhusu unabii wa Ezekieli?” Kitabu Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa! kinatimiza uhitaji huo. Unaposoma sura zake 22 na kutafakari mifano yenye kupendeza iliyomo, utashangaa kuona utafiti mwingi uliofanywa ili kukiandaa. Tumesali na kuchunguza kwa makini ili kujua kwa nini Yehova alituandalia kitabu chenye kusisimua cha Ezekieli. Maswali yafuatayo yalifikiriwa kwa makini: Kitabu cha Ezekieli kilikuwa na masomo gani kwa watu walioishi katika siku za Ezekieli na kwetu leo? Ni unabii gani unaozungumzia mambo yatakayotokea wakati ujao? Je, tunapaswa kutafuta ulinganifu wa kinabii katika kitabu cha Ezekieli? Majibu ya maswali hayo yanatoa uelewaji ulio wazi zaidi kufikia sasa wa kitabu hiki cha Ezekieli tunachofurahia kukisoma.

Bila shaka, unaposoma kitabu cha Ezekieli kuanzia mwanzo hadi mwisho, utashangazwa na sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova. Vilevile, utashangazwa na viwango vya juu ambavyo Yehova ameweka kwa ajili ya wale walio mbinguni na walio duniani wanaotaka kumwabudu kwa njia inayokubalika. Kitabu Ibada Safi kitakusaidia uthamini zaidi mambo ambayo tayari Yehova amewafanyia watu wake na mambo atakayowafanyia hivi karibuni. Utatambua kwamba kitabu hiki kinakazia tena na tena mambo mawili makuu. Kwanza, ili tumpendeze Yehova tunapaswa tumjue na kutambua kwamba yeye ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Pili, tunapaswa kumwabudu Yehova kwa njia anayoikubali, na kupatanisha maisha yetu na viwango vyake vya juu.

Tunatumaini kwamba kitabu hiki kitaimarisha azimio lako la kumwabudu Yehova kwa njia inayoliheshimu jina lake kuu na takatifu. Wakati huohuo, na kikuchochee kuendelea kutarajia wakati ambapo mataifa yote yatalazimika kujua kwamba yeye ni Yehova.—Eze. 36:23; 38:23.

Baba yetu mpendwa Yehova na abariki jitihada zako za kuelewa kitabu ambacho alimwongoza nabii Ezekieli aandike.

Ndugu zenu,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova