Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 5

“Huyu Ni Mwanangu”

“Huyu Ni Mwanangu”

WATOTO wanapofanya mambo mazuri, wale wanaowatunza wanafurahi. Msichana anapofanya vizuri, baba yake anafurahi kuwaambia wengine hivi: “Huyu ni binti yangu.” Au mvulana akifanya vizuri, baba yake anafurahi kusema: “Huyu ni mwanangu.”

Kila wakati Yesu hufanya mambo ambayo yanampendeza Baba yake. Kwa hiyo, Baba yake anampenda. Siku moja Yesu alipokuwa na wanafunzi wake watatu, unakumbuka Baba yake alifanya nini?— Ndiyo, Mungu alizungumza kutoka kule mbinguni na kuwaambia: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” —Mathayo 17:5.

Yesu anafurahia kila wakati kufanya mambo ambayo yanampendeza Baba yake. Unajua ni kwa nini? Kwa sababu anampenda Baba yake sana. Mtu akifanya mambo kwa sababu tu analazimika kuyafanya, hatafurahia kuyafanya. Lakini ikiwa anayafanya kwa hiari, inakuwa rahisi zaidi. Je, unajua maana ya hiari?— Inamaanisha kutaka kufanya jambo.

Hata kabla ya Yesu kuja duniani, alikuwa tayari kufanya chochote ambacho Baba yake angemwambia. Hii ni kwa sababu anampenda Baba yake, Yehova Mungu. Yesu alikuwa na cheo cha pekee alipokuwa mbinguni pamoja na Baba yake. Lakini Mungu alitaka Yesu afanye kazi ya pekee. Ili kufanya kazi hiyo, ilikuwa lazima Yesu atoke mbinguni, azaliwe akiwa mtoto duniani. Yeye alikuwa tayari kufanya kazi hiyo kwa sababu Yehova alitaka aifanye.

Malaika Gabrieli alimwambia nini Maria?

Ili azaliwe duniani akiwa mtoto, Yesu alihitaji mama. Unajua mama yake?— Ni Maria. Yehova alimtuma malaika Gabrieli kutoka mbinguni ili azungumze na Maria. Gabrieli alimwambia kwamba atazaa mwana. Mtoto huyo ataitwa Yesu. Na baba yake angekuwa nani? Malaika alisema kwamba Baba yake angekuwa Yehova Mungu. Hiyo ndiyo sababu Yesu angeitwa Mwana wa Mungu.

Unafikiri Maria alisikiaje alipoambiwa maneno hayo?— Je, alisema, “Sitaki kuwa mama ya Yesu”? La, Maria alikuwa tayari kufanya mapenzi ya Mungu. Lakini Mwana wa Mungu aliyeishi mbinguni angezaliwaje akiwa mtoto hapa duniani? Je, unajua ni kwa nini kuzaliwa kwa Yesu ni tofauti na kuzaliwa kwa watoto wengine? —

Mungu aliwaumba wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, kwa njia ya kwamba wangeweza kuungana kwa njia ya kipekee. Baadaye, mtoto angeweza kukua ndani ya tumbo la mama. Watu wanasema kwamba huo ni muujiza! Nina hakika hata wewe unakubali, sivyo?

Mungu alifanya muujiza mkubwa hata zaidi. Alichukua uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni na kuuweka ndani ya tumbo la Maria. Mungu hakupata kufanya hivyo wakati mwingine, wala hajapata kufanya hivyo tena. Baada ya kufanya muujiza huo, Yesu alianza kukua ndani ya tumbo la Maria kama vile watoto wengine wanavyokua ndani ya tumbo. Baadaye, Maria aliolewa na Yosefu.

Ilipofika wakati wa Yesu kuzaliwa, Maria na Yosefu walikuwa wametembelea mji wa Bethlehemu. Lakini mji huo ulijaa watu wengi sana. Maria na Yosefu hata hawakupata mahali pa kukaa, basi wakalazimika kukaa katika zizi la wanyama. Akiwa hapo Maria akamzaa Yesu, akamweka katika hori, kama unavyoona katika picha hii. Hori ni kitu kinachotumiwa kuwalisha ng’ombe au wanyama wengineo.

Kwa nini Yesu anawekwa katika hori?

Mambo ya kupendeza yalitokea usiku ule Yesu alizaliwa. Karibu na Bethlehemu, malaika aliwatokea wachungaji fulani. Akawaambia kwamba Yesu ni mtu wa maana sana. Malaika akasema: ‘Tazama! ninawatangazia habari njema itakayowafurahisha. Leo amezaliwa mtu atakayewaokoa wanadamu.’ —Luka 2:10, 11.

Mmoja wa malaika hawa aliwaambia wachungaji habari gani njema?

Malaika aliwaambia wachungaji kwamba wangempata Yesu huko Bethlehemu akiwa amelala katika hori. Kisha, kwa ghafula malaika wengine wakajiunga na yule wa kwanza kumsifu Mungu. Malaika hao waliimba hivi: ‘Utukufu kwa Mungu, na juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.’ —Luka 2:12-14.

Malaika walipoondoka, wachungaji wale walienda Bethlehemu na kumpata Yesu huko. Wakawaambia Yosefu na Maria mambo mazuri waliyokuwa wamesikia. Hebu fikiria jinsi Maria alivyofurahi kwamba alikubali kuwa mama ya Yesu!

Baadaye, Yosefu na Maria walimpeleka Yesu katika mji wa Nazareti. Yesu akakulia huko. Alipokuwa mkubwa, alianza kazi yake kubwa ya kufundisha. Hii ilikuwa sehemu ya kazi ambayo Yehova Mungu alitaka Mwana wake aifanye duniani. Yesu alikuwa tayari kufanya kazi hiyo kwa sababu alimpenda sana Baba yake wa mbinguni.

Kabla ya Yesu kuanza kazi yake akiwa Mwalimu Mkuu, Yohana Mbatizaji alimbatiza katika Mto Yordani. Kisha jambo la ajabu likatokea! Yesu alipokuwa akiinuka kutoka majini, Yehova alizungumza kutoka mbinguni, akasema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Unafurahi sana wazazi wako wanapokuambia kwamba wanakupenda, sivyo?— Tuna hakika kwamba Yesu alifurahi pia.

Kila wakati Yesu alifanya mema. Yeye hakujipendekeza kuwa na cheo ambacho si chake. Hakusema yeye ni Mungu. Malaika Gabrieli alimwambia Maria kwamba Yesu ataitwa Mwana wa Mungu. Yesu mwenyewe alisema kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. Na hakusema kwamba anajua mengi kuliko Baba yake. Yeye alisema: “Baba ni mkuu kuliko mimi.” —Yohana 14:28.

Hata akiwa mbinguni, Yesu alifanya kazi aliyopewa na Baba yake. Yeye hakusema kwamba ataifanya na badala yake, akafanya jambo lingine. Alimpenda Baba yake. Kwa hiyo alisikiliza kile ambacho Baba yake anasema. Halafu alipokuja duniani, alifanya kazi ambayo Baba yake wa mbinguni alimtuma afanye. Hakufanya mambo mengine badala yake. Hiyo ndiyo sababu Yehova anampenda Mwana wake.

Sisi pia tunataka kumfurahisha Yehova, sivyo?— Basi ni lazima tumsikilize Mungu kama Yesu alivyomsikiliza. Mungu anazungumza nasi kupitia Biblia. Si vizuri kujifanya tunamsikiliza Mungu na huku tunaamini na kufanya mambo yanayopingana na Biblia, sivyo?— Kumbuka pia kwamba tutafurahi kumpendeza Yehova ikiwa kwa kweli tunampenda.

Sasa soma haya Maandiko mengine yanayoonyesha tunachohitaji kujua na kuamini kuhusu Yesu: Mathayo 7:21-23; Yohana 4:25, 26; na 1 Timotheo 2:5, 6