Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 47

Jinsi Tunavyoweza Kujua Har-magedoni Imekaribia

Jinsi Tunavyoweza Kujua Har-magedoni Imekaribia

UNAJUA ishara ni nini, sivyo?— Katika Sura ya 46 tulisoma kuhusu ishara ambayo Mungu alitoa kuonyesha kwamba hataharibu dunia kwa gharika tena. Pia, mitume walitaka ishara ya kuwaonyesha wakati Yesu angerudi na ya mwisho wa ulimwengu.—Mathayo 24:3.

Kwa sababu Yesu yuko mbinguni na haonekani, watu wanahitaji ishara wanayoweza kuona ili kujua kwamba ameanza kutawala. Kwa hiyo Yesu alitaja mambo ambayo wanafunzi wake wanapaswa kutazamia hapa duniani. Wakati mambo hayo yangetokea, ingemaanisha kwamba amerudi na ameanza kutawala akiwa Mfalme.

Ili kuwafundisha wanafunzi wake umuhimu wa kuwa macho, Yesu aliwaambia: “Angalieni mtini na miti mingine yote: Wakati inapokuwa tayari imechipuka, kwa kuangalia mnajua wenyewe kwamba sasa kiangazi kiko karibu.” Unaweza kujua wakati kiangazi kinakaribia. Na unaweza kujua Har-Magedoni ikaribiapo unapoona mambo ambayo Yesu alizungumzia yakitendeka.—Luka 21:29, 30.

Yesu alifunza somo gani alipozungumzia mtini?

Kwenye ukurasa huu na ule unaofuata, tutatazama picha za mambo ambayo Yesu alisema yangekuwa sehemu ya ishara kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia. Kama tulivyosoma katika Sura ya 46, baada ya mambo hayo yote kutokea, Kristo akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu ataharibu serikali nyingine zote.

Basi tazama kwa makini picha zilizo kwenye kurasa mbili zilizotangulia huu, kisha tutazizungumzia. Unaweza kusoma kuhusu yale unayoona katika picha hizi kwenye Mathayo 24:6-14 na Luka 21:9-11. Pia kila picha ina namba ndogo. Namba iyo hiyo pia inaonyeshwa mwanzoni mwa fungu linalozungumzia picha yenyewe. Sasa tuone kama sehemu nyingi za ishara ambayo Yesu alitoa zinatimizwa leo.

(1) Yesu alisema: “Mtasikia juu ya vita na habari za vita; . . . taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” Je, umesikia habari za vita?— Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilipiganwa kuanzia mwaka wa 1914 hadi 1918, na Vita ya Pili ya Ulimwengu kuanzia mwaka wa 1939 hadi 1945. Kabla ya wakati huo, vita ya ulimwengu haikuwahi kutokea. Sasa kuna vita ulimwenguni pote. Yaelekea kila siku kwenye televisheni, redio, na magazetini, tunasikia au kusoma kuhusu vita.

(2) Yesu alisema pia: “Kutakuwa na upungufu wa chakula . . . mahali pamoja baada ya pengine.” Kama ujuavyo si kila mtu ana chakula cha kutosha. Kila siku maelfu ya watu hufa kwa sababu ya kukosa chakula cha kutosha.

(3) Yesu aliongezea: “Mahali pamoja baada ya pengine kutakuwa na tauni.” Je, unajua tauni?— Ni magonjwa ambayo yanasababisha vifo vya watu wengi. Ugonjwa mmoja wa tauni unaoitwa homa ya Hispania ulisababisha vifo vya watu milioni 20 hivi kwa muda wa mwaka mmoja hivi. Wakati huu, inaelekea watu zaidi ya milioni 20 watakufa kutokana na ugonjwa wa UKIMWI. Pia kuna kansa, maradhi ya moyo, na magonjwa mengine yanayosababisha maelfu ya vifo vya watu kila mwaka.

(4) Yesu alitaja sehemu nyingine ya ishara ile aliposema: “Kutakuwa na . . . matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine.” Tetemeko la dunia ni nini?— Matetemeko ya dunia hufanya ardhi itikisike. Nyumba huanguka na mara nyingi watu hufa. Tangu mwaka wa 1914, kumekuwa na matetemeko mengi ya dunia kila mwaka. Je, umewahi kusikia kuhusu matetemeko ya dunia?—

(5) Yesu alisema kwamba sehemu nyingine ya ishara hiyo ingekuwa ‘kuongezeka kwa maovu.’ Hiyo ndiyo sababu kuna wizi na ujeuri mwingi. Kila mahali watu wana hofu kwamba huenda nyumba zao zikavunjwa na vitu vyao kuibwa. Hakujawahi kuwa na uhalifu na ujeuri mwingi ulimwenguni pote kama ulivyo leo.

(6) Yesu alitaja sehemu muhimu ya ishara hiyo aliposema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Iwapo unaamini “habari njema,” unapaswa kuwaambia wengine juu yake. Kwa kufanya hivyo utashiriki kutimiza sehemu hiyo ya ishara.

Watu wengine wanaweza kusema kwamba mambo ambayo Yesu alisema yamekuwa yakitendeka kila wakati. Lakini mambo hayo hayajawahi kutendeka yote kwa wakati mmoja katika sehemu nyingi ulimwenguni. Je, unaelewa maana ya ishara hiyo?— Inamaanisha kwamba tuonapo mambo hayo yakitendeka, tujue kwamba karibuni ulimwengu mpya wa Mungu utaondolea mbali ulimwengu huu mwovu.

Yesu alipotaja ishara hiyo, alitaja pia majira ya pekee ya mwaka. Alisema: “Endeleeni kusali kwamba kukimbia kwenu kusiwe wakati wa majira ya baridi kali.” (Mathayo 24:20) Unafikiri alimaanisha nini aliposema hivyo?—

Itakuwaje mtu akitaka kutoroka hatari wakati wa baridi kali, wakati hali ya hewa ni mbaya sana au inafanya iwe hatari kusafiri?— Akiokoka, atakuwa amepitia magumu mengi. Je, si jambo la kusikitisha mtu akifa katika dhoruba yenye baridi kali kwa sababu alijishughulisha na mambo mengine tu badala ya kuanza safari mapema?—

Yesu alifunza somo gani alipozungumzia kukimbia wakati wa baridi kali?

Je, unaelewa alilomaanisha Yesu aliposema tusingojee mpaka wakati wa majira ya baridi kali ili tukimbie?— Alimaanisha kwamba kwa sababu tunajua Har-Magedoni inakaribia, tusikawie kuchukua hatua inayothibitisha kwamba tunampenda Mungu kwa kumtumikia. Tukisita-sita huenda tusiweze kumtumikia Yehova. Na tukifanya hivyo tutakuwa kama wale waliomsikiliza Noa wakati wa Gharika lakini wakakosa kuingia ndani ya safina.

Hebu sasa tuone jinsi hali itakavyokuwa baada ya vita kuu ya Har-Magedoni. Tutajifunza yale ambayo Mungu ametutayarishia sote tunaompenda na kumtumikia leo.

Yafuatayo ni maandiko mengine yanayoonyesha kwamba Har-Magedoni imekaribia: 2 Timotheo 3:1-5 na 2 Petro 3:3, 4.