Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 20

‘Mtaigawa Nchi Iwe Urithi’

‘Mtaigawa Nchi Iwe Urithi’

EZEKIELI 45:1

WAZO KUU: Maana ya kuigawa nchi

1, 2. (a) Ezekieli anapokea maagizo gani kutoka kwa Yehova? (b) Tutachunguza maswali gani?

EZEKIELI ametoka tu kuona maono ambayo yamemkumbusha miaka 900 hivi iliyopita katika siku za Musa na Yoshua. Wakati huo, Yehova alimweleza Musa kuhusu mipaka ya Nchi ya Ahadi na baadaye akamwambia Yoshua jinsi ambavyo nchi hiyo ingegawanywa kati ya makabila ya Israeli. (Hes. 34:1-15; Yos. 13:7; 22:4, 9) Lakini sasa, katika mwaka wa 593 K.W.K., Yehova anamwagiza Ezekieli na wahamishwa wenzake waigawe tena Nchi ya Ahadi kati ya makabila ya Israeli!—Eze. 45:1; 47:14; 48:29.

2 Maono hayo yalikuwa na ujumbe gani kwa Ezekieli na wahamishwa wenzake? Kwa nini maono hayo yanawatia moyo watu wa Mungu leo? Je, yatatimizwa kwa njia kubwa zaidi wakati ujao?

Maono Yanayotoa Uhakikisho kwa Njia Nne

3, 4. (a) Ni mambo gani manne katika maono ya mwisho ya Ezekieli yaliyowapa wahamishwa uhakikisho? (b) Tutachunguza uhakikisho gani katika sura hii?

3 Maono aliyoona Ezekieli yanazungumziwa katika sura tisa za kitabu chake. (Eze. 40:1–48:35) Yaliwatia moyo wahamishwa kwa kutaja mambo manne yaliyowapa uhakika kuhusu taifa la Israeli lililorudishwa. Ni mambo gani hayo yaliyowapa uhakika? Kwanza, ibada safi ingerudishwa katika hekalu la Mungu. Pili, makuhani na wachungaji waadilifu wangeongoza taifa hilo lililorudishwa. Tatu, wote ambao wangerudi Israeli wangepata urithi wa nchi. Na nne, Yehova angekuwa pamoja nao, na kukaa katikati yao tena.

4 Sura ya 13 na 14 ya kitabu hiki zilizungumzia jinsi ambavyo mambo mawili ya kwanza yangetimizwa, yaani, kurudishwa kwa ibada safi na kuongozwa na wachungaji waadilifu. Katika sura hii, tutakazia uhakikisho wa tatu, ahadi ya kurithi nchi. Katika sura inayofuata tutachunguza ahadi kuhusu kuwapo kwa Yehova.—Eze. 47:13-21; 48:1-7, 23-29.

‘Mmegawiwa Nchi Hii Iwe Urithi Wenu’

5, 6. (a) Katika maono ya Ezekieli ni nchi gani waliyopaswa kuigawa? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.) (b) Maono kuhusu kugawa nchi yalikuwa na kusudi gani?

5 Soma Ezekieli 47:14. Katika maono, Yehova alimwonyesha Ezekieli sehemu ya nchi ambayo baadaye ingekuwa kama “bustani ya Edeni.” (Eze. 36:35) Kisha Yehova akasema: “Hili ndilo eneo ambalo mtayagawia yale makabila 12 ya Israeli kuwa urithi wao wa ardhi.” (Eze. 47:13) “Eneo” ambalo wangegawiwa lilikuwa nchi ya Israeli iliyorudishwa ambako wahamishwa wangerudishwa. Baadaye, kama ilivyoandikwa kwenye Ezekieli 47:15-21, Yehova alifafanua kwa undani mipaka hususa ya nchi yote.

6 Maono hayo ya kuigawa nchi yalikuwa na kusudi gani? Ufafanuzi wa vipimo hususa vya mipaka ulimhakikishia Ezekieli na wahamishwa wenzake kwamba kwa hakika nchi yao waliyoipenda ingerudishwa. Wazia jinsi ambavyo uhakikisho huo kutoka kwa Yehova, wenye habari nyingi na maelezo yaliyo wazi, ulivyowatia moyo wahamishwa hao! Je, kweli watu hao wa Mungu waligawiwa urithi katika nchi waliyopewa? Ndiyo.

7. (a) Ni matukio gani yaliyoanza mwaka wa 537 K.W.K., na yanatukumbusha nini? (b) Tutachunguza swali gani kwanza?

7 Mwaka wa 537 K.W.K., miaka 56 hivi baada ya Ezekieli kupata maono, maelfu ya wahamishwa walianza kurudi katika nchi ya Israeli na kuimiliki. Matukio hayo makubwa ya zamani yanatukumbusha jambo kama hilo ambalo wakati wetu limekuwa likitokea kati ya watu wa Mungu. Kwa njia fulani, wao pia walipokea urithi wa nchi. Jinsi gani? Yehova aliwaruhusu watu wake waingie katika nchi ya kiroho na kuimiliki. Kwa hiyo, kurudishwa kwa Nchi ya Ahadi zamani kunatufundisha mengi kuhusu kurudishwa kwa nchi ya kiroho ya watu wa Mungu leo. Lakini kabla ya kuchunguza mambo hayo, acheni kwanza tujibu swali hili, “Kwa nini tunaweza kusema kwamba kwa kweli leo kuna nchi ya kiroho?”

8. (a) Yehova alichagua taifa gani baada ya kuwakataa Waisraeli wa asili? (b) Nchi, au paradiso ya kiroho ni nini? (c) Ilianzishwa lini, na ni nani wanaoishi humo?

8 Katika maono ambayo Ezekieli aliona awali, Yehova alionyesha kwamba unabii kuhusu kurudishwa kwa Israeli ungetimizwa kwa njia kubwa zaidi baada ya ‘mtumishi wake Daudi,’ yaani, Yesu Kristo, kuanza kutawala akiwa Mfalme. (Eze. 37:24) Jambo hilo lilitokea mwaka wa 1914 W.K. Kufikia wakati huo, muda mrefu ulikuwa umepita tangu Waisraeli wa asili walipoacha kuwa watu wa Mungu na nafasi yao kuchukuliwa na taifa la Israeli wa kiroho, lililofanyizwa na Wakristo waliotiwa mafuta. (Soma Mathayo 21:43; 1 Petro 2:9.) Hata hivyo, Yehova hakulikataa tu taifa la asili la Israeli na kuanzisha taifa la kiroho bali pia aliikataa nchi halisi ya Israeli na kuanzisha nchi, au paradiso ya kiroho. (Isa. 66:8) Kama tulivyoona katika Sura ya 17 ya kitabu hiki, nchi ya kiroho ni mazingira salama ya kiroho, au mahali pa utendaji, ambapo watiwa mafuta waliobaki wamekuwa wakimwabudu Yehova tangu mwaka wa 1919. (Tazama sanduku la 9B, “Kwa Nini 1919?”) Muda ulipozidi kupita, wale walio na tumaini la kuishi duniani, yaani, “kondoo wengine,” walianza pia kuingia katika nchi hiyo ya kiroho. (Yoh. 10:16) Ingawa paradiso ya kiroho inazidi kukua na kupanuka leo, baraka zake zitaonekana kikamili baada ya Har–Magedoni.

Kuigawa Nchi kwa Usawa na Kikamili

9. Yehova alitoa maagizo gani yenye kina kuhusu kuigawa nchi?

9 Soma Ezekieli 48:1, 28. Baada ya kuweka mipaka ya nje ya nchi hiyo, Yehova alieleza kwa undani jinsi ya kuigawa nchi hiyo. Aliagiza maeneo ya urithi ya makabila 12 yapimwe kwa usawa na ukamili kuanzia kaskazini hadi kusini, akianza na kabila la Dani upande wa kaskazini wa nchi na kumalizia na kabila la Gadi kwenye mpaka wa kusini. Kila eneo la urithi la makabila yote 12 lilikuwa na mipaka iliyonyooka kutoka mpaka wa mashariki wa nchi hadi Bahari Kuu, yaani, Bahari ya Mediterania, upande wa magharibi.—Eze. 47:20.

10. Inaelekea sehemu hii ya maono iliwapa wahamishwa uhakikisho gani?

10 Inaelekea sehemu hii ya maono iliwapa wahamishwa uhakikisho gani? Ufafanuzi wenye kina ambao Ezekieli alitoa kuhusu kuigawa nchi uliwasadikishia wahamishwa kwamba nchi hiyo ingegawanywa kwa mpangilio mzuri. Isitoshe, kuigawa nchi kihususa kati ya makabila yote 12 kulikazia kwamba kwa hakika kila mhamishwa aliyerudi angepata urithi katika nchi iliyorudishwa. Hakuna mtu aliyerudi ambaye angekosa ardhi au makazi.

11. Tunapata masomo gani kutokana na maono kuhusu kuigawa nchi? (Tazama sanduku “Kuigawa Nchi.”)

11 Leo tunapata masomo gani yenye kuimarisha kutokana na maono hayo? Nchi ya Ahadi iliyorudishwa haikuwa tu na eneo kwa ajili ya makuhani, Walawi, na wakuu, bali pia kulikuwa na maeneo kwa ajili ya watu wengine wote wa makabila 12. (Eze. 45:4, 5, 7, 8) Vivyo hivyo, leo paradiso ya kiroho ina nafasi kwa ajili ya watiwa mafuta waliobaki, washiriki wa “umati mkubwa” wanaoongoza, na pia washiriki wengine wote wa umati mkubwa. * (Ufu. 7:9) Hata iwe tunatimiza jukumu dogo kadiri gani katika tengenezo, tuna hakika kwamba tuna mahali na mgawo wenye thamani katika nchi ya kiroho. Huo ni uhakikisho wenye kutia moyo!

Hata iwe tunatimiza jukumu gani katika tengenezo la Mungu, Yehova anathamini jitihada zetu (Tazama fungu la 11)

Tofauti Mbili Kubwa—Zina Maana Gani Kwetu?

12, 13. Yehova alitoa maagizo gani hususa kuhusu kuyagawia makabila urithi katika nchi?

12 Huenda Ezekieli alishangazwa na baadhi ya maagizo ambayo Yehova alimpatia kwa sababu yalitofautiana na maagizo ambayo Mungu alimpa Musa. Fikiria tofauti mbili. Moja inahusu nchi, na nyingine wakaaji wake.

13 Kwanza, nchi. Musa aliagizwa ayagawie makabila makubwa eneo kubwa kuliko makabila madogo. (Hes. 26:52-54) Hata hivyo, katika maono ya Ezekieli, Yehova alitoa maagizo hususa ya kuyagawia urithi makabila yote “kwa usawa [“kila mtu kama ndugu yake,” maelezo ya chini].” (Eze. 47:14) Basi umbali kutoka mpaka wa kaskazini hadi mpaka wa kusini katika urithi wa kila kabila ulipaswa kulingana katika maeneo yote 12. Waisraeli wote—bila kuzingatia kabila lao—wangepata kwa usawa mazao mengi ambayo yangetokezwa na Nchi ya Ahadi yenye maji mengi.

14. Maagizo ya Yehova kuhusu wakaaji wageni yalitofautianaje na maagizo katika Sheria ya Musa?

14 Pili, wakaaji. Sheria ya Musa iliwalinda wageni na kuwaruhusu washiriki katika ibada ya Yehova, lakini hawangepata urithi katika nchi. (Law. 19:33, 34) Hata hivyo, jambo ambalo Yehova alimwambia Ezekieli ni tofauti na jambo alilokuwa amesema kwenye Sheria. Yehova alimwagiza hivi: “Mnapaswa kumpa mkaaji mgeni urithi katika eneo la kabila analoishi ndani yake.” Kupitia amri hiyo, Yehova alifutilia mbali tofauti kubwa kati ya “Waisraeli wenyeji” na wakaaji wageni katika nchi. (Eze. 47:22, 23) Katika nchi iliyorudishwa ambayo Ezekieli aliona katika maono, aliona kwamba wakaaji wake walikuwa na usawa na umoja wa ibada.—Law. 25:23.

15. Ni jambo gani lisilobadilika kumhusu Yehova ambalo lilithibitishwa na maagizo yake kuhusu nchi na wakaaji wake?

15 Maagizo hayo muhimu ambayo Ezekieli alipokea kuhusu nchi na wakaaji wake yaliwafariji wahamishwa. Walijua kwamba Yehova angewagawia maeneo yaliyo sawa, iwe walikuwa Waisraeli kwa kuzaliwa au wageni waliomwabudu Yehova. (Ezra 8:20; Neh. 3:26; 7:6, 25; Isa. 56:3, 8) Maagizo hayo pia yalitoa uhakikisho wenye kutia moyo na usiobadilika kwamba Yehova anawaona watumishi wake wote kuwa wenye thamani. (Soma Hagai 2:7.) Leo, iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au kuishi duniani, tunaamini jambo hilo.

16, 17. (a) Tunafaidikaje kwa kuchunguza habari kuhusu nchi na wakaaji wake? (b) Tutachunguza nini katika sura inayofuata?

16 Tunafaidikaje kwa kuchunguza habari hizo kuhusu nchi na wakaaji wake? Tunakumbushwa kwamba leo usawa na umoja unapaswa kuonekana waziwazi katika undugu wetu wa ulimwenguni pote. Yehova hana ubaguzi. Tunapaswa kujiuliza: ‘Je, ninamwiga Yehova kwa kuepuka ubaguzi? Je, ninamtendea kila mmoja kati ya waabudu wenzangu kwa heshima inayotoka moyoni, bila kuangalia jamii aliyotoka na hali zake maishani?’ (Rom. 12:10) Tunashangilia kwamba Yehova ametupatia sisi sote nafasi sawa katika paradiso ya kiroho, ambapo tunamtolea Baba yetu wa mbinguni utumishi mtakatifu kwa nafsi yote na kufurahia baraka kutoka kwake.—Gal. 3:26-29; Ufu. 7:9.

Je, tunamwiga Yehova kwa kuwaheshimu wengine kutoka moyoni na kuepuka ubaguzi? (Tazama fungu la 15 na 16)

17 Acheni sasa tuchunguze uhakikisho wa nne katika sehemu ya kumalizia ya maono ya mwisho ya Ezekieli—ahadi kwamba Yehova atakuwa pamoja na wahamishwa. Tunajifunza masomo gani kutokana na ahadi hiyo? Tutapata jibu katika sura inayofuata.

^ fu. 11 Ili upate habari kuhusu mahali pa pekee na mgawo ambao Yehova ameweka kwa ajili ya makuhani na mkuu katika paradiso ya kiroho, tazama Sura ya 14 ya kitabu hiki.