Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 14A

Masomo Kutokana na Hekalu Aliloona Ezekieli

Masomo Kutokana na Hekalu Aliloona Ezekieli

Ibada Safi Yainuliwa na Kulindwa

Hekalu hilo limekwezwa juu ya “mlima mrefu sana” (1). Je, tumeiinua ibada safi, na kuitanguliza kabisa katika maisha yetu?

Ukuta (2), uliozunguka majengo ya hekalu yaliyokuwa katikati ya eneo pana (3), unatukumbusha kwamba hatupaswi kamwe kuruhusu chochote kichafue ibada yetu kwa Yehova. Ikiwa hata vitu kwa ajili ya “matumizi ya kawaida” vinapaswa kuwekwa mbali na ibada safi, basi waabudu wa Yehova leo wanapaswa kuepuka kabisa mwenendo mchafu au uliopotoka!—Eze. 42:20.

Baraka za Milele

Kijito kinatiririka kutoka patakatifu pa hekalu, kisha kinapanuka na kuwa mto mkubwa na kuleta uhai na rutuba katika nchi (4). Baraka hizi zitazungumziwa katika sura ya 19 ya kitabu hiki.

Viwango Sawa kwa Wote

Malango marefu ya nje (5) na malango ya ndani (9) yanatukumbusha kwamba Yehova anatazamia wote wanaoshiriki katika ibada safi wafuate viwango vya juu vya mwenendo. Ona kwamba kwa ujumla malango ya nje na malango ya ndani yana vipimo na ukubwa uleule. Hilo linafaa, kwa sababu viwango vya uadilifu vya Yehova ni vilevile kwa watumishi wake wote, bila kuzingatia cheo au majukumu yao.

Mlo Kwenye Meza ya Yehova

Vyumba vya kulia chakula (8) vinatukumbusha kwamba nyakati za kale, watu wangeshiriki kula baadhi ya dhabihu walizoleta hekaluni, na hivyo kula mlo pamoja na Yehova. Hilo ni tofauti na hekalu la kiroho ambamo Wakristo wanaabudu leo, kwa maana tayari “dhabihu moja” imetolewa. (Ebr. 10:12) Hata hivyo, bado tunatoa dhabihu yetu ya sifa.—Ebr. 13:15.

Uhakikisho Kutoka kwa Mungu

Huenda usikumbuke vipimo vyote vinavyotajwa katika maono hayo. Lakini vinatufundisha jambo muhimu: Vinatuhakikishia kwamba kusudi la Yehova la kurudisha ibada safi ni hakika kabisa, ni kamili na kama vipimo hivyo, haliwezi kubadilika. Ingawa Ezekieli hataji kwamba alimwona mtu yeyote katika maono hayo, aliandika shauri zito la Yehova kwa makuhani, wakuu, na watu. Watumishi wote wa Yehova wanapaswa kufuata viwango vyake vya uadilifu.