Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 40

Jinsi ya Kumfurahisha Mungu

Jinsi ya Kumfurahisha Mungu

TUNAWEZA kufanya nini kumfurahisha Mungu? Je, tunaweza kumpa chochote?— Yehova anasema: “Kila mnyama wa mwituni ni wangu.” Anasema pia: “Fedha ni yangu, na dhahabu ni yangu.” (Zaburi 24:1; 50:10; Hagai 2:8) Hata hivyo kuna kitu tunachoweza kumpa Mungu. Ni kitu gani?—

Yehova huturuhusu tuchague kama tutamtumikia au la. Hatulazimishi tufanye yale anayotaka. Hebu tujaribu kuelewa ni kwa nini Mungu alituumba na uhuru wa kuchagua kama tutamtumikia au la.

Huenda unajua mashine ambazo hutumiwa kufanya kazi. Mashine hizo hufanya tu yale ambayo wenye kuzitengeneza hutaka zifanye. Kwa hiyo haziwezi kujichagulia jambo la kufanya. Kama Yehova angetaka, angetuumba sisi sote kama mashine. Angetuumba ili tufanye tu yale ambayo anataka. Lakini Mungu hakufanya hivyo. Unajua ni kwa nini?—Ni kweli kwamba vitu vingine vya kuchezea ni kama mashine. Vinapobonyezwa, vinafanya tu yale ambayo aliyevitengeneza alivipangia. Umewahi kuona kitu kama hicho?— Mara nyingi watu huchoka kucheza na kitu ambacho kinaweza kufanya tu yale ambayo mwenye kukitengeneza alikipangia. Mungu hataki tumtii kwa kulazimishwa. Yehova anataka tumtumikie kwa sababu tunampenda na tunataka kumtii.

Kwa nini Mungu hakutuumba kama mashine hii?

Unafikiri Baba yetu wa mbinguni anahisije tunapomtii kwa kupenda?— Hebu niambie, tabia yako hufanya wazazi wako wahisije?— Biblia inasema kwamba mwana mwenye hekima ‘humfurahisha babake’ bali mwana mpumbavu “ni huzuni ya mama yake.” (Mithali 10:1) Je, umeona kwamba unawafurahisha baba na mama unapofanya kile ambacho wanakuambia?— Lakini wanahisije unapokosa kuwatii?—

Unawezaje kumfurahisha Yehova na wazazi wako?

Sasa hebu tumfikirie Baba yetu wa mbinguni, Yehova. Anatuambia namna tunavyoweza kumfurahisha. Tafadhali chukua Biblia yako na ufungue Mithali 27:11. Mungu anazungumza nasi anaposema: “Uwe na hekima, mwanangu [au binti yangu], na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” Je, unajua maana ya kumdhihaki mtu?— Mtu anaweza kukudhihaki kwa kukucheka akisema eti huwezi kufanya jambo ulilosema utafanya. Shetani humdhihakije Yehova?— Hebu tuone.

Kumbuka kwamba tulijifunza katika Sura ya 8 ya kitabu hiki kwamba Shetani hujitanguliza na anataka kila mtu amtii. Shetani husema kwamba watu humwabudu Yehova kwa sababu tu Yehova atawapa uzima wa milele wakimwabudu. Shetani alimpinga Mungu alipowashawishi Adamu na Hawa kumwasi Yehova. Alimwambia Mungu: ‘Watu wanakutumikia tu kwa sababu ya kile unachowapa. Nipe nafasi, nami nitafanya wakuache.’

Shetani alimpingaje Yehova baada ya uasi wa Adamu na Hawa?

Ni kweli kwamba maneno hayo hususa hayako katika Biblia. Lakini tunaposoma kuhusu Ayubu, ni wazi kwamba Shetani alimwambia Mungu jambo kama hilo. Lilikuwa jambo muhimu kwa Shetani na kwa Yehova kama Ayubu angekuwa mwaminifu kwa Mungu au la. Na tufungue Biblia zetu kwenye Ayubu sura ya 1 na ya 2 tuone jinsi mambo yalivyokuwa.

Ona kwamba katika Ayubu sura ya 1 Shetani yuko mbinguni malaika wanapoenda mbele za Yehova. Yehova anamwuliza Shetani: “Unatoka wapi?” Shetani anajibu kwamba amekuwa akizunguka-zunguka duniani. Kwa hiyo Yehova anamwuliza: ‘Umemwona Ayubu, kwamba ananitumikia wala hafanyi mabaya?’—Ayubu 1:6-8.

Mara moja Shetani anajitetea. ‘Ayubu anakutumikia tu kwa sababu hana matatizo. Ukiacha kumlinda na kumbariki, atakulaani mbele za uso wako.’ Yehova anamjibu: ‘Haya Shetani, unaweza kumfanyia chochote utakacho, lakini usimwumize Ayubu mwenyewe.—Ayubu 1:9-12.

Shetani anafanya nini?— Anapanga watu wamwibie Ayubu ng’ombe na punda na kuwaua wachungaji wao. Kisha radi inapiga na kuwaua kondoo na wachungaji wao. Baadaye, watu wanakuja na kuiba ngamia na kuwaua wachungaji wao. Hatimaye, Shetani anasababisha upepo mkali unaoiangusha nyumba walimokuwamo watoto kumi wa Ayubu na wote wanakufa. Licha ya hayo yote, Ayubu anaendelea kumtumikia Yehova.—Ayubu 1:13-22.

Yehova anapomwona Shetani tena, Yehova anamwambia kwamba Ayubu bado ni mwaminifu. Shetani anatoa udhuru akisema: ‘Ukiniacha tu niumize mwili wake, atakulaani mbele za uso wako.’ Yehova anamruhusu Shetani amwumize Ayubu lakini anamwonya asimwue.

Shetani alimpingaje Yehova baada ya uasi wa Adamu na Hawa?

Shetani anampiga Ayubu kwa ugonjwa, mwili wake wote unakuwa na vidonda. Vidonda hivyo vinanuka sana hivi kwamba hakuna anayetaka kumkaribia. Hata mke wa Ayubu anamwambia: “Mlaani Mungu, ufe!” Watu wanaojifanya kuwa rafiki za Ayubu wanapomtembelea wanamhuzunisha hata zaidi wanapomwambia kwamba ni lazima awe anateseka kwa sababu ya maovu anayotenda. Hata hivyo, Ayubu anaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu kujapokuwa matatizo na maumivu mengi yanayosababishwa na Shetani.—Ayubu 2:1-13; 7:5; 19:13-20.

Unafikiri uaminifu wa Ayubu ulimfanya Yehova ahisije?— Ulimfurahisha Yehova kwa sababu Yehova aliweza kumwambia Shetani: ‘Mwone Ayubu! Ananitumikia kwa sababu anataka.Je, utakuwa kama Ayubu, mtu ambaye Yehova anaweza kumtumia kama mfano wa kumthibitisha Shetani kuwa mwongo?— Kwa kweli, ni pendeleo kujibu mashtaka ya Shetani kwamba anaweza kuwafanya watu waache kumtumikia Yehova. Bila shaka Yesu aliliona kuwa pendeleo.

Mwalimu Mkuu hakumruhusu Shetani kamwe amwongoze kufanya mabaya. Wazia jinsi mfano wake ulivyomfurahisha Baba yake! Yehova aliweza kumjibu Shetani hivi kumhusu Yesu: ‘Ona Mwana wangu! Amekuwa mwaminifu kabisa kwangu kwa sababu ananipenda!’ Wazia pia shangwe ya Yesu kwa kufurahisha moyo wa Baba yake. Kwa sababu ya shangwe hiyo, Yesu hata alivumilia kifo kwenye mti wa mateso.—Waebrania 12:2.

Je, unataka kuwa kama Mwalimu wetu Mkuu kwa kumfurahisha Yehova?— Basi endelea kujifunza kuhusu yale Yehova anataka ufanye, na umfurahishe kwa kuyafanya!

Soma mambo ambayo Yesu alifanya ili kumfurahisha Mungu na yale ambayo tunahitaji kufanya pia, kwenye Mithali 23:22-25; Yohana 5:30; 6:38; 8:28; na 2 Yohana 4.