Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 42

Kwa Nini Tufanye Kazi?

Kwa Nini Tufanye Kazi?

UNAPENDA kufanya nini zaidi, kazi au kucheza?— Kwa kweli si vibaya kucheza. Biblia inasema kwamba Yerusalemu ‘itajaa wavulana na wasichana wakicheza katika viwanja vyake.’—Zekaria 8:5.

Mwalimu Mkuu alifurahia kuona watoto wakicheza. Kabla ya kuja duniani, alisema: “Ndipo nilipokuwa kando yake [Mungu] nikiwa stadi wa kazi . . . nikifurahi mbele zake wakati wote.” Ona kwamba Yesu alifanya kazi pamoja na Yehova mbinguni. Na alipokuwa huko alisema: “Vitu nilivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.” Ndiyo, kama tulivyojifunza hapo awali, Mwalimu Mkuu alipendezwa kikweli na kila mtu, kutia ndani watoto.—Mithali 8:30, 31.

Mwalimu Mkuu alifurahia nini kabla ya kuja duniani?

Unafikiri Yesu alicheza alipokuwa mtoto?— Labda. Lakini kwa sababu alikuwa “stadi wa kazi” mbinguni, je, alifanya kazi duniani pia?— Yesu aliitwa ‘mwana wa seremala.’ Lakini aliitwa pia “seremala.” Hii inamaanisha nini?— Ni lazima Yosefu, baba-mlezi wa Yesu, alimfundisha useremala. Basi Yesu akawa seremala pia.—Mathayo 13:55; Marko 6:3.

Yesu alikuwa seremala wa aina gani?— Kwa sababu alikuwa stadi wa kazi mbinguni, je, si wazi pia kwamba alikuwa seremala stadi duniani?— Ona jinsi ilivyokuwa kazi ngumu kuwa seremala wakati huo. Huenda Yesu alilazimika kuukata mti, kuupasua vipande-vipande, kubeba mbao zake na kuzipeleka nyumbani, kisha akatengeneza meza, benchi, na vitu vinginevyo.

Unafikiri Yesu alifurahia kazi hiyo?— Je, ungefurahi ikiwa ungetengeneza meza nzuri na viti vizuri na vitu vingine ili vitumiwe?— Biblia inasema ni vizuri mtu “afurahie kazi zake.” Kazi huleta shangwe ambayo huwezi kupata katika mchezo.—Mhubiri 3:22.

Kwa kweli, kazi inanufaisha akili zetu na miili yetu. Katika nchi nyingine watoto wengi huketi tu wakitazama televisheni au kujishughulisha na michezo ya video. Kisha wanakuwa wanene kupita kiasi na dhaifu, bila furaha. Wala hawawafurahishi wengine. Tunahitaji kufanya nini ili tuwe na furaha?—

Tulijifunza katika Sura ya 17 ya kitabu hiki kwamba kuwapa watu vitu na kuwasaidia wengine huleta furaha. (Matendo 20:35) Biblia humwita Yehova “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Na kama tunavyosoma kwenye Mithali, Yesu alikuwa ‘akifurahi mbele zake wakati wote.’ Kwa nini Yesu alikuwa mwenye furaha?— Alisema hivi: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, na mimi ninaendelea kufanya kazi.”—Yohana 5:17.

Yesu alipokuwa duniani, hakufanya useremala maisha yake yote. Yehova Mungu alimpa kazi ya pekee duniani. Unajua ni kazi gani?— Yesu alisema: ‘Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.’ (Luka 4:43) Wakati mwingine Yesu alipowahubiria watu, walimwamini na wakawaambia wengine waliyosikia, kama alivyofanya mwanamke huyu Msamaria unayemwona kwenye picha.—Yohana 4:7-15, 27-30.

Yesu alifanya kazi zipi mbili alipokuwa duniani?

Yesu aliionaje kazi hiyo? Unafikiri alitaka kuifanya?— Yesu alisema: ‘Chakula changu ni kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.’ (Yohana 4:34) Wewe hufurahia kula chakula ukipendacho kadiri gani?— Basi unaweza kuelewa jinsi Yesu alivyofurahia kufanya kazi aliyopewa na Mungu.

Mungu ametuumba tufurahie kujifunza kufanya kazi. Anasema kwamba zawadi Yake kwa mwanadamu ni kwamba mwanadamu ‘afurahie kazi zake.’ Kwa hiyo ukijifunza kufanya kazi ukiwa ungali mchanga, maisha yako yatakuwa yenye kupendeza.—Mhubiri 5:19.

Hiyo haimaanishi kwamba mtoto anaweza kufanya kazi ya mtu mzima, lakini angalau sote tunaweza kufanya kazi. Huenda wazazi wako wakalazimika kufanya kazi kila siku ili wapate pesa za kuwanunulia chakula na kuwa na mahali pa kuishi. Na kama ujuavyo, kuna kazi nyingi inayopaswa kufanywa nyumbani ili kuhakikisha nyumba ni safi na nadhifu.

Ni kazi gani unayoweza kufanya ifaidi familia nzima?— Unaweza kusaidia kupanga vitu mezani, kuosha vyombo, kutupa takataka, kufagia chumba cha kulala, na kuweka vitu vyako vya kuchezea mahali panapofaa. Huenda tayari unafanya baadhi ya mambo hayo. Kwa hakika kazi hiyo inafaidi familia.

Kwa nini ni muhimu kuweka mbali vitu vya kuchezea baada ya kuvitumia?

Hebu tuone faida ya kazi kama hiyo. Baada ya kucheza, vitu vya kuchezea vinapaswa kuwekwa. Kwa nini hiyo ni muhimu?— Inafanya nyumba kuwa safi na salama. Usipokusanya vitu vyako vya kuchezea na kuviweka, mama yako anaweza kuingia chumbani akiwa amebeba vitu na kuvikanyaga. Anaweza kuanguka na kuumia. Huenda hata akalazimika kwenda hospitalini. Hiyo ni mbaya sana, sivyo?— Kwa hiyo unapoweka vitu vyako baada ya kucheza, wengine watafaidika.

Pia kuna kazi nyingine za watoto. Kwa mfano kazi za shule. Shuleni unajifunza kusoma. Watoto wengine hufurahia kusoma lakini wengine husema kusoma si kazi rahisi. Hata ikionekana kuwa kazi ngumu mwanzoni, utafurahi ukijifunza kusoma vizuri. Ukijua kusoma, unaweza kujifunza mambo mengi yenye kupendeza. Hata unaweza kujisomea Biblia, kitabu cha Mungu mwenyewe. Hivyo, ukifanya kazi za shule vizuri, unafaidika kwelikweli, sivyo?—

Kuna watu ambao hawapendi kufanya kazi. Labda unamjua mtu wa namna hiyo. Lakini kwa sababu Mungu alituumba tufanye kazi, tunahitaji kujifunza kuifurahia. Mwalimu Mkuu alifurahia kazi yake kadiri gani?— Ilikuwa kama kula chakula anachokipenda sana. Na alimaanisha kazi gani?— Kuwaambia wengine kumhusu Yehova Mungu na namna wanavyoweza kupata uzima wa milele.

Basi hapa pana kitu kinachoweza kutusaidia tufurahie kazi. Jiulize, ‘Kwa nini kazi hii inapaswa kufanywa?’ Inakuwa rahisi kufanya kazi unapojua umuhimu wake. Iwe kazi hiyo ni kubwa au la, ifanye kwa bidii. Ukiifanya vizuri, utafurahia kazi ya mikono yako kama Mwalimu wetu Mkuu.