Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 17

“Niko Dhidi Yako, Ewe Gogu”

“Niko Dhidi Yako, Ewe Gogu”

EZEKIELI 38:3

WAZO KUU: Ufafanuzi kuhusu “Gogu” na “nchi” anayovamia

1, 2. Hivi karibuni kutakuwa na vita gani kubwa, na tunaweza kujiuliza maswali gani kuvihusu? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

KWA maelfu ya miaka, dunia imejaa umwagaji wa damu kutokana na vita vya wanadamu, kutia ndani mauaji makubwa yaliyosababishwa na vita vya kwanza na vya pili vya ulimwengu katika karne ya 20. Lakini vita kubwa zaidi katika historia ya wanadamu vitatokea hivi karibuni. Hata hivyo, vita hivyo havitakuwa mgogoro wa wanadamu, yaani, mataifa kupigana kwa sababu za kibinafsi. Badala yake, vita hivyo vitakuwa “vita vya siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufu. 16:14) Adui mwenye kiburi atasababisha vita hivyo kwa kushambulia nchi yenye thamani machoni pa Mungu; shambulizi hilo litafanya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atumie nguvu zake kuleta uharibifu mkubwa zaidi kuwahi kutokea duniani.

2 Maswali fulani yanatokea: Adui huyo ni nani? Atashambulia nchi gani? Atashambulia nchi hiyo lini, jinsi gani, na kwa nini? Tunahitaji kujua majibu kwa sababu tukiwa waabudu wa kweli wa Yehova, tutahusika katika matukio hayo ya wakati ujao. Tunaweza kupata majibu kwa kuchunguza unabii wenye kusisimua katika Ezekieli sura ya 38 na 39.

Adui—Gogu wa Magogu

3. Elezea mambo makuu ya unabii wa Ezekieli kuhusu Gogu wa Magogu.

 3 Soma Ezekieli 38:1, 2, 8, 18; 39:4, 11. Haya ndiyo mambo makuu ya unabii huo: “Katika miaka ya mwisho,” adui anayeitwa “Gogu wa . . . Magogu” anashambulia “nchi” ya watu wa Mungu. Lakini shambulizi hilo kali litafanya ‘ghadhabu kali’ ya Yehova iwake, na Yehova ataingilia kati na kumshinda Gogu. * Baada ya kushinda, Yehova atamfanya adui huyo aliyeshindwa pamoja na walio pamoja naye wawe “chakula cha kila aina ya ndege wanaowinda na wanyama wa mwituni.” Mwishowe, Yehova atampa Gogu “kaburi.” Ili kuelewa jinsi unabii huo utakavyotimizwa hivi karibuni, kwanza tunahitaji kumjua Gogu.

4. Tunaweza kusema Gogu wa Magogu ni nani?

4 Basi, Gogu wa Magogu ni nani? Kutokana na maelezo ya Ezekieli, tunaweza kusema kwamba Gogu ni adui wa ibada safi. Je, Gogu ni jina la kinabii la Shetani—adui mkubwa zaidi wa ibada ya kweli? Kwa miaka mingi, machapisho yetu yalisema hivyo. Hata hivyo, baada ya kuchunguza zaidi unabii wa Ezekieli tulirekebisha uelewaji wetu. Gazeti la Mnara wa Mlinzi lilieleza kwamba jina Gogu wa Magogu halirejelei kiumbe wa roho asiyeonekana, bali adui wa kibinadamu anayeonekana, yaani, mataifa yatakayoungana ili kupinga ibada safi. * Kabla ya kuzungumzia kwa nini tunaamini hivyo, acheni kwanza tuchunguze mambo mawili katika unabii wa Ezekieli yanayoonyesha kwamba Gogu si kiumbe wa roho.

5, 6. Unabii wa Ezekieli unaonyeshaje kwamba Gogu wa Magogu si kiumbe wa roho?

5 “Nitakufanya uwe chakula cha kila aina ya ndege wanaowinda.” (Eze. 39:4) Mara nyingi Maandiko hutaja ndege wanaowinda wakila mzoga kama onyo kuhusu hukumu ya Mungu. Mungu alitoa maonyo kama hayo kwa taifa la Israeli na pia kwa mataifa mengine. (Kum. 28:26; Yer. 7:33; Eze. 29:3, 5) Hata hivyo, ona kwamba maonyo hayo hayakutolewa kwa viumbe wa roho, bali kwa wanadamu wenye nyama na damu. Wanyama wa mwituni na ndege wanaowinda hula nyama, na si roho. Basi onyo hilo la Mungu katika unabii wa Ezekieli linaonyesha kwamba Gogu si kiumbe wa roho.

6 “Nitampa Gogu kaburi katika Israeli.” (Eze. 39:11) Maandiko hayataji kwamba viumbe wa roho wanazikwa duniani. Badala yake, Shetani na roho wake waovu watatupwa katika shimo refu lisilo na mwisho kwa miaka 1,000, na baadaye watatupwa katika ziwa la moto la mfano, ikimaanisha wataharibiwa milele. (Luka 8:31; Ufu. 20:1-3, 10) Kwa kuwa inasemwa kwamba Gogu atapewa “kaburi” duniani, tunaweza kusema kwamba yeye si kiumbe wa roho.

7, 8. “Mfalme wa kaskazini” atafikia mwisho wake lini, na hilo linafananaje na jambo litakalompata Gogu wa Magogu?

7 Ikiwa yeye si kiumbe wa roho, basi Gogu, adui atakayefanya shambulizi la mwisho dhidi ya waabudu wa kweli ni nani au ni nini? Acheni tuzungumzie mambo mawili katika unabii wa Biblia yanayotusaidia kumtambua Gogu wa Magogu.

8 “Mfalme wa kaskazini.” (Soma Danieli 11:40-45.) Danieli alitabiri jinsi ambavyo serikali za ulimwengu zingetokea kuanzia siku zake mpaka wakati wetu. Unabii huo unataja pia serikali zinazopingana—“mfalme wa kusini” na “mfalme wa kaskazini”—kwa karne nyingi kila serikali imekuwa ikibadilika mataifa mbalimbali ya dunia yanapopigania mamlaka. Kuhusu shambulizi la mwisho la mfalme wa kaskazini “wakati wa mwisho,” Danieli alisema: “Naye atatoka kwa hasira kali ili kuwaangamiza na kuwaua wengi.” Mfalme wa kaskazini atawashambulia hasa waabudu wa Yehova. * Lakini kama Gogu wa Magogu, mfalme wa kaskazini atafikia “mwisho wake” baada ya kushindwa atakapowashambulia watu wa Mungu.

9. Kuna ulinganifu gani kati ya jambo linalompata Gogu wa Magogu na jambo linalowapata “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa”?

9 “Wafalme wa dunia nzima inayokaliwa.” (Soma Ufunuo 16:14, 16; 17:14; 19:19, 20.) Kitabu cha Ufunuo kilitabiri shambulizi la “wafalme wa dunia” dhidi ya “Mfalme wa wafalme,” Yesu aliye mbinguni. Kwa kuwa hawawezi kufika mbinguni, waasi hao wanawashambulia raia wa Ufalme huo hapa duniani. Wafalme wa dunia wanashindwa katika vita hivyo wakati wa Har–Magedoni. Ona kwamba wanafikia mwisho wao baada ya kuwashambulia watu wa Yehova. Hilo linafanana na jambo linalosemwa kumhusu Gogu wa Magogu. *

10. Tunaweza kusema Gogu wa Magogu ni nani?

10 Baada ya kuchunguza mambo hayo, tunaweza kusema Gogu ni nani? Kwanza, Gogu si kiumbe wa roho. Pili, Gogu ni mataifa yaliyo duniani ambayo yatawashambulia watu wa Mungu hivi karibuni. Bila shaka, mataifa hayo yatafanyiza muungano. Kwa nini? Kwa kuwa watu wa Mungu wako duniani kote, mataifa hayo yatahitaji kuwa na kusudi moja ili kuwashambulia. (Mt. 24:9) Hata hivyo, Shetani ndiye atakayepanga shambulizi hilo. Kwa muda mrefu amechochea mataifa duniani kupinga ibada ya kweli. (1 Yoh. 5:19; Ufu. 12:17) Lakini unabii wa Ezekieli kuhusu Gogu wa Magogu unakazia jukumu la mataifa yaliyo duniani ambayo yatawashambulia watu wa Mungu. *

Ni “Nchi” Gani Itakayoshambuliwa?

11. Unabii wa Ezekieli unafafanuaje “nchi” ambayo Gogu ataishambulia?

11 Kama tulivyozungumzia kwenye  fungu la 3, Gogu wa Magogu ataamsha ghadhabu kali ya Yehova kwa kushambulia nchi yenye thamani machoni pa Yehova. Hiyo ni nchi gani? Acheni tuchunguze tena unabii wa Ezekieli. (Soma Ezekieli 38:8-12.) Tunasoma kwamba Gogu ataishambulia “nchi ambayo watu wake wamerudishwa” na kukusanywa “pamoja kutoka katika mataifa.” Ona pia jambo linalosemwa kuhusu waabudu hao waliorudishwa wanaokaa katika nchi hiyo: “Wanakaa kwa usalama”; makazi yao ni “vijiji visivyolindwa na ukuta, makomeo, au malango”; na “wanajikusanyia utajiri.” Hiyo ndiyo nchi ambayo waabudu wa kweli wa Yehova duniani kote wanakaa. Tunawezaje kuitambua?

12. Ni kurudishwa gani kulikotokea katika nchi ya Israeli nyakati za Biblia?

12 Inafaa tuchunguze kurudishwa kwa ibada safi katika Israeli la kale, nchi ambamo kwa karne nyingi watu wa Mungu waliochaguliwa waliishi, walifanya kazi, na kuabudu. Waisraeli walipokosa kuwa waaminifu, Yehova alitabiri kupitia Ezekieli kwamba nchi yao ingeharibiwa na kuachwa ukiwa. (Eze. 33:27-29) Lakini Yehova alitabiri pia kwamba watu wachache wangerudi kutoka uhamishoni Babiloni na kurudisha ibada safi katika nchi hiyo. Kupitia baraka za Yehova, nchi ya Israeli ingebadilika, ingesitawi “kama bustani ya Edeni.” (Eze. 36:34-36) Hilo lilitokea kuanzia mwaka wa 537 K.W.K. wahamishwa Wayahudi waliporudi Yerusalemu na kurudisha ibada safi katika nchi yao waliyoipenda.

13, 14. (a) Nchi ya kiroho ni nini? (b) Kwa nini nchi hiyo ni yenye thamani machoni pa Yehova?

13 Katika nyakati zetu, waabudu wa kweli wa Mungu waliona kurudishwa kama huko. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 9 ya kitabu hiki, mwaka wa 1919, watu wa Mungu walikuwa wamewekwa huru baada ya kuwa utekwani kwa muda mrefu katika Babiloni Mkubwa. Mwaka huo, Yehova aliwaleta waabudu wake waliorudishwa katika nchi ya kiroho. Nchi hiyo ni paradiso ya kiroho—mazingira salama yenye ufanisi wa kiroho, au mahali pa utendaji ambapo tunamwabudu Mungu wa kweli. Tunakaa katika nchi hiyo pamoja kwa usalama, tukiwa na amani ya akilini na moyoni. (Met. 1:33) Tunapokea chakula kingi cha kiroho, na tuna kazi nyingi yenye kuridhisha katika kutangaza Ufalme wa Mungu. Kwa kweli, tunaona ukweli wa methali hii: “Baraka ya Yehova ndiyo inayomtajirisha mtu, naye haichanganyi na maumivu.” (Met. 10:22) Popote tunapoishi duniani, tunakaa katika nchi hiyo—paradiso ya kiroho—maadamu tu tunaunga mkono kwa bidii ibada safi kwa maneno na matendo.

14 Nchi hii ya kiroho ni yenye thamani machoni pa Yehova. Kwa nini? Machoni pake, wakaaji wake ni “vitu vyenye thamani vya mataifa yote,” watu ambao amewavuta wajiunge na ibada safi. (Hag. 2:7; Yoh. 6:44) Wanajitahidi kuvaa utu mpya, unaopatana na viwango vya juu vya Mungu. (Efe. 4:23, 24; 5:1, 2) Wakiwa waabudu wa kweli, wanajitoa kikamili katika utumishi wake, wakifanya hivyo kwa njia zinazomletea sifa na kuonyesha kwamba wanampenda. (Rom. 12:1, 2; 1 Yoh. 5:3) Tunaweza kuwazia jinsi Yehova anavyopata shangwe nyingi anapoona waabudu wake wakijitahidi kurembesha nchi hiyo ya kiroho. Fikiria jambo hili: Unapotanguliza ibada ya kweli maishani, unarembesha paradiso ya kiroho na pia unafanya moyo wa Yehova ushangilie!—Met. 27:11.

Hata iwe tunaishi wapi, tuko katika nchi ya kiroho maadamu tunaunga mkono ibada safi kwa bidii (Tazama fungu la 13 na 14)

Gogu Ataishambulia Nchi Hiyo Lini, Kwa Nini, na Jinsi Gani?

15, 16. Gogu wa Magogu atashambulia lini nchi yetu ya kiroho iliyorudishwa?

15 Tunapaswa kukumbuka kwamba hivi karibuni muungano wa mataifa duniani utashambulia nchi yetu ya kiroho yenye thamani. Kwa kuwa sisi waabudu wa kweli wa Yehova tutahusika katika shambulizi hilo lililotabiriwa, tungependa kujua mengi kulihusu. Chunguza maswali matatu yanayojitokeza.

16 Gogu wa Magogu atashambulia lini nchi yetu ya kiroho iliyorudishwa? Unabii huo unajibu hivi: “Katika miaka ya mwisho utaishambulia nchi [hiyo].” (Eze. 38:8) Hilo linamaanisha kipindi kilicho karibu na mwisho wa mfumo huu wa mambo. Kumbuka kwamba dhiki kuu itaanza na kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo. Baada ya mashirika ya dini ya uwongo kuharibiwa na kabla ya Har–Magedoni kuanza, Gogu atafanya shambulizi kali la mwisho dhidi ya waabudu wa kweli.

17, 18. Yehova ataongozaje mambo wakati wa dhiki kuu?

17 Kwa nini Gogu atashambulia nchi iliyorudishwa ya waabudu wa kweli wa Yehova? Unabii wa Ezekieli unafunua mambo mawili—kwanza, jinsi Yehova atakavyoongoza mambo, na pili, nia mbaya ya Gogu.

18 Jinsi Yehova atakavyoongoza mambo. (Soma Ezekieli 38:4, 16.) Ona jambo ambalo Yehova anamwambia Gogu: “[Nitatia] kulabu katika mataya yako” na, “nitakuleta uishambulie nchi yangu.” Je, maneno hayo yanamaanisha kwamba Yehova atayalazimisha mataifa kuwashambulia waabudu wake? Hapana! Hawezi kamwe kufanya watu wake wapatwe na mambo maovu. (Ayu. 34:12) Lakini Yehova anawajua adui zake—kwamba watawachukia waabudu wa kweli na hawatakosa kutumia fursa ya kujaribu kuwaangamiza kabisa. (1 Yoh. 3:13) Yehova atatia kulabu katika mataya ya Gogu na kumwongoza kwa njia ya mfano, kwa kufanya mambo yatukie kulingana na mapenzi Yake na ratiba Yake. Muda fulani baada ya kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa, huenda Yehova atayashawishi mataifa kutekeleza jambo ambalo tayari liko moyoni mwao. Hivyo, Yehova ataandaa hali itakayotokeza shambulizi la mwisho litakaloongoza kwenye Har–Magedoni, vita vikubwa zaidi duniani. Kisha atawakomboa watu wake, atatukuza enzi yake kuu, na kulitakasa jina lake takatifu.—Eze. 38:23.

Mataifa yatajaribu kuipora ibada safi kwa sababu wanaichukia na pia wanawachukia wale wanaoiendeleza

19. Ni nini kitakachomchochea Gogu ajaribu kuipora ibada ya kweli?

19 Nia mbaya ya Gogu. Mataifa yatapanga “njama ya uovu.” Watamwaga ghadhabu yao na chuki yao ya muda mrefu juu ya waabudu wa Yehova, ambao wataonekana kana kwamba wanaishi katika “vijiji visivyolindwa na ukuta, makomeo, au malango.” Mataifa yatatamani pia “kupora na kuchukua nyara nyingi” kutoka kwa wale “ambao wanajikusanyia utajiri.” (Eze. 38:10-12) Ni “utajiri” gani? Watu wa Yehova wana utajiri mwingi wa kiroho; mali yetu yenye thamani zaidi ni ibada yetu safi, ambayo tunamtolea Yehova peke yake. Mataifa yatajaribu kuipora ibada safi, si kwa sababu wanaiona kuwa yenye thamani, bali kwa sababu wanaichukia na pia wanawachukia wale wanaoiendeleza.

Gogu atapanga “njama ya uovu” ya kuangamiza ibada safi lakini njama hiyo itashindwa (Tazama fungu la 19)

20. Gogu atashambuliaje nchi ya kiroho, au paradiso ya kiroho?

20 Gogu ataishambuliaje nchi hiyo ya kiroho, au paradiso ya kiroho? Huenda mataifa yatajaribu kuvuruga maisha yetu na kutuzuia kuabudu. Ili kufanya hivyo, labda watajaribu kuzuia kusambazwa kwa chakula cha kiroho, watajaribu kutuzuia kukutana, watajaribu kuvunja umoja tulio nao, na kujaribu kutuzuia kuhubiri kwa bidii ujumbe wa Mungu. Mambo hayo yote ni sehemu ya paradiso ya kiroho. Shetani atayashawishi mataifa yajaribu kuwaangamiza waabudu wa kweli—pamoja na ibada safi—duniani.

21. Kwa nini unashukuru kwamba Yehova ametuonya kuhusu jambo litakalotokea hivi karibuni?

21 Shambulizi linalokuja la Gogu wa Magogu litawaathiri waabudu wote wa kweli katika nchi ya kiroho waliyopewa na Mungu. Tunashukuru sana kwa sababu Yehova ametuonya kuhusu jambo litakalotokea hivi karibuni! Sasa, tunaposubiri dhiki kuu, acheni tuazimie kuunga mkono ibada safi na kuitanguliza maishani mwetu. Kwa kufanya hivyo, tutachangia kurembesha nchi iliyorudishwa. Na tutakuwa na tumaini la kujionea jambo hili la kustaajabisha hivi karibuni: Jinsi Yehova atakavyowapigania watu wake na jina lake takatifu katika Har–Magedoni, kama tutakavyoona katika sura inayofuata.

^ fu. 3 Katika sura inayofuata ya kitabu hiki, tutazungumzia ghadhabu kali ya Yehova itawaka lini na jinsi gani dhidi ya Gogu wa Magogu na maana ya jambo hilo kwa waabudu wa kweli.

^ fu. 4 Tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2015, uku. 29-30.

^ fu. 8 Andiko la Danieli 11:45 linaonyesha kwamba mfalme wa kaskazini atawashambulia watu wa Mungu, linasema mfalme huyo “atapiga mahema yake ya kifalme kati ya bahari kuu [Mediterania] na mlima mtakatifu wa lile Pambo [mahali lilipokuwa hekalu la Mungu na ambamo watu wa Mungu waliabudu].”

^ fu. 9 Biblia inazungumzia pia shambulizi la “Mwashuru” wa siku zetu ambaye atajaribu kuwaangamiza watu wa Mungu. (Mik. 5:5) Huenda mashambulizi manne yaliyotabiriwa kuwapata watu wa Mungu—shambulizi la Gogu wa Magogu, la mfalme wa kaskazini, la wafalme wa dunia, na la Mwashuru—yanarejelea kwa majina tofauti shambulizi lilelile.

^ fu. 10 Tazama Sura ya 22 ya kitabu hiki ili upate maelezo kuhusu kumtambulisha “Gogu na Magogu” anayetajwa katika Ufunuo 20:7-9.