Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 6

“Sasa Mwisho Umekufikia”

“Sasa Mwisho Umekufikia”

EZEKIELI 7:3

WAZO KUU: Jinsi hukumu ya kinabii dhidi ya Yerusalemu​—ilivyotimizwa

1, 2. (a) Ezekieli alifanya matendo gani yenye kushangaza? (Tazama picha iliyo mwanzoni mwa sura hii.) (b) Matendo yake yalitabiri nini?

HABARI zinazohusu matendo ya nabii Ezekieli yasiyo ya kawaida zinaenea haraka sana miongoni mwa Wayahudi waliohamishwa wanaoishi katika nchi ya Babiloni. Kwa juma moja hivi, alikuwa ameketi akiwa ameduwaa na kunyamaza tu kati ya wahamishwa, lakini ghafla akasimama na kujifungia ndani. Sasa jirani zake wakimtazama kwa mshangao, nabii huyo anatoka nje, anachukua tofali na kuliweka mbele yake kisha anachonga mchoro juu yake. Halafu bila kusema chochote, Ezekieli anaanza kujenga ukuta mdogo.​—Eze. 3:10, 11, 15, 24-26; 4:1, 2.

2 Watazamaji ambao bila shaka wanazidi kuongezeka, lazima wanajiuliza, ‘Mambo haya yote yanamaanisha nini?’ Wayahudi hao walio uhamishoni wataelewa kikamili baadaye kwamba matendo hayo ya nabii Ezekieli yasiyo ya kawaida, yalitabiri tukio la kuogopesha ambalo lingeonyesha hasira ya uadilifu ya Yehova Mungu. Ni tukio gani hilo? Liliathirije taifa la kale la Israeli? Leo tukio hilo lina umuhimu gani kwa waabudu wa Yehova?

“Chukua Tofali . . . Uchukue Ngano . . . Chukua Upanga Mkali”

3, 4. (a) Ezekieli alionyesha mambo gani matatu kuhusu hukumu ya Mungu? (b) Ezekieli aliigizaje kuzingirwa kwa Yerusalemu?

3 Karibu mwaka wa 613 K.W.K., Yehova alimwamuru Ezekieli aonyeshe kwa ishara mambo matatu kuhusu hukumu ya Mungu iliyokuwa ikija dhidi ya Yerusalemu. Mambo hayo ni: kuzingirwa kwa jiji, kuteseka kwa wakaaji wake, na kuharibiwa kwa jiji na watu wake. * Acheni tuchunguze mambo hayo matatu kwa undani zaidi.

4 Kuzingirwa kwa Yerusalemu. Yehova alimwambia Ezekieli: “Chukua tofali na uliweke mbele yako. . . . Lizingire.” (Soma Ezekieli 4:1-3.) Tofali liliwakilisha jiji la Yerusalemu, na Ezekieli mwenyewe aliwakilisha jeshi la Wababiloni kama lilivyotumiwa na Yehova. Pia, Ezekieli aliamuriwa ajenge ukuta mdogo na boma la kuzingira na mitambo ya kubomolea. Kisha alipaswa kuweka vitu hivyo kulizunguka tofali. Viliwakilisha vifaa vya vita ambavyo maadui wa Yerusalemu wangetumia kulizunguka jiji na kulishambulia. Ili kuonyesha uimara ulio kama chuma wa wanajeshi wanaoshambulia, Ezekieli alitakiwa kuweka “kiokeo cha chuma,” au sahani kati yake na jiji. Kisha akaelekeza “uso [wake] dhidi” ya jiji. Matendo hayo yaliyoonyesha mashambulizi, yalikuwa “ishara kwa watu wa nyumba ya Israeli” kwamba jambo lisilowaziwa lingetokea hivi karibuni. Yehova angetumia jeshi la maadui kuzingira Yerusalemu, jiji kuu la watu wa Mungu, mahali ambapo hekalu la Mungu lilikuwa limejengwa!

5. Fafanua jinsi ambavyo Ezekieli alionyesha mambo ambayo yangewapata wakaaji wa Yerusalemu.

5 Kuteseka kwa wakaaji wa Yerusalemu. Yehova alimwamuru Ezekieli achukue: “Ngano, shayiri, maharagwe mapana, dengu, mtama, na kusemethi [aina ya ngano] . . . na [atengeneze] mkate,” kisha apime na “kula shekeli 20 za chakula kwa siku.” Pia, Yehova akafafanua hivi: “Nitafanya chakula kikosekane.” (Eze. 4:9-16) Katika kisa hiki, Ezekieli hawakilishi tena jeshi la Wababiloni badala yake aliwakilisha wakaaji wa Yerusalemu. Matendo ya nabii huyo yalionyesha kwamba kuzingirwa kulikotabiriwa kungesababisha upungufu wa chakula. Wakati huo, mkate ungetengenezwa kwa mchanganyiko usio wa kawaida, kumaanisha kwamba watu wangekula chochote ambacho wangepata. Njaa ingekuwa kali kadiri gani? Akiongea kana kwamba anazungumza moja kwa moja na wakaaji wa Yerusalemu, Ezekieli alisema: “Akina baba miongoni mwenu watawala wana wao, nao wana watawala baba zao.” Mwishowe wengi wangeteseka kwa sababu ya “mishale hatari ya njaa kali,” na watu ‘wangedhoofika.’—Eze. 4:17; 5:10, 16.

6. (a) Ezekieli aliwakilisha mambo gani mawili kwa wakati mmoja alipokuwa akiigiza? (b) Amri ya Mungu ya ‘kupima nywele na kuzigawa’ inamaanisha nini?

6 Kuharibiwa kwa Yerusalemu na watu wake. Katika sehemu hii ya unabii wa kuigiza, Ezekieli aliwakilisha mambo mawili kwa wakati mmoja. Kwanza, aliigiza jambo ambalo Yehova angefanya. Yehova alimwambia hivi Ezekieli: “Chukua upanga mkali ili uutumie kama wembe wa kinyozi.” (Soma Ezekieli 5:1, 2.) Mkono wa Ezekieli ulioshika upanga uliwakilisha mkono wa Yehova—hukumu ya Yehova—kama ilivyotekelezwa kupitia jeshi la Babiloni. Pili, Ezekieli aliigiza jambo ambalo lingewapata Wayahudi. Yehova alimwambia Ezekieli hivi: “Nyoa kichwa chako na ndevu zako.” Kunyolewa kwa kichwa cha Ezekieli kuliwakilisha jinsi ambavyo Wayahudi wangeshambuliwa na kuangamizwa. Pia, amri ya ‘kuzipima nywele hizo na kuzigawa katika mafungu’ kulimaanisha kwamba hukumu ya Yehova dhidi ya Yerusalemu haingetekelezwa ovyoovyo bali ingetekelezwa kwa makini na kikamili.

7. Kwa nini Yehova alimwambia Ezekieli azigawe nywele katika mafungu matatu na kulitendea kila fungu kwa njia tofauti?

 7 Kwa nini Yehova alimwambia Ezekieli azigawe nywele zake katika mafungu matatu na kulitendea kila fungu jambo tofauti? (Soma Ezekieli 5:7-12.) Ezekieli alichoma sehemu moja ya nywele “ndani ya jiji” kuwaonyesha watazamaji kwamba baadhi ya wakaaji wa Yerusalemu wangekufa jijini. Ezekieli aliipiga sehemu nyingine ya nywele kwa upanga “kulizunguka jiji pande zote” kuonyesha kwamba wakaaji wengine wangeuawa nje ya jiji. Aliitawanya hewani sehemu ya mwisho ya nywele kuonyesha kwamba bado wakaaji wengine wangetawanyika miongoni mwa mataifa, lakini “upanga” ‘ungewakimbiza.’ Hivyo, popote pale ambapo waokokaji hao wangeishi, hawangepata amani.

8. (a) Igizo la Ezekieli lilikuwa na ujumbe gani wa tumaini? (b) Unabii kuhusu “nywele chache” ulitimiaje?

8 Hata hivyo, Ezekieli alipotoa unabii kwa kuigiza, alitoa pia ujumbe wa tumaini. Kuhusu nywele ambazo Ezekieli alinyoa, Yehova alimwambia nabii huyo: “Utachukua nywele chache na kuzifunga katika pindo za vazi lako.” (Eze. 5:3) Amri hiyo ilionyesha kwamba Wayahudi wachache ambao wangetawanyika kati ya mataifa wangeokolewa. Baadhi ya “nywele [hizo] chache” zingekuwa kati ya wahamishwa ambao walirudi Yerusalemu baada ya kipindi kirefu cha miaka 70 utekwani Babiloni. (Eze. 6:8, 9; 11:17) Je, maneno hayo ya kinabii yalitimia? Ndiyo. Miaka mingi baada ya utekwa wa Wababiloni kwisha, nabii Hagai aliandika kwamba baadhi ya Wayahudi waliokuwa wametawanyika kwa kweli walirudi Yerusalemu. Walikuwa “wazee ambao walikuwa wameona ile nyumba ya kwanza,” yaani, hekalu la Sulemani. (Ezra 3:12; Hag. 2:1-3) Yehova alihakikisha kwamba ibada safi iliendelezwa kama tu alivyokuwa ameahidi. Sura ya 9 ya kitabu hiki, itazungumzia habari zaidi kuhusu kurudishwa huko.—Eze. 11:17-20.

Unabii Huo Unatufundisha Nini Kuhusu Wakati Ujao?

9, 10. Maigizo ya kinabii  ya Ezekieli yanatukumbusha matukio gani yaliyotabiriwa kuhusu wakati wetu ujao?

9 Matukio ambayo Ezekieli aliigiza yanatukumbusha matukio muhimu ambayo Neno la Mungu linatabiri kuhusu wakati wetu ujao. Ni nini baadhi ya matukio hayo? Kama ilivyokuwa kwa jiji la kale la Yerusalemu, Yehova atatumia mamlaka za kilimwengu kutekeleza jambo lisilowaziwa—kushambulia mashirika yote ya dini za uwongo duniani. (Ufu. 17:16-18) Kama vile kuharibiwa kwa Yerusalemu kulivyokuwa “msiba wa pekee,” ndivyo “dhiki kuu” pamoja na vita ya Har–Magedoni itakavyokuwa tukio ambalo ‘halijawahi kutokea.’—Eze. 5:9; 7:5; Mt. 24:21.

10 Neno la Mungu linaonyesha kwamba wafuasi mmoja-mmoja wa dini ya uwongo wataokoka dini za uwongo zitakapoharibiwa. Wakiwa na hofu, waokokaji hao wataungana na watu wengine watakaokuwa wakitafuta mahali pa kujificha. (Zek. 13:4-6; Ufu. 6:15-17) Hali yao inatukumbusha jambo lililowapata wakaaji wa Yerusalemu la kale ambao waliokoka lilipoharibiwa na kutawanyika “kwenye upepo.” Kama tulivyoona katika  fungu la 7, ingawa kwa muda fulani uhai wao uliokolewa, Yehova alichomoa “upanga ili kuwakimbiza.” (Eze. 5:2) Vivyo hivyo, mahali popote ambapo waokokaji wa shambulio dhidi ya dini huenda wakakimbilia hawatalindwa kutokana na upanga wa Yehova. Wakati wa Har–Magedoni, watauawa, pamoja na wale wote walio kama mbuzi.— Eze. 7:4; Mt. 25:33, 41, 46; Ufu. 19:15, 18.

Kuhusu kuhubiri habari njema, tutakuwa “bubu”

11, 12. (a) Kuelewa unabii wa Ezekieli kuhusu kuzingirwa kwa Yerusalemu kunaathirije maoni yetu kuhusu huduma leo? (b) Huenda kazi yetu ya kuhubiri na ujumbe wetu utabadilikaje?

11 Kuelewa unabii huu kunaathirije maoni yetu kuhusu huduma na jinsi inavyopaswa kutimizwa haraka? Kunatufundisha kwamba tunapaswa kuwa na bidii leo katika kuwasaidia watu wamtumikie Yehova. Kwa nini? Wakati uliobaki wa ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote’ ni mfupi. (Mt. 28:19, 20; Eze. 33:14-16) Wakati “fimbo” (mamlaka za kilimwengu) itakapoanza kushambulia dini, hatutahubiri tena ujumbe wa wokovu. (Eze. 7:10) Kuhusu kuhubiri habari njema, tutakuwa “bubu,” kama tu Ezekieli alivyokuwa bubu au alivyoacha kutangaza ujumbe wake pindi fulani wakati wa huduma yake. (Eze. 3:26, 27; 33:21, 22) Kwa njia ya mfano, baada ya dini ya uwongo kuharibiwa, watu wakiwa wamekata tamaa watajaribu ‘kutafuta maono kutoka kwa nabii,’ lakini hawatapata habari zozote za kuokoa uhai. (Eze. 7:26) Wakati wa kupata habari hizo na kuwa wanafunzi wa Kristo utakuwa umekwisha.

12 Hata hivyo, kazi yetu ya kuhubiri haitakoma. Kwa nini? Wakati wa dhiki kuu, huenda tutaanza kutangaza ujumbe wa hukumu utakaokuwa kama mvua ya mawe. Ujumbe huo utaonyesha wazi kwamba mwisho wa ulimwengu mwovu umefika.—Ufu. 16:21.

“Tazama, Inakuja!”

13. Kwa nini Yehova alimwambia Ezekieli alalie upande wake wa kushoto na kisha upande wa kulia?

13 Mbali na kutabiri jinsi ambavyo Yerusalemu lingeharibiwa, Ezekieli aliigiza pia wakati ambao lingeharibiwa. Ezekieli aliambiwa na Yehova alalie upande wake wa kushoto kwa siku 390 na upande wa kulia kwa siku 40. Kila siku moja iliwakilisha mwaka mmoja. (Soma Ezekieli 4:4-6; Hes. 14:34) Unabii huo ambao Ezekieli aliigiza kwa muda fulani tu kila siku, ulionyesha mwaka hususa ambao Yerusalemu lingeharibiwa. Bila shaka, miaka 390 ya makosa ya Waisraeli ilianza mwaka wa 997 K.W.K., mwaka ambao ufalme wa makabila 12 uligawanyika na kuwa sehemu mbili. (1 Fal. 12:12-20) Huenda dhambi ya Yuda ya miaka 40 ilianza mwaka wa 647 K.W.K., mwaka ambao Yeremia alipewa utume wa kuwa nabii ili kuonya ufalme wa Yuda, kupitia ujumbe ulio wazi, kuhusu uharibifu uliokuwa ukija. (Yer. 1:1, 2, 17-19; 19:3, 4) Kwa hiyo, vipindi vyote viwili vingekwisha mwaka wa 607 K.W.K., mwaka hususa ambao Yerusalemu lilianguka na kuharibiwa, kama tu Yehova alivyotabiri. *

Ezekieli alionyeshaje mwaka hususa wa kuharibiwa kwa Yerusalemu? (Tazama fungu la 13)

14. (a) Ezekieli alionyeshaje kwamba alikuwa na uhakika Yehova angechukua hatua wakati barabara? (b) Ni mambo gani yangetokea kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu?

14 Ezekieli alipopewa unabii kuhusu siku 390 na siku 40, huenda hakutambua mwaka hususa wa kuharibiwa kwa Yerusalemu. Hata hivyo, miaka iliyotangulia kuharibiwa kwa Yerusalemu, aliwaonya Wayahudi tena na tena kwamba hukumu ya Yehova ilikuwa inakuja. Alitangaza hivi: “Sasa mwisho umekufikia.” (Soma Ezekieli 7:3, 5-10.) Ezekieli hakuwa na shaka kwamba Yehova atachukua hatua wakati barabara. (Isa. 46:10) Pia, nabii huyo alitabiri matukio ambayo yangetokea kabla Yerusalemu halijaharibiwa: “Msiba utakuja juu ya msiba.” Matukio hayo yangesababisha kusambaratika kwa jamii, dini, na mifumo ya serikali.—Eze. 7:11-13, 25-27.

Kuzingirwa kwa Yerusalemu kulifananishwa na “chungu cha kupikia” kilichowekwa “motoni” (Tazama fungu la 15)

15. Ni sehemu gani za unabii wa Ezekieli zilizoanza kutimizwa kuanzia mwaka wa 609 K.W.K. na kuendelea?

15 Miaka michache baada ya Ezekieli kutangaza kuhusu kuanguka kwa Yerusalemu, unabii huo ulianza kutimia. Mwaka wa 609 K.W.K., Ezekieli alipata habari kwamba Yerusalemu limeanza kushambuliwa. Wakati huo, watu waliposikia mlio wa tarumbeta walikusanyika ili kulinda jiji lao, lakini kama Ezekieli alivyotabiri, ‘hakuna aliyeenda vitani.’ (Eze. 7:14) Wakaaji wa Yerusalemu hawakukusanyika ili kulinda jiji lao na kupigana na wavamizi Wababiloni. Huenda baadhi ya Wayahudi walidhani kwamba Yehova angewakomboa. Alikuwa amewakomboa wakati uliopita Waashuru walipotishia kuteka Yerusalemu na malaika wa Yehova akawaangamiza wanajeshi wengi Waashuru. (2 Fal. 19:32) Lakini wakati huu hawakupata msaada wowote kutoka kwa malaika. Baada ya muda mfupi, jiji hilo lililozingirwa lilifanana na “chungu cha kupikia” kilichowekwa “motoni,” na wakaaji wake walinaswa kama “vipande vya nyama” ndani ya chungu. (Eze. 24:1-10) Baada ya kipindi kigumu cha kuzingirwa kwa miezi 18, Yerusalemu liliharibiwa.

“Jiwekeeni Hazina Mbinguni”

16. Leo tunawezaje kuonyesha kwamba tunaamini Yehova atachukua hatua wakati barabara?

16 Tunajifunza nini kutokana na sehemu hii ya unabii wa Ezekieli? Je, inahusiana na huduma yetu na jinsi watu tunaowahubiria wanavyoitikia? Tayari Yehova ameamua wakati ambao dini ya uwongo itaharibiwa—hivi karibuni, kwa mara nyingine tena atachukua hatua wakati barabara. (2 Pet. 3:9, 10; Ufu. 7:1-3) Hatujui tarehe hususa ambayo jambo hilo litatokea. Hata hivyo, kama Ezekieli, tunaendelea kutii maagizo ya Yehova ya kuwaonya watu tena na tena, tukisema: ‘Sasa mwisho umewafikia.’ Kwa nini tunahitaji kurudia ujumbe huo? Ni sababu ileile iliyomfanya Ezekieli afanye hivyo. * Watu wengi ambao aliwatangazia unabii wa Mungu kuhusu kuanguka kwa Yerusalemu hawakuamini. (Eze. 12:27, 28) Lakini baadaye, baadhi ya Wayahudi waliokuwa uhamishoni Babiloni walisitawisha moyo unaopenda uadilifu, nao wakarudi katika nchi yao. (Isa. 49:8) Vivyo hivyo, watu wengi leo hawaamini kwamba ulimwengu utafikia mwisho. (2 Pet. 3:3, 4) Hata hivyo, kabla wakati wa wanadamu kukubali ujumbe wa Mungu haujakwisha, tunataka kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu waipate barabara inayoongoza kwenye uzima.—Mt. 7:13, 14; 2 Kor. 6:2.

Ingawa watu wengi hawasikilizi, tunaendelea kuwatafuta watu wenye mioyo minyoofu (Tazama fungu la 16)

Kwa nini wakaaji wa Yerusalemu la kale ‘walitupa fedha zao barabarani’? (Tazama fungu la 17)

17. Tutaona matukio na hali gani wakati wa dhiki kuu inayokuja?

17 Pia, unabii wa Ezekieli unatukumbusha kwamba shambulizi linalokuja dhidi ya mashirika ya kidini litakapotokea, wafuasi wa makanisa hawataenda “vitani” ili kutetea dini zao. Badala yake, watakapotambua kwamba kilio chao cha kuomba msaada, “Bwana, Bwana,” hakisikilizwi, ‘mikono yao italegea’ nao watakuwa ‘wakitetemeka.’ (Eze. 7:3, 14, 17, 18; Mt. 7:21-23) Watafanya nini kingine? (Soma Ezekieli 7:19-21.) Yehova anasema: “Watatupa fedha yao barabarani.” Maneno hayo yanayowahusu wakaaji wa Yerusalemu la kale, kwa kweli pia yanafafanua jambo ambalo litatukia wakati wa dhiki kuu. Wakati huo, watu watatambua kwamba pesa haziwezi kuwaokoa kutokana na msiba unaokuja.

18. Tunajifunza somo gani kutokana na unabii wa Ezekieli kuhusu mambo tunayopaswa kutanguliza?

18 Je, unatambua somo tunalojifunza katika sehemu hii ya unabii wa Ezekieli? Linahusu uhitaji wa kutanguliza mambo muhimu. Fikiria hali hii: Baada tu ya wakaaji wa Yerusalemu kuelewa kwamba mwisho wa jiji lao na uhai wao ulikuwa umefika, na kwamba vitu vya kimwili havingeweza kuwaokoa, ndipo walipobadili mambo waliyoyatanguliza. Walitupa mali zao na kuanza ‘kutatafuta maono kutoka kwa nabii’—lakini walikuwa wamechelewa. (Eze. 7:26) Tofauti nao, tayari tunajua kwamba mwisho wa ulimwengu huu mwovu umefika. Kwa hiyo, imani yetu katika ahadi za Mungu imetuchochea kutanguliza mambo muhimu maishani. Basi, tunatafuta kwa bidii utajiri wa kiroho, ambao una thamani ya kudumu na ambao hautatupwa kamwe “barabarani.”—Soma Mathayo 6:19-21, 24.

19. Tunachochewaje na unabii wa Ezekieli leo?

19 Kwa ufupi, maneno ya Ezekieli ya kinabii kuhusu kuanguka kwa Yerusalemu yanatuhusuje leo? Yanatukumbusha kwamba wakati uliobaki wa kuwasaidia wengine kuwa watumishi wa Mungu ni mfupi. Kwa hiyo, tunatimiza kazi ya kufanya wanafunzi kwa uharaka. Tunashangilia sana watu wenye mioyo minyoofu wanapoanza kumwabudu Baba yetu, Yehova. Hata hivyo, kwa wale ambao hawachukui hatua, tunaendelea kutoa onyo ambalo Ezekieli aliwapa watu wa siku zake: ‘Mwisho umewafikia.’ (Eze. 3:19, 21; 7:3) Wakati huohuo, tumeazimia kuendelea kumtegemea Yehova na kutanguliza ibada yake safi katika maisha yetu.—Zab. 52:7, 8; Met. 11:28; Mt. 6:33.

^ fu. 3 Ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba Ezekieli aliigiza ishara hizo zote mbele ya watazamaji. Kwa nini? Kwa sababu kuhusu baadhi ya maigizo, kama vile kuoka mkate na kubeba mizigo, Yehova alimwamuru kihususa Ezekieli afanye mambo hayo “mbele ya macho yao.”Eze. 4:12; 12:7.

^ fu. 13 Kwa kuruhusu Yerusalemu liharibiwe, Yehova alionyesha kwamba hukumu yake ilikuwa juu ya ufalme wa Yuda wenye makabila mawili, na pia ufalme wa Israeli wenye makabila kumi. (Yer. 11:17; Eze. 9:9, 10) Ona Insight on the Scriptures, Buku la 1, uku. 462, “Chronology—From 997 B.C.E. to Desolation of Jerusalem.

^ fu. 16 Kumbuka kwamba katika ujumbe mfupi unaopatikana kwenye Ezekieli 7:5-7, Yehova anatumia maneno “unakuja,” na “utakuja” mara tano.