Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 5

‘Ona Mambo Maovu na Yenye Kuchukiza Wanayofanya’

‘Ona Mambo Maovu na Yenye Kuchukiza Wanayofanya’

EZEKIELI 8:9

WAZO KUU: Taifa la Yuda lililoasi imani lazorota kiroho na kimaadili

1-3. Yehova alitaka Ezekieli aone nini hekaluni huko Yerusalemu, na kwa nini? (Tazama Sehemu ya 2)

AKIWA mwana wa kuhani, nabii Ezekieli anaifahamu vizuri Sheria ya Musa. Basi analifahamu hekalu lililo Yerusalemu na ibada safi ya Yehova inayopaswa kufanywa humo. (Eze. 1:3; Mal. 2:7) Lakini sasa katika mwaka wa 612 K.W.K., mambo yanayotendeka hekaluni yanawashtua Wayahudi waaminifu kutia ndani Ezekieli.

2 Yehova anataka Ezekieli aone hali yenye kuchukiza katika hekalu, kisha awaambie mambo anayoona “wazee wa Yuda,” yaani, wayahudi wenzake waliohamishwa ambao wamekusanyika katika nyumba yake. (Soma Ezekieli 8:1-4; Eze. 11:24, 25; 20:1-3) Kupitia roho takatifu, Yehova anamsafirisha Ezekieli (katika maono) kutoka katika nyumba yake iliyo Tel-abib, karibu na mto Kebari huko Babiloni, mamia ya kilomita upande wa magharibi wa Yerusalemu. Yehova anampeleka nabii huyo katika hekalu, kwenye lango la kaskazini la ua wa ndani. Akianzia hapo, Yehova anamtembeza hekaluni katika maono.

3 Sasa Ezekieli anaona matukio manne yanayoonyesha jinsi taifa hilo lilivyopotoka kiroho. Ibada safi ya Yehova imepatwa na nini? Na maono hayo yana maana gani kwetu leo? Acheni tufuatane na Ezekieli katika matembezi yake. Hata hivyo, kwanza tunahitaji kuchunguza jambo ambalo Yehova anataka kutoka kwa waabudu wake.

“Mimi . . . Ni Mungu Ninayetaka Watu Waniabudu Mimi Peke Yangu”

4. Yehova anataka nini kutoka kwa waabudu wake?

4 Karne tisa hivi kabla ya siku za Ezekieli, Yehova alisema waziwazi jambo ambalo alitaka kutoka kwa waabudu wake. Katika amri ya pili kati ya zile Amri Kumi, aliwaambia hivi Waisraeli: * “Mimi, Yehova Mungu wako, ni Mungu ninayetaka watu waniabudu mimi peke yangu.” (Kut. 20:5) Maneno “waniabudu mimi peke yangu,” yanaonyesha kwamba Yehova hangekubali ibada ya miungu mingine. Kama tulivyoona katika Sura ya 2 ya kitabu hiki, takwa la kwanza la ibada safi ni kwamba ibada yetu inapaswa kuelekezwa kwa Yehova. Waabudu wake wanapaswa kumtanguliza katika maisha yao. (Kut. 20:3) Kwa ufupi, Yehova angependa waabudu wake waendelee kuwa safi kiroho kwa kuepuka kuchanganya ibada ya kweli na ibada ya uwongo. Mwaka wa 1513 K.W.K., Waisraeli waliingia kwa hiari katika agano la Sheria. Kwa kufanya hivyo, walikubali kumwabudu Yehova peke yake. (Kut. 24:3-8) Yehova ni mshikamanifu kwa maagano yake naye alitarajia watu wake wawe washikamanifu kwa agano lake.—Kum. 7:9, 10; 2 Sam. 22:26.

5, 6. Kwa nini Waisraeli walipaswa kumwabudu Yehova peke yake?

5 Je, ilifaa kwa Yehova kuamuru Waisraeli wamwabudu yeye peke yake? Bila shaka, ndiyo! Yeye ndiye Mungu Mweza Yote, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, na Chanzo na Mtegemezaji wa uhai. (Zab. 36:9; Mdo. 17:28) Yehova pia alikuwa Mkombozi wa Waisraeli. Alipokuwa akiwapa Amri Kumi aliwakumbusha watu hivi: “Mimi ni Yehova Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa.” (Kut. 20:2) Kwa kweli, Waisraeli walipaswa kumwabudu Yehova peke yake.

6 Yehova habadiliki. (Mal. 3:6) Sikuzote ametaka aabudiwe yeye peke yake. Sasa, wazia jinsi alivyohisi kuhusu matukio manne yenye kuchukiza aliyomwonyesha Ezekieli.

Tukio la Kwanza: Sanamu ya Ishara ya Wivu

7. (a) Wayahudi walioasi imani walikuwa wakifanya nini katika lango la kaskazini la hekalu, na Yehova alihisije? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.) (b) Ni nini kilichomfanya Yehova awe na wivu? (Tazama maelezo ya chini ya 2.)

7 Soma Ezekieli 8:5, 6Ezekieli alishtuka sana! Kwenye lango la kaskazini la hekalu, Wayahudi walioasi imani walikuwa wakiabudu sanamu ya ishara. Labda ilikuwa nguzo takatifu iliyomwakilisha Ashera, mungu wa kike wa uwongo wa Wakanaani waliyeamini kuwa ni mke wa Baali. Vyovyote vile, Waisraeli hao walioabudu sanamu walivunja makubaliano ya agano lao pamoja na Yehova. Kwa kuabudu sanamu badala ya Yehova anayestahili kuabudiwa peke yake—walimfanya Yehova awe na wivu; walimchochea awe na hasira ya uadilifu. * (Kum. 32:16; Eze. 5:13) Hebu wazia: Kwa zaidi ya miaka 400, patakatifu pa hekalu palihusianishwa na kuwapo kwa Yehova. (1 Fal. 8:10-13) Lakini sasa kwa kuleta ibada ya sanamu katika hekalu, waabudu hao wa sanamu walimfanya Yehova aende “mbali sana na mahali [pake] patakatifu.”

8. Maono ya Ezekieli kuhusu ishara ya wivu yana maana gani kwetu leo?

8 Maono ya Ezekieli kuhusu ishara ya wivu yana maana gani kwetu leo? Bila shaka, taifa la Yuda lililoasi imani linatukumbusha kuhusu dini zinazodai kuwa za Kikristo. Ibada ya sanamu imejaa katika makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo, na hivyo kufanya ibada ambayo watu wanadai kumtolea Mungu isiwe halali. Kwa kuwa Yehova habadiliki, tunaweza kuwa na hakika kwamba dini zinazodai kuwa za Kikristo, kama Yuda lililoasi imani zimemfanya Yehova awe na hasira ya uadilifu. (Yak. 1:17) Kwa kweli, Yehova yuko mbali sana na Ukristo huo uliopotoka!

9, 10. Tunapata onyo gani kutoka kwa waabudu sanamu katika hekalu?

9 Tunapata onyo gani kutoka kwa wale waabudu sanamu katika hekalu? Ili kumwabudu Yehova peke yake, tunapaswa ‘kuikimbia ibada ya sanamu.’ (1 Kor. 10:14) Huenda tukasema, ‘Siwezi kamwe kutumia sanamu ninapomwabudu Yehova!’ Lakini kuna sanamu za aina mbalimbali, nyingine si za moja kwa moja. Kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinasema hivi: “Ibada ya sanamu inaweza kuhusisha vitu vingine, yaani, kumpuuza Mungu na kuhangaikia kitu chochote chenye thamani, bei, au nguvu.” Kwa hiyo, ibada ya sanamu inaweza kuhusisha mali, pesa, ngono, burudani, yaani, kitu chochote kinachoweza kuchukua nafasi ya kwanza katika maisha yetu na kutuzuia kumwabudu Yehova peke yake. (Mt. 6:19-21, 24; Efe. 5:5; Kol. 3:5) Tunapaswa kuepuka kila aina ya ibada ya sanamu, kwa sababu tunapaswa kumwabudu Yehova peke yake!—1 Yoh. 5:21.

10 Tukio la kwanza ambalo Yehova alimwonyesha Ezekieli lilihusisha “mambo mabaya sana na yenye kuchukiza.” Lakini Yehova alimwambia hivi nabii wake mwaminifu: “Utaona mambo yanayochukiza yaliyo mabaya hata zaidi.” Je, kungekuwa na mambo mengine yenye kuchukiza kuliko kuabudu sanamu ya ishara ya wivu katika hekalu?

Tukio la Pili: Wazee 70 Wakiitolea Miungu ya Uwongo Uvumba

11. Ezekieli aliona mambo gani yenye kuchukiza alipoingia katika ua wa ndani karibu na madhabahu ya hekalu?

11 Soma Ezekieli 8:7-12. Ezekieli alipotoboa ukuta na kuingia katika ua wa ndani karibu na madhabahu ya hekalu, aliona michoro yenye kuchukiza ya “viumbe wanaotambaa na wanyama wanaochukiza na sanamu zote zinazochukiza.” * Michoro hiyo iliyokuwa ukutani iliwakilisha miungu ya uwongo. Kisha jambo ambalo Ezekieli aliona lilikuwa lenye kuchukiza sana: “Wazee 70 wa nyumba ya Israeli” walikuwa wamesimama “gizani” wakiitolea miungu ya uwongo uvumba. Chini ya Sheria, kufukiza uvumba wenye harufu tamu kuliwakilisha sala zilizokubaliwa ambazo zilitolewa na waabudu waaminifu. (Zab. 141:2) Hata hivyo, uvumba ambao wale wazee 70 waliitolea miungu ya uwongo ulikuwa uvundo mchafu kwa Yehova. Sala zao zilikuwa kama harufu mbaya inayomchukiza. (Met. 15:8) Wazee hao walijidanganya hivi: “Yehova hatuoni.” Lakini Yehova aliwaona, na alimwonyesha Ezekieli mambo ambayo hasa walikuwa wakifanya katika hekalu lake!

Yehova anaona kila jambo lenye kuchukiza linalofanywa “gizani” (Tazama fungu la 11)

12. Kwa nini tunapaswa kuendelea kuwa waaminifu “gizani,” na ni nani hasa wanapaswa kuweka mfano mzuri katika jambo hilo?

12 Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi la Ezekieli kuhusu wale wazee 70 Waisraeli walioitolea miungu ya uwongo uvumba? Ili Mungu asikilize sala zetu na ibada yetu iwe safi machoni pake, tunapaswa kuendelea kuwa waaminifu hata tukiwa “gizani.” (Met. 15:29) Acheni tukumbuke kwamba sikuzote Yehova anaona kila kitu tunachofanya. Ikiwa Yehova ni halisi kwetu, hatutafanya jambo lolote faraghani ambalo tunajua halimpendezi. (Ebr. 4:13) Hasa wazee wa kutaniko wanapaswa kuweka mfano mzuri katika kufuata kanuni za Biblia. (1 Pet. 5:2, 3) Washiriki wa kutaniko wanatazamia kwamba mzee anayesimama mbele yao na kuwaongoza katika ibada mikutanoni anaishi kulingana na kanuni za Biblia hata akiwa “gizani,” yaani, wakati wengine hawamwoni.—Zab. 101:2, 3.

Tukio la Tatu: “Wanawake . . . Wakimlilia Mungu Tamuzi”

13. Ezekieli aliona wanawake walioasi imani wakifanya nini kwenye lango moja la hekalu?

13 Soma Ezekieli 8:13, 14. Baada ya kuona matukio mawili ya mazoea yenye kuchukiza, Yehova alimwambia tena Ezekieli: “Utaona mambo yanayochukiza yaliyo mabaya hata zaidi ambayo wanafanya.” Basi, nabii huyo aliona nini kingine? Kwenye “lango la kaskazini la nyumba ya Yehova,” aliona “wanawake wameketi wakimlilia mungu Tamuzi.” Tamuzi, mungu wa Mesopotamia, anaitwa Dumuzi katika maandishi ya Kisumeria na inaaminiwa kwamba ni mpenzi wa mungu wa kike wa uzazi, Ishtari. * Inaonekana wanawake Waisraeli walikuwa wakilia kama sehemu ya desturi ya kidini iliyohusiana na kifo cha Tamuzi. Kwa kumlilia Tamuzi katika hekalu la Yehova, wanawake hao walikuwa wakifanya desturi ya kipagani katika kituo cha ibada safi. Lakini kushiriki ibada ya uwongo katika hekalu la Mungu hakukufanya ibada hiyo ya uwongo iwe safi. Kwa kuwa kulingana na maoni ya Yehova, wanawake hao walioasi imani walikuwa wakifanya “mambo yanayochukiza”!

14. Tunajifunza nini kutokana na maoni ya Yehova kuhusu mambo ambayo wanawake walioasi imani walikuwa wakifanya?

14 Tunajifunza nini kutokana na maoni ya Yehova kuhusu mambo ambayo wanawake hao walikuwa wakifanya? Ili ibada yetu iwe safi, hatupaswi kamwe kuichanganya na mazoea machafu ya kipagani. Basi tunapaswa kuepuka kabisa desturi zinazotokana na dini za kipagani. Je, ni muhimu kuchunguza chanzo? Ndiyo! Leo, desturi zinazohusiana na sherehe fulani, kama vile Krismasi na Ista, huenda zikaonekana kuwa hazina madhara. Lakini tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova alijionea mazoea ya dini za kipagani ambayo hatimaye yamekuwa sherehe za kisasa. Yehova hayakubali mazoea ya kipagani kwa sababu tu watu wameyafanya kwa muda mrefu au wameyachanganya na ibada safi.—2 Kor. 6:17; Ufu. 18:2, 4.

Tukio la Nne: Wanaume 25 “Walikuwa Wakiliinamia Jua”

15, 16. Wanaume 25 walikuwa wakifanya nini katika ua wa ndani wa hekalu, na kwa nini matendo yao yalimkasirisha sana Yehova?

15 Soma Ezekieli 8:15-18. Kabla ya tukio la nne na la mwisho, Yehova alisema tena maneno haya: “Utaona mambo yanayochukiza ambayo ni mabaya hata zaidi kuliko haya.” Labda nabii huyo alijiuliza: ‘Je, kuna jambo lingine baya zaidi kuliko mambo ambayo tayari nimeona?’ Sasa, Ezekieli alikuwa katika ua wa ndani wa hekalu. Akiwa kwenye mwingilio wa hekalu aliona wanaume 25 wakiinama ili kuabudu “jua kuelekea mashariki.” Wanaume hao walimkasirisha Yehova kwa njia kubwa zaidi. Jinsi gani?

16 Wazia tukio hilo: Mwingilio wa hekalu ulijengwa kuelekea mashariki. Watu walipoingia hekaluni kuabudu walitazama upande wa magharibi, na migongo yao ikielekea mashariki ambako jua huchomoza. Lakini wale wanaume 25 katika maono “migongo yao ilielekea hekalu” na walitazama mashariki ili waabudu jua. Kwa kufanya hivyo, walimgeuzia Yehova mgongo, kwa maana hekalu hilo lilikuwa “nyumba ya Yehova.” (1 Fal. 8:10-13) Wanaume hao 25 walikuwa waasi imani. Walimdharau Yehova, nao wakavunja amri iliyo kwenye Kumbukumbu la Torati 4:15-19. Walimkasirisha sana Mungu, kwa kuwa ndiye anayepaswa kuabudiwa peke yake!

Yehova anataka waabudu wake wamwabudu yeye peke yake

17, 18. (a) Tunajifunza somo gani kutokana na waabudu wa jua katika hekalu? (b) Waisraeli walioasi imani waliharibu uhusiano gani, na jinsi gani?

17 Tunajifunza nini kutokana na simulizi la waabudu hao wa jua? Ili kudumisha ibada yetu ikiwa safi tunapaswa kutafuta mwongozo wa kiroho kutoka kwa Yehova. Kumbuka kwamba “Yehova Mungu ni jua,” na Neno lake ni “nuru” ya njia yetu. (Zab. 84:11; 119:105) Kupitia Neno lake na machapisho yanayotegemea Biblia kutoka kwa tengenezo lake, anaangazia mioyo na akili zetu, akituonyesha njia inayoongoza kwenye maisha yanayoridhisha sasa na uzima wa milele wakati ujao. Hata hivyo, ikiwa tutatafuta mwongozo wa jinsi ya kuishi kutoka kwa ulimwengu, tutakuwa tukimgeuzia Yehova mgongo. Jambo hilo litamkasirisha sana na kumwumiza moyoni. Hatungependa kamwe kumtendea hivyo Mungu wetu! Maono ya Ezekieli yanatuonya pia tuwaepuke wale wanaopinga ukweli, yaani, waasi imani.—Met. 11:9.

18 Kama tulivyoona, Ezekieli aliona matukio manne yenye kushtua ya ibada ya sanamu na ibada ya uwongo, ambayo yanaonyesha jinsi ibada ya Yuda lililoasi imani ilivyokuwa imepotoka. Kwa kujichafua kiroho, Waisraeli hao waliharibu uhusiano kati ya Mungu na taifa lao. Lakini uchafu wa kiroho unahusiana na uchafu wa kimaadili. Basi haishangazi kwamba Waisraeli walioasi imani walifanya kila aina ya upotovu wa maadili ambao uliharibu uhusiano wao na Mungu, na pia uhusiano na watu wengine. Acheni sasa tuone jinsi nabii Ezekieli, akiongozwa na roho, alivyofafanua upotovu wa kimaadili wa Yuda lililoasi imani.

Uchafu wa Kimaadili—“Mwenendo Mchafu Ndani Yako”

19. Ezekieli alifafanuaje upotovu wa maadili wa watu wa Yehova?

19 Soma Ezekieli 22:3-12. Kila mtu katika taifa hilo alikuwa amepotoka kimaadili kutia ndani watawala. “Wakuu,” au viongozi walitumia mamlaka yao kuua watu wasio na hatia. Kwa ujumla inaonekana watu waliwaiga viongozi wao katika kupuuza Sheria ya Mungu. Katika familia, watoto ‘waliwadharau’ wazazi na ngono kati ya watu wa familia moja lilikuwa jambo la kawaida. Katika nchi hiyo, Waisraeli waasi waliwapunja wakaaji wageni na wakawatendea vibaya mayatima na wajane. Wanaume Waisraeli walilala na wake wa majirani wao. Watu walikuwa na pupa kupita kiasi kwa kuchukua rushwa, kupunja, na kukopesha kwa riba. Yehova aliumia sana kuona Waisraeli wakivunja kimakusudi Sheria yake na kupuuza kusudi la upendo la Sheria hiyo! Yehova aliumizwa sana na upotovu wao wa kimaadili. Alimwongoza Ezekieli kuwaambia hivi watu hao waliopotoka: ‘Mmenisahau kabisa.’

Dini zinazodai kuwa za Kikristo zinachochea ulimwengu uzidi kuzama katika ukatili na upotovu wa maadili (Tazama fungu la 20)

20. Kwa nini maneno ya Ezekieli kuhusu upotovu wa maadili wa Yuda yana maana kwetu leo?

20 Kwa nini maneno ya Ezekieli kuhusu upotovu wa maadili wa Yuda yana maana kwetu leo? Upotovu wa Yuda lililoasi imani unatukumbusha kuhusu upotovu wa maadili katika ulimwengu tunamoishi leo. Viongozi wa kisiasa wanatumia vibaya mamlaka yao na kuwakandamiza watu wa hali ya chini. Viongozi wa kidini—hasa makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo—wamebariki vita kati ya mataifa ambavyo vimesababisha vifo vya mamilioni ya watu. Makasisi wamepotosha viwango vya Biblia vilivyo safi na wazi kuhusu maadili ya ngono. Matokeo ni kwamba viwango vya maadili vya ulimwengu unaotuzunguka vinazidi kuzorota. Kwa hakika, Yehova anaziambia dini zinazodai kuwa za Kikristo kama alivyoliambia Yuda lililoasi: ‘Mmenisahau kabisa.’

21. Tunajifunza nini kutokana na upotovu wa maadili wa Yuda la kale?

21 Tukiwa watu wa Yehova tunajifunza nini kutokana na upotovu wa maadili wa Yuda la kale? Ili Yehova akubali ibada yetu, tunapaswa kudumisha mwenendo safi katika mambo yote. Ni vigumu kufanya hivyo katika ulimwengu huu uliopotoka kimaadili. (2 Tim. 3:1-5) Hata hivyo, tunajua maoni ya Yehova kuhusu upotovu wa maadili wa kila aina. (1 Kor. 6:9, 10) Tunatii viwango vya Yehova vya maadili kwa sababu tunampenda yeye na sheria zake. (Zab. 119:97; 1 Yoh. 5:3) Tukiwa na maadili mapotovu tutaonyesha kwamba hatumpendi Mungu wetu aliye safi na mtakatifu. Hatungependa Yehova atuambie hivi: ‘Mmenisahau kabisa.’

22. (a) Baada ya kuchunguza mambo ambayo Yehova alifunua kuhusu Yuda la kale, umeazimia kufanya nini? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?

22 Tumejifunza masomo muhimu kwa kuchunguza mambo ambayo Yehova alifunua kuhusu upotovu wa maadili na wa kiroho wa Yuda la kale. Kwa kweli tumeazimia kumwabudu Yehova peke yake kwa kuwa yeye ndiye anayestahili kuabudiwa. Ili tufanye hivyo, tunapaswa kuepuka kila aina ya ibada ya sanamu na kuendelea kuwa safi kimaadili. Hata hivyo, Yehova aliwachukulia hatua gani watu wake wasio waaminifu? Mwishoni mwa matembezi ya Ezekieli hekaluni, Yehova alimwambia hivi waziwazi nabii huyo: “Nitatenda kwa ghadhabu.” (Eze. 8:17, 18) Tungependa kujua hatua ambayo Yehova alilichukulia taifa la Yuda lililoasi, kwa kuwa ulimwengu huu mwovu utachukuliwa hatua kama hiyo. Sura inayofuata itazungumzia jinsi hukumu ya Yehova dhidi ya Yuda ilivyotekelezwa.

^ fu. 4 Katika kitabu cha Ezekieli, jina “Israeli” linarejelea wakaaji wa Yuda na Yerusalemu.—Eze. 12:19, 22; 18:2; 21:2, 3.

^ fu. 7 Neno “wivu” linaonyesha jinsi Yehova anavyothamini uaminifu. Tunaweza kufikiria jinsi mume anavyokasirika na kuwa na wivu ikiwa mke wake anakosa kuwa mwaminifu. (Met. 6:34) Kama mume huyo, Yehova alikasirika Waisraeli walipokosa kuwa waaminifu kwa kuabudu sanamu. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema: “Wivu wa Mungu . . . unachochewa na utakatifu wake. Kwa kuwa yeye peke yake ndiye mtakatifu . . . , Hakubali ibada nyingine.”—Kut. 34:14.

^ fu. 11 Maneno ya Kiebrania yanayotafsiriwa kuwa “sanamu zinazochukiza” huenda yanahusiana na neno la Kiebrania “mavi” na yanatumiwa kuonyesha dharau.

^ fu. 13 Hakuna msingi hakika wa madai kwamba Tamuzi ni jina lingine la Nimrodi.