Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 15

“Nitakomesha Ukahaba Wako”

“Nitakomesha Ukahaba Wako”

EZEKIELI 16:41

WAZO KUU: Mambo tunayojifunza kutokana na ufafanuzi wa makahaba katika Ezekieli na Ufunuo

1, 2. Huenda hasa tukachukizwa na kahaba wa aina gani?

INAHUZUNISHA kumwona kahaba. Huenda tukajiuliza, nini kinachomfanya aishi maisha hayo ya aibu? Je, alianza ukahaba akiwa na umri mdogo kwa sababu ya kutendewa kikatili au kunyanyaswa nyumbani? Au je, alilazimika kujiuza kwa sababu ya umaskini? Au je, alikuwa anamkimbia mume wake mkatili? Mambo hayo yenye kuhuzunisha hutokea mara nyingi katika ulimwengu huu mwovu. Basi haishangazi kwamba Yesu Kristo aliwatendea kwa fadhili baadhi ya makahaba. Alikazia kwamba wale waliotubu na kubadili maisha yao wangekuwa na tumaini la kuwa na maisha bora.—Mt. 21:28-32; Luka 7:36-50.

2 Hata hivyo, acheni tuzungumzie kahaba wa aina nyingine. Mwazie mwanamke ambaye anachagua maisha hayo kwa kupenda. Haoni maisha hayo kuwa ya aibu bali yenye kuheshimika! Anatamani kupata pesa na umashuhuri kutokana na kazi hiyo. Isitoshe, namna gani ikiwa mwanamke huyo alikuwa na mume mzuri na mshikamanifu lakini akaamua kumsaliti kimakusudi ili awe kahaba? Tunachukizwa na mwanamke huyo na maisha aliyochagua kuishi. Hisia kali tunazohisi ndiyo sababu kuu inayomfanya Yehova Mungu atumie tena na tena mfano wa kahaba kuonyesha jinsi anavyohisi kuhusu ibada ya uwongo.

3. Tutazungumzia masimulizi gani katika sura hii?

3 Kitabu cha Ezekieli kina masimulizi mawili ambayo yanatumia mfano wa makahaba kufafanua ukosefu mwingi wa uaminifu wa watu wa Mungu katika Israeli na Yuda. (Eze., sura ya 16 na 23) Hata hivyo, kabla hatujachunguza kwa undani masimulizi hayo, acheni tuzungumzie kahaba mwingine wa mfano. Alianza ukahaba muda mrefu kabla ya siku za Ezekieli—hata kabla ya taifa la Israeli kuanzishwa—na bado anaendelea leo. Kahaba huyo anatambulishwa katika Ufunuo, kitabu cha mwisho cha Biblia.

“Mama wa Makahaba”

4, 5. “Babiloni Mkubwa,” ni nani na tunajuaje hivyo? (Ona picha mwanzoni mwa sura hii.)

4 Katika maono ambayo Yesu alimpa mtume Yohana mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., Yohana alimwona kahaba huyo waziwazi. Anaitwa “kahaba mkubwa” na “Babiloni Mkubwa, mama wa makahaba.” (Ufu. 17:1, 5) Kwa karne nyingi, viongozi wa kidini na wasomi wa Biblia wameshindwa kumtambua. Wana maoni mbalimbali, wanasema kwamba anawakilisha Babiloni, Roma, au Kanisa Katoliki. Hata hivyo, kwa miaka mingi Mashahidi wa Yehova wamemtambua “kahaba [huyo] mkubwa.” Ni milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo. Tunajuaje hivyo?

5 Kahaba huyo ana hatia ya kufanya uasherati na “wafalme wa dunia,” au mamlaka za kisiasa. Basi, ni wazi kwamba yeye si mamlaka ya kisiasa. Isitoshe, kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba “wafanyabiashara wa dunia” au mfumo wa kibiashara wa ulimwengu huu, unaomboleza kifo cha Babiloni Mkubwa. Basi Babiloni Mkubwa hawakilishi mfumo wa kibiashara. Basi, yeye ni nani? Ana hatia ya ‘mazoea ya kuwasiliana na roho,’ hatia ya ibada ya sanamu, na kusema uwongo. Kwa kweli, mashirika ya kidini yaliyopotoka ya ulimwengu huu yana hatia kama hiyo, sivyo? Pia, ona kwamba kahaba huyo anaonyeshwa akiwa juu ya mnyama, au akiwa na uvutano fulani juu ya mamlaka za kisiasa za ulimwengu huu. Pia, anawatesa watumishi waaminifu wa Yehova Mungu. (Ufu. 17:2, 3; 18:11, 23, 24) Dini ya uwongo imeendelea kufanya hivyo, hadi leo, sivyo?

Babeli la kale, ambalo baadaye liliitwa Babiloni, lilitokeza kila aina ya mazoea, mafundisho, na mashirika ya dini ya uwongo (Tazama Fungu la 6)

6. Kwa nini Babiloni Mkubwa ni “mama wa makahaba”?

6 Hata hivyo, kwa nini Babiloni Mkubwa anaitwa “kahaba mkubwa” na pia “mama wa makahaba”? Dini ya uwongo imegawanyika sana. Kuna vikundi na madhehebu mengi sana. Tangu lugha zilipovurugwa katika Babeli, au Babiloni la kale, mafundisho mengi ya uwongo ya kidini yameenezwa kila mahali na kutokeza dini nyingi sana. Inafaa kwamba “Babiloni Mkubwa” alipata jina kutokana na jiji la Babiloni, chanzo cha dini za uwongo! (Mwa. 11:1-9) Hivyo, dini hizo zote zinaweza kuitwa “mabinti” wa shirika moja, kahaba mmoja mkubwa. Mara nyingi Shetani hutumia dini hizo kuwadanganya watu wawasiliane na roho, waabudu sanamu, na kuwa na itikadi na mazoea yanayomvunjia Mungu heshima. Ndiyo sababu watu wa Mungu wanaonywa hivi kuhusu shirika hilo la ulimwenguni pote lililopotoka: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake”!—Soma Ufunuo 18:4, 5.

7. Kwa nini tunapaswa kutii onyo la ‘kutoka’ katika Babiloni Mkubwa?

7 Je, umetii onyo hilo? Kumbuka kwamba Yehova ndiye aliyewaumba wanadamu wakiwa na ‘uhitaji wa kiroho.’ (Mt. 5:3) Uhitaji huo unaweza kutoshelezwa vizuri kupitia tu ibada safi ya Yehova. Watumishi wa Yehova wanaepuka kabisa ukahaba wa kiroho. Lakini Shetani Ibilisi ana lengo tofauti. Angependa kuwadanganya watu wa Mungu waingie katika mtego huo wa ukahaba. Mara nyingi amefaulu. Katika siku za Ezekieli, watu wa Mungu walikuwa wamejihusisha na ukahaba wa kiroho kwa muda mrefu. Acheni tuchunguze jambo hilo, kwa maana linaweza kutufundisha mengi kuhusu viwango vya Yehova, haki, na rehema yake.

“Nawe Ukawa Kahaba”

8-10. Ni takwa gani muhimu la ibada safi linalotusaidia kuelewa hisia za Yehova kuhusu kujihusisha na dini ya uwongo? Fafanua.

8 Katika kitabu cha Ezekieli, Yehova anatumia mfano wa kahaba kueleza hisia zake. Ezekieli aliongozwa na roho kuandika masimulizi mawili yaliyo wazi yanayoonyesha jinsi Yehova alivyohisi uchungu na alivyosalitiwa na watu wake waliokosa kuwa washikamanifu na wakafanya uasherati. Kwa nini aliwalinganisha na kahaba?

9 Ili kupata jibu, tunapaswa kukumbuka jambo muhimu kuhusu ibada safi ambalo tulizungumzia katika Sura ya 5 ya kitabu hiki. Katika Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli, alisema: “Usiwe na miungu mingine yoyote ila mimi [au “na kuniasi mimi,” maelezo ya chini]. . . . mimi, Yehova Mungu wako, ni Mungu ninayetaka watu waniabudu mimi peke yangu.” (Kut. 20:3, 5) Baadaye alikazia hivi ukweli huohuo: “Msimwinamie mungu mwingine, kwa sababu mimi Yehova ninajulikana kuwa Mungu ninayetaka watu waniabudu mimi peke yangu. Naam, mimi ni Mungu ninayetaka watu waniabudu mimi peke yangu.” (Kut. 34:14) Yehova alieleza jambo hilo waziwazi kabisa. Hatuwezi kumwabudu Yehova kwa njia inayokubalika ikiwa hatutamwabudu yeye peke yake.

10 Tunaweza kutumia mfano wa ndoa. Mume na mke wana haki ya kutazamia kutendewa kwa njia ya pekee. Mwenzi mmoja akimwonyesha mapenzi mtu mwingine nje ya ndoa au kufanya ngono naye, mwenzi wake atakuwa na haki ya kuwa na wivu na kuhisi amesalitiwa. (Soma Waebrania 13:4.) Vivyo hivyo, kuhusu ibada, Yehova anahisi amesalitiwa na watu wake waliojiweka wakfu kwake, ikiwa wataabudu miungu ya uwongo. Anaeleza hisia zake za kusalitiwa kwa maneno mazito katika Ezekieli sura ya 16.

11. Yehova alisimulia nini kuhusu Yerusalemu na asili yake?

11 Ezekieli sura ya 16 ina mazungumzo marefu zaidi ya Yehova katika kitabu cha Ezekieli—na ni mojawapo ya unabii wake mrefu zaidi katika Maandiko yote ya Kiebrania. Yehova anakazia jiji la Yerusalemu kana kwamba linawakilisha Yuda. Anasimulia hadithi yenye kusikitisha na kushtua kuhusu asili ya jiji la Yerusalemu na jinsi lilivyomsaliti. Lilianza kama mtoto mchanga, asiye safi na asiye na mtu wa kumtunza. Wazazi wake walikuwa Wakanaani wapagani katika nchi hiyo. Kwa muda mrefu, Yerusalemu lilitawaliwa na kabila la Wakanaani, Wayebusi, hadi Daudi alipoliteka jiji hilo. Yehova alimhurumia mtoto huyo, akamsafisha na kumtunza. Baadaye, akawa kama mke wake. Kwa kweli, Waisraeli ambao baadaye waliishi katika jiji hilo walikuwa wamefanya agano pamoja na Yehova, agano ambalo walifanya kwa hiari katika siku za Musa. (Kut. 24:7, 8) Baada ya Yerusalemu kuwa jiji kuu la nchi hiyo, Yehova alilibariki, akalipa utajiri, na kulipamba, kama vile mume tajiri na mwenye uwezo anavyomnunulia mke wake mapambo maridadi.—Eze. 16:1-14.

Sulemani aliruhusu wake zake wa kigeni wamshinikize kuchafua Yerusalemu kwa ibada ya sanamu (Tazama Fungu la 12)

12. Ukosefu wa ushikamanifu uliingiaje katika jiji la Yerusalemu?

12 Ona jambo lililotokea. Yehova alisema: “Ulianza kuutumaini urembo wako, nawe ukawa kahaba kwa sababu ya sifa zako. Ulimmwagia kila mpita-njia matendo yako ya ukahaba, na urembo wako ukawa wake.” (Eze. 16:15) Katika siku za Sulemani, Yehova aliwabariki na kuwatajirisha watu wake hivi kwamba Yerusalemu likawa jiji lenye fahari zaidi, jiji la kipekee katika siku hizo. (1 Fal. 10:23, 27) Lakini wakaanza kukosa ushikamanifu. Sulemani alitamani kuwapendeza wake zake wengi wa kigeni, basi, akaanza kuchafua Yerusalemu kwa ibada ya miungu ya kipagani. (1 Fal. 11:1-8) Na baadhi ya wafalme waliotawala baada yake walifanya mambo mabaya hata zaidi, waliichafua nchi yote kwa ibada ya sanamu. Yehova alihisije kuhusu matendo hayo ya ukahaba na kusalitiwa? Alisema: “Mambo hayo hayapaswi kufanywa, wala hayapaswi kutendeka kamwe.” (Eze. 16:16) Lakini watu wake walioasi walizidi kupotoka!

Baadhi ya Waisraeli waliwatoa watoto wao dhabihu kwa miungu ya uwongo, kama vile Moleki

13. Watu wa Mungu huko Yerusalemu walikuwa na hatia ya kutenda uovu gani?

13 Wazia jinsi Yehova alivyohisi uchungu na kuchukizwa alipofunua uovu wa watu wake waliochaguliwa: “Uliwachukua wana na mabinti wako uliokuwa umenizalia, nawe ukawatoa dhabihu kwa sanamu hizo ili waangamizwe—je, matendo yako ya ukahaba hayajatosha? Uliwachinja wanangu, nawe ukawatoa wawe dhabihu kwa kuwateketeza motoni.” (Eze. 16:20, 21) Mambo hayo yenye kutisha yanafunua jinsi Shetani alivyo mwovu. Angependa sana kuwadanganya watu wa Yehova wafanye mambo hayo yenye kuchukiza! Lakini Yehova anaona kila jambo. Mungu anaweza kuondoa hata madhara ya uovu mkubwa zaidi wa Shetani, na atatekeleza haki.—Soma Ayubu 34:24.

14. Katika mfano ambao Yehova alitoa, ni nani waliokuwa dada wawili wa Yerusalemu, na kati yao watatu ni yupi aliyekuwa mwovu zaidi?

14 Hata hivyo, Yerusalemu hakuchukizwa na uovu wake mwenyewe. Aliendelea na ukahaba. Yehova alisema kwamba hata alitenda kwa aibu kuliko makahaba wengine kwa sababu aliwalipa watu ili wafanye uasherati naye! (Eze. 16:34) Mungu alisema kwamba Yerusalemu lilikuwa kama “mama” yake, yaani, makabila ya kipagani yaliyoishi katika nchi hiyo zamani. (Eze. 16:44, 45) Akiendelea na mfano wa familia, alisema kwamba dada mkubwa wa Yerusalemu alikuwa Samaria, aliyemtangulia kuingia katika ukahaba wa kiroho. Mungu alimtaja pia dada yake wa pili, Sodoma. Alimtaja kwa njia ya mfano kwa kuwa muda mrefu ulikuwa umepita tangu alipoharibiwa kwa sababu ya kiburi na uovu mwingi. Yehova alimaanisha kwamba Yerusalemu alikuwa mwovu kuliko dada zake wawili, Samaria na Sodoma! (Eze. 16:46-50) Watu wa Mungu walipuuza maonyo mengi na wakaendelea kuasi.

15. Yehova alikuwa na kusudi gani alipotekeleza hukumu dhidi ya Yerusalemu, na alitoa tumaini gani?

15 Yehova angefanya nini? Alimwahidi hivi Yerusalemu: “Ninawakusanya pamoja wapenzi wote ambao umewapa raha” na, “nitakutia mikononi mwao.” Marafiki wa kipagani wa watu wake wangeliangamiza Yerusalemu na kuuondoa urembo na mali zake. Alisema: “Watakupiga mawe na kukuchinja kwa panga zao.” Yehova alikuwa na kusudi gani alipotekeleza hukumu hiyo? Hakutaka kuwaangamiza watu wake. Badala yake, alisema: “Nitakomesha ukahaba wako.” Mungu aliongezea kusema: “Nitaitosheleza ghadhabu yangu dhidi yako, na hasira yangu itakuacha; nami nitatulia na sitaendelea kukasirika.” Kama ilivyozungumziwa katika Sura ya 9 ya kitabu hiki, kusudi la kudumu la Yehova lilikuwa kuwarudisha watu wake kutoka uhamishoni. Kwa nini? Alisema: “Mimi mwenyewe nitalikumbuka agano nililofanya pamoja nawe katika siku za ujana wako.” (Eze. 16:37-42, 60) Tofauti na watu wake, Yehova angethibitika kuwa mshikamanifu kabisa!—Soma Ufunuo 15:4.

16, 17. (a) Kwa nini hatusemi tena kwamba Ohola na Oholiba wanawakilisha dini zinazodai kuwa za Kikristo? (Tazama sanduku “Dada Waliokuwa Makahaba.”) (b) Tunaweza kujifunza masomo gani muhimu kutokana na Ezekieli sura ya 16 na 23?

16 Mazungumzo marefu na yenye uzito ya Yehova yaliyo katika Ezekieli sura ya 16 yanatufundisha mengi kuhusu viwango vyake vya uadilifu, haki yake, na rehema zake nyingi. Tunaweza kusema hivyo pia kuhusu Ezekieli sura ya 23. Leo, Wakristo wa kweli wanachukua kwa uzito ujumbe wa Yehova ulio wazi kuhusu ukahaba wa watu wake. Hatungependa kamwe kumuumiza Yehova kama Yuda na Yerusalemu walivyofanya! Basi tunapaswa kuepuka kila aina ya ibada ya sanamu. Hilo linatia ndani pupa na kupenda vitu vya kimwili, ambayo ni aina ya ibada ya sanamu. (Mt. 6:24; Kol. 3:5) Tungependa kuendelea kumshukuru Yehova kwa sababu kwa rehema amerudisha ibada safi katika siku hizi za mwisho na hataruhusu tena kamwe ichafuliwe! Amefanya “agano la kudumu” pamoja na Israeli wa kiroho, na halitavunjwa kamwe kwa sababu ya kukosa ushikamanifu au ukahaba. (Eze. 16:60) Basi acheni tuthamini pendeleo tulilo nalo leo la kushirikiana na watu wa Yehova walio safi.

17 Hata hivyo, mazungumzo ya Yehova dhidi ya makahaba wanaoelezwa katika kitabu cha Ezekieli yanatufundisha nini kuhusu yule “kahaba mkubwa,” yaani, Babiloni Mkubwa? Acheni tuone.

“Naye Hatapatikana Tena”

18, 19. Kuna ulinganifu gani kati ya makahaba wanaofafanuliwa katika Ezekieli na kahaba anayefafanuliwa katika Ufunuo?

18 Yehova habadiliki. (Yak. 1:17) Maoni yake kuhusu dini ya uwongo hayajabadilika tangu ukahaba wa kiroho ulipoanza. Basi haishangazi kuona ulinganifu mwingi kati ya hukumu yake dhidi ya makahaba katika kitabu cha Ezekieli na hukumu dhidi ya “kahaba mkubwa” anayefafanuliwa katika kitabu cha Ufunuo.

19 Kwa mfano, ona kwamba makahaba katika kitabu cha Ezekieli hawaadhibiwi moja kwa moja na Yehova, bali wanaadhibiwa na mataifa ambayo watu wa Mungu wasio washikamanifu walifanya uasherati wa kiroho nayo. Vivyo hivyo, milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo ina hatia ya kufanya uasherati kama huo na “wafalme wa dunia.” Ni nani anayemwadhibu? Tunasoma kwamba watawala hao wa kisiasa “watamchukia yule kahaba na kumfanya kuwa ukiwa na uchi, nao watakula nyama yake na kumteketeza kabisa kwa moto.” Kwa nini serikali za ulimwengu huu zitachukua hatua hiyo ya kushangaza? Kwa sababu Mungu atalitia “hilo ndani ya mioyo yao ili kutekeleza wazo lake.”—Ufu. 17:1-3, 15-17.

20. Ni nini kinachoonyesha kwamba hukumu dhidi ya Babiloni itakuwa ya mwisho?

20 Basi Yehova atatumia mataifa ya ulimwengu huu kutekeleza hukumu yake dhidi ya dini zote za uwongo, kutia ndani dini zinazodai kuwa za Kikristo. Hiyo itakuwa hukumu ya mwisho; hakutakuwa na msamaha, hakutakuwa na fursa nyingine za dini ya uwongo kubadilika. Kitabu cha Ufunuo kinafunua kwamba Babiloni “hatapatikana tena.” (Ufu. 18:21) Malaika wa Mungu watashangilia kifo chake, wakisema: “Msifuni Yah! Na moshi kutoka kwake unaendelea kupanda milele na milele.” (Ufu. 19:3) Hukumu hiyo itakumbukwa milele na milele. Dini yoyote ya uwongo haitaruhusiwa kamwe kuinuka tena na kupotosha ibada safi. Kwa njia ya mfano, moshi wa hukumu ya moto na kuharibiwa kwa Babiloni utaendelea kupanda milele.

Mataifa ambayo Babiloni Mkubwa ameyashawishi kwa muda mrefu yatamgeukia na kumwangamiza (Tazama Fungu la 19, 20)

21. Kuharibiwa kwa dini ya uwongo kutakuwa mwanzo wa kipindi gani, na mwisho wa kipindi hicho utakuwaje?

21 Serikali za ulimwengu zitakapogeuka na kumshambulia Babiloni Mkubwa, zitakuwa zikitekeleza hukumu ya Mungu, hilo ni tukio muhimu katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Huo utakuwa mwanzo wa dhiki kuu, kipindi cha taabu ambayo haijawahi kutokea. (Mt. 24:21) Dhiki hiyo itaishia kwenye Har–Magedoni, vita vya Yehova dhidi ya mfumo huu mwovu wa mambo. (Ufu. 16:14, 16) Kama sura zinazofuata katika kitabu hiki zinavyoonyesha, kitabu cha Ezekieli kinatueleza mengi kuhusu jinsi dhiki kuu itakavyotokea. Hata hivyo, tungependa kukumbuka na kutumia masomo gani kutokana na Ezekieli sura ya 16 na 23?

Serikali za ulimwengu zitashambulia Babiloni Mkubwa, ili kutekeleza hukumu ya Mungu (Tazama Fungu la 21)

22, 23. Kuchunguza ufafanuzi wa makahaba katika Ezekieli na Ufunuo kunapaswa kutuchochea tufanye nini katika utumishi wetu mtakatifu?

22 Shetani angependa kuwapotosha watu walio katika ibada safi. Angependa sana kutuondoa kwenye ibada safi ili tuishi maisha kama ya makahaba wanaofafanuliwa katika kitabu cha Ezekieli. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova havumilii ushindani wowote, hapendi ukosefu wa ushikamanifu! (Hes. 25:11) Tunakuwa waangalifu ili tuepuke kabisa dini ya uwongo, hatugusi “kitu chochote kichafu” machoni pa Mungu. (Isa. 52:11) Vivyo hivyo, tunaendelea kuwa washikamanifu kwa kutounga mkono upande wowote inapohusu mizozo ya kisiasa na migogoro ya ulimwengu huu uliogawanyika. (Yoh. 15:19) Tunaona utaifa kuwa aina ya dini ambayo Shetani anaendeleza, nasi hatujihusishi nayo.

23 Zaidi ya yote, acheni tuendelee kuthamini pendeleo letu la kumwabudu Yehova katika hekalu lake la kiroho lililo safi na takatifu. Huku tukithamini mpango huo mtakatifu, acheni tuazimie kuepuka kabisa dini ya uwongo na ukahaba wake!