Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 11

“Nimekuweka Kuwa Mlinzi”

“Nimekuweka Kuwa Mlinzi”

EZEKIELI 33:7

WAZO KUU: Yehova amweka mlinzi na kufafanua wajibu wake

1. Fafanua mambo ambayo manabii walinzi waliowekwa na Yehova wamekuwa wakifanya na matukio yanayofuata.

MLINZI anasimama kwenye kuta za Yerusalemu na kukinga macho yake kutokana na jua linalotua. Anatazama kule mbali. Ghafla, anainua tarumbeta yake, anavuta pumzi kwa nguvu na kuipuliza ili kutoa onyo kwamba wanajeshi wa Babiloni wanakuja! Ingawa mlinzi amepiga tarumbeta, tayari wakaaji wa jiji hilo wasiojali wamechelewa kuchukua hatua. Kwa miaka mingi, Yehova amewaweka walinzi, au manabii, ambao wamekuwa wakitoa onyo kwamba siku hiyo itafika; lakini watu hawakusikiliza. Sasa wanajeshi Wababiloni wanalizunguka jiji. Baada ya kulizingira kwa miezi mingi, wanajeshi wanabomoa kuta za jiji na kuingia, wanaliharibu hekalu, kisha wanaua au kuwateka wakaaji wa Yerusalemu wasio na imani na wanaoabudu sanamu.

2, 3. (a) Wakaaji wa dunia wanakabili hali gani leo? (b) Tutachunguza maswali gani?

2 Leo, majeshi ya Yehova yako mwendoni kwenda kupigana na wakaaji wa dunia wasio na imani. (Ufu. 17:12-14) Vita hivyo vitakuwa upeo wa dhiki kuu zaidi katika historia ya wanadamu. (Mt. 24:21) Lakini kuna muda wa kutii onyo linalotolewa na wale waliochaguliwa na Yehova kufanya kazi ya mlinzi.

3 Ni nini kilichomchochea Yehova kuwaweka walinzi? Mlinzi anatangaza ujumbe gani? Ni nani wanaotimiza jukumu hilo, nasi tunatimiza wajibu gani? Acheni tuchunguze majibu ya maswali hayo.

“Lazima Uwape Onyo Langu”

4. Kwa nini Yehova aliwaweka walinzi? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

4 Soma Ezekieli 33:7. Mara nyingi walinzi walisimama kwenye kuta za jiji ili kuwalinda wakaaji wa jiji. Hilo lilithibitisha kwamba mtawala wa jiji aliwajali raia wake. Ingawa mlio wa tarumbeta ya mlinzi ungewaamsha watu wanaolala, mlio huohuo ungeokoa uhai wa wale tu ambao wangetii. Vivyo hivyo, Yehova aliwaweka walinzi, si kwa sababu alitaka kuwatisha Waisraeli kwa ujumbe wa maangamizi, bali kwa sababu aliwajali watu wake na alitaka kuokoa uhai.

5, 6. Haki ya Yehova inaonekana kupitia njia gani?

5 Alipomweka Ezekieli kuwa mlinzi, Yehova alifunua mambo fulani kuhusu utu wake ambayo yanatuimarisha. Acheni tuzungumzie sifa mbili kati ya hizo.

6 Haki: Haki ya Yehova inaonekana kwa sababu anashughulika nasi bila ubaguzi tukiwa mtu mmoja-mmoja. Kwa mfano, ingawa watu wengi sana walisikia ujumbe wa Ezekieli na kuukataa, Yehova hakuwaona Waisraeli wote kuwa kundi la waasi; badala yake, alitaka kuona jinsi mtu mmoja-mmoja atakavyotenda. Mara nyingi anazungumza kuhusu “mtu mwovu” na “mtu mwadilifu.” Kwa hiyo, Yehova hutoa hukumu kulingana na jinsi kila mtu anavyoitikia ujumbe.—Eze. 33:8, 18-20.

7. Yehova anawahukumu watu kwa msingi gani?

7 Haki ya Yehova inaonekana pia kupitia jinsi anavyowahukumu watu. Watu hawahukumiwi kwa kutegemea mambo waliyofanya zamani, bali jinsi wanavyoitikia onyo linalotolewa sasa. Yehova alimwambia hivi Ezekieli: “Ninapomwambia mtu mwovu: ‘Hakika utakufa,’ naye aiache dhambi yake na kutenda mambo ya haki na ya uadilifu, . . . hakika ataendelea kuishi.” Kisha Yehova anasema maneno haya ya kupendeza: “Hataadhibiwa kwa sababu ya dhambi yoyote aliyotenda.” (Eze. 33:14-16) Kwa upande mwingine, wale waliofuata njia ya uadilifu zamani, ikiwa wanaasi sasa hawawezi kutarajia kusamehewa kwa kutegemea mambo waliyofanya wakati huo. Yehova alisema kwamba mtu akiutumaini “uadilifu wake mwenyewe na kutenda kosa, hakuna tendo lolote la uadilifu alilotenda litakalokumbukwa, lakini atakufa kwa sababu ya kosa alilotenda.”—Eze. 33:13.

8. Maonyo ya kinabii yanatufundisha nini kuhusu haki ya Yehova?

8 Haki ya Yehova inaonekana pia kwa kuwa anatoa onyo kabla ya kuchukua hatua. Ezekieli alianza kazi yake miaka sita hivi kabla ya jeshi la Babiloni kuharibu Yerusalemu. Lakini Ezekieli hakuwa wa kwanza kuwaonya watu wa Mungu kwamba watahukumiwa. Zaidi ya karne moja kabla ya Yerusalemu kuharibiwa, Yehova aliwatuma manabii Hosea, Isaya, Mika, Odedi, na Yeremia wawe walinzi. Yehova alimwagiza Yeremia awakumbushe Waisraeli hivi: “[Niliwaweka] walinzi waliosema, ‘Isikilizeni sauti ya pembe!’” (Yer 6:17) Yehova na walinzi hao hawangelaumiwa kwa vifo vilivyotokea Wababilioni walipotekeleza hukumu ya Yehova hatimaye.

9. Yehova alionyeshaje upendo mshikamanifu?

9 Upendo: Yehova alionyesha upendo mshikamanifu kwa kuwatuma walinzi wake wawaonye waadilifu na pia waovu—watu walewale waliomvunja moyo na kuletea suto jina lake. Hebu fikiria—Waisraeli waliitwa watu wa Yehova, lakini walimpa kisogo tena na tena na kufuata miungu ya uwongo! Yehova alionyesha jinsi alivyoumia kihisia walipomsaliti kwa kulinganisha taifa hilo na mke mzinzi. (Eze. 16:32) Hata hivyo, hakukata tamaa upesi. Alitafuta njia ya kuwasamehe, bali si kulipiza kisasi. Alitumia upanga wa hukumu baada ya kujaribu njia nyingine zote. Kwa nini? Alimwambia hivi Ezekieli: “Mimi sifurahishwi na kifo cha mwovu, bali kwamba mtu mwovu abadili njia yake na kuendelea kuishi.” (Eze 33:11) Hivyo ndivyo Yehova alivyohisi wakati huo, na ndivyo Yehova anavyohisi leo.—Mal. 3:6.

10, 11. Tunajifunza somo gani kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na watu wake?

10 Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na Waisraeli kwa njia ya haki na upendo? Somo moja ni kwamba hatupaswi kuwaona watu tunaowahubiria kama kikundi tu, bali kama mtu mmoja-mmoja. Ni kosa kuamua kwamba mtu hastahili kusikia ujumbe wetu kwa sababu ya matendo yake ya zamani au kwa sababu ya jamii, kabila, lugha, au hali yake ya kiuchumi! Yehova alimfundisha mtume Petro somo ambalo linafaa leo: “Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.”—Mdo. 10:34, 35.

Je, tunawaona watu kama Yehova anavyowaona? (Tazama fungu la 10)

11 Somo lingine muhimu ni kwamba tunapaswa kujichunguza kwa makini; matendo yetu ya uadilifu ya zamani si kisingizio cha kutenda makosa sasa. Tunapaswa kukumbuka kwamba tuna mwelekeo wa kutenda dhambi kama tu watu tunaowahubiria. Ushauri ambao mtume Paulo alitoa kwa kutaniko la Korintho unatuhusu sisi pia: “Basi yule anayefikiri amesimama na ajihadhari asije akaanguka. Hakuna majaribu ambayo yamewapata ninyi ila yale yaliyo ya kawaida kwa watu.” (1 Kor. 10:12, 13) Hatupaswi kamwe kuwa kama mtu ‘anayeutumaini uadilifu wake,’ na kufikiri kwamba tukifanya makosa hatutaadhibiwa kwa sababu tunafanya mambo mema pia. (Eze. 33:13) Hata kama tumemtumikia Yehova kwa muda mrefu, ni muhimu tuendelee kuwa wanyenyekevu na watiifu.

12. Ikiwa tulifanya dhambi nzito wakati uliopita, tunapaswa kukumbuka nini?

12 Namna gani ikiwa tulifanya dhambi nzito zamani na sasa tunajuta? Tunajifunza kutokana na ujumbe wa Ezekieli kwamba Yehova atawaadhibu watenda dhambi wasiotubu. Hata hivyo, pia tunajifunza kwamba kimsingi Yehova ni Mungu mwenye upendo, bali si kisasi. (1 Yoh. 4:8) Tukithibitisha kwa matendo yetu kwamba tumetubu, hatupaswi kufikiri Mungu hawezi kutuonyesha rehema kwa sababu ya dhambi zetu. (Yak. 5:14, 15) Yehova alikuwa tayari kuwasamehe Waisraeli waliofanya uzinzi wa kiroho naye yuko tayari kutusamehe.—Zab. 86:5.

“Zungumza na Wana wa Watu Wako”

13, 14. (a) Walinzi walipaswa kutangaza ujumbe gani? (b) Isaya alitangaza ujumbe gani?

13 Soma Ezekieli 33:2, 3Walinzi wa Yehova walipaswa kutangaza ujumbe gani? Sehemu kubwa ya kazi yao ilikuwa kutangaza maonyo. Lakini pia walitangaza habari njema. Fikiria mifano ifuatayo.

14 Isaya, ambaye alitumikia kuanzia karibu mwaka wa 778 hadi 732 K.W.K., alionya kwamba Wababiloni wangeteka Yerusalemu na kuwapeleka wakaaji wake uhamishoni. (Isa. 39:5-7) Lakini pia aliongozwa na roho kuandika hivi: “Sikiliza! Walinzi wako wanapaza sauti. Wanapiga vigelegele kwa shangwe pamoja, kwa maana wataona waziwazi Yehova atakapokusanya Sayuni tena.” (Isa 52:8) Isaya alitangaza habari njema kabisa—ibada ya kweli ingerudishwa!

15. Yeremia alitangaza ujumbe gani?

15 Yeremia, ambaye alitumikia kuanzia mwaka wa 647 hadi mwaka wa 580 K.W.K., mara nyingi anaitwa “mtangazaji wa misiba.” Bila shaka, alifanya kazi nzuri ya kuwaonya Waisraeli waovu kuhusu msiba ambao Yehova angeleta juu yao. * Lakini pia alitangaza habari njema, na kutabiri kwamba watu wa Mungu wangerudi katika nchi yao na ibada safi ingerudishwa huko.—Yer. 29:10-14; 33:10, 11.

16. Ujumbe wa Ezekieli uliwanufaishaje mateka huko Babiloni?

16 Ezekieli aliwekwa kuwa mlinzi mwaka wa 613 K.W.K., na aliendelea kufanya kazi hiyo mpaka mwaka wa 591 K.W.K. Kama ilivyozungumziwa katika Sura ya 5 na 6 ya kitabu hiki, Ezekieli aliwaonya Waisraeli kwa bidii kuhusu uharibifu ambao ungewapata, na hivyo kujiondolea hatia ya damu ya watu ambao wangekufa. Kwa kufanya hivyo, aliwaonya wahamishwa kwamba Yehova angewaadhibu waasi imani huko Yerusalemu na pia aliwasaidia mateka huko Babiloni waendelee kuwa na hali nzuri kiroho na kuwa tayari kwa kazi wakati ujao. Baada ya kuwa uhamishoni kwa miaka 70, Yehova angewarudisha katika nchi ya Israeli watu wachache waliobaki. (Eze. 36:7-11) Watu hao hasa wangekuwa watoto na wajukuu wa watu waliosikiliza ujumbe wa Ezekieli. Kama sura nyingine katika Sehemu ya 3 ya kitabu hiki zinavyoonyesha, Ezekieli alitangaza habari nyingi njema, na kuthibitisha kwamba ibada safi ingerudishwa Yerusalemu.

17. Yehova amekuwa akiwaweka walinzi wakati gani?

17 Je, manabii hao waliozungumza na watu wa Mungu karibu na kipindi cha kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. ndio tu ambao Yehova amewatumia kama walinzi? Jibu ni hapana. Katika kila kipindi muhimu cha kutimizwa kwa kusudi lake, Yehova amewaweka walinzi ili wawaonye waovu na kutangaza habari njema.

Walinzi Katika Karne ya Kwanza

18. Yohana Mbatizaji alifanya kazi gani?

18 Katika karne ya kwanza W.K., Yohana Mbatizaji alifanya kazi ya mlinzi. Aliwaonya Waisraeli wa asili kwamba baada ya muda mfupi wangekataliwa. (Mt. 3:1, 2, 9-11) Lakini alifanya mengi zaidi. Yesu alisema kwamba Yohana alikuwa “mjumbe” aliyetabiriwa ambaye alimtayarishia Masihi njia. (Mal. 3:1; Mt. 11:7-10) Kazi hiyo ilihusisha kutangaza habari njema kwamba Yesu, “Mwanakondoo wa Mungu,” alikuwa amewasili na angeondoa “dhambi ya ulimwengu.”—Yoh. 1:29, 30.

19, 20. Yesu na wanafunzi wake walitendaje kama walinzi?

19 Yesu alikuwa mlinzi mkuu kati ya walinzi wote. Kama Ezekieli, alitumwa na Yehova kwa “nyumba ya Israeli.” (Eze. 3:17; Mt. 15:24) Yesu alionya taifa la asili la Israeli kwamba hivi karibuni lingekataliwa na kwamba Yerusalemu lingeharibiwa. (Mt. 23:37, 38; 24:1, 2; Luka 21:20-24) Lakini kazi yake kuu ilikuwa kutangaza habari njema.—Luka 4:17-21.

20 Alipokuwa duniani, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi kihususa: “Endeleeni kukesha.” (Mt. 24:42) Walitii amri yake na kuwa walinzi, wakitangaza kwamba Yehova alikuwa amekataa taifa la asili la Israeli na jiji la kidunia la Yerusalemu. (Rom. 9:6-8; Gal. 4:25, 26) Kama walinzi waliowatangulia, wao pia walitangaza habari njema. Ujumbe wao ulitia ndani tangazo muhimu kwamba sasa Watu wa Mataifa wangekuwa sehemu ya Israeli wa Mungu waliotiwa mafuta kwa roho na wangefurahia pendeleo la kumsaidia Kristo kurudisha ibada safi duniani.—Mdo. 15:14; Gal. 6:15, 16; Ufu. 5:9, 10.

21. Paulo aliweka mfano gani?

21 Mtume Paulo aliweka mfano mzuri sana kati ya walinzi wa karne ya kwanza. Alichukua mgawo wake kwa uzito. Kama Ezekieli, alijua kwamba angekuwa na hatia ya damu ikiwa angekosa kutimiza mgawo wake. (Mdo. 20:26, 27) Kwa kufuata mfano wa walinzi wengine, mbali na kuwaonya watu, Paulo alitangaza pia habari njema. (Mdo. 15:35; Rom. 1:1-4) Kwa kweli, akiongozwa na roho takatifu, alinukuu unabii ulioandikwa na Isaya: “Jinsi inavyopendeza miguu ya wale wanaotangaza habari njema,” na aliuhusianisha unabii huo na kazi iliyofanywa na wafuasi wa Kristo walipohubiri kuhusu Ufalme wa Mungu.—Isa. 52:7, 8; Rom. 10:13-15.

22. Ni nini kilichotokea baada ya mitume kufa?

22 Baada ya mitume kufa, uasi imani uliotabiriwa ulitokea kwa kiwango kikubwa katika kutaniko la Kikristo. (Mdo. 20:29, 30; 2 The. 2:3-8) Katika kipindi kirefu cha ukuzi, Wakristo wa uwongo wanaofananishwa na magugu walikuwa wengi kuliko wafuasi wa Kristo waliofananishwa na ngano, na ujumbe ulio wazi kuhusu Ufalme wa Mungu ukafunikwa na mafundisho ya uwongo. (Mt. 13:36-43) Hata hivyo, wakati wa Yehova kuingilia kati ulipokaribia, alionyesha tena upendo na haki yake kwa kuweka wachungaji ili watoe onyo lililo wazi na kutangaza habari njema. Walinzi hao walikuwa nani?

Yehova Aweka Tena Walinzi Ili Kuwaonya Waovu

23. C. T. Russell na wenzake walitimiza jukumu gani?

23 Miaka iliyotangulia mwaka wa 1914, Charles Taze Russell na wenzake walitenda kama “mjumbe” ambaye ‘angefungua njia’ kabla Ufalme wa Kimasihi haujaanza kutawala. * (Mal. 3:1) Kikundi hicho pia kilifanya kazi ya mlinzi, kwa kutumia gazeti la Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence (Mnara wa Mlinzi wa Sayuni Unaotangaza Kuwapo kwa Kristo) ili kutoa onyo kuhusu hukumu ya Mungu na kutangaza habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu.

24. (a) Mtumwa mwaminifu ametendaje kama mlinzi? (b) Umejifunza nini kutokana na mfano wa walinzi wa zamani? (Tazama chati “Baadhi ya Walinzi Walioweka Mfano Mzuri.”)

24 Baada ya Ufalme kuanzishwa, Yesu alichagua kikundi kidogo cha wanaume ili watumikie wakiwa mtumwa mwaminifu. (Mt. 24:45-47) Tangu wakati huo, mtumwa mwaminifu, ambaye sasa anajulikana kuwa Baraza Linaloongoza, amefanya kazi ya mlinzi. Anaongoza katika kuonya kuhusu “siku ya kisasi” na pia kutangaza “mwaka wa nia njema ya Yehova.”—Isa. 61:2; ona pia 2 Wakorintho 6:1, 2.

25, 26. (a) Wafuasi wote wa Kristo wanapaswa kufanya kazi gani, nayo inafanywaje? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?

25 Ingawa mtumwa mwaminifu anaongoza katika kazi ya mlinzi, Yesu aliwaagiza wafuasi wake ‘wote waendelee kukesha.’ (Marko 13:33-37) Tunatii amri hiyo kwa kuendelea kuwa macho kiroho, tukimuunga mkono kwa ushikamanifu mlinzi wa siku hizi. Tunathibitisha kwamba tuko macho kwa kutimiza jukumu letu la kuhubiri. (2 Tim. 4:2) Ni nini kinachotuchochea? Sababu moja ni kwamba tunatamani kuokoa uhai. (1 Tim. 4:16) Hivi karibuni watu wengi sana watapoteza uhai wao kwa sababu ya kupuuza onyo la mlinzi wa siku zetu. (Eze. 3:19) Lakini lengo letu kuu ni kutangaza habari nzuri sana kwamba ibada safi imerudishwa! Hivi sasa, katika “mwaka wa nia njema ya Yehova,” mlango uko wazi ili watu wengi wajiunge nasi kumwabudu Yehova, Mungu wetu mwenye upendo na haki. Hivi karibuni watu wote duniani ambao wataokoka mwisho wa mfumo huu watanufaika na utawala wenye rehema wa Mwana wake, Yesu Kristo. Tunajitahidi kabisa kumuunga mkono mlinzi wa siku zetu kuwatangazia wengine habari hizo njema!—Mt. 24:14.

Tunamuunga mkono mlinzi wa siku zetu kwa kuhubiri habari njema (Tazama fungu la 25)

26 Hata kabla ya mfumo huu mwovu kwisha, tayari Yehova amewaunganisha watu wake kimuujiza. Sura inayofuata itazungumzia unabii unaohusu vijiti viwili vinavyotumiwa kuonyesha jinsi ambavyo jambo hilo limefanyika.

^ fu. 15 Neno “msiba” linapatikana zaidi ya mara 60 katika kitabu cha Yeremia.

^ fu. 23 Ili upate habari zaidi kuhusu unabii huu na jinsi ulivyotimia, tazama kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala!, sura ya 2, “Ufalme Unazaliwa Mbinguni.”