Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 16

“Uyatie Alama Mapaji ya Nyuso”

“Uyatie Alama Mapaji ya Nyuso”

EZEKIELI 9:4

WAZO KUU: Jinsi watu waaminifu katika siku za Ezekieli walivyotiwa alama ya kuokoka na maana ya alama hiyo siku zetu

1-3. (a) Kwa nini Ezekieli anashangaa, na anatambua jambo gani kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu? (b) Tutachunguza maswali gani?

EZEKIELI anashangaa! Ametoka tu kuona katika maono mambo yenye kuchukiza ambayo Wayahudi walioasi imani wanafanya hekaluni huko Yerusalemu. * Waasi hao wamepachafua mahali ambapo pamekuwa kituo cha ibada safi katika Israeli. Lakini hawajachafua hekalu peke yake. Nchi ya Yuda imejaa ukatili na haiwezi kupona. Akiwa amekasirishwa sana na mambo ambayo watu wake waliochaguliwa wanafanya, Yehova anamwambia hivi Ezekieli: “Nitatenda kwa ghadhabu.”—Eze. 8:17, 18.

2 Ezekieli anaumia sana kujua kwamba Yehova ana ghadhabu dhidi ya Yerusalemu na hekalu lake ambalo wakati fulani lilikuwa takatifu na ataliangamiza hekalu na jiji hilo! Bila shaka, Ezekieli anajiuliza: ‘Namna gani watu waaminifu walio jijini? Je, wataokoka? Ikiwa ndivyo, jinsi gani?’ Ezekieli anapata jibu baada ya muda mfupi. Baada tu ya kusikia hukumu kali dhidi ya Yerusalemu, anasikia sauti kubwa ikiwaita watekelezaji wa hukumu ya Mungu. (Eze. 9:1) Maono hayo yanapoendelea, nabii huyo anatambua kwamba si watu wote watakaoangamizwa, jambo hilo linamfariji. Naam, watu wasio na hatia wataokoka!

3 Tunapokabili mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo, sisi pia huenda tukajiuliza ni nani watakaookoka uharibifu mkubwa unaokuja. Basi acheni tuchunguze mambo yafuatayo: (1) Ezekieli aliona nini kingine katika maono hayo? (2) Maono hayo yalitimizwaje katika siku zake? (3) Maono hayo ya kinabii yana maana gani siku zetu?

“Waiteni Wale Watakaoliadhibu Jiji”

4. Fafanua jambo lingine ambalo Ezekieli aliona na kusikia katika maono.

4 Ezekieli aliona na kusikia nini kingine katika maono hayo? (Soma Ezekieli 9:1-11.) Wanaume saba walitokea “kutoka upande wa lango la juu linalotazama kaskazini,” labda karibu na mahali ambapo ishara ya wivu ilikuwa au mahali ambapo wanawake walikuwa wakimlilia mungu Tamuzi. (Eze. 8:3, 14) Wanaume hao saba waliingia katika ua wa ndani wa hekalu na kusimama karibu na madhabahu ya shaba ya kutolea dhabihu. Lakini wanaume hao hawakuja kuleta dhabihu. Yehova hangekubali tena dhabihu zilizotolewa katika hekalu hilo. Wanaume sita kati yao walisimama “kila mmoja akiwa na silaha yake ya kuponda mkononi mwake.” Mwanamume wa saba alikuwa tofauti sana. Alikuwa amevalia kitani, na hakuwa na silaha, bali “kidau cha wino cha mwandishi” au, kulingana na maelezo ya chini “chombo cha kuwekea wino cha mwandishi.”

5, 6. Tunaweza kufikia mkataa gani kuhusu wale waliotiwa alama? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

5 Mwanamume aliyekuwa na kidau cha wino alipaswa kufanya nini? Alipokea mgawo mzito kutoka kwa Yehova mwenyewe: “Pita kotekote jijini, katika jiji lote la Yerusalemu, nawe uyatie alama mapaji ya nyuso za watu wanaolia kwa uchungu na kwa maumivu makali kwa sababu ya mambo yote yanayochukiza yanayofanywa jijini.” Labda wakati huohuo, Ezekieli aliwakumbuka wazazi waaminifu Waisraeli waliotia alama ya damu kwenye kizingiti cha juu cha milango yao kuwa ishara ili watoto wao wazaliwa wa kwanza waokoke uharibifu. (Kut. 12:7, 22, 23) Katika maono ya Ezekieli, je, alama iliyowekwa kwenye paji la uso na mwanamume aliyekuwa na kidau cha wino ingetimiza kusudi kama hilo la kuwa ishara kwamba yule aliyetiwa alama angeokoka kuharibiwa kwa Yerusalemu?

6 Tunapata jibu kwa kuchunguza kusudi la alama hiyo. Ilipaswa kuwekwa kwenye mapaji ya nyuso za wale waliokuwa “[wakilia] kwa uchungu na kwa maumivu makali” kwa sababu ya mambo yenye kuchukiza yaliyokuwa yakifanywa “jijini.” Basi tunafikia mkataa gani kuhusu wale waliotiwa alama? Jambo moja ni kwamba, walihuzunishwa sana moyoni si tu na ibada ya sanamu iliyokuwa ikifanywa hekaluni bali pia na ukatili, uasherati, na upotovu uliokuwa umejaa Yerusalemu. (Eze. 22:9-12) Isitoshe, huenda hawakuficha hisia zao. Bila shaka, maneno na matendo ya watu hao wanyoofu yalionyesha jinsi walivyochukizwa na mambo yaliyokuwa yakitendeka nchini na jinsi walivyopenda ibada safi. Kwa rehema, Yehova angewaokoa watu hao waaminifu.

7, 8. Wanaume waliokuwa na silaha za kuponda wangefanyaje kazi yao, na matokeo yalikuwaje?

7 Basi, wale wanaume sita wenye silaha za kuponda wangetimizaje kazi yao? Ezekieli alisikia maagizo ambayo Yehova aliwapa: Mfuateni mwanamume mwenye kidau cha wino na muue kila mtu isipokuwa mtu yeyote aliye na alama kwenye paji la uso. Yehova aliwaagiza hivi: “Mnapaswa kuanzia mahali pangu patakatifu.” (Eze. 9:6) Watekelezaji hao wa hukumu walipaswa kuanzia katikati ya Yerusalemu, katika hekalu, ambalo halikuwa tena takatifu mbele za Yehova. Kwanza, walipaswa kuwaua “wazee waliokuwa mbele ya ile nyumba”—wale wazee 70 wa Israeli waliokuwa hekaluni wakiifukizia uvumba miungu ya uwongo.—Eze. 8:11, 12; 9:6.

8 Matokeo yalikuwaje? Ezekieli alipoendelea kutazama na kusikiliza, mwanamume aliyekuwa na kidau cha wino alimpa Yehova ripoti hii: “Nimefanya kama ulivyoniamuru.” (Eze. 9:11) Huenda tukajiuliza: ‘Ni nini kilichowapata wakaaji wa Yerusalemu? Je, kuna watu waaminifu waliookoka uharibifu wa Yerusalemu?’

Maono Hayo Yalitimizwaje Katika Siku za Ezekieli?

9, 10. Taja baadhi ya watu waliookoka uharibifu wa Yerusalemu, na tunaweza kusema nini kuwahusu?

9 Soma 2 Mambo ya Nyakati 36:17-20. Unabii wa Ezekieli ulitimizwa mwaka wa 607 K.W.K. jeshi la Babiloni lilipoharibu Yerusalemu na hekalu lake. Wababiloni walikuwa kama ‘kikombe mkononi mwa Yehova,’ ambacho alikitumia kumwaga adhabu juu ya jiji la Yerusalemu lililokosa uaminifu. (Yer. 51:7) Je, kila mtu aliuawa? Hapana. Maono ya Ezekieli yalikuwa yametabiri kwamba baadhi ya watu hawangeuawa na Wababiloni.—Mwa. 18:22-33; 2 Pet. 2:9.

10 Watu waaminifu waliokoka, kutia ndani Warekabu, Ebed-meleki Mwethiopia, Nabii Yeremia, na Baruku, mwandishi wake. (Yer. 35:1-19; 39:15-18; 45:1-5) Kulingana na maono ya Ezekieli, tunaweza kusema kwamba watu hao walikuwa “[wakilia] kwa uchungu na kwa maumivu makali kwa sababu ya mambo yote yanayochukiza” yaliyokuwa yakifanywa Yerusalemu. (Eze. 9:4) Bila shaka, kabla ya uharibifu walionyesha kwamba walichukia kabisa uovu na kwamba waliipenda ibada safi, na hivyo wakapata fursa ya kuokolewa.

11. Ni nani wanaowakilishwa na wanaume sita wenye silaha za kuponda na mwanamume mwenye kidau cha wino cha mwandishi?

11 Je, watu hao waaminifu walitiwa alama halisi ya kuokoka? Hakuna rekodi yeyote inayoonyesha kwamba mtu yeyote—iwe ni Ezekieli au nabii mwingine—alipita Yerusalemu na kutia alama halisi kwenye mapaji ya nyuso za watu waaminifu. Basi, inaonekana maono ya kinabii ya Ezekieli yanafunua mambo yaliyokuwa yakitokea mbinguni na hivyo hayangeonekana kwa macho ya kibinadamu. Mwanamume mwenye kidau cha wino cha mwandishi na wanaume sita wenye silaha za kuponda walikuwa mifano ya kinabii ya viumbe waaminifu wa kiroho wa Yehova, ambao sikuzote wako tayari kufanya mapenzi yake. (Zab. 103:20, 21) Bila shaka, Yehova aliwatumia malaika wake kutekeleza hukumu dhidi ya jiji la Yerusalemu lililokosa uaminifu. Kwa kuweka alama ya mfano kwenye mapaji ya nyuso za wale ambao wangeokolewa, malaika walihakikisha kwamba baadhi ya watu wangeokoka.

Maono ya Ezekieli Yana Maana Gani Siku Zetu?

12, 13. (a) Kwa nini Yehova alimwaga hasira yake juu ya Yerusalemu, na kwa nini tutazamie jambo kama hilo leo? (b) Je, Yerusalemu lisilo na uaminifu linawakilisha dini zinazodai kuwa za Kikristo? Eleza. (Tazama sanduku “Je, Yerusalemu Linawakilisha Dini Zinazodai Kuwa za Kikristo?”)

12 Hivi karibuni, Mungu atatekeleza hukumu kwa njia ambayo haijawahi kutokea—“dhiki kuu ambayo haijawahi kutokea tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatokea tena.” (Mt. 24:21) Tunaposubiri tukio hilo la mwisho, tunabaki na maswali haya muhimu: Je, kuna watu watakaookoka uharibifu huo? Je, waabudu wa kweli wa Yehova watatiwa alama ya kuokoka? Kwa maneno mengine, je maono ya kinabii ya Ezekieli ya mwanamume mwenye kidau cha wino yanatimizwa siku zetu? Jibu la maswali hayo matatu ni ndiyo. Kwa nini tunasema hivyo? Ili kupata jibu acheni tuchunguze tena maono ya Ezekieli.

13 Je, unakumbuka sababu iliyofanya Yehova amwage hasira yake juu ya Yerusalemu la kale? Tusome tena Ezekieli 9:8, 9. (Soma.) Ezekieli alipokuwa na wasiwasi kwamba uharibifu unaokuja ungekuwa mwisho wa “Waisraeli wote wanaobaki,” Yehova alitaja sababu nne za kuleta hukumu hiyo. Kwanza, “kosa” la taifa hilo lilikuwa “kubwa sana, kubwa kwelikweli.” * Pili, nchi ya Yuda ilijaa “umwagaji wa damu.” Tatu, Yerusalemu, jiji kuu la ufalme wa Yuda, lilijaa “ufisadi.” Nne, watu walitenda uovu wakisingizia kwamba Yehova “haoni” matendo yao maovu. Je, maneno hayo hayaonyeshi jinsi ulimwengu wa leo ulivyopotoka kimaadili, ulivyojaa ukatili, ufisadi, na ukosefu wa imani? Kwa hakika, kwa kuwa Yehova “habadiliki au kugeuka,” mambo yaliyomkasirisha katika siku za Ezekieli yanamkasirisha pia hata katika siku zetu. (Yak. 1:17; Mal. 3:6) Basi, tunapaswa kutazamia kwamba wale wanaume sita wenye silaha za kuponda na mwanamume mwenye kidau cha wino watafanya kazi katika siku zetu!

Hivi karibuni wanaume sita wenye silaha za kuponda wataanza kazi (Tanzama fungu la 12 na 13)

14, 15. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Yehova huwaonya watu kabla ya kuleta uharibifu?

14 Hata hivyo, maono ya kinabii ya Ezekieli yanatimizwaje leo? Tunapochunguza jinsi maono hayo yalivyotimizwa wakati uliopita, tunaweza kutambua mambo tunayotazamia yatokee sasa na wakati ujao. Hebu chunguza baadhi ya mambo ambayo tumeona au tutakayoona yakitimiza unabii wa Ezekieli.

15 Yehova huwaonya watu kabla ya kuleta uharibifu. Kama tulivyoona katika Sura ya 11 ya kitabu hiki, Yehova alimwamuru Ezekieli awe “mlinzi wa watu wa nyumba ya Israeli.” (Eze. 3:17-19) Kuanzia mwaka wa 613 K.W.K., Ezekieli aliwaonya Waisraeli waziwazi kuhusu uharibifu uliokuwa karibu. Manabii wengine pia, kutia ndani Isaya na Yeremia, walionya pia kuhusu msiba ambao ungepata Yerusalemu. (Isa. 39:6, 7; Yer. 25:8, 9, 11) Katika siku zetu, Yehova, kupitia Kristo, ametumia kikundi kidogo cha watiwa mafuta kuwalisha waabudu wa kweli, yaani, watumishi wa nyumbani, na pia kuwaonya watu wengine kuhusu dhiki kuu iliyo karibu sana.—Mt. 24:45.

16. Je, tukiwa watu wa Yehova tunawatia alama wale watakaookoka? Eleza.

16 Watu wa Yehova hawawatii alama wale watakaookoka. Kumbuka kwamba Ezekieli hakuagizwa apite katikati ya Yerusalemu na kuwatia alama watu ambao wangeokoka. Vivyo hivyo, leo watu wa Yehova hawajaagizwa wawatie alama watu wanaostahili kuokoka. Badala yake, tukiwa watumishi katika nyumba ya kiroho ya Kristo, tumeagizwa tuhubiri. Tunaonyesha kwamba tunachukua kazi hiyo kwa uzito kwa kuhubiri kwa bidii kuhusu Ufalme wa Mungu na kutangaza kwa bidii onyo kwamba mwisho wa ulimwengu huu mwovu uko karibu sana. (Mt. 24:14; 28:18-20) Kwa hiyo, tunashiriki kuwasaidia watu wanyoofu wajiunge na ibada safi.—1 Tim. 4:16.

17. Watu wanahitaji kufanya nini sasa ili wakati ujao wastahili kutiwa alama ya kuokoka?

17 Ili watu waokoke uharibifu unaokuja, wanapaswa kuonyesha imani sasa. Kama tulivyoona, wale waliookoka Yerusalemu lilipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. walionyesha kabla ya uharibifu kwamba walichukia uovu na kwamba waliipenda ibada safi. Ndivyo ilivyo leo. Kabla ya mwisho kuja, watu wanahitaji kulia “kwa uchungu na kwa maumivu makali”—kuhuzunika sana—kwa sababu ya uovu ulio ulimwenguni. Badala ya kuficha hisia zao, wanapaswa kuonyesha kwa maneno na matendo kwamba wanaipenda ibada safi. Wanawezaje kufanya hivyo? Wanapaswa kusikiliza habari njema inayohubiriwa leo, waendelee kuvaa utu kama wa Kristo, wabatizwe ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova, na kuwaunga mkono kwa ushikamanifu ndugu za Kristo. (Eze. 9:4; Mt. 25:34-40; Efe. 4:22-24; 1 Pet. 3:21) Wale tu wanaofanya mambo hayo sasa—na ambao wataingia katika dhiki kuu wakiwa katika ibada safi—ndio watakaotiwa alama ya kuokoka.

18. (a) Yesu atawatia lini alama watu wanaostahili na atafanya hivyo jinsi gani? (b) Je, watiwa mafuta waaminifu wanahitaji kutiwa alama? Eleza.

18 Kutiwa alama kwa wale wanaostahili kutafanyiwa mbinguni. Katika siku za Ezekieli, malaika walikuwa na jukumu la kuwatia alama watu waaminifu ili waokoke. Katika utimizo wa siku zetu, mwanamume aliye na kidau cha wino cha mwandishi anawakilisha Yesu Kristo “atakapokuja katika utukufu wake” akiwa Hakimu wa mataifa yote. (Mt. 25:31-33) Yesu atakuja wakati wa dhiki kuu, baada ya dini ya uwongo kuharibiwa. * Katika kipindi hicho muhimu, kabla tu ya Har–Magedoni kuanza, Yesu atawahukumu watu kuwa kondoo au mbuzi. Washiriki wa “umati mkubwa” watahukumiwa, au kutiwa alama, ili kuonyesha kwamba wao ni kondoo, na basi “watapata uzima wa milele.” (Ufu. 7:9-14; Mt. 25:34-40, 46) Namna gani watiwa mafuta waaminifu? Hawahitaji kutiwa alama ya kuokoka Har–Magedoni. Badala yake, watatiwa muhuri wa mwisho kabla ya kufa au kabla ya dhiki kuu kuanza. Kisha, wakati fulani kabla ya Har–Magedoni kuanza, watainuliwa kwenda mbinguni.—Ufu. 7:1-3.

19. Ni nani watakaokuwa pamoja na Yesu atakapotekeleza hukumu dhidi ya mfumo huu wa mambo? (Tazama sanduku “Kulia kwa Uchungu na kwa Maumivu Makali, Kutiwa Alama, Kuponda​—Lini na Jinsi Gani?”)

19 Yesu Kristo, Mfalme aliye mbinguni, pamoja na jeshi lake la mbinguni watatekeleza hukumu dhidi ya mfumo huu wa mambo. Katika maono ya Ezekieli, wanaume sita wenye silaha za kuponda walianza kuharibu baada ya yule mwanamume aliyevalia kitani kumaliza kazi yake. (Eze. 9:4-7) Vivyo hivyo, uharibifu unaokuja utaanza baada ya Yesu kuhukumu watu wa mataifa yote na kuwatia kondoo alama ya kuokoka. Kisha, wakati wa vita vya Har–Magedoni, Yesu ataliongoza jeshi la kimbingu, ambalo litatia ndani malaika watakatifu na watawala wenzake wote 144,000, dhidi ya ulimwengu huu mwovu, atauharibu kabisa na kuwaingiza waabudu wa kweli katika ulimwengu mpya wenye uadilifu.—Ufu. 16:14-16; 19:11-21.

20. Tumejifunza masomo gani yenye kutia moyo kutokana na maono ya Ezekieli ya mwanamume mwenye kidau cha wino cha mwandishi?

20 Tunathamini sana masomo yenye kutia moyo tunayojifunza kutokana na maono ya Ezekieli kuhusu mwanamume mwenye kidau cha wino cha mwandishi! Tunaweza kuwa na hakika kabisa kwamba Yehova hatawaangamiza waadilifu pamoja na waovu. (Zab. 97:10) Tunajua mambo tunayopaswa kufanya sasa ili wakati ujao tutiwe alama ya kuokoka. Tukiwa waabudu wa Yehova, tumeazimia kushiriki kikamili zaidi kutangaza habari njema na kuwatolea onyo wale wanaolia kwa uchungu na kwa maumivu makali kwa sababu ya uovu ulio katika ulimwengu wa Shetani. Kwa kufanya hivyo, tunaweza kupata pendeleo la kuwasaidia watu wenye “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” wajiunge nasi katika ibada safi, na hivyo wapate fursa ya kutiwa alama ya kuokoka na kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu.—Mdo. 13:48.

^ fu. 1 Maono ya Ezekieli kuhusu mambo yenye kuchukiza yaliyokuwa yakifanywa hekaluni yanazungumziwa katika Sura ya 5 ya kitabu hiki.

^ fu. 13 Kulingana na kitabu kimoja cha marejezo, neno la Kiebrania “kosa” linaweza kuwa na maana ya “upotovu.” Kitabu kingine cha marejezo kinasema kwamba neno hilo “linahusiana hasa na dini, na karibu mara zote linatumiwa kuonyesha hatia ya kimaadili au dhambi mbele za Mungu.”

^ fu. 18 Inaonekana kwamba, kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa hakutamaanisha kwamba wafuasi wote wa dini ya uwongo watauawa. Wakati huo, huenda hata baadhi ya makasisi wataiacha dini ya uwongo na kudai kwamba hawakuwahi kujihusisha nayo.—Zek. 13:3-6.