Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 14

“Hii Ndiyo Sheria ya Hekalu”

“Hii Ndiyo Sheria ya Hekalu”

EZEKIELI 43:12

WAZO KUU: Maono ya hekalu—masomo muhimu kwa ajili ya watu wa siku za Ezekieli na jinsi yanavyotuhusu leo

1, 2. (a) Tulijifunza nini kuhusu hekalu aliloona Ezekieli katika sura iliyotangulia? (b) Tutazungumzia maswali gani mawili katika sura hii?

HEKALU ambalo Ezekieli aliona halikuwa hekalu kubwa la kiroho ambalo mtume Paulo alilizungumzia karne nyingi baadaye. Tulijifunza jambo hilo katika sura iliyotangulia. Pia, tulijifunza kwamba maono hayo yalikusudiwa kuwafundisha watu wa Mungu umuhimu wa viwango vya Mungu kuhusu ibada safi. Watu wangefurahia uhusiano mpya pamoja na Yehova ikiwa tu wangefuata viwango hivyo. Basi tunaona ni kwa nini Yehova alikazia mara mbili wazo hili kuu katika mstari mmoja: “Hii ndiyo sheria ya hekalu.”—Soma Ezekieli 43:12.

2 Sasa tunahitaji kuchunguza maswali mengine mawili. Kwanza: Ni masomo gani hususa kuhusu viwango vya Yehova vya ibada safi ambayo huenda Wayahudi wa siku za Ezekieli walijifunza kutokana na maono hayo ya hekalu? Jibu la swali hilo litatusaidia kujibu swali la pili: Maono hayo yana maana gani kwetu katika siku hizi za mwisho zenye taabu?

Walijifunza Masomo Gani Kutokana na Maono Hayo Nyakati za Kale?

3. Kwa nini hekalu hilo lililo juu ya mlima mrefu lingewafanya watu waaibike?

3 Ili kujibu swali la kwanza acheni tuzungumzie mambo kadhaa ya pekee kuhusu maono ya hekalu. Mlima mrefu. Huenda watu walihusianisha mahali palipozungumziwa katika maono ya Ezekieli na unabii wa Isaya wenye kugusa moyo kuhusu kurudishwa. (Isa. 2:2) Lakini walijifunza nini walipoona nyumba ya Yehova juu ya mlima huo mrefu? Walijifunza kwamba ibada safi inapaswa kukwezwa, kuinuliwa, na kuwekwa juu ya kila kitu. Bila shaka, ni wazi kwamba ibada safi imekwezwa, kwa maana ni mpango unaotoka kwa Yule ambaye amekwezwa “juu zaidi ya miungu mingine yote.” (Zab. 97:9) Lakini watu hawakuwa wakitimiza sehemu yao. Kwa karne nyingi, walikuwa wameacha ibada safi ipotoshwe, ipuuzwe, na kuchafuliwa. Bila shaka, watu wenye mioyo minyoofu waliaibika walipoona nyumba takatifu ya Mungu ikiwa imekwezwa, na kuinuliwa mahali panapostahili penye utukufu na fahari.

4, 5. Huenda watu waliomsikiliza Ezekieli walijifunza somo gani kutokana na malango marefu ya hekalu?

4 Malango marefu. Mwanzoni mwa maono hayo, Ezekieli alimtazama malaika akipima malango. Malango hayo yalikuwa na urefu wa karibu mita 30! (Eze. 40:14) Kulikuwa na vyumba vya walinzi ndani ya malango hayo. Hilo lilimaanisha nini kwa wale waliochunguza ramani hiyo? Yehova alimwambia Ezekieli: “Tazama kwa makini sana njia ya kuingia hekaluni.” Kwa nini? Kwa sababu watu walikuwa wakiwaingiza wale “ambao hawajatahiriwa moyoni na mwilini” ndani ya nyumba takatifu ya ibada ya Mungu. Matokeo yalikuwa nini? Yehova alisema: “Wanalitia unajisi hekalu langu.”—Eze. 44:5, 7.

5 Wale “ambao hawajatahiriwa . . . mwilini” walikosa kutii agizo lililo wazi kutoka kwa Mungu la tangu siku za Abrahamu. (Mwa. 17:9, 10; Law. 12:1-3) Lakini wale “ambao hawajatahiriwa moyoni” walikuwa na tatizo kubwa zaidi. Walikuwa waasi wenye vichwa vigumu, ambao hawakutii mwongozo na maagizo ya Yehova. Watu hao hawakupaswa kuruhusiwa kuingia katika nyumba takatifu ya ibada ya Yehova! Yehova anachukia unafiki, lakini watu wake waliruhusu unafiki usitawi katika nyumba yake. Malango na vyumba vya walinzi katika maono ya hekalu yaliwafundisha waziwazi somo hili: Uovu huo ungekomeshwa! Viwango vya juu vya kuingia katika nyumba ya Mungu vilipaswa kudumishwa. Ikiwa watu wangefanya hivyo, Yehova angebariki ibada yao.

6, 7. (a) Yehova anatumiaje ukuta unaozunguka majengo ya hekalu kuwatangazia watu wake ujumbe? (b) Mwanzoni watu wa Yehova walikuwa wameitendeaje nyumba yake? (Tazama maelezo ya chini.)

6 Ukuta uliozunguka hekalu. Jambo lingine la pekee kuhusu maono hayo ya hekalu ni ukuta uliozunguka eneo lote la hekalu. Ezekieli anasema kwamba kila upande ukuta ulikuwa na urefu wa tete 500, au mita 1,555, karibu kilomita 1.6! (Eze. 42:15-20) Hata hivyo, majengo ya hekalu na nyua zake zilifanyiza mraba uliokuwa na urefu wa mikono 500, au mita 259 kila upande. Basi kulikuwa na eneo pana kuzunguka hekalu, na lilizingirwa kwa ukuta. * Kwa kusudi gani?

7 Yehova alisema: “Basi sasa na wauweke mbali nami ukahaba wao wa kiroho na maiti za wafalme wao, nami nitakaa miongoni mwao milele.” (Eze. 43:9) Huenda “maiti za wafalme wao” zilimaanisha ibada ya sanamu. Basi Yehova alitumia ukuta huo wa maono ya Ezekieli kusema hivi kwa njia ya mfano: “Ondoeni kabisa uchafu huo wote. Hata msiulete karibu.” Ikiwa wangedumisha ibada yao ikiwa safi, Yehova angewabariki kwa kuwapo kwake.

8, 9. Huenda watu walijifunza nini kutokana na ushauri mzito ambao Yehova aliwapa wanaume wenye majukumu?

8 Shauri zito kwa wanaume wenye majukumu. Yehova pia aliwapa shauri zito na lenye upendo wanaume waliokuwa na majukumu makubwa kati ya watu wake. Aliwarekebisha kwa uthabiti Walawi waliomwacha Yehova watu walipoanza kuabudu sanamu, lakini akawapongeza wana wa Sadoki, ‘walioshughulikia majukumu ya mahali pake patakatifu Waisraeli walipomwacha.’ Alishughulika na kila kikundi kwa haki na rehema, kulingana na matendo yao. (Eze. 44:10, 12-16) Vilevile, wakuu wa Waisraeli walirekebishwa kwa uthabiti.—Eze. 45:9.

9 Hivyo, Yehova akaonyesha waziwazi kwamba wanaume wenye mamlaka na wanaosimamia waliwajibika kwake kwa jinsi walivyotimiza majukumu yao. Wao pia walihitaji kushauriwa, kurekebishwa, na kutiwa nidhamu. Walipaswa kuongoza katika kufuata viwango vya Yehova!

10, 11. Ni uthibitisho gani unaoonyesha kwamba baadhi ya wahamishwa waliorudi walijifunza masomo kutokana na maono ya Ezekieli?

10 Je, wahamishwa waliorudi walitumia masomo ya maono ya Ezekieli? Bila shaka, hatuwezi kujua wanaume na wanawake waaminifu wa wakati huo walikuwa wakifikiria nini kuhusu maono hayo yenye kustaajabisha. Hata hivyo, Neno la Mungu linatuambia mengi kuhusu mambo ambayo wahamishwa waliorudi walifanya na jinsi walivyoiona ibada safi ya Yehova. Je, walitumia kanuni zilizo katika maono ya Ezekieli? Walifanya hivyo kwa kadiri fulani—hasa ukiwalinganisha na mababu zao walioasi kabla ya kupelekwa uhamishoni Babiloni.

11 Wanaume waaminifu kama vile nabii Hagai na Zekaria, kuhani na mwandishi Ezra, na gavana Nehemia walijitahidi sana kuwafundisha watu kanuni kama zile zilizo katika maono ya hekalu la Ezekieli. (Ezra 5:1, 2) Waliwafundisha watu kwamba ibada safi inapaswa kukwezwa na inapaswa kutangulizwa badala ya mahangaiko ya kimwili na miradi ya kibinafsi. (Hag. 1:3, 4) Walisisitiza kwamba viwango vinavyohusu ibada safi vinapaswa kufuatwa. Kwa mfano, Ezra na Nehemia waliwashauri kwa uthabiti watu wawafukuze wake zao wa kigeni waliokuwa wakiwadhoofisha watu kiroho. (Soma Ezra 10:10, 11; Neh. 13:23-27, 30) Namna gani kuhusu ibada ya sanamu? Inaonekana baada ya kutoka uhamishoni, mwishowe taifa hilo lilichukia dhambi hiyo, ambayo ilikuwa imewanasa mara nyingi katika historia yao. Namna gani makuhani na wakuu? Kama maono ya Ezekieli yalivyoonyesha, walikuwa kati ya wale walioshauriwa na kurekebishwa na Yehova. (Neh. 13:22, 28) Wengi walitii ushauri huo kwa unyenyekevu.—Ezra 10:7-9, 12-14; Neh. 9:1-3, 38.

Nehemia aliwafundisha watu kuhusu ibada safi alipokuwa akifanya kazi pamoja nao (Tazama fungu la 11)

12. Yehova aliwabariki jinsi gani wahamishwa baada ya kurudi?

12 Kwa sababu hiyo, Yehova aliwabariki watu wake. Nchi hiyo ilisitawi kiroho, watu walifurahia hali nzuri ya kiroho na utaratibu ambao hawakuwa nao kwa muda mrefu. (Ezra 6:19-22; Neh. 8:9-12; 12:27-30, 43) Kwa nini? Kwa sababu hatimaye watu walianza kufuata viwango vya uadilifu vya Yehova kuhusu ibada safi. Watu wengi wenye mioyo minyoofu walijifunza masomo kutokana na maono ya hekalu. Kwa ufupi, tunaona kwamba maono ya Ezekieli yaliwanufaisha wahamishwa kwa njia mbili muhimu. (1) Yaliwafundisha masomo muhimu kuhusu viwango vya ibada safi na jinsi wanavyopaswa kufuata viwango hivyo. (2) Yalitoa uhakikisho wa kinabii. Yalitabiri kwamba ibada safi ingerudishwa, na pia jinsi ambavyo Yehova angewabariki watu wake ikiwa wangekuwa na ibada safi. Hata hivyo, leo tungependa kujua: Je, maono hayo yanatimizwa siku zetu?

Maono ya Ezekieli Yanatufundisha Nini Leo?

13, 14. (a) Tunajuaje kwamba maono ya hekalu aliloona Ezekieli yanatimizwa katika siku zetu? (b) Tunafaidika kwa njia gani mbili na maono hayo leo? (Tazama sanduku 13A, “Mahekalu Tofauti, Masomo Tofauti.”)

13 Je, tunaweza kuwa na uhakika kwamba hekalu aliloona Ezekieli linatuhusu leo? Ndiyo! Kumbuka uhusiano kati ya maono ya Ezekieli kuhusu nyumba takatifu ya Mungu juu ya “mlima mrefu sana” na unabii wa Isaya kwamba “mlima wa nyumba ya Yehova” ungeimarishwa “kabisa juu ya vilele vya milima.” Isaya alisema kihususa kwamba unabii wake ungetimizwa “siku za mwisho,” au “katika kipindi cha mwisho cha zile siku.” (Eze. 40:2; Isa. 2:2-4; maelezo ya chini; tazama pia Mika 4:1-4.) Unabii huo unahusu kipindi cha siku za mwisho tangu 1919 ibada safi ilipoinuliwa, na kurudishwa, kana kwamba imewekwa juu ya mlima mrefu sana. *

14 Basi ni wazi kabisa kwamba maono ya Ezekieli yanahusiana na ibada safi leo. Kama maono hayo yalivyowanufaisha wahamishwa Wayahudi nyakati za kale, yanatunufaisha leo kwa njia mbili. (1) Tunapata masomo muhimu kuhusu jinsi ya kufuata viwango vya Yehova katika ibada safi. (2) Tunapata uhakikisho wa kinabii kuhusu kurudishwa kwa ibada safi na baraka za Yehova.

Viwango vya Ibada Safi Leo

15. Tunapaswa kukumbuka nini tunapojifunza masomo kutokana na hekalu aliloona Ezekieli?

15 Acheni sasa tuchunguze mambo hususa katika maono ya Ezekieli. Wazia kwamba unatembea pamoja na Ezekieli katika hekalu kubwa aliloona kwenye maono. Kumbuka kwamba hatuoni hekalu kubwa la kiroho; badala yake tunapata masomo tunayoweza kutumia katika ibada leo. Tunajifunza masomo gani?

16. Tunajifunza nini kutokana na vipimo vingi katika maono ya Ezekieli? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

16 Kwa nini kuna vipimo vingi? Huku Ezekieli akitazama, malaika aliyeonekana kama shaba anapima hekalu kwa makini, kutia ndani kuta, malango, vyumba vya walinzi, nyua, na madhabahu. Msomaji anaweza kulemewa na habari nyingi zinazotajwa. (Eze. 40:1–42:20; 43:13, 14) Hata hivyo, fikiria mambo muhimu tunayoweza kupata kutokana na habari hizo. Kwa njia hiyo, Yehova anasisitiza kwa mkazo umuhimu wa viwango vyake. Yeye ndiye anayeviweka, si wanadamu. Wale wanaosema kwamba ni sawa kumwabudu Yehova kwa njia yoyote wamekosea sana. Isitoshe, kwa kupima hekalu kwa makini, Yehova anatoa uhakikisho kwamba kurudishwa kwa ibada safi ni jambo hakika kabisa. Kutimizwa kikamili kwa ahadi ya Mungu ni hakika kama vipimo hivyo. Basi Ezekieli anathibitisha kwamba kurudishwa kwa ibada safi katika siku za mwisho ni jambo hakika!

Unajifunza nini kutokana na vipimo hususa vya hekalu? (Tazama fungu la 16)

17. Ukuta unaozunguka hekalu unatukumbusha nini leo?

17 Ukuta unaozunguka hekalu. Kama tulivyozungumzia, eneo lote la hekalu ambalo Ezekieli aliona lilikuwa limezungukwa na ukuta. Ukuta huo uliwakumbusha watu wa Mungu kwamba walipaswa kuondolea mbali uchafu wote wa kidini kutoka kwenye ibada safi, na kutochafua kamwe nyumba ya Mungu. (Soma Ezekieli 43:7-9.) Sisi pia tunahitaji ushauri huo leo! Baada ya watu wa Mungu kuwekwa huru kutoka utekwa wa kiroho wa karne nyingi katika Babiloni Mkubwa, Kristo alimweka mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara mwaka wa 1919. Tangu wakati huo, watu wa Mungu wamejitahidi kuondoa mafundisho ya uwongo na matendo yanayohusiana na ibada ya sanamu na upagani. Tunajitahidi kuondolea mbali uchafu wa kiroho kutoka kwenye ibada safi. Isitoshe, hata hatufanyi biashara katika Majumba yetu ya Ufalme, na hivyo hatuhusishi kamwe mambo hayo ya kawaida katika ibada yetu.—Marko 11:15, 16.

18, 19. (a) Tunajifunza nini kutokana na malango marefu ya hekalu? (b) Tunapaswa kutendaje tunapokabili watu wanaotaka kulegeza viwango vya juu vya Yehova? Toa mfano.

18 Malango marefu. Tunapofikiria malango marefu ambayo Ezekieli aliona, tunajifunza somo gani? Bila shaka, malango hayo yaliwafundisha wahamishwa Wayahudi kwamba Yehova ana viwango vya juu sana vya maadili. Kama ilikuwa hivyo zamani, namna gani leo? Tunaabudu katika hekalu kubwa la kiroho la Yehova. Je, si jambo muhimu hata zaidi kuwa na mwenendo safi usio na unafiki leo? (Rom. 12:9; 1 Pet. 1:14, 15) Katika siku za mwisho Yehova amewaongoza watu wake hatua kwa hatua wafuate kwa ukaribu viwango vyake vya maadili. * Kwa mfano, watenda dhambi wasiotubu huondolewa kutanikoni. (1 Kor. 5:11-13) Isitoshe, vyumba vya walinzi katika malango hayo vinatukumbusha leo kwamba inapohusu kumwabudu Yehova, mtu ambaye hana kibali cha Mungu haruhusiwi kuingia. Kwa mfano, mtu anayefanya dhambi kisiri anaweza kuingia kwenye Jumba la Ufalme, lakini hawezi kupata kibali cha Yehova hadi afanye mambo ambayo Mungu anataka. (Yak. 4:8) Huo ni ulinzi mkubwa wa ibada safi katika nyakati hizi zilizopotoka kimaadili!

19 Biblia ilitabiri kwamba kabla ya mwisho kufika ulimwengu huu ungekuwa umepotoka. Tunasoma hivi: “Watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa.” (2 Tim. 3:13) Watu wengi wanazidi kupotoshwa waamini kwamba viwango vya juu vya Yehova vinabana sana, vimepitwa na wakati, au havifai. Je, utapotoshwa? Kwa mfano, mtu fulani akijaribu kukushawishi uamini kwamba viwango vya Yehova kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja havifai, je, utakubaliana naye? Au, je utakubaliana na Yehova Mungu, ambaye Neno lake linasema waziwazi kwamba wale wanaofanya mambo hayo wanatenda “mambo machafu”? Mungu anatuonya kwamba tusikubaliane na mwenendo mpotovu. (Rom. 1:24-27, 32) Tunapokabiliana na masuala kama hayo, tunapaswa kufikiria kuhusu hekalu aliloona Ezekieli lenye malango marefu na kukumbuka: Yehova halegezi viwango vyake vya uadilifu licha ya mkazo kutoka kwa ulimwengu mwovu. Je, tunakubaliana na Baba yetu wa mbinguni na kutetea mambo yanayofaa?

Tunatoa “dhabihu ya sifa” tunaposhiriki katika ibada safi

20. “Umati mkubwa” unatiwa moyo na vikumbusho gani katika maono ya Ezekieli?

20 Nyua. Ezekieli alipoona ua mkubwa wa nje wa hekalu, bila shaka alifurahi alipofikiria jinsi ambavyo waabudu wengi wenye furaha wa Yehova wangekusanyika hapo. Leo, Wakristo wanaabudu wakiwa katika sehemu takatifu zaidi. Watu wanaofanyiza “umati mkubwa” wa wale wanaoabudu katika ua wa nje wa hekalu la kiroho la Yehova wanakumbushwa mambo yenye kutia moyo na maono ya Ezekieli. (Ufu. 7:9, 10, 14, 15) Ezekieli aliona kwamba nyua zilikuwa na safu za vyumba vya kulia chakula ambamo waabudu wangekula dhabihu za ushirika walizoleta. (Eze. 40:17) Kwa njia fulani, wangefurahia mlo pamoja na Yehova Mungu—ishara ya urafiki na amani! Leo, hatutoi dhabihu kama Wayahudi walivyofanya chini ya Sheria ya Musa. Badala yake, tunatoa “dhabihu ya sifa” tunaposhiriki katika ibada safi, kwa mfano kwa kutoa maelezo na kusema maneno yanayochochewa na imani kwenye mikutano yetu au katika utumishi wa shambani. (Ebr. 13:15) Tunanufaika pia na chakula cha kiroho ambacho Yehova anaandaa. Basi tunahisi kama wana wa Kora waliomwimbia hivi Yehova: “Siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu moja kwingineko!”—Zab. 84:10.

21. Watiwa mafuta wanajifunza nini kutokana na ukuhani katika maono ya Ezekieli?

21 Ukuhani. Ezekieli aliona kwamba makuhani na Walawi wangeingia kwenye ua wa ndani kupitia malango yaliyofanana na malango ambayo watu wa makabila yasiyo ya kikuhani wangepitia walipoingia kwenye ua wa nje. Hiyo ilikuwa njia nzuri ya kuwakumbusha makuhani hao kwamba wao pia walipaswa kufuata viwango vya Yehova kuhusu ibada safi. Namna gani leo? Hakuna mpango wa kurithi ukuhani kati ya watumishi wa Mungu leo, lakini Wakristo watiwa mafuta wanaambiwa hivi: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme.’” (1 Pet. 2:9) Makuhani katika Israeli la kale waliabudu katika ua tofauti. Leo, Wakristo watiwa mafuta hawajatenganishwa na waabudu wenzao kihalisi, lakini wanafurahia uhusiano wa pekee pamoja na Yehova wakiwa wamefanywa kuwa watoto wake. (Gal. 4:4-6) Wakati huohuo, watiwa mafuta wanaweza kupata vikumbusho muhimu katika maono ya Ezekieli. Wanatambua kwamba makuhani pia walihitaji kushauriwa na kutiwa nidhamu. Wakristo wote wanapaswa kukumbuka kwamba sisi ni “kundi moja” linalotumikia chini ya “mchungaji mmoja.”—Soma Yohana 10:16.

22, 23. (a) Wazee Wakristo leo wanajifunza somo gani kutokana na mkuu anayefafanuliwa katika maono ya Ezekieli? (b) Huenda jambo gani likatokea wakati ujao?

22 Mkuu. Katika maono ya Ezekieli, mkuu anaheshimiwa sana. Yeye si wa kabila la kikuhani, na akiwa hekaluni, angefuata mwongozo wa makuhani. Hata hivyo, ni wazi kwamba anatumikia kama msimamizi kati ya watu na anawasaidia kutoa dhabihu. (Eze. 44:2, 3; 45:16, 17; 46:2) Basi anawawekea mfano mzuri wanaume Wakristo leo ambao wanatimiza majukumu mbalimbali kutanikoni. Kwa kweli, wazee Wakristo, kutia ndani waangalizi wanaosafiri wanahitaji kujitiisha chini ya mtumwa mwaminifu aliyetiwa mafuta. (Ebr. 13:17) Wazee hujitahidi sana kuwasaidia watu wa Mungu watoe dhabihu za sifa katika mikutano ya Kikristo na katika huduma. (Efe. 4:11, 12) Na pia wazee wanakumbuka kwamba Yehova aliwakemea wakuu Waisraeli walipotumia mamlaka yao vibaya. (Eze. 45:9) Vivyo hivyo, wazee hawapaswi kufikiria kwamba hawahitaji kushauriwa na kurekebishwa. Badala yake, wanathamini nafasi yoyote ya kurekebishwa na Yehova ili wawe wachungaji na waangalizi wazuri zaidi.—Soma 1 Petro 5:1-3.

23 Yehova ataendelea kuandaa waangalizi wenye uwezo na wenye upendo katika Paradiso duniani wakati ujao. Leo, wazee wengi wanazoezwa ili wawe wachungaji wenye uwezo watakaotoa msaada katika Paradiso. (Zab. 45:16) Je, haifurahishi kufikiria jinsi wanaume hao watakavyokuwa baraka katika ulimwengu mpya? Kama unabii mwingine wa kurudishwa, huenda uelewaji wetu kuhusu maono ya Ezekieli utakuwa wazi zaidi muda wa Yehova wa kuyafunua utakapofika. Labda mambo fulani yatatimizwa kwa njia ya kustaajabisha wakati ujao, utimizo ambao hatuwezi kamwe kuuelewa sasa. Tutajua wakati ujao.

Tunajifunza nini kuhusu ibada yetu kutokana na malango marefu na nyua? (Tazama fungu la 18-21)

Yehova Abariki Ibada Safi

24, 25. Maono ya Ezekieli yalionyeshaje baraka za Yehova juu ya watu wake wanaposhikamana na ibada safi?

24 Kwa kumalizia, acheni tujikumbushe tukio kubwa linalotokea katika maono ya Ezekieli. Yehova anakuja katika hekalu hilo, na anawaahidi watu wake kwamba atabaki hapo ikiwa wataendelea kufuata kwa uaminifu viwango vyake vya ibada safi. (Eze. 43:4-9) Kuwapo kwa Yehova kutakuwa na matokeo gani kwa watu wake na nchi yao?

25 Maono hayo yanafafanua baraka za Mungu kwa kutumia mambo mawili ya kinabii: (1) Mto unatiririka kutoka patakatifu pa hekalu na kuleta uhai na rutuba katika nchi; na (2) nchi inagawanywa kwa mpangilio na kwa vipimo kamili, hekalu likiwa katikati pamoja na eneo linalolizunguka. Tunaelewaje masimulizi hayo leo? Leo tunaishi katika kipindi ambacho Yehova ameingia na kulisafisha hekalu kubwa la kiroho, na kukubali mpango huo wa ibada takatifu. (Mal. 3:1-4) Tutazungumzia mambo hayo mawili ya kinabii katika Sura ya 19 hadi 21 ya kitabu hiki.

^ fu. 6 Yehova alikuwa akionyesha tofauti ya jinsi watu wake walivyokuwa wameitendea nyumba yake takatifu hapo zamani: “Kwa kuweka kizingiti chao kando ya kizingiti changu na mwimo wa mlango wao kando ya mwimo wa mlango wangu, kukiwa na ukuta tu kati yangu nao, walilichafua jina langu takatifu kwa mambo yanayochukiza waliyotenda.” (Eze. 43:8) Katika Yerusalemu la kale, hekalu la Yehova na nyumba za watu zilitenganishwa tu na ukuta. Watu walipoacha kufuata viwango vya Yehova vya uadilifu, walileta uchafu wao, sanamu zao, karibu sana na nyumba ya Yehova. Yehova hangevumilia hali hiyo!

^ fu. 13 Hekalu aliloona Ezekieli pia linapatana na unabii mwingine wa kurudishwa ambao umetimizwa katika siku za mwisho. Kwa mfano ona ulinganifu kati ya Ezekieli 43:1-9 na Malaki 3:1-5; Ezekieli 47:1-12 na Yoeli 3:18.

^ fu. 18 Hekalu la kiroho lilianzishwa mwaka wa 29 W.K. Yesu alipobatizwa na kuanza kazi yake akiwa Kuhani Mkuu. Hata hivyo, kwa karne nyingi ibada safi duniani ilipuuzwa kwa kiwango kikubwa baada ya mitume wa Yesu kufa. Ibada safi imeinuliwa juu hasa tangu mwaka wa 1919.