Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 9

“Nitawapa Moyo Wenye Umoja”

“Nitawapa Moyo Wenye Umoja”

EZEKIELI 11:19

WAZO KUU: Ujumbe wa kurudishwa na jinsi unavyofafanuliwa katika unabii wa Ezekieli

1-3. Wababiloni wanawadhihaki jinsi gani waabudu wa Yehova, na kwa nini?

WAZIA kwamba wewe ni Myahudi mwaminifu unayeishi katika jiji la Babiloni. Watu wa jamii yako wamekuwa uhamishoni kwa miaka hamsini hivi. Kama ilivyo desturi yenu siku ya Sabato, unaenda kukutana na waamini wenzako ili kumwabudu Yehova. Unapopita kwenye barabara zenye shughuli nyingi, unaona mahekalu makubwa na pia sehemu nyingi takatifu. Watu wengi wanakusanyika kwenye maeneo hayo wakitoa dhabihu na kuimba nyimbo zinazosifu miungu kama vile Marduki.

2 Mbali kidogo na umati huo unakutana na kikundi kidogo cha waabudu wenzako. * Mnatafuta sehemu tulivu—labda kando ya mojawapo ya mifereji ya jiji—ili kusali, kuimba zaburi, na kutafakari Neno la Mungu pamoja. Mnaposali pamoja, mnasikia sauti za mashua za mbao zilizoegeshwa kando ya mfereji huo. Mnafurahi kwamba sehemu hiyo ina utulivu. Mnatumaini kwamba watu wa eneo hilo hawatakuja kuvuruga mkutano huo kama wanavyofanya. Kwa nini wanafanya hivyo?

3 Jiji la Babiloni limeshinda vita mara nyingi, na watu wanasema kwamba nguvu za jiji hilo zinatokana na miungu yao ya uwongo. Wababiloni wanaona kwamba kuharibiwa kabisa kwa Yerusalemu kunathibitisha mungu wao Marduki ana nguvu kuliko Yehova! Kwa hiyo, wanamdhihaki Mungu wenu na watu wake. Nyakati nyingine wanawadhihaki kwa kuwaambia: “Tuimbieni mojawapo ya nyimbo za Sayuni”! (Zab. 137:3) Zaburi nyingi zinashangilia ushindi wa Sayuni dhidi ya adui za Yehova. Labda Wababiloni hasa wanapenda kudhihaki zaburi hizo. Hata hivyo, baadhi ya zaburi zinazungumzia Wababiloni wenyewe. Kwa mfano, zaburi moja inasema: “[Wamebadili] Yerusalemu kuwa rundo la magofu. . . . Wale wanaotuzunguka wanatudhihaki na kutufanyia mzaha.”—Zab. 79:1, 3, 4.

4, 5. Unabii wa Ezekieli ulitoa tumaini gani, na tutazungumzia nini katika sura hii? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

4 Pia, kuna Wayahudi waasi imani, ambao wanapenda kuwadhihaki kuwa mnamwamini Yehova na manabii wake. Licha ya dhihaka hizo, ibada safi inakufariji wewe na familia yako. Mnafurahia kusali na kuimba pamoja. Mnafarijika kwa kusoma Neno la Mungu. (Zab. 94:19; Rom. 15:4) Wazia kwamba siku hiyo, mmoja wa waabudu wenzako ameleta kitu cha pekee kwenye mkutano—kitabu cha kukunjwa kilicho na unabii wa Ezekieli. Unafurahi kusikia ahadi ya Yehova ya kuwarudisha watu wake katika nchi yao. Moyo wako unachangamka unaposikia unabii huo ukisomwa kwa sauti kubwa, na unatafakari tumaini la kwamba siku moja wewe na familia yako mtarudi na kusaidia kufanya kazi hiyo yenye kusisimua ya kurudisha ibada safi!

5 Unabii wa Ezekieli unazungumzia tena na tena ahadi za kurudishwa. Acheni tuchunguze ujumbe huo wenye tumaini. Ahadi hizo zilitimizwaje kwa watu waliokuwa uhamishoni? Unabii huo una maana gani siku hizi? Katika visa fulani, tutachunguza pia utimizo wa mwisho wa unabii huo wakati ujao.

“Watapelekwa Uhamishoni, Utekwani”

6. Mungu alikuwaje amewaonya tena na tena watu wake walioasi?

6 Kupitia Ezekieli, Yehova aliwaambia waziwazi watu wake jinsi atakavyowaadhibu kwa sababu ya kuasi. “Watapelekwa uhamishoni, utekwani.” (Eze. 12:11) Kama tulivyoona katika Sura ya 6 ya kitabu hiki, Ezekieli aliigiza hukumu hiyo. Lakini hiyo haikuwa mara ya kwanza kuonywa. Tangu siku za Musa, karibu miaka elfu moja mapema, Yehova alikuwa amewaonya watu wake kwamba ikiwa wangeendelea kuasi, wangepelekwa uhamishoni. (Kum. 28:36, 37) Manabii Isaya na Yeremia walikuwa wametoa maonyo kama hayo.—Isa. 39:5-7; Yer. 20:3-6.

7. Yehova aliwaadhibu watu wake jinsi gani?

7 Inasikitisha kwamba watu wengi hawakusikiliza. Baada ya muda, Yehova alivunjika moyo kwa sababu watu wake waliasi, wakaabudu sanamu, na kupotoka wakichochewa na wachungaji wabaya. Kwa hiyo, akaruhusu wapatwe na njaa, ambayo ilikuwa msiba na aibu, kwa kuwa nchi yao ilikuwa “nchi inayotiririka maziwa na asali.” (Eze. 20:6, 7) Kisha, kama alivyotabiri mapema, Yehova aliruhusu watu wake walioasi waadhibiwe kwa kupelekwa uhamishoni. Mwaka wa 607 K.W.K., Nebukadneza wa Babiloni alifanya shambulizi la mwisho, akaharibu Yerusalemu na hekalu lake. Maelfu ya Wayahudi waliookoka walipelekwa uhamishoni Babiloni. Wakiwa huko walidhihakiwa na kupingwa kama tulivyoona mwanzoni mwa sura hii.

8, 9. Mungu alilionyaje kutaniko la Kikristo dhidi ya uasi imani?

8 Je, kutaniko la Kikristo lilipatwa na jambo kama lile lililowapata wahamishwa waliokuwa Babiloni? Ndiyo! Kama Wayahudi wa kale, wafuasi wa Kristo walionywa mapema. Mwanzoni mwa huduma yake Yesu alisema: “Jihadharini na manabii wa uwongo ambao huja kwenu katika mavazi ya kondoo, lakini ndani wao ni mbwamwitu wakali.” (Mt. 7:15) Miaka mingi baadaye, mtume Paulo aliongozwa na roho kutoa onyo kama hilo: “Ninajua kwamba nitakapoondoka mbwamwitu wenye kukandamiza wataingia miongoni mwenu nao hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka miongoni mwenu watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.”—Mdo. 20:29, 30.

9 Wakristo walifundishwa jinsi ya kuwatambua na kuwaepuka watu hao hatari. Wazee Wakristo waliagizwa wawaondoe kutanikoni waasi imani. (1 Tim. 1:19; 2 Tim. 2:16-19; 2 Pet. 2:1-3; 2 Yoh. 10) Hata hivyo, kama ilivyokuwa kwa Israeli na Yuda hapo zamani, pole kwa pole Wakristo wengi hawakusikiliza maonyo yenye upendo. Mwishoni mwa karne ya kwanza uasi imani ulikuwa umetia mizizi katika kutaniko. Yohana, mtume wa mwisho aliyekuwa hai mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., alisema kwamba kutaniko lilikuwa limeathiriwa na upotovu na uasi mwingi. Yeye ndiye aliyekuwa kizuizi pekee dhidi ya uovu huo. (2 The. 2:6-8; 1 Yoh. 2:18) Ni nini kilichotokea baada ya Yohana kufa?

10, 11. Mfano wa Yesu kuhusu ngano na magugu ulitimizwaje kuanzia karne ya pili W.K. na kuendelea?

10 Baada ya Yohana kufa, mfano wa Yesu kuhusu ngano na magugu ulianza kutimizwa. (Soma Mathayo 13:24-30.) Kama Yesu alivyokuwa ametabiri, Shetani alipanda kutanikoni “magugu,” yaani, Wakristo wa uwongo, na uasi ukaenea haraka kutanikoni. Yehova alivunjika moyo sana kuona kutaniko lililoanzishwa na Mwana wake likichafuliwa na ibada ya sanamu, sikukuu na mazoea ya kipagani, na mafundisho ya uwongo yaliyotokana na dini za kishetani na wanafalsafa wasiomwogopa Mungu! Yehova alifanya nini? Kama alivyowatendea Waisraeli wasio waaminifu, aliruhusu watu wake wapelekwe uhamishoni. Kuanzia kipindi fulani katika karne ya pili W.K. na kuendelea, watu walio kama ngano walifunikwa na Wakristo wa uwongo. Kwa hiyo, kutaniko la Kikristo likaenda uhamishoni katika Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, nao Wakristo wa uwongo wakamezwa na milki hiyo iliyopotoka. Wakristo wa uwongo walipozidi kuongezeka, dini zinazodai kuwa za Kikristo zikasitawi.

11 Katika kipindi chote cha giza la utawala wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, kulikuwa na baadhi ya Wakristo wa kweli, “ngano” ambayo Yesu alitaja kwenye mfano wake. Kama Wayahudi waliokuwa uhamishoni wanaotajwa katika Ezekieli 6:9, walimkumbuka Mungu wa kweli. Baadhi yao walipinga kwa ujasiri mafundisho ya uwongo ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Walidhihakiwa na kuteswa. Je, Yehova alikusudia kuwaacha watu wake katika giza hilo la kiroho milele? Hapana! Kama ilivyokuwa kwa Waisraeli wa zamani, Yehova alionyesha hasira kwa kiwango kinachofaa na kwa kipindi kinachofaa cha wakati. (Yer. 46:28) Isitoshe, Yehova hakuwaacha watu wake bila tumaini. Acheni tuzungumzie tena wale Wayahudi waliokuwa uhamishoni katika Babiloni la kale na tuone jinsi Yehova alivyowapa tumaini la kuwatoa utekwani.

Kwa karne nyingi, Wakristo wa kweli walikabili mateso mikononi mwa Babiloni Mkubwa (Tazama fungu la 10, 11)

‘Hasira Yangu Itakoma’

12, 13. Kwa nini mwishowe Yehova angeacha kuwakasirikia watu wake waliohamishwa katika siku za Ezekieli?

12 Yehova aliwaambia waziwazi watu wake kuhusu hasira yake, lakini pia aliwahakikishia kwamba hasira yake ya uadilifu haingedumu milele. Kwa mfano, ona maneno haya: “Ndipo hasira yangu itakapokoma, na ghadhabu yangu dhidi yao itatulia, nami nitaridhika. Nitakapomaliza kuwamwagia ghadhabu yangu, watalazimika kujua kwamba mimi, Yehova, ninasisitiza watu waniabudu mimi peke yangu.” (Eze. 5:13) Kwa nini hatimaye Yehova angeacha kukasirika?

13 Kati ya mateka kulikuwa na Wayahudi waaminifu waliopelekwa uhamishoni pamoja na watu wasio waaminifu. Isitoshe, kupitia Ezekieli, Mungu alitabiri kwamba baadhi ya watu wake wangetubu wakiwa uhamishoni. Wayahudi hao waliotubu wangesimulia mambo ya kuaibisha ambayo walifanya walipomwasi Mungu wao, nao wangemwomba Yehova msamaha na kibali. (Eze. 6:8-10; 12:16) Ezekieli, nabii Danieli na wenzake watatu, walikuwa miongoni mwa watu hao waaminifu. Danieli aliishi muda mrefu hivi kwamba aliona mwanzo na mwisho wa uhamisho. Sala yake ya kutoka moyoni ya kutubu dhambi za Israeli imeandikwa katika Danieli sura ya 9. Bila shaka, maneno yake yaliwakilisha hisia za maelfu ya watu waliokuwa uhamishoni ambao walitamani kusamehewa na Yehova na kupata baraka tena. Walichochewa sana na ahadi za Ezekieli zilizoongozwa na roho kuhusu kuwekwa huru na kurudishwa katika nchi yao!

14. Kwa nini Yehova angewarudisha watu wake kwenye nchi yao?

14 Hata hivyo, kulikuwa na sababu muhimu zaidi ya kuwekwa huru na kurudishwa kwa watu wa Yehova. Kipindi kirefu cha wao kuwa uhamishoni kingekwisha, si kwa sababu walistahili kuwekwa huru, bali kwa sababu ulikuwa wakati mwingine wa Yehova kulitakasa jina lake mbele ya mataifa yote. (Eze. 36:22) Wababiloni hao wangejua tena kwamba miungu yao yote ya kishetani, kama vile Marduki, haingeweza kulinganishwa na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Acheni tuchunguze ahadi tano ambazo Yehova alimwongoza Ezekieli awatangazie wahamishwa wenzake. Kwanza, acheni tuchunguze kila ahadi ingekuwa na maana gani kwa watu hao waaminifu. Kisha tutaona jinsi ahadi hizo zilivyotimizwa kwa njia kubwa zaidi.

15. Ni mabadiliko gani ambayo yangefanywa katika ibada ya wale waliorudi?

15 AHADI YA KWANZA. Hakutakuwa tena na ibada ya sanamu na matendo mengine yenye kuchukiza yanayohusiana na ibada ya uwongo. (Soma Ezekieli 11:18; 12:24.) Kama ilivyozungumziwa katika Sura ya 5 ya kitabu hiki, Yerusalemu na hekalu lake lilikuwa limechafuliwa na mazoea ya dini ya uwongo, kama vile ibada ya sanamu. Kwa hiyo, watu walikuwa wamepotoka na kujitenga na Yehova. Kupitia Ezekieli, Yehova alitabiri kwamba wahamishwa wangetazamia wakati ambapo wangeshiriki tena katika ibada safi isiyo na upotovu. Baraka nyingine zote za kurudishwa zingetegemea jambo hili muhimu: kurudishwa kwa mpango wa Mungu wa ibada safi.

16. Yehova alitoa ahadi gani kuhusu nchi ya watu wake?

16 AHADI YA PILI. Kurudi katika nchi yao. Yehova aliwaambia hivi watu waliohamishwa: “Nitawapa nchi ya Israeli.” (Eze. 11:17) Hii ilikuwa ahadi muhimu, kwa kuwa Wababiloni, waliowadhihaki watu wa Mungu waliotekwa, hawakuwapa kamwe tumaini kwamba wangerudi katika nchi yao waliyoipenda. (Isa. 14:4, 17) Isitoshe, ikiwa watu waliorudi wangeendelea kuwa waaminifu, nchi hiyo ingekuwa na rutuba na ingetoa mazao, pia ingewategemeza na wangekuwa na kazi nzuri. Aibu na taabu ya njaa ingesahaulika kabisa.—Soma Ezekieli 36:30.

17. Ingekuwaje kuhusu kumtolea Yehova dhabihu?

17 AHADI YA TATU. Kutolewa tena kwa dhabihu katika madhabahu ya Yehova. Kama ilivyotajwa katika Sura ya 2 ya kitabu hiki, chini ya Sheria, dhabihu na matoleo yalikuwa sehemu muhimu ya ibada safi. Ikiwa wahamishwa waliorudi wangeendelea kuwa watiifu na safi kiroho, Yehova angekubali dhabihu zao. Kwa hiyo, dhambi za watu zingefunikwa na wangeendelea kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu. Yehova aliahidi hivi: “Watu wote wa nyumba ya Israeli, wote, watanitumikia nchini. Nitafurahishwa nao huko, nami nitadai mnipe michango yenu na matunda ya kwanza ya matoleo yenu, vitu vyenu vyote vitakatifu.” (Eze. 20:40) Kwa kweli, ibada safi ingerudishwa na kuwaletea watu wa Mungu baraka.

18. Yehova angewachungaje watu wake?

18 AHADI YA NNE. Kupepetwa kwa wachungaji wabaya. Sababu kuu iliyofanya watu wa Mungu wafanye makosa mazito ni kupotoshwa na wanaume waliokuwa wakiongoza. Yehova aliahidi kwamba angebadili jambo hilo. Kuhusu wachungaji hao wabaya, aliahidi hivi: “Nitawafukuza ili wasiwalishe kondoo wangu . . . Nitawaokoa kondoo wangu kutoka kinywani mwao.” Kinyume chake, Yehova aliwaahidi hivi watu wake waaminifu: “Nitawatunza kondoo wangu.” (Eze. 34: 10, 12) Angefanyaje hivyo? Angewatumia wanaume waaminifu na walio washikamanifu wawe wachungaji.

19. Yehova aliahidi nini kuhusu umoja?

19 AHADI YA TANO. Umoja kati ya waabudu wa Yehova. Wazia jinsi waabudu waaminifu walivyosikitika kuona mgawanyiko kati ya watu wa Mungu kabla ya kwenda uhamishoni. Wakichochewa na manabii wa uwongo na wachungaji waovu, watu waliwaasi manabii waaminifu waliomwakilisha Yehova; hata watu waligawanyika katika makundi yaliyopingana. Kwa hiyo, mojawapo ya mambo yenye kupendeza kuhusu kurudishwa ni ahadi hii iliyotolewa kupitia Ezekieli: “Nitawapa moyo wenye umoja, nami nitatia roho mpya ndani yao.” (Eze. 11:19) Ikiwa Wayahudi waliorudi wangeendelea kuwa na uhusiano mzuri na Yehova Mungu na kati yao wenyewe, hakuna mpinzani ambaye angewashinda. Wakiwa taifa, wangemletea tena Yehova utukufu badala ya aibu na fedheha.

20, 21. Ahadi za Mungu zilitimizwaje kwa wahamishwa waliorudi?

20 Je, Wayahudi waliorudi kutoka uhamishoni waliona ahadi zote tano zikitimizwa? Tunapaswa kukumbuka maneno ya Yoshua mwaminifu aliyeishi zamani: “Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya ahadi zote nzuri ambazo Yehova Mungu wenu aliwaahidi. Zote zimetimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja aliloahidi.” (Yos. 23:14) Kama ilivyokuwa katika siku za Yoshua; ingekuwa hivyo pia katika siku za wahamishwa waliorudi katika nchi yao.

21 Wayahudi waliacha ibada ya sanamu na mazoea mengine yenye kuchukiza ya dini ya uwongo yaliyowatenganisha na Yehova. Ingawa ilionekana kuwa jambo lisilowezekana, walianza kuishi tena katika nchi yao, wakilima na kufurahia maisha mazuri huko. Mojawapo ya mambo waliyofanya kwanza ni kurudisha madhabahu ya Yehova huko Yerusalemu na kutoa dhabihu zinazokubalika juu yake. (Ezra 3:2-6) Yehova aliwabariki kwa kuwapa wachungaji wazuri wa kiroho, wanaume kama vile Ezra aliyekuwa mwandishi na kuhani mwaminifu, magavana Nehemia na Zerubabeli, Kuhani Mkuu Yoshua, na manabii wenye ujasiri Hagai, Zekaria, na Malaki. Ikiwa watu wangeendelea kufuata mwongozo na maagizo ya kiroho, wangefurahia umoja ambao waliukosa kwa muda mrefu, muda mrefu sana.—Isa. 61:1-4; soma Yeremia 3:15.

22. Tunajuaje kwamba utimizo wa kwanza wa unabii wa kurudishwa ulikuwa kionjo tu cha jambo kubwa zaidi?

22 Bila shaka, utimizo wa kwanza wa ahadi za Yehova kuhusu kurudishwa ulitia moyo sana! Hata hivyo, utimizo huo ulikuwa kionjo tu cha jambo kubwa zaidi. Tunajuaje jambo hilo? Ahadi hizo zilikuwa na masharti; Yehova angezitimiza ikiwa tu watu wangeendelea kuwa watiifu na wasikivu. Baada ya muda, Wayahudi walikosa kutii na wakaasi tena. Lakini kama Yoshua alivyosema, sikuzote Yehova hutimiza ahadi zake. Kwa hiyo, ahadi hizo zingetimizwa kwa njia kubwa zaidi na ya kudumu. Acheni tuone jinsi jambo hilo lilivyotimizwa.

“Nitafurahishwa Nanyi”

23, 24. “Nyakati za kurudishwa kwa mambo yote” zilianza lini na jinsi gani?

23 Tukiwa wanafunzi wa Biblia tunajua kwamba mfumo huu mwovu wa mambo uliingia katika kipindi chake cha mwisho, yaani, siku za mwisho, mwaka wa 1914. Hata hivyo, kwa watumishi wa Yehova, hiki si kipindi cha kuhuzunika. Kwa kweli, Biblia inaonyesha kwamba jambo fulani lenye kusisimua lilianza kutokea mwaka wa 1914—“nyakati za kurudishwa kwa mambo yote.” (Mdo. 3:21) Tunajuaje jambo hilo? Ni nini kilichotokea mbinguni mwaka wa 1914? Yesu Kristo aliwekwa kuwa Mfalme wa Kimasihi! Kwa nini hilo lilikuwa tukio la kurudishwa? Kumbuka Yehova alimwahidi Mfalme Daudi kwamba ufalme ungekuwa katika ukoo wake milele. (1 Nya. 17:11-14) Ufalme huo ulikatishwa mwaka wa 607 K.W.K. Wababiloni walipoharibu Yerusalemu na kukomesha utawala wa wafalme wa ukoo wa Daudi.

24 Akiwa “Mwana wa binadamu,” Yesu alikuwa mzao wa Daudi na hivyo akawa mrithi wa kisheria wa ufalme katika ukoo wa Daudi. (Mt. 1:1; 16:13-16; Luka 1:32, 33) Mwaka wa 1914 Yehova alipompa Yesu kiti cha ufalme mbinguni, “nyakati za kurudishwa kwa mambo yote” zikaanza! Sasa njia ilikuwa wazi kwa Yehova kumtumia Mfalme huyo mkamilifu kuendeleza kazi ya kurudishwa.

25, 26. (a) Kipindi kirefu cha uhamisho katika Babiloni Mkubwa kilifikia mwisho lini, na tunajuaje hivyo? (Pia, tazama sanduku “Kwa Nini 1919?”) (b) Ni jambo gani lililoanza kutimizwa kuanzia 1919 na kuendelea?

25 Mojawapo ya hatua ambazo Kristo alichukua kwanza akiwa Mfalme ni kujiunga na Baba yake kukagua mpango wa ibada safi duniani. (Mal. 3:1-5) Kama Yesu alivyokuwa ametabiri katika mfano wake wa ngano na magugu, kwa muda mrefu ilikuwa vigumu kutofautisha kati ya ngano na magugu, yaani, Wakristo wa kweli waliotiwa mafuta, na Wakristo wa uwongo. * Hata hivyo, sasa kipindi cha mavuno kilifika mwaka wa 1914, na tofauti kati ya ngano na magugu ilikuwa wazi. Miaka mingi kabla ya 1914, Wanafunzi waaminifu wa Biblia walikuwa wakifunua makosa makubwa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo na walikuwa wameanza kujitenga na dini ya uwongo. Wakati ulikuwa umefika wa Yehova kuwarudisha kikamili. Basi, mwanzoni mwa mwaka wa 1919, miaka michache baada ya “wakati wa mavuno” kuanza, watu wa Mungu waliwekwa huru kabisa kutoka katika utekwa wa Babiloni Mkubwa. (Mt. 13:30) Walikuwa wametoka uhamishoni!

26 Unabii wa Ezekieli kuhusu kurudishwa ulianza kutimizwa kwa njia kubwa zaidi kuliko utimizo ambao watu wa Mungu waliona nyakati za kale. Acheni sasa tuchunguze jinsi ambavyo ahadi tano ambazo tayari tumezungumzia zimetimizwa kwa njia kubwa zaidi.

27. Mungu aliwasafishaje watu wake ili waache ibada ya sanamu?

27 AHADI YA KWANZA. Mwisho wa ibada ya sanamu na mazoea mengine ya kidini yenye kuchukiza. Mwishoni mwa karne ya 19 na mwanzoni mwa karne ya 20, Wakristo waaminifu walikuwa wakikusanyika pamoja na walikuwa wameanza kuacha mazoea ya dini ya uwongo. Waliacha kuamini mafundisho yaliyotokana na dini ya uwongo ambayo hayapatani na Maandiko kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi ya mwanadamu, na moto wa mateso. Walifunua waziwazi kwamba kutumia mifano katika ibada ni ibada ya sanamu. Hatua kwa hatua, watu wa Mungu wakatambua kwamba kutumia msalaba katika ibada ni kuabudu sanamu.—Eze. 14:6.

28. Watu wa Yehova walirudishwaje katika nchi yao?

28 AHADI YA PILI. Kurudishwa katika nchi ya kiroho ya watu wa Mungu. Wakristo waaminifu walipoondoka katika dini za Kibabiloni walijikuta katika nchi yao nzuri ya kiroho, hali nzuri, au mazingira mazuri, ambako hawangekuwa tena na njaa kiroho. (Soma Ezekieli 34:13, 14.) Kama tutakavyoona katika Sura ya 19 ya kitabu hiki, Yehova ameibariki nchi hiyo kwa chakula kingi sana cha kiroho kuliko wakati mwingine wowote.—Eze. 11:17.

29. Kazi ya kuhubiri ilitiliwaje mkazo mwaka wa 1919?

29 AHADI YA TATU. Kutolewa tena kwa dhabihu kwenye madhabahu ya Yehova. Katika karne ya kwanza, Wakristo walifundishwa kwamba hawangemtolea Mungu dhabihu halisi za wanyama, bali wangemtolea dhabihu zenye thamani zaidi—maneno waliyosema ili kumtukuza Yehova na kuwahubiria wengine kumhusu. (Ebr. 13:15) Kwa karne nyingi walizokuwa uhamishoni, hakukuwa na mpango rasmi wa kutoa dhabihu hizo. Hata hivyo, walipokuwa karibu kutoka uhamishoni, tayari watu wa Mungu walikuwa wakitoa dhabihu hizo za sifa. Walifanya kazi ya kuhubiri kwa bidii na walikuwa wakimsifu Mungu kwa furaha katika mikutano yao. Tangu mwaka wa 1919, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alikazia zaidi kazi ya kuhubiri na kuipanga vizuri hata zaidi. (Mt. 24:45-47) Kwa hiyo, madhabahu ya Yehova ilifurika dhabihu za jeshi lililokuwa likiongezeka la watu waliokuwa wakilisifu jina lake takatifu!

30. Yesu alifanya nini ili kutimiza uhitaji wa watu wake wa kuwa na wachungaji wazuri?

30 AHADI YA NNE. Kupepetwa kwa wachungaji wabaya. Kristo aliwaweka huru watu wa Mungu kutoka kwa wachungaji wasio wanyoofu na wenye ubinafsi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Katika kundi la Kristo, wachungaji waliotenda kama wachungaji hao wa uwongo waliondolewa. (Eze. 20:38) Yesu akiwa Mchungaji Mwema alihakikisha kwamba kondoo wake wanatunzwa. Mwaka wa 1919 alimweka rasmi mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara. Kikundi hicho kidogo cha Wakristo washikamanifu waliotiwa mafuta kiliongoza katika kuandaa chakula cha kiroho, ili kuwatunza watu wa Mungu. Baadaye, wazee walizoezwa ili kusaidia kulitunza “kundi la Mungu.” (1 Pet. 5:1, 2) Ufafanuzi ulioongozwa na roho katika Ezekieli 34:15, 16 umetumiwa mara kwa mara kuwakumbusha wachungaji Wakristo viwango vilivyowekwa na Yehova Mungu na Yesu Kristo.

31. Yehova alitimizaje unabii wa Ezekieli 11:19?

31 AHADI YA TANO. Umoja kati ya waabudu wa Yehova. Kwa karne nyingi, dini zinazodai kuwa za Kikristo zimegawanyika katika maelfu ya madhehebu, kutia ndani vikundi vingi vinavyopingana sana. Kinyume chake, kwa kweli Yehova amefanya muujiza kuhusiana na watu wake waliorudishwa. Aliahidi hivi kupitia Ezekieli: “Nitawapa moyo wenye umoja.” Ahadi hiyo imetimizwa kwa njia kubwa sana. (Eze. 11:19) Ulimwenguni kote, Kristo ana mamilioni ya wafuasi kutoka katika jamii, dini, hali za kiuchumi, na utamaduni mbalimbali. Hata hivyo, wote wanafundishwa kweli zilezile na wanafanya kazi ileile kwa upatano kabisa. Usiku wa mwisho wa uhai wake duniani, Yesu alisali kwa bidii kwamba wafuasi wake wawe na umoja. (Soma Yohana 17:11, 20-23.) Katika siku zetu, Yehova ametimiza sala hiyo kwa njia kubwa zaidi.

32. Unahisije kuhusu kutimizwa kwa unabii wa kurudishwa? (Pia, tazama sanduku “Unabii Kuhusu Utekwa na Kurudishwa.”)

32 Inafurahisha sana kuishi katika kipindi hiki chenye kusisimua cha kurudishwa kwa ibada safi, sivyo? Tunaona unabii wa Ezekieli ukitimizwa katika kila sehemu ya ibada yetu leo. Tuna uhakika kwamba sasa Yehova anawapa kibali watu wake kama alivyotabiri kupitia Ezekieli: “Nitafurahishwa nanyi.” (Eze. 20:41) Je, unatambua pendeleo lako la kuwa sehemu ya watu wenye umoja na wanaolishwa vizuri na kumsifu Yehova ulimwenguni pote—watu waliowekwa huru baada ya kuwa katika utekwa wa kiroho kwa karne nyingi? Hata hivyo, baadhi ya unabii wa Ezekieli bado utatimizwa kwa njia kubwa zaidi.

“Kama Bustani ya Edeni”

33-35. (a) Unabii wa Ezekieli 36:35 ulikuwa na maana gani kwa Wayahudi waliokuwa uhamishoni? (b) Unabii huo una maana gani kwa watu wa Yehova leo? (Pia, tazama sanduku “Nyakati za Kurudishwa kwa Mambo Yote.”)

33 Kama tulivyoona, “nyakati za kurudishwa kwa mambo yote” zilianza kwa kurudishwa kwa ufalme wa ukoo wa Daudi, Yesu alipowekwa kuwa mfalme mwaka wa 1914. (Eze. 37:24) Kisha, Yehova akamwezesha Kristo kurudisha ibada safi kati ya watu Wake baada ya karne nyingi za uhamisho wa kiroho. Hata hivyo, je, kazi ya Kristo ya kurudisha iliishia hapo? Hapana! Kazi hiyo itaendelea kwa njia yenye kustaajabisha wakati ujao, na unabii wa Ezekieli unatoa habari nyingi zenye kusisimua.

34 Kwa mfano, fikiria maneno haya yaliyoongozwa na roho: “Watu watasema: ‘Nchi iliyokuwa ukiwa imekuwa kama bustani ya Edeni.’” (Eze. 36:35) Ahadi hiyo ilimaanisha nini kwa Ezekieli na wahamishwa wenzake? Kwa kweli, hawakutazamia kwamba ahadi hiyo ingetimizwa kikamili kwa njia halisi, yaani, nchi iliyorudishwa iwe kama bustani ya mwanzoni, au Paradiso, ambayo ilipandwa na Mungu mwenyewe! (Mwa. 2:8) Badala yake, bila shaka walielewa Yehova alikuwa akiwahakikishia kwamba nchi yao iliyorudishwa ingekuwa maridadi na yenye mazao mengi.

35 Ahadi hiyo ina maana gani kwetu leo? Hatutazamii kwamba itatimizwa kihalisi leo katika ulimwengu huu mwovu unaotawaliwa na Shetani Ibilisi. Badala yake, tunaelewa kwamba leo maneno hayo yanatimizwa kwa njia ya kiroho. Tukiwa watumishi wa Yehova tunakaa katika nchi ya kiroho iliyorudishwa, hali, au mazingira, ambamo tunatumikia kwa bidii na jambo kuu maishani mwetu ni utumishi wake mtakatifu. Nchi hii ya kiroho, inazidi kuwa kama paradiso hatua kwa hatua. Namna gani kuhusu wakati ujao?

36, 37. Ni ahadi gani zitakazotimizwa katika Paradiso wakati ujao?

36 Baada ya vita vya Har–Magedoni, Yesu atafanya kihalisi kazi yake ya kurudisha katika dunia nzima. Wakati wa Utawala Wake wa Miaka Elfu Moja, atawaongoza wanadamu kuibadili dunia kuwa kama bustani ya Edeni, paradiso, kama vile ambavyo sikuzote Yehova amekusudia iwe! (Luka 23:43) Kisha wanadamu wote watakuwa na umoja kati yao wenyewe na pia dunia itakuwa makao salama. Hakutakuwa na hatari, wala vitisho mahali popote. Wazia wakati ambapo ahadi hii itatimizwa: “Nitafanya agano la amani pamoja nao, na kuwaondoa kabisa nchini wanyama hatari wa mwituni, ili wakae kwa usalama nyikani na kulala misituni.”—Eze. 34:25.

37 Je, unaweza kuwazia hali hiyo? Utatembelea sehemu yoyote ya dunia hii kubwa bila kuogopa. Hakuna mnyama atakayekushambulia. Hakuna hatari itakayotishia amani yako. Utatembea peke yako katika msitu mkubwa, ukifurahia umaridadi wake, hata utalala huko ukiwa salama kabisa, ukiwa na hakika kwamba utaamka ukiwa umepumzika vya kutosha bila kushambuliwa!

Wazia wakati ambapo itakuwa salama “kulala misituni” (Tazama fungu la 36, 37)

38. Unahisije kuhusu kuona ahadi iliyo kwenye Ezekieli 28:26 ikitimizwa?

38 Pia, tutaona ahadi hii ikitimizwa: “Wataishi [katika nchi] kwa usalama na watajenga nyumba na kupanda mashamba ya mizabibu na watakaa kwa usalama nitakapotekeleza hukumu dhidi ya wote wanaowazunguka ambao wanawadhihaki; nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova Mungu wao.” (Eze. 28:26) Baada ya adui wote wa Mungu kuondolewa, tutafurahia amani na usalama duniani kote. Tutakapokuwa tukiitunza dunia, tutajitunza sisi wenyewe pia na wapendwa wetu, tutajenga nyumba nzuri na kupanda mashamba ya mizabibu.

39. Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba unabii ulioandikwa na Ezekieli utatimizwa?

39 Je, unaona ahadi hizi kuwa ndoto tu? Basi, kumbuka mambo ambayo tayari umeona katika kipindi hiki cha “kurudishwa kwa mambo yote.” Licha ya upinzani mkali zaidi wa Shetani, Yesu amepewa uwezo wa kurudisha ibada safi katika kipindi hiki kigumu zaidi ulimwenguni. Huo ni uthibitisho wenye nguvu kwamba ahadi zote za Mungu kupitia Ezekieli zitatimia!

^ fu. 2 Wayahudi wengi wahamishwa waliishi katika vijiji vilivyokuwa mbali na jiji la Babiloni. Kwa mfano, Ezekieli aliishi kati ya Wayahudi walioishi kando ya mto Kebari. (Eze. 3:15) Hata hivyo, kuna wahamishwa wachache Wayahudi walioishi jijini. Walitia ndani wale waliotoka katika “uzao wa kifalme na wa watu mashuhuri.”—Dan. 1:3, 6; 2 Fal. 24:15.

^ fu. 25 Kwa mfano, hatuwezi kuthibitisha ni nani kati ya wanaharakati wa karne ya 16 waliokuwa Wakristo watiwa mafuta.