Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 11

Msaada wa Malaika wa Mungu

Msaada wa Malaika wa Mungu

WATU wengine husema kwamba wao wanaamini tu kile wanachoweza kuona. Lakini huo ni upumbavu. Kuna vitu vingi vilivyoko ambavyo hatujawahi kuviona kwa macho yetu. Unaweza kutaja kimoja?—

Namna gani hewa tunayopumua? Je, tunaweza kuihisi?— Nyosha mkono wako, kisha uupulizie hewa. Umesikia chochote?— Ndiyo, lakini huwezi kuiona hewa yenyewe, sivyo?—

Tayari tumezungumza kuhusu watu wenye miili ya roho, ambao hatuwezi kuwaona. Tulijifunza kwamba wengine ni wazuri na wengine ni wabaya. Hebu taja watu wazuri wenye miili ya roho ambao hatuwezi kuwaona.— Kuna Yehova Mungu, Yesu, na kuna malaika wazuri. Je, kuna malaika wabaya pia? — Biblia inasema wako. Hebu niambie umejifunza nini kuwahusu.—

Tunajua kwamba malaika wote wazuri na wabaya wana nguvu kutushinda. Mwalimu Mkuu alijua mambo mengi kuhusu malaika. Na hiyo ni kwa sababu yeye alikuwa malaika kabla ya kuzaliwa akiwa mtoto duniani. Aliishi na malaika wengine mbinguni. Alijua mamilioni ya malaika. Je, malaika hao wote wana majina?—

Tulijifunza kwamba Mungu alizipatia nyota majina. Kwa hiyo tuna hakika kwamba malaika wote wana majina pia. Na tunajua kwamba wanaweza kuongea pamoja kwa sababu Biblia inataja ‘lugha ya malaika.’ (1 Wakorintho 13:1) Unafikiri malaika huongea juu ya nini? Je, wao huongea juu yetu tukiwa duniani?—

Tunajua kwamba malaika wa Shetani, wale roho waovu, wanajaribu kutufanya tusimtii Yehova. Kwa hiyo ni lazima wazungumze namna wanavyoweza kutufanya tusitii. Wanataka tuwe kama wao ili Yehova asitupende pia. Lakini namna gani malaika waaminifu wa Mungu? Je, unafikiri wao pia huzungumza juu yetu?— Ndiyo. Wao wanataka kutusaidia. Hebu nikuambie namna malaika wengine wa Mungu walivyowasaidia watu waliompenda Yehova na kumtumikia.

Kwa mfano, kuna mtu aliyeitwa Danieli ambaye aliishi Babiloni. Watu wengi wa Babiloni hawakumpenda Yehova. Watu hata walitunga sheria ya kuadhibu mtu yeyote anayesali kwa Yehova Mungu. Lakini Danieli hakuacha kusali kwa Yehova. Je, unajua walimfanyia Danieli nini?—

Watu wabaya walimtupa Danieli ndani ya shimo la simba. Danieli alikaa humo ndani peke yake pamoja na simba wenye njaa. Kisha kukatokea nini?— Danieli alisema, ‘Mungu alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.’ Hakuumizwa hata kidogo! Malaika wanaweza kuwafanyia mazuri wale wanaomtumikia Yehova. —Danieli 6:18-22.

Danieli alifanya nini ili kumwokoa Danieli?

Kisha kuna wakati Petro alikuwa gerezani. Kumbuka kwamba Petro alikuwa rafiki ya Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo. Watu wengine hawakufurahi Petro alipowaambia kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. Basi wakamfunga Petro gerezani. Askari walimlinda Petro ili kuhakikisha kwamba hatoroki. Je, kuna mtu yeyote ambaye angeweza kumsaidia?—

Petro alikuwa amelala katikati ya askari wawili akiwa amefungwa minyororo mikononi. Lakini Biblia inasema: ‘Tazama! malaika wa Yehova akaja, na nuru ikang’aa katika chumba cha gereza. Akampiga Petro ubavuni, akamwamsha, akisema, “Amka upesi!”’

Malaika alimsaidiaje Petro kutoka gerezani?

Mara tu minyororo ya Petro ikaanguka kutoka mikononi mwake! Na malaika akamwambia: ‘Vaa vazi lako na viatu vyako, unifuate.’ Askari hawangewazuia kwa sababu malaika alikuwa akimsaidia Petro. Halafu wakafika kwenye lango la chuma, na jambo la ajabu likafanyika. Lango likajifungua! Malaika huyo alimweka huru Petro ili aendelee kuhubiri.—Matendo 12:3-11.

Je, malaika wa Mungu wanaweza kutusaidia pia?— Ndiyo. Je, hiyo inamaanisha kwamba hawatatuacha tuumie hata kidogo?— La, malaika hawawezi kuzuia tusiumie ikiwa tunafanya mambo ya upumbavu. Lakini hata kama hatufanyi mambo ya upumbavu, huenda bado tukaumia. Malaika hawajaambiwa wazuie mabaya yasitupate. Badala yake Mungu amewapa kazi muhimu ya kufanya.

Biblia inataja malaika ambaye anawaambia watu kila mahali wamwabudu Mungu. (Ufunuo 14:6, 7) Malaika anafanyaje hivyo? Je, anapiga kelele kutoka mbinguni ili kila mtu asikie?— La, badala yake wafuasi wa Yesu duniani wanawaambia wengine kuhusu Mungu, na malaika wanawaongoza katika kazi yao. Malaika wanahakikisha kwamba wale wanaotaka kumjua Mungu kikweli wanapata nafasi ya kusikia. Tunaweza kufanya kazi hiyo ya kuhubiri, na malaika watatusaidia.

Namna gani ikiwa watu wasiompenda Mungu wanatusumbua? Vipi wakitufunga gerezani? Je, malaika watatuweka huru pia?— Wanaweza. Lakini hawafanyi hivyo kila wakati.

Malaika anamwambia Paulo nini?

Paulo, ambaye alikuwa mfuasi wa Yesu, alikuwa gerezani wakati mmoja. Alikuwa anasafiri kwa meli wakati wa upepo mkali. Lakini malaika hawakumsaidia wakati huo kwa sababu kulikuwa na watu ambao walihitaji kusikia habari kumhusu Mungu. Malaika alimwambia: “Usiogope, Paulo. Utasimama mbele ya Kaisari.” Bila shaka, Paulo angepelekwa kwa Kaisari, mtawala wa ulimwengu ili Paulo amhubirie. Kila mara malaika walijua mahali Paulo alikuwa, nao walimsaidia. Watatusaidia pia ikiwa kwa kweli tutamtumikia Mungu. —Matendo 27:23-25.

Kuna kazi nyingine kubwa ambayo malaika watafanya, nao wataifanya hivi karibuni. Wakati wa Mungu wa kuwaharibu waovu umekaribia sana. Wale wote wasiomwabudu Mungu wa kweli wataharibiwa. Wale wanaosema kwamba hawaamini malaika eti kwa sababu hawawezi kuwaona malaika hao watatambua kwamba wamekosea sana. —2 Wathesalonike 1:6-8.

Hiyo itamaanisha nini kwetu?— Ikiwa sisi tutakuwa upande wa malaika wa Mungu, watatusaidia. Lakini, je, tuko upande wao?— Ndiyo, iwapo sisi tunamtumikia Yehova. Na ikiwa tunamtumikia Yehova, tutawaambia wengine wamtumikie pia.

Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu namna malaika wanavyohusika katika maisha ya watu, soma Zaburi 34:7; Mathayo 4:11; 18:10; Luka 22:43; na Matendo 8:26-31.