Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 19

“Mahali Ambapo Kijito Hicho Kinapita, Kila Kitu Kitaishi”

“Mahali Ambapo Kijito Hicho Kinapita, Kila Kitu Kitaishi”

EZEKIELI 47:9

WAZO KUU: Jinsi maono ya mto unaotiririka kutoka hekaluni yalivyotimizwa nyakati za kale, yanavyotimiza sasa, na wakati ujao

1, 2. Kulingana na Ezekieli 47:1-12, Ezekieli anaona na kujifunza nini? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

EZEKIELI anaona jambo lingine lenye kushangaza katika maono ya hekalu: Kijito kinachotiririka kutoka katika jengo takatifu! Mwazie akichunguza mkondo wa maji hayo yaliyo safi kabisa. (Soma Ezekieli 47:1-12.) Yanatiririka kutoka patakatifu; kisha yanatoka kwenye majengo ya hekalu karibu na lango la mashariki. Malaika anamwongoza Ezekieli kwenda nje ya hekalu, wanapima huku wakienda. Malaika anamwagiza Ezekieli tena na tena apite katika maji, na nabii huyo anatambua kwamba kina cha maji kinaongezeka haraka, na baada ya muda mfupi yanakuwa mengi sana hivi kwamba anaweza tu kuvuka kwa kuogelea!

2 Ezekieli anatambua kwamba mto huo unaingia kwenye Bahari ya Chumvi na kila mahali ambapo maji ya mto yanafika yanaponya maji yenye chumvi yasiyo na uhai, na kufanya yawe na samaki wengi. Kwenye kingo za mto, anaona miti mingi ya kila aina ikikua. Kila mwezi, inazaa matunda yenye lishe na kuchipua majani yanayoponya. Ezekieli anapoona mambo hayo yote, moyo wake unakuwa na amani na tumaini. Lakini sehemu hii ya maono ya hekalu ilimaanisha nini kwa Ezekieli na kwa wahamishwa wenzake? Na inamaanisha nini kwetu leo?

Mto Alioona Ezekieli Ulimaanisha Nini kwa Wahamishwa?

3. Kwa nini Wayahudi wa nyakati za kale walijua kwamba mto ambao Ezekieli aliona haukuwa halisi?

3 Kwa kweli, Wayahudi wa kale walijua kwamba mto huo haukuwa halisi. Badala yake, inaelekea kwamba simulizi hilo la Maandiko liliwakumbusha unabii mwingine wa kurudishwa, ambao nabii Yoeli aliandika labda zaidi ya karne mbili mapema. (Soma Yoeli 3:18.) Wahamishwa Wayahudi waliposoma unabii wa Yoeli, hawakutazamia kwamba milima ‘ingedondosha divai tamu’ kihalisi au vilima ‘vingetiririka maziwa’; wala hawakutazamia kwamba kijito kingetiririka “kutoka katika nyumba ya Yehova.” Vivyo hivyo, huenda Wayahudi wenzake walielewa kwamba ujumbe wa maono ya nabii Ezekieli haukuhusu mto halisi. * Basi, Yehova alikuwa akitoa ujumbe gani? Maandiko yanatusaidia kuelewa baadhi ya mambo katika maono hayo. Hata hivyo, kwa ujumla tutachunguza katika simulizi hili la kinabii mambo matatu yaliyo wazi yanayotupatia uhakika.

4. (a) Mto ambao Ezekieli aliona ulifanya Wayahudi watazamie baraka gani kutoka kwa Yehova? (b) Katika Biblia maneno “mto” na “maji” yanatuhakikishiaje kwamba Yehova atawabariki watu wake? (Tazama sanduku “Mito ya Baraka Kutoka kwa Yehova.”)

4 Mto wa baraka. Katika Biblia, mara nyingi mito na maji hutumiwa kuonyesha kutiririka kwa baraka za Yehova zinazoleta uhai. Ezekieli aliona mto kama huo ukitiririka kutoka hekaluni, basi maono hayo yangewafanya watu wa Mungu watazamie kupata baraka za kiroho za Yehova zinazoleta uhai ikiwa tu wangeshikamana na ibada safi. Ni baraka gani? Wangepokea tena maagizo ya kiroho kutoka kwa makuhani. Dhabihu zingetolewa hekaluni, na hivyo wangekuwa tena na uhakika kwamba dhambi zao zingefunikwa. (Eze. 44:15, 23; 45:17) Hivyo, wangekuwa safi tena, kana kwamba wameoshwa kwa maji safi yanayotoka hekaluni.

5. Maono ya mto yanaonyeshaje kwamba kutakuwa na baraka za kuwatosha watu wote?

5 Je, sikuzote kungekuwa na baraka za kuwatosha watu wote? Maono hayo yanatoa uhakikisho kwa kuonyesha maji yanayoongezeka kimuujiza—maji kidogo yanayotiririka ambayo baada ya kilomita mbili hivi yanakuwa mengi sana! (Eze. 47:3-5) Huenda idadi ya Wayahudi waliorudishwa ingeongezeka; lakini baraka za Yehova zingeongezeka ili kutosheleza uhitaji huo. Mto huo uliwakilisha maandalizi mengi sana!

6. (a) Maono hayo ya kinabii yalitoa ahadi gani yenye kufariji? (b) Maono hayo pia yalitoa onyo gani? (Tazama maelezo ya chini.)

6 Maji yanayoleta uhai. Katika maono ya Ezekieli, mto uliingia kwenye Bahari ya Chumvi, na kuponya sehemu kubwa ya bahari hiyo. Ona kwamba maji hayo yalitokeza samaki wengi wa aina mbalimbali kama samaki walio katika Bahari Kuu, yaani, Bahari ya Mediterania. Pia, kulikuwa na biashara kubwa ya uvuvi kwenye ufuo wa Bahari ya Chumvi katika miji miwili ambayo haikuwa imekaribiana sana. Malaika alisema: “Mahali ambapo kijito hicho kinapita, kila kitu kitaishi.” Je, hilo linamaanisha kwamba maji yanayotoka katika nyumba ya Yehova yalifika kila mahali katika Bahari ya Chumvi? Hapana. Malaika alieleza kwamba kulikuwa na sehemu zenye matope ambazo hazikufikiwa na maji yanayoleta uhai. Sehemu hizo ‘zingebaki zikiwa sehemu za chumvi.’ * (Eze. 47:8-11) Basi maono hayo ya kinabii yalitoa ahadi yenye kufariji kwamba ibada safi ingewafanya watu wawe hai, na wasitawi. Lakini pia onyo hili lililotolewa: Si watu wote ambao wangekubali baraka za Yehova; wala si wote wangeponywa.

7. Miti iliyo kwenye kingo za mto katika maono iliwapa Wayahudi waliohamishwa uhakikisho gani?

7 Miti kwa ajili ya chakula na kuponya. Namna gani miti iliyokuwa kwenye kingo za mto? Inafanya maono hayo yapendeze zaidi, sivyo? Pia, inaongeza maana ya maono hayo. Kwa hakika, Ezekieli na Wayahudi wenzake walifurahia kufikiria kuhusu matunda matamu ya miti hiyo, ambayo ingezaa kila mwezi! Unabii huo wenye kuvutia uliwahakikishia kwamba Yehova angewalisha kiroho. Uliwahakikishia jambo gani lingine? Ona kwamba majani ya miti hiyo ‘yangetumiwa kuponya.’ (Eze. 47:12) Yehova alijua kwamba kuliko jambo lingine lolote, wahamishwa waliorudishwa wangehitaji kuponywa kiroho, na aliahidi kufanya hivyo. Unabii mwingine wa kurudishwa ulionyesha jinsi alivyofanya hivyo, kama tulivyoona kwenye Sura ya 9 ya kitabu hiki.

8. Ni nini kinachoonyesha kwamba unabii wa Ezekieli ungetimizwa kwa njia kubwa zaidi?

8 Hata hivyo, kama tulivyozungumzia kwenye Sura ya 9, wahamishwa waliorudi waliona utimizo mdogo tu wa unabii huo. Watu ndio waliofanya unabii huo utimizwe kwa njia ndogo. Yehova angewezaje kuwabariki kikamili huku wakirudia njia zao mbaya, wakikosa kutii, na kupuuza ibada safi mara kwa mara? Watu waaminifu waliumia na kuvunjwa moyo na mwenendo wa Wayahudi wenzao. Hata hivyo, waabudu washikamanifu wa Yehova walijua kwamba ahadi zake hazikosi kamwe kutimia; zinatimia sikuzote. (Soma Yoshua 23:14.) Hivyo, siku moja unabii wa Ezekieli ungetimizwa kwa njia kubwa zaidi. Ungetimizwa lini?

Jinsi Mto Huo Unavyotiririka Leo!

9. Maono ya hekalu aliloona Ezekieli yanatimizwa lini kwa njia kubwa zaidi?

9 Kama tulivyoona kwenye Sura ya 14 ya kitabu hiki, maono ya hekalu aliloona Ezekieli yanatimizwa kwa njia kubwa zaidi katika “siku za mwisho,” ambapo ibada safi imeinuliwa kuliko wakati mwingine wowote. (Isa. 2:2) Maono hayo ya Ezekieli yanatimizwaje leo?

10, 11. (a) Leo, tunapata baraka gani zinazotiririka kama mto? (b) Baraka zinazotiririka kutoka kwa Yehova zimeongezekaje ili kutimiza uhitaji unaoongezeka katika siku za mwisho?

10 Mto wa baraka. Maji yanayotiririka kutoka kwenye nyumba ya Yehova yanatukumbusha baraka gani leo? Kwa kweli, yanatukumbusha mambo mengi ambayo Yehova anatuandalia ili kutunufaisha kiroho. Jambo muhimu zaidi ni dhabihu ya fidia ya Kristo inayosafisha, ambayo hutuwezesha kupata msamaha wa dhambi. Kweli safi za Neno la Mungu zinalinganishwa pia na maji yanayoleta uhai, ambayo husafisha. (Efe. 5:25-27) Baraka hizo zimetiririkaje leo?

11 Mwaka wa 1919 idadi ya watumishi wa Yehova ilikuwa elfu kadhaa, na walishangilia kupata chakula cha kiroho walichohitaji. Miaka iliyofuata, idadi yao ilizidi kuongezeka. Leo, idadi ya watu wa Mungu ni zaidi ya milioni nane. Je, maji safi ya kweli yamezidi kuongezeka? Ndiyo! Tumepata ufafanuzi mwingi sana wa kweli za kiroho. Katika karne iliyopita mabilioni ya Biblia, vitabu, magazeti, broshua, na trakti zimetiririka kwa watu wa Mungu. Kama mto ambao Ezekieli aliona, kweli safi zimezidi kutiririka kwa kasi ili kutimiza uhitaji unaoongezeka wa kutosheleza kiu ya kiroho ya watu ulimwenguni kote. Machapisho yanayotegemea Biblia yamechapishwa kwa muda mrefu. Na sasa kupitia tovuti ya jw.org, habari hizo zinapatikana kielektroniki katika lugha zaidi ya 900! Maji hayo ya kweli yana matokeo gani kwa watu wenye mioyo minyoofu?

12. (a) Tumeona jinsi gani ujumbe wa kweli ukiwaletea watu uhai na afya ya kiroho? (b) Maono hayo yanatupatia onyo gani leo? (Pia, tazama maelezo ya chini.)

12 Maji yanayoleta uhai. Ezekieli aliambiwa: “Mahali ambapo kijito hicho kinapita, kila kitu kitaishi.” Fikiria jinsi ambavyo ujumbe wa kweli umetiririka kwa wote ambao wamekuja katika nchi yetu ya kiroho iliyorudishwa. Kweli za Biblia zimegusa mioyo ya mamilioni ya watu na kuwafanya wawe hai na wenye afya kiroho. Lakini maono hayo pia yanatoa onyo muhimu kwamba si watu wote wanaoendelea kufuata kweli hizo. Kama sehemu zenye majimaji na matope katika Bahari ya Chumvi kwenye maono ya Ezekieli, mioyo fulani inakuwa migumu, haikubali kweli na inakataa kuifuata. * Tusiwe hivyo kamwe!​—Soma Kumbukumbu la Torati 10:16-18.

13. Leo, tunaweza kupata masomo gani kutokana na miti aliyoona Ezekieli?

13 Miti kwa ajili ya chakula na kuponya. Je, leo tunapata masomo yanayotutia moyo kutokana na ile miti iliyo kwenye kingo za mto? Bila shaka! Kumbuka kwamba miti hiyo inazaa matunda matamu kila mwezi, na majani yake yanaponya. (Eze. 47:12) Inatukumbusha kwamba tunamtumikia Mungu anayetulisha kwa ukarimu na kutuponya kwa njia muhimu zaidi, yaani, kiroho. Ulimwengu wa leo ni mgonjwa na una njaa kiroho. Kinyume chake, fikiria mambo ambayo Yehova anaandaa. Baada ya kusoma makala katika machapisho yetu, kuimba wimbo wa mwisho kusanyikoni, au kutazama video au programu ya JW Broadcasting, je, umewahi kuhisi umebarikiwa kwa kupata chakula hicho cha kiroho? Kwa kweli tunalishwa vizuri. (Isa. 65:13, 14) Je, chakula chetu cha kiroho kinatusaidia kuwa na afya kiroho? Ushauri wenye manufaa tunaopata unaotegemea kabisa Neno la Mungu, hutusaidia kuepuka dhambi kama vile uasherati, pupa, na kukosa imani. Pia, Yehova amefanya mpango wa kuwasaidia Wakristo washinde ugonjwa wa kiroho unaoletwa na dhambi nzito. (Soma Yakobo 5:14.) Kwa kweli tumebarikiwa, kama inavyoonyeshwa na miti katika maono ya Ezekieli.

14, 15. (a) Tunapata somo gani kutokana na sehemu zenye matope ambazo hazikuponywa katika maono ya Ezekieli? (b) Leo tunafaidikaje kutokana na maono ya Ezekieli kuhusu mto?

14 Wakati huohuo, tunajifunza somo kutokana na maeneo hayo yenye matope yasiyoweza kuponywa. Hatungependa kamwe kuzuia baraka za Yehova kutiririka kwenye maisha yetu. Lingekuwa jambo hatari kukataa kuponywa, kama ilivyo kwa wengi katika ulimwengu huu mgonjwa. (Mt. 13:15) Kinyume chake, tunafurahia na kufaidika kutokana na mto wa baraka. Tunapokunywa kwa bidii maji safi ya kweli za Neno la Mungu, tunapowahubiria wengine kweli hizo, tunapopokea mwongozo wenye upendo, faraja, na msaada kutoka kwa wazee waliozoezwa na mtumwa mwaminifu, tunaweza kukumbuka mto wa maono ya Ezekieli. Mto huo unaendeleza uhai na kuponya popote unapoenda!

15 Namna gani kuhusu utimizo wa wakati ujao wa maono ya mto huo? Kama tutakavyoona, mto huo utatiririka kwa kiwango kikubwa zaidi katika Paradiso inayokuja.

Maono Hayo Yatamaanisha Nini Katika Paradiso?

16, 17. (a) Maji ya uzima yataongezekaje hata zaidi katika Paradiso? (b) Tutafaidikaje kutokana na mto huo wa baraka katika Paradiso?

16 Je, unajiwazia katika Paradiso, ukiwa umezungukwa na marafiki na familia, ukifurahia maisha kikamili? Kuchunguza maono ya Ezekieli kuhusu mto kunaweza kukusaidia uone jambo hilo waziwazi. Jinsi gani? Fikiria tena mambo matatu yaliyo wazi na yenye upendo katika maono hayo.

17 Mto wa baraka. Katika Paradiso, mto huo wa mfano utapanuka hata zaidi kwa kuwa utaleta baraka za kiroho na pia za kimwili. Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu, Ufalme wa Mungu utawasaidia watu waaminifu wafaidike na fidia kwa njia kubwa zaidi. Hatua kwa hatua, watakuwa wakamilifu! Hakutakuwa tena na magonjwa, madaktari, wauguzi, hospitali, wala bima ya afya! Maji hayo ya uzima yatatiririka kwa mamilioni watakaooka Har–Magedoni, yaani, “umati mkubwa” watakaotoka kwenye “dhiki kuu.” (Ufu. 7:9, 14) Hata hivyo, ingawa mwanzo huo wa kutiririka kwa mto wa baraka utakuwa wenye kustaajabisha, ni mdogo kwa kulinganishwa na mambo yatakayotokea baadaye. Kama inavyoonyeshwa na maono ya Ezekieli, mto huo utapanuka ili kutimiza uhitaji mkubwa zaidi.

Katika Paradiso, mto wa baraka utafanya kila mtu awe kijana na mwenye afya (Tazama fungu la 17)

18. “Mto wa maji ya uzima” utafurikaje wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja?

18 Maji yanayoleta uhai. Wakati wa ile Miaka Elfu Moja, “mto wa maji ya uzima” utafurika. (Ufu. 22:1) Mamilioni, au hata mabilioni, watafufuliwa na kupewa nafasi ya kuishi milele katika Paradiso! Baraka za Yehova kupitia Ufalme zitatia ndani kuwafufua watu wengi sana waliokufa, yaani, wanadamu ambao kwa muda mrefu wamelala mavumbini. (Isa. 26:19) Hata hivyo, je, watu hao wote waliofufuliwa wataendelea kuwa hai milele?

19. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba maji ya kweli mpya kutoka kwa Mungu yataandaliwa katika Paradiso? (b) Ni kwa njia gani baadhi ya watu watabaki ‘wakiwa chumvi’ wakati ujao?

19 Lazima kila mmoja aamue. Wakati huo, vitabu vipya vya kukunjwa vitafunguliwa. Basi maji yenye kuburudisha kutoka kwa Yehova yatatia ndani kweli mpya zitakazofunuliwa, yaani, mwongozo mpya wa kiroho. Je, si jambo lenye kupendeza kufikiria tumaini hilo? Hata hivyo, baadhi ya watu watakataa mwongozo huo na kuamua kutomtii Yehova. Huenda baadhi ya watu wataasi wakati wa ile Miaka Elfu Moja, lakini hawataruhusiwa kuvuruga Paradiso. (Isa. 65:20) Tunaweza kukumbuka maono ya Ezekieli kuhusu maeneo yenye matope ambayo hayakuponywa, ‘yaliyobaki yakiwa sehemu za chumvi.’ Wale watakaokataa kwa ukaidi kunywa maji yenye thamani yanayoleta uhai watakuwa wapumbavu kwelikweli! Baada ya ile Miaka Elfu Moja, kundi la waasi litajiunga na Shetani. Wote watakaokataa utawala wa Yehova wa uadilifu watapatwa na jambo lilelile: kifo cha milele.—Ufu. 20:7-12.

20. Ni mpango gani utakaotunufaisha wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja unaotukumbusha miti aliyoona Ezekieli?

20 Miti kwa ajili ya chakula na kuponya. Yehova hangependa yeyote kati yetu akose uzima wa milele. Ili kutusaidia kunufaika na nafasi ya kipekee anayotupatia, atahakikisha tena kwamba kuna mpango kama wa miti ambayo Ezekieli aliona. Hata hivyo, katika Paradiso Yehova atatubariki kimwili na pia kiroho. Huko mbinguni, Yesu Kristo pamoja na watawala wenzake 144,000 watatawala wakiwa wafalme kwa Miaka Elfu Moja. Wakiwa makuhani, wale 144,000 watatumia thamani ya dhabihu ya fidia ya Kristo, kuwasaidia wanadamu waaminifu kuwa wakamilifu. (Ufu. 20:6) Mpango huo wa uponyaji wa kimwili na kiroho unatukumbusha miti aliyoona Ezekieli kwenye kingo za mto, ambayo ilizaa matunda yenye lishe na iliyokuwa na majani yanayoponya. Maono ya Ezekieli yanapatana na unabii mwingine wenye kupendeza ulioandikwa na mtume Yohana. (Soma Ufunuo 22:1, 2.) Majani ya miti ambayo Yohana aliona “yalikuwa ya kuponya mataifa.” Mamilioni ya wanadamu watafaidika kutokana na utumishi wa kikuhani wa wale 144,000.

21. Unafaidikaje kwa kutafakari kuhusu mto alioona Ezekieli, na sasa tutachunguza nini? (Tazama sanduku “Kijito Kinakuwa Mto Mkubwa!”)

21 Unapotafakari mto alioona Ezekieli, je moyo wako unajawa na amani na tumaini? Tunatazamia kipindi kizuri sana wakati ujao! Fikiria jambo hilo—maelfu ya miaka iliyopita Yehova alitoa unabii mwingi ili kutusaidia kuwazia jinsi Paradiso itakavyokuwa, na kutualika kwa subira tuone utimizo mkubwa, uhalisi wa mambo yaliyotabiriwa. Je, utakuwapo? Huenda ukajiuliza kama kweli utapata nafasi katika Paradiso. Acheni sasa tuchunguze jinsi masimulizi ya mwisho ya unabii wa Ezekieli yanavyotupatia uhakikisho.

^ fu. 3 Isitoshe, Wayahudi wahamishwa ambao walikumbuka mandhari ya kijiografia ya nchi yao inaelekea walijua kwamba mto huo haukuwa halisi kwa sababu ulitiririka kutoka hekaluni kwenye mlima mrefu sana, ambao kihalisi haukuwepo katika eneo lililotajwa. Pia, maono hayo yalidokeza kwamba mto huo ulitiririka moja kwa moja hadi kwenye Bahari ya Chumvi, jambo ambalo halingewezekana kulingana na mandhari ya kijiografia ya eneo hilo.

^ fu. 6 Baadhi ya wasomi wanaelewa kwamba maneno haya yanatoa wazo zuri, wanasema kwamba kuvuna chumvi ili kuitumia kuhifadhi vitu ni biashara ya muda mrefu yenye faida katika eneo la Bahari ya Chumvi. Hata hivyo, ona kwamba simulizi hilo lilisema waziwazi kwamba sehemu hizo zenye matope “hazitaponywa.” Zinabaki bila uhai, bila kuponywa, kwa sababu maji yanayoleta uhai kutoka katika nyumba ya Yehova hayafiki huko. Basi inaonekana kwamba katika simulizi hili chumvi ya maeneo hayo yenye matope inatajwa kwa njia isiyo nzuri.—Zab. 107:33, 34; Yer. 17:6.

^ fu. 12 Kuhusiana na hilo, kumbuka mfano wa Yesu wa wavu wa kukokotwa. Samaki wengi wananaswa na wavu, lakini si wote walio “wazuri.” Samaki wasiofaa wanatupwa. Basi Yesu alionya kwamba huenda baadaye idadi kubwa ya watu wanaoingia katika tengenezo la Yehova wakakosa kuwa waaminifu.—Mt. 13:47-50; 2 Tim. 2:20, 21.