Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Muhtasari wa Ufafanuzi Mpya

Muhtasari wa Ufafanuzi Mpya

Kadiri miaka inavyopita, gazeti Mnara wa Mlinzi limerekebisha uelewaji wetu wa mambo fulani kuhusu unabii wa Ezekieli. Kitabu hiki, Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!, kina ufafanuzi zaidi. Je, unaweza kujibu maswali yafuatayo.

Nyuso nne za wale viumbe hai zinawakilisha nini?

Uelewaji wa awali: Kila uso kati ya nyuso nne za wale viumbe hai, au makerubi, unawakilisha mojawapo ya sifa nne kuu za Yehova.

Ufafanuzi mpya: Ingawa kila uso kati ya nyuso nne za wale viumbe hai unawakilisha mojawapo ya sifa nne kuu za Yehova, kwa pamoja nyuso hizo nne zinawakilisha sifa zote za Yehova. Pia, nyuso hizo nne zinakazia ukuu wa nguvu na utukufu wa Yehova.

Sababu ya badiliko hilo: Katika Neno la Mungu, mara nyingi namba nne hutumiwa kuwakilisha mambo yote, au kuonyesha ukamili. Basi, nyuso nne zinapoonekana pamoja, haziwakilishi tu sifa nne​—bali ni msingi wa utu wa Yehova wenye kustaajabisha. Pia, kila uso ni wa kiumbe mwenye ukuu, nguvu, na uwezo. Hata hivyo, viumbe wanne wenye uwezo wanaowakilisha uumbaji wako chini ya kiti cha ufalme cha Yehova. Hilo linakazia kwamba Yehova ndiye Mtawala Mkuu aliye juu ya wote.

Mwanamume mwenye kidau cha wino anawakilisha nani?

Uelewaji wa awali: Mwanamume wenye kidau cha wino anawakilisha watiwa mafuta waliobaki duniani. Kupitia kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, watiwa mafuta wanaweka alama ya mfano kwenye mapaji ya nyuso za wale wanaofanyiza “umati mkubwa.”​—Ufu. 7:9.

Ufafanuzi mpya: Mwanamume mwenye kidau cha wino anawakilisha Yesu Kristo. Atawatia alama wale wanaofanyiza umati mkubwa watakapohukumiwa kuwa kondoo wakati wa “dhiki kuu.”​—Mt. 24:21.

Sababu ya badiliko hilo: Yehova amemkabidhi Mwana wake jukumu la kuhukumu. (Yoh. 5:​22, 23) Kulingana na Mathayo 25:31-​33, Yesu ndiye atakayefanya hukumu ya mwisho kuamua wale walio “kondoo” na wale walio “mbuzi.”

Je, dada makahaba, Ohola na Oholiba, wanawakilisha dini zinazodai kuwa za Kikristo zilizogawanyika, yaani, Wakatoliki na Waprotestanti?

Uelewaji wa awali: Ohola (Samaria, jiji kuu la Israeli), yule dada mkubwa, anawakilisha Ukatoliki; Oholiba (Yerusalemu, jiji kuu la Yuda), yule dada mdogo, anawakilisha Uprotestanti.

Ufafanuzi mpya: Dada hao makahaba si ufananisho wa kinabii wa sehemu yoyote ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Badala yake, dada hao wanatufundisha jinsi Yehova anavyohisi wakati watu waliokuwa washikamanifu kwake wanapofanya ukahaba wa kiroho. Hivyo ndivyo anavyohisi kuhusu dini zote za uwongo.

Sababu ya badiliko hilo: Hakuna uthibitisho wowote katika Maandiko unaoonyesha kwamba Ohola na Oholiba ni mifano ya kinabii ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Wakati fulani Israeli na Yuda walikuwa kama wake waliokuwa waaminifu kwa Yehova, lakini dini zinazodai kuwa za Kikristo hazijawahi kuwa na uhusiano kama huo na Yehova. Isitoshe, ufananisho wa watu wa Mungu na makahaba katika Ezekieli sura ya 16 na 23 unatoa tumaini la mabadiliko na kurudishwa. Dini zinazodai kuwa za Kikristo, ambazo ni sehemu ya Babiloni Mkubwa, hazina tumaini kama hilo.

Je, jiji la kale la Yerusalemu liliwakilisha dini zinazodai kuwa za Kikristo?

Uelewaji wa awali: Jiji la Yerusalemu lililokosa uaminifu lilikuwa ufananisho wa kinabii wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Basi, kuharibiwa kwa Yerusalemu kuliwakilisha kuharibiwa kwa dini zinazodai kuwa za Kikristo.

Ufafanuzi mpya: Hali zilizokuwa katika Yerusalemu lililokosa uaminifu​—kama vile ibada ya sanamu na upotovu ulioenea​—zinatukumbusha kuhusu dini zinazodai kuwa za Kikristo, lakini hatusemi tena kwamba Yerusalemu liliwakilisha dini zinazodai kuwa za Kikristo.

Sababu ya badiliko hilo: Hakuna msingi wowote wa Kimaandiko ulio wazi kuhusu ufananisho huo. Tofauti na Yerusalemu la kale, dini zinazodai kuwa za Kikristo hazijawahi kamwe kuwa na ibada safi. Na ingawa kwa muda fulani Yerusalemu lilisamehewa na Yehova, dini zinazodai kuwa za Kikristo hazina tumaini kama hilo.

Maono ya bonde la mifupa mikavu yalitimizwaje?

Uelewaji wa awali: Mwaka wa 1918 watiwa mafuta waliteswa na kupelekwa katika utekwa wa Babiloni Mkubwa na hawakuwa na utendaji wowote, ni kana kwamba walikuwa wamekufa. Utekwa huo mfupi uliisha mwaka wa 1919 Yehova alipowafanya kuwa hai tena wakiwa watangazaji wa Ufalme.

Ufafanuzi mpya: Utekwa wa kiroho unaofananishwa na kifo ambao ulidumu kwa muda mrefu sana ulianza miaka mingi kabla ya 1918. Ulianza katika karne ya pili W.K. na kufikia mwisho mwaka wa 1919 W.K. na unalingana na kipindi kirefu cha ukuzi katika mfano wa Yesu wa ngano na magugu.

Sababu ya badiliko hilo: Utekwa wa Israeli la kale ulidumu kwa kipindi kirefu, kuanzia mwaka wa 740 K.W.K. hadi mwaka wa 537 K.W.K. Unabii wa Ezekieli unataja mifupa kuwa “mikavu” au “mikavu sana,” kuonyesha kwamba wale wanaofananishwa na mifupa hiyo walikuwa wamekufa kwa muda mrefu sana. Na kurudishwa kwa mifupa hiyo kunatokea hatua kwa hatua jambo linalochukua muda.

Ni nini maana ya kuunganishwa kwa vijiti viwili?

Uelewaji wa awali: Baada ya kipindi kifupi cha mgawanyiko wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, watiwa mafuta waaminifu waliungana tena mwaka wa 1919.

Ufafanuzi mpya: Unabii huo unakazia kwamba Yehova atafanya waabudu wake wawe kitu kimoja. Baada ya mwaka wa 1919, kadiri muda ulivyozidi kusonga, idadi inayoongezeka ya watu walio na tumaini la kuishi duniani walijiunga na watiwa mafuta waliobaki. Vikundi hivyo viwili vinamwabudu Yehova pamoja kwa umoja.

Sababu ya badiliko hilo: Unabii huo hausemi kwamba kijiti kimoja kilivunjwa na kuwa vijiti viwili na kisha kuunganishwa. Basi, unabii huo haufafanui kwamba kikundi kimoja kitagawanyika na baadaye kiungane tena. Badala yake, unaonyesha kwamba vikundi viwili tofauti vitaungana na kuwa na umoja.

Gogu wa Magogu Ni Nani?

Uelewaji wa awali: Gogu wa Magogu ni jina la kinabii ambalo Shetani alipewa baada ya kufukuzwa mbinguni.

Ufafanuzi mpya: Gogu wa Magogu ni muungano wa mataifa yatakayowashambulia waabudu wa kweli wakati wa dhiki kuu.

Sababu ya badiliko hilo: Ufafanuzi wa kinabii kuhusu Gogu​—kwamba atatolewa awe chakula cha ndege wanaowinda na kupewa kaburi duniani​—unaonyesha kwamba Gogu si kiumbe wa roho. Isitoshe, shambulizi la Gogu linalingana na mambo ambayo vitabu vya Danieli na Ufunuo vinasema kuhusu jinsi mataifa yaliyo duniani yatakavyowashambulia watu wa Mungu.​—Dan. 11:40, 44, 45; Ufu. 17:14; 19:19.

Je, Ezekieli aliona na kuingia katika hekalu la kiroho ambalo baadaye Paulo alilifafanua?

Uelewaji wa awali: Hekalu aliloona Ezekieli ni hekalu lilelile ambalo mtume Paulo alilifafanua.

Ufafanuzi mpya: Ezekieli hakuona hekalu la kiroho lililoanzishwa mwaka wa 29 W.K., bali maono hayo yalionyesha jinsi ambavyo ibada safi inayofafanuliwa katika Sheria ya Musa ingerudishwa baada ya Waisraeli kutoka uhamishoni. Ufafanuzi wa Paulo ulioongozwa na roho kuhusu hekalu la kiroho unakazia kazi ambayo Yesu, akiwa Kuhani Mkuu Zaidi, alitimiza kuanzia mwaka wa 29 hadi 33 W.K. Katika hekalu aliloona, Ezekieli hataji kamwe kuhani mkuu, bali anakazia kurudishwa kwa kiroho kulikoanza mwaka wa 1919 W.K. Basi hatutafuti ufananisho wa kinabii wa vipimo na mambo mengi yanayofafanuliwa katika hekalu aliloona Ezekieli. Badala yake, tunakazia hasa masomo tunayojifunza kuhusu viwango vya Yehova vya ibada safi kutokana na hekalu aliloona Ezekieli.

Sababu ya badiliko hilo: Kuna tofauti kubwa kati ya hekalu aliloona Ezekieli na hekalu la kiroho. Kwa mfano, katika hekalu aliloona Ezekieli dhabihu nyingi za wanyama zilitolewa; katika hekalu la kiroho, dhabihu moja tu ndiyo inayotolewa, “mara moja kwa wakati wote.” (Ebr. 9:​11, 12) Karne nyingi kabla ya Kristo kuja, wakati wa Yehova kufunua kweli zenye kina kuhusu hekalu la kiroho haukuwa umefika.