Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 10

“Mtakuwa Hai”

“Mtakuwa Hai”

EZEKIELI 37:5

WAZO KUU: Maono ya “mifupa mikavu” inayokuwa hai tena na utimizo wake mkubwa

1-3. Ni nini kinachofanya hisia za Wayahudi walio Babiloni zibadilike? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

HISIA za Wayahudi walio Babiloni zimebadilika! Kwa miaka mitano hivi, Ezekieli alikuwa amevunja matumaini yao ya uwongo, lakini jitihada zake hazikufanikiwa. Licha ya mambo aliyoigiza, mifano aliyotoa, ujumbe aliotangaza, wahamishwa walikataa kuamini kwamba Yehova angeruhusu Yerusalemu liharibiwe. Hata walipopata habari kwamba jiji hilo limezingirwa na jeshi la Babiloni, bado walikuwa na uhakika kwamba wakaaji wake wangekuwa salama.

2 Lakini sasa, miaka miwili baada ya kuanza kuzingirwa, mkimbizi kutoka Yerusalemu amewasili Babiloni, analeta habari hii: “Jiji limeangamizwa!” Habari hizo zinawavunja moyo wahamishwa. Wanashindwa kuelewa ujumbe huo kikamili: jiji walilolipenda, hekalu takatifu, nchi waliyoipenda—vyote vimeharibiwa! Tumaini lao la muda mrefu linageuka na kuwa huzuni.—Eze. 21:7; 33:21.

3 Hata hivyo, watu wakiwa wamevunjika moyo, Ezekieli anapokea maono yenye nguvu yanayoleta tumaini. Maono hayo yana ujumbe gani kwa wahamishwa waliokata tamaa? Maono hayo yanawahusuje watu wa Mungu leo, na sisi binafsi tunawezaje kufaidika kutokana nayo? Ili tupate majibu, acheni tuchunguze mambo ambayo Yehova anamfunulia Ezekieli.

“Itabirie Mifupa Hii” na “Utabirie Upepo”

4. Ezekieli alitambua mambo gani hasa katika maono aliyopewa?

4 Soma Ezekieli 37:1-10. Katika maono, Ezekieli anapelekwa katika bonde tambarare lililojaa mifupa. Ili kuhakikisha kwamba Ezekieli anaelewa vizuri maono hayo, Yehova anamwamuru nabii huyo ‘azunguke’ mifupa hiyo yote iliyotapakaa. Ezekieli anapotembea katika lile bonde tambarare, anatambua mambo mawili hasa kuhusu ile mifupa: idadi yake na hali yake. Alisema, “kulikuwa na mifupa mingi sana,” na “ilikuwa mikavu sana.”

5. Yehova alimpa Ezekieli amri gani mbili, na nini kilichotokea Ezekieli alipotii amri hizo?

5 Kisha Yehova akampa Ezekieli amri mbili ambazo zingeanzisha hatua kwa hatua matukio ya kurudishwa. Amri ya kwanza ilikuwa: “Itabirie mifupa hii,” iambie, “mtakuwa hai.” (Eze. 37:4-6) Mara tu Ezekieli alipotabiri, kukawa na “sauti ya vitu vinavyogongana, nayo mifupa ikaanza kukaribiana,” kisha “kano na nyama” zikaja juu ya mifupa, “na ngozi ikazifunika.” (Eze. 37:7, 8) Amri ya pili ilikuwa: “Utabirie upepo,” uuambie ‘upulize’ miili. Ezekieli alipotabiri, “pumzi ikaingia ndani yao, nao wakaanza kuishi na kusimama kwa miguu yao, walikuwa jeshi kubwa ajabu.”—Eze. 37:9, 10.

“Mifupa Yetu Imekauka, Nalo Tumaini Letu Limepotea”

6. Ni maneno gani ya Yehova yaliyomsaidia Ezekieli kuelewa maono hayo?

6 Kisha Yehova akamfunulia Ezekieli maana ya maono hayo, akisema: “Mifupa hii ni watu wote wa nyumba ya Israeli.” Kwa kweli, baada ya wahamishwa kusikia Yerusalemu limeharibiwa, walihisi kana kwamba wamekufa. Kwa hiyo, wakaomboleza hivi: “Mifupa yetu imekauka, nalo tumaini letu limepotea. Tumeangamizwa kabisa.” (Eze. 37:11; Yer. 34:20) Kisha akijibu maombolezo yao, Yehova alifunua kwamba maono hayo ya mifupa kwa kweli yalikuwa na ujumbe wenye kupendeza wa tumaini kwa Israeli.

7. Kama ilivyoandikwa katika Ezekieli 37:12-14, Yehova alimfunulia nini Ezekieli, na hilo liliwapa uhakikisho gani watu Wake waliohamishwa?

7 Soma Ezekieli 37:12-14. Kupitia maono hayo, Yehova aliwahakikishia wahamishwa kwamba angewafanya wawe hai, awarudishe katika nchi yao, na waishi huko. Isitoshe, Yehova aliwaita tena “watu wangu.” Maneno hayo yaliwatia moyo sana wahamishwa hao waliovunjika moyo! Kwa nini wangekuwa na uhakika kwamba ahadi hiyo ya kurudishwa ingetimizwa? Kwa sababu Yehova mwenyewe ndiye aliyeahidi. Alisema hivi: “Mimi mwenyewe, Yehova, nimesema, nami nimelitenda.”

8. (a) “Watu wote wa nyumba ya Israeli” walikuwa katika hali gani inayofanana na kifo? (b) Andiko la Ezekieli 37:9 linaonyeshaje sababu ya kifo cha mfano cha Israeli? (Tazama maelezo ya chini.)

8 Taifa la kale la Israeli lilikuwa limeonaje utimizo wa sehemu yenye kuhuzunisha ya maono hayo ya kinabii? Kwa njia ya mfano, tayari taifa la Israeli lilikuwa limeanza kufa mwaka wa 740 K.W.K. wakati ufalme wenye makabila kumi ulipoanguka na kupelekwa uhamishoni. Miaka 130 hivi baadaye, watu wa Yuda pia walipopelekwa uhamishoni, “watu wote wa nyumba ya Israeli” wakaenda utekwani. (Eze. 37:11) Kwa njia ya mfano, kikundi chote cha wahamishwa kilikuwa kimekufa kama mifupa ambayo Ezekieli aliona katika maono. * Pia, kumbuka kwamba Ezekieli hakuona tu mifupa bali mifupa “mikavu sana,” jambo lililoonyesha kwamba walikuwa wamekufa kwa muda mrefu sana. Kwa kweli, kwa ujumla Israeli na Yuda walikaa utekwani zaidi ya miaka 200, kuanzia 740 hadi 537 K.W.K.—Yer. 50:33.

9. Kuna ulinganifu gani kati ya mambo yaliyowapata Waisraeli wa kale wa asili na yaliyowapata “Israeli wa Mungu”?

9 Unabii kuhusu kurudishwa kwa Israeli, kama ule uliotolewa na Ezekieli, ulitimizwa kwa njia kubwa zaidi. (Mdo. 3:21) Kama vile taifa la kale la Israeli wa kimwili ‘lilivyouawa’ na kufa kwa njia ya kiroho kwa muda mrefu, ndivyo “Israeli wa Mungu,” kutaniko la Wakristo waliotiwa mafuta, lilivyouawa kwa njia ya mfano na kupatwa na utekwa ulio kama kifo kwa kipindi kirefu. (Gal. 6:16) Kwa kweli, utekwa wa kutaniko la watiwa mafuta kwa ujumla uliendelea kwa muda mrefu sana hivi kwamba hali yao ya kiroho ingeweza kulinganishwa na mifupa “mikavu sana.” (Eze. 37:2) Kama ilivyozungumziwa katika sura iliyotangulia, utekwa wa kutaniko la Wakristo waliotiwa mafuta ulianza karne ya pili W.K. na kuendelea kwa karne nyingi, kama vile Yesu alivyosema katika mfano wake wa ngano na magugu unaohusu Ufalme.—Mt. 13:24-30.

Mifupa “mikavu sana” ambayo Ezekieli aliona katika maono iliwakilisha kipindi kirefu cha utekwa unaofanana na kifo cha watiwa mafuta wa Mungu (Tazama fungu la 8 na 9)

“Mifupa Ikaanza Kukaribiana”

10. (a) Andiko la Ezekieli 37:7, 8 lilitabiri jambo gani kuhusu watu wa Mungu? (b) Ni mambo gani ambayo yaliwasaidia hatua kwa hatua watu wanaomwogopa Mungu waliokuwa uhamishoni wawe na imani?

10 Nyakati za kale, Yehova alitabiri kwamba watu wake wangefanywa tena kuwa hai hatua kwa hatua. (Eze. 37:7, 8) Basi ni mambo gani ambayo yaliwafanya watu wanaomwogopa Mungu waliokuwa uhamishoni wawe na imani kwamba tumaini lao la kurudi Israeli lingetimizwa? Chanzo kimoja cha tumaini kilikuwa maneno ya unabii yaliyosemwa zamani na manabii. Kwa mfano, Isaya alikuwa ametabiri kwamba watu waliobaki, “mbegu takatifu,” wangerudi katika nchi yao. (Isa. 6:13; Ayu. 14:7-9) Pia, unabii mwingi kuhusu kurudishwa ambao Ezekieli alikuwa ameandika bila shaka uliendelea kuwapa tumaini. Isitoshe, kuwepo kwa wanaume waaminifu kama vile nabii Danieli huko Babiloni—na pia kuanguka kwa jiji la Babiloni mwaka wa 539 K.W.K.—kuliimarisha tumaini la wahamishwa kwamba wangerudi.

11, 12. (a) “Israeli wa Mungu” walirudishwaje hatua kwa hatua? (Tazama pia sanduku “Ibada Safi—Yarudishwa Hatua kwa Hatua.”) (b) Maneno ya Ezekieli 37:10 yanatokeza swali gani?

11 “Israeli wa Mungu,” yaani, kutaniko la Wakristo waliotiwa mafuta walirudishwaje hatua kwa hatua kwa njia kama hiyo? Kwa karne nyingi, wakiwa katika hali ya utekwa ulio kama kifo, “sauti ya vitu vinavyogongana,” ilisikika watu wanaomwogopa Mungu walipotetea ibada ya kweli. Kwa mfano, katika karne ya 16, William Tyndale alitafsiri Biblia katika Kiingereza. Makasisi wa kanisa Katoliki walikasirika kwa sababu hawakutaka Biblia isomwe na watu wa kawaida. Tyndale aliuawa. Hata hivyo, watu wengine wenye ujasiri waliendelea kutafsiri Biblia katika lugha nyingine, na hatua kwa hatua nuru ya kiroho ikaenea katika ulimwengu wote wenye giza.

12 Baadaye, Charles T. Russell na washiriki wake walijitahidi kurudisha kweli za Biblia, ni kana kwamba “kano na nyama” ziliungana na mifupa. Gazeti la Zion’s Watch Tower na machapisho mengine yaliwasaidia watu wenye mioyo minyoofu watambue kweli za Biblia, ambazo ziliwachochea kujiunga na watumishi wa Mungu waliotiwa mafuta. Mwanzoni mwa miaka ya 1900, watumishi wa Mungu waliotiwa mafuta walizidi kutiwa nguvu na vifaa kama vile “Photo-Drama of Creation” na kitabu The Finished Mystery. Baada ya muda mfupi, wakati wa Mungu kufanya watu wake ‘wasimame kwa miguu yao’ ukafika. (Eze. 37:10) Jambo hilo lilitukia lini na jinsi gani? Matukio yaliyotukia katika Babiloni la kale yanatusaidia kujibu swali hilo.

“Wakaanza Kuishi na Kusimama kwa Miguu Yao”

13. (a) Kuanzia mwaka wa 537 K.W.K., maneno ya Ezekiel 37:10, 14 yalitimizwaje? (b) Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba baadhi ya watu kutoka ufalme wa makabila kumi walirudi Israeli?

13 Kuanzia mwaka wa 537 K.W.K, Wayahudi waliokuwa Babiloni waliona utimizo wa maono hayo. Jinsi gani? Yehova aliwafanya wawe hai na kufanya ‘wasimame kwa miguu yao’ kwa kuwakomboa kutoka katika utekwa na kuwaruhusu warudi Israeli. Kikundi cha Waisraeli 42,360 na watu 7,000 wasio Waisraeli waliondoka Babiloni kwenda kujenga upya Yerusalemu na hekalu lake, na kuishi katika nchi ya Israeli. (Ezra 1:1-4; 2:64, 65; Eze. 37:14) Kisha, miaka 70 hivi baadaye, karibu wahamishwa 1,750 walijiunga na Ezra kurudi Yerusalemu. (Ezra 8:1-20) Basi, kwa ujumla, zaidi ya Wayahudi 44,000 walirudi—kwa kweli lilikuwa “jeshi kubwa.” (Eze. 37:10) Isitoshe, Neno la Mungu linaonyesha kwamba watu wa kutoka ufalme wenye makabila kumi, ambao babu zao walikuwa wamepelekwa utekwani na Waashuru katika karne ya nane K.W.K., pia walirudi Israeli ili kusaidia kujenga upya hekalu.—1 Nya. 9:3; Ezra 6:17; Yer. 33:7; Eze. 36:10.

14. (a) Maneno ya Ezekieli 37:24 yanatusaidiaje kutambua wakati wa utimizo mkuu wa unabii huo? (b) Ni jambo gani lililotukia mwaka wa 1919? (Tazama pia sanduku “Kuna Uhusiano Gani Kati ya ‘Mifupa Mikavu’ na “Mashahidi Wawili””)

14 Sehemu hii ya unabii wa Ezekieli ilitimizwaje kwa njia kubwa zaidi? Kama Yehova alivyomfunulia Ezekieli katika unabii unaohusiana na huu, sehemu kuu ya utimizo wa unabii huu wa kurudishwa ingetimizwa muda fulani baada ya Daudi Mkuu, Yesu Kristo, kuanza kutawala akiwa Mfalme. * (Eze. 37:24) Na kwa kweli, mwaka wa 1919, Yehova aliweka roho yake ndani ya watu wake. Matokeo ni kwamba wakawa “hai” na wakawekwa huru kutoka kwa utekwa wa Babiloni Mkubwa. (Isa. 66:8) Baada ya hapo, Yehova aliwaruhusu waishi katika “nchi” yao, yaani, paradiso ya kiroho. Hata hivyo, watumishi wa siku hizi wa Yehova wamekuwaje “jeshi kubwa”?

15, 16. (a) Leo, watu wa Yehova wamekuwaje “jeshi kubwa”? (b) Unabii huu wa Ezekieli unatusaidiaje kukabiliana na hali ngumu maishani? (Tazama sanduku “Msaada wa Kusimama Tena.”)

15 Muda mfupi baada ya Kristo kumweka rasmi mtumwa mwaminifu mwaka wa 1919, watumishi wa Mungu walianza kupatwa na jambo ambalo Zekaria, nabii wa Mungu aliyetumikia kati ya wahamishwa, alikuwa ametabiri aliposema: “Mataifa mengi na mataifa yenye nguvu yatakuja . . . kumtafuta Yehova.” Nabii huyo aliwalinganisha watu hao wanaomtafuta Yehova na “watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa.” Watu hao wangeshika kwa nguvu mavazi ya “Myahudi,” Israeli wa kiroho wakisema: “Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yupo pamoja nanyi.”—Zek. 8:20-23.

16 Leo, Israeli wa kiroho (watiwa mafuta waliobaki) na vilevile “wanaume kumi” (kondoo wengine) kwa pamoja wanafanyiza “jeshi kubwa ajabu,” lenye mamilioni ya watu. (Eze. 37:10) Tukiwa wanajeshi wa Kristo katika jeshi hilo linalozidi kuongezeka, tunamfuata kwa ukaribu Mfalme wetu Yesu, tukielekea kwenye baraka zilizo mbele yetu.—Zab. 37:29; Eze. 37:24; Flp. 2:25; 1 The. 4:16, 17.

17. Tutachunguza nini katika sura inayofuata?

17 Kurudishwa huku kwa ibada safi kungewapa watu wa Mungu jukumu muhimu. Jukumu gani? Ili kupata jibu la swali hilo tunahitaji kurudi nyuma na kuchunguza mgawo ambao Ezekieli alipewa na Yehova hata kabla Yerusalemu halijaharibiwa. Tutachunguza jambo hilo katika sura inayofuata ya kitabu hiki.

^ fu. 8 Mifupa ambayo Ezekieli aliona katika maono, haikuwa ya watu waliokufa kifo cha kawaida, bali ya “watu waliouawa.” (Eze. 37:9) “Watu wote wa nyumba ya Israeli” waliuawa kwa njia ya mfano wakati wakaaji wa ufalme wa Israeli wenye makabila kumi na wale wa ufalme wa Yuda wenye makabila mawili waliposhindwa, wakatekwa, na kupelekwa uhamishoni na Waashuru na Wababiloni.

^ fu. 14 Unabii huu wa Kimasihi umezungumziwa katika Sura ya 8 ya kitabu hiki.