Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 30

Jinsi Tunavyoweza Kuushinda Woga

Jinsi Tunavyoweza Kuushinda Woga

JE, UNAONA ikiwa rahisi kumtumikia Yehova?— Mwalimu Mkuu hakusema itakuwa rahisi. Usiku kabla ya Yesu kuuawa, aliwaambia mitume wake hivi: ‘Ulimwengu ukiwachukia ninyi, mnajua kwamba huo umenichukia kabla ya kuwachukia.’—Yohana 15:18.

Petro alijigamba kwamba hawezi kamwe kumwacha Yesu, lakini Yesu akasema kwamba Petro angemkana mara tatu usiku huohuo. Na kwa kweli Petro akamkana! (Mathayo 26:31-35, 69-75) Iliwezekanaje hivyo?— Iliwezekana kwa sababu kama wale mitume wengine, Petro pia alishikwa na woga.

Je, unajua ni kwa nini mitume waliogopa?— Walikosa kufanya jambo fulani muhimu. Kujifunza kuhusu jambo hilo kutatusaidia tumtumikie Yehova bila kujali watu watasema nini au kututendea nini. Kwanza, hebu tujikumbushe matukio ya usiku wa mwisho wa Yesu akiwa pamoja na mitume wake.

Kwanza, walisherehekea pamoja Pasaka. Huo ulikuwa mlo wa pekee ulioadhimishwa kila mwaka kuwakumbusha watu wa Mungu kuhusu ukombozi wao kutoka utumwani huko Misri. Kisha Yesu akaanzisha mlo mwingine wa pekee pamoja na mitume. Tutazungumzia mlo huo katika sura nyingine baadaye na tueleze namna mlo huo unavyotusaidia kumkumbuka Yesu. Baada ya mlo huo na baada ya Yesu kuwatia moyo mitume wake, Yesu akawapeleka nje katika bustani ya Gethsemane. Walipenda mahali hapo sana na mara nyingi walienda huko.

Yesu anaenda mbali kidogo peke yake ili asali kwenye bustani. Anawaambia pia Petro, Yakobo, na Yohana wasali. Lakini usingizi unawashika na wanaanza kulala. Mara tatu Yesu anaenda mbali peke yake ili asali, na mara tatu anaporudi anawakuta Petro na wenzake wamelala usingizi! (Mathayo 26:36-47) Unajua ni kwa nini walipaswa kukesha na kusali?— Hebu tuzungumzie jambo hilo.

Kwa nini Petro, Yakobo, na Yohana walipaswa kukesha?

Mapema jioni hiyo, Yuda Iskariote pamoja na Yesu na mitume wengine walihudhuria sherehe ya Pasaka. Kumbuka kwamba Yuda alikuwa amekuwa mwizi. Na sasa anakuwa msaliti. Anajua mahali ambapo Yesu na mitume wake walizoea kukutana katika bustani ya Gethsemane. Kwa hiyo, Yuda anawapeleka askari huko ili wamkamate Yesu. Wanapofika, Yesu anawauliza: “Mnamtafuta nani?”

Askari wanamjibu: “Yesu.” Yesu anawajibu bila woga: ‘Ndiye mimi.’ Askari wanashangazwa na ujasiri wa Yesu, wanarudi nyuma na kuanguka chini. Kisha Yesu anasema: ‘Ikiwa ni mimi mnayetafuta, acheni mitume wangu waende.’—Yohana 18:1-9.

Askari wanapomkamata Yesu na kumfunga mikono, mitume wanaogopa na kutoroka. Lakini Petro na Yohana wanawafuata kwa umbali ili kujua kitakachotokea. Hatimaye, Yesu anapelekwa kwa Kayafa, kuhani mkuu. Kwa sababu Yohana anajulikana na kuhani mkuu, mtunza-mlango anawaruhusu yeye na Petro waingie ndani ya ua wake.

Makuhani tayari wamekuja nyumbani kwa Kayafa ili kuanzisha kesi. Wanataka Yesu auawe. Basi wanaleta mashahidi ambao wanasema uwongo kumhusu Yesu. Watu wanampiga Yesu ngumi na kumzaba makofi. Petro yuko karibu mambo hayo yanapoendelea.

Msichana mmoja mtumishi, mtunza-mlango aliyewaruhusu Petro na Yohana kuingia, anamtambua. Anamwambia, “Wewe, pia, ulikuwa pamoja na Yesu!” Lakini Petro anakataa kwamba hamjui Yesu. Baadaye kidogo msichana mwingine anamtambua Petro na kuwaambia watu waliokuwa wamesimama karibu nao: “Mtu huyu alikuwa pamoja na Yesu.” Kwa mara nyingine Petro anasema hamjui Yesu. Baadaye tena watu wengine wanamwona Petro na kumwambia: “Hakika wewe pia ni mmoja wao.” Kwa mara ya tatu, Petro anakataa na kusema: “Simjui mtu huyo!” Petro hata anaapa kwamba anasema kweli, na Yesu anageuka na kumtazama.—Mathayo 26:57-75; Luka 22:54-62; Yohana 18:15-27.

Kwa nini Petro aliogopa sana hata akadanganya kwamba hamjui Yesu?

Unajua ni kwa nini Petro alisema uwongo?— Ndiyo, kwa sababu aliogopa. Lakini kwa nini aliogopa? Alikosa kufanya nini ili kupata ujasiri? Lifikirie jambo hilo. Yesu alifanya nini ili kupata ujasiri?— Alisali kwa Mungu, naye Mungu akamsaidia kuwa na ujasiri. Kumbuka pia kwamba Yesu alikuwa amemwambia Petro mara tatu asali na kukesha na kuendelea kuwa macho. Lakini ikawaje?—

Kila mara Petro alilala. Hakusali, wala hakuendelea kulinda. Kwa hiyo Yesu alipokamatwa Petro hakutazamia. Baadaye kesi ilipokuwa ikiendelea, Petro aliogopa alipoona Yesu akipigwa na mipango ikifanywa auawe. Lakini muda wa saa chache tu awali, Yesu aliwaambia mitume wake watazamie nini?— Yesu aliwaambia kwamba kama vile ulimwengu ulivyomchukia, ungewachukia wao pia.

Unawezaje kujikuta katika hali kama ya Petro?

Sasa tufikirie jambo ambalo linaweza kutupata ambalo ni sawa na lililompata Petro. Vipi ukiwa darasani na wengine wanaanza kusema mambo mabaya kuhusu watu wasioisalimu bendera au wasiosherehekea Krismasi. Utafanyaje mmoja akikugeukia na kukuuliza: “Je, ni kweli kwamba wewe husalimu bendera?” Au wengine wanaweza kusema: “Tunasikia eti husherehekei Krismasi kamwe!” Je, utaogopa kusema kweli?— Je, utashawishika kudanganya kama Petro?—

Baadaye, Petro alisikitika sana kwamba amemkana Yesu. Alipogundua alilokuwa amefanya, alitoka nje akalia sana. Ndiyo, alirudi kwa Yesu. (Luka 22:32) Hebu fikiria. Ni nini kinachoweza kutusaidia tusiwe na woga sana hivi kwamba tuseme kama Petro?— Kumbuka, Petro alikosa kusali na kuendelea kuwa macho. Basi, unafikiri tunahitaji kufanya nini ili tuwe wafuasi wa Mwalimu Mkuu?—

Bila shaka tunahitaji kusali ili Yehova atusaidie. Yesu aliposali, unajua Mungu alifanya nini?— Alimtuma malaika ili amtie nguvu. (Luka 22:43) Je, malaika wa Mungu wanaweza kutusaidia?— Biblia inasema: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.” (Zaburi 34:7) Lakini ili tupate msaada wa Mungu, tunahitaji kufanya zaidi ya kusali tu. Unajua kitu kingine tunachohitaji kufanya?— Yesu aliwaambia wafuasi wake wakeshe na kuendelea kuwa macho. Unafikiri tunaweza kufanyaje hivyo?—

Tunaweza kupata msaada tukisikiliza kwa makini yale yanayosemwa katika mikutano yetu ya Kikristo na kutilia maanani yale tunayosoma katika Biblia. Lakini tunahitaji pia kusali kwa Yehova kwa ukawaida na kumwomba atusaidie tumtumikie. Tukifanya hivyo, tutapata msaada wa kuushinda woga. Kisha tutafurahi tunapokuwa na nafasi ya kuwaambia wengine kumhusu Mwalimu Mkuu na Baba yake.

Maandiko haya yanaweza kutusaidia tusiruhusu kuogopa watu kutuzuie kufanya yaliyo mema: Mithali 29:25; Yeremia 26:12-15, 20-24; na Yohana 12:42, 43.