Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 11

Baada ya Siku ya Harusi

Baada ya Siku ya Harusi

“Upendo haushindwi kamwe.”—1 WAKORINTHO 13:8.

1, 2. Je, kuwa na matatizo katika ndoa kunamaanisha kwamba lazima ndoa ivunjike? Eleza.

NDOA ni zawadi kutoka kwa Yehova. Inaweza kufanya maisha ya mtu yawe na furaha zaidi. Hata hivyo, kila ndoa ina matatizo yake. Na huenda ikaonekana kana kwamba matatizo hayatakwisha hivyo kuwafanya mume na mke wahisi wamepoteza uhusiano wa karibu waliokuwa nao mwanzoni.

2 Hatupaswi kushangaa ndoa zetu zinapokuwa na matatizo mara kwa mara. Hata hivyo, kuwa na matatizo hakumaanishi kwamba ndoa haijafanikiwa. Hata wenzi waliokuwa na matatizo mazito katika ndoa zao wamepata njia ya kuboresha uhusiano wao na kufanya ndoa zao ziwe imara. Jinsi gani?

MKARIBIE MUNGU NA MWENZI WAKO

3, 4. Ni mambo gani yanayoweza kutokea katika ndoa?

3 Ndoa ni muungano wa watu wawili wanaotofautiana. Kila mmoja ana mambo anayopenda na asiyopenda, mawazo yake, na njia yake ya kufanya mambo. Pia, mume na mke wanaweza kuwa na malezi au tamaduni zinazotofautiana. Wakati na jitihada zinahitajika ili wenzi wa ndoa wafahamiane vizuri.

4 Kadiri muda unavyopita, mume na mke wanaweza kujihusisha zaidi katika mambo yao ya kibinafsi hivi kwamba wanaanza kupoteza uhusiano wa karibu. Inaweza kuonekana kana kwamba kila mmoja ana maisha yake. Ni nini kinachoweza kuwasaidia kuwa na uhusiano wa karibu?

Ushauri wa Biblia ni muhimu ili tuwe na ndoa nzuri

5. (a) Ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo kuwa na uhusiano wa karibu na mwenzi wake? (b) Kulingana na Waebrania 13:4, tunapaswa kuionaje ndoa?

5 Yehova anatoa ushauri mzuri ambao unaweza kukusaidia wewe na mwenzi wako kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kati yenu wenyewe. (Zaburi 25:4; Isaya 48:17, 18) Anatuambia hivi: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote.” (Waebrania 13:4) Unapoheshimu kitu unakiona kuwa chenye thamani sana. Unakilinda na kukitunza sana. Hivyo ndivyo Yehova anataka tuione ndoa.

KUMPENDA YEHOVA KUNAWEZA KUIMARISHA NDOA YAKO

6. Kulingana na Mathayo 19:4-6 Yehova ana maoni gani kuhusu ndoa?

6 Yehova ndiye aliyeanzisha ndoa ya kwanza. Mwana wake, Yesu alisema hivi: “Je, hamkusoma kwamba yule aliyewaumba tangu mwanzo aliwaumba mwanamume na mwanamke na kusema: ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Basi wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mathayo 19:4-6) Tangu mwanzo, Yehova alikusudia ndoa idumu. Alitaka familia ziwe na uhusiano wa karibu, ziwe na furaha, na zifurahie maisha pamoja.

7. Waume na wake wanaweza kuimarishaje ndoa zao?

7 Hata hivyo, wenzi wa ndoa leo wanakabili mikazo mingi sana kuliko wakati mwingine wowote. Nyakati nyingine mikazo hiyo inakuwa mikali sana hivi kwamba wanafikiri ndoa yao haiwezi kuokolewa, na hivyo wanakata tamaa. Lakini kuelewa maoni ya Yehova kuhusu ndoa kunaweza kutusaidia.—1 Yohana 5:3.

8, 9. (a) Ni wakati gani tunapopaswa kufuata mwongozo wa Yehova kuhusu ndoa? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba ndoa yetu ina thamani?

8 Sikuzote mwongozo wa Yehova ni kwa faida yetu. Kama tulivyoona, anatushauri hivi: “Ndoa na iheshimiwe.” (Waebrania 13:4; Mhubiri 5:4) Ikiwa tutafuata mwongozo wa Yehova hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo, bila shaka tutafaidika.—1 Wathesalonike 1:3; Waebrania 6:10.

9 Kwa kuwa ndoa yetu ina thamani kubwa kwetu, tunataka kuepuka kufanya au kusema jambo lolote ambalo linaweza kuiharibu. Badala yake, tunataka kuimarisha uhusiano wetu na mwenzi wetu. Tunawezaje kufanya hivyo?

HESHIMU NDOA YAKO KWA MAMBO UNAYOSEMA NA KUTENDA

10, 11. (a) Ni tatizo gani zito linalokumba baadhi ya ndoa? (b) Kwa nini ni muhimu kufikiria jinsi tunavyozungumza na mume au mke wetu?

10 Kuna njia nyingi ambazo mtu anaweza kumwumiza mwenzi wake. Tunajua kwamba Mkristo hapaswi kumpiga au kufanya jambo lolote litakalomwumiza kimwili mwenzi wake. Hata hivyo, tunaweza kumwumiza mwenzi wetu kwa maneno tunayosema. Maneno yanaweza kuwa silaha. Mwanamke mmoja alisema hivi: “Mume wangu hunishambulia kwa maneno. Sina majeraha mwilini, lakini maneno yake yenye kuchoma anayosema kila wakati, kama vile ‘Umenichosha!’ na ‘Wewe ni bure kabisa!’ yananiumiza sana moyoni.” Mume mmoja alisema kwamba mke wake humvunjia heshima kila wakati kwa maneno na kwa kumwita majina yasiyofaa. Mume huyo alisema hivi: “Siwezi kurudia maneno ambayo yeye husema nikiwa mbele ya watu. Ndiyo sababu siwezi kuzungumza naye na ninachelewa kutoka kazini. Kazini ni salama zaidi kuliko nyumbani.” Ni kawaida leo kwa watu kutumia matusi au kusema maneno yenye kuumiza na yasiyo na fadhili ambayo husababisha maumivu ya kihisia.

11 Mume na mke wanapotupiana maneno yenye kuumiza, wanasababisha vidonda vya kihisia ambavyo huchukua muda mrefu sana kupona. Kwa kweli, Yehova hataki mume na mke watendeane kwa njia hiyo. Lakini unaweza kumwumiza mwenzi wako hata bila kujua. Unaweza kuhisi kwamba unamtendea mwenzi wako kwa fadhili, lakini yeye anahisije? Ikiwa ulisema jambo lililomwumiza mwenzi wako, je, utakuwa tayari kuepuka kulirudia?—Wagalatia 5:15; soma Waefeso 4:31.

12. Uhusiano wa mtu na Yehova unaweza kuathiriwaje na jinsi anavyozungumza na mwenzi wake?

12 Machoni pa Yehova, ni jambo zito jinsi unavyozungumza na mwenzi wako, iwe faraghani au hadharani. (Soma 1 Petro 3:7.) Yakobo 1:26 inatukumbusha hivi: “Ikiwa mtu yeyote anafikiri yeye ni mwabudu wa Mungu lakini haudhibiti kabisa ulimi wake, anaudanganya moyo wake, na ibada yake ni ubatili.”

13. Ni kwa njia gani nyingine mtu anaweza kuumiza hisia za mwenzi wake wa ndoa?

13 Mtu anapaswa kufikiria hisia za mwenzi wake kuhusu mambo mengine pia. Kwa mfano, mwenzi wako angehisije ikiwa ungetumia wakati mwingi pamoja na mtu mwingine? Ingawa huenda ukawa na sababu nzuri, kama vile kwenda katika huduma au kumsaidia mtu huyo kushughulikia tatizo fulani, je, mwenzi wako ataumia unapofanya hivyo? Mke mmoja Mkristo alisema hivi: “Ninaumia ninapoona mume wangu akitumia muda mwingi sana ili kumhangaikia dada mwingine kutanikoni. Hilo hunifanya nihisi kwamba sifai.”

14. (a) Ni kweli gani ya msingi tunayojifunza katika Mwanzo 2:24? (b) Tunapaswa kujiuliza swali gani?

14 Tukiwa Wakristo tuna wajibu kuelekea wazazi wetu na ndugu na dada katika kutaniko letu. Hata hivyo, tunapofunga ndoa wajibu wetu mkuu unakuwa kwa mume au mke wetu. Yehova alisema kwamba mume “atashikamana na mke wake.” (Mwanzo 2:24) Hisia za mwenzi wetu zinapaswa kuwa muhimu sana kwetu. Jiulize hivi: ‘Je, ninampa mwenzi wangu wakati, uangalifu, na upendo anaohitaji na anaostahili?’

15. Kwa nini wenzi wa ndoa Wakristo wanapaswa kuepuka kuwa na uhusiano wa karibu sana na mtu ambaye si mume au mke wao?

15 Tukiwa na uhusiano wa karibu sana na mtu ambaye si mwenzi wetu wa ndoa, tutasababisha matatizo katika ndoa yetu. Huenda tukaanza kuvutiwa kihisia na mtu huyo na kusitawisha hisia za kimahaba kumwelekea. (Mathayo 5:28) Hisia hizo zinaweza kukua na kusababisha ufanye jambo litakalovunjia ndoa yako heshima.

“KITANDA CHA NDOA KISIWE NA UNAJISI”

16. Biblia inatoa amri gani kuhusu ndoa?

16 Baada ya kusema: “Ndoa na iheshimiwe,” Biblia inasema hivi: “Kitanda cha ndoa kisiwe na unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Maneno “kitanda cha ndoa” yanarejelea uhusiano wa ngono kati ya mume na mke. (Methali 5:18) Tunaweza kuonyeshaje heshima kwa uhusiano huo na kutoutia unajisi?

17. (a) Watu wengi leo wanauonaje uzinzi? (b) Wakristo wanapaswa kuuonaje uzinzi?

17 Watu fulani leo wanafikiri kwamba hakuna ubaya wa kutokuwa waaminifu kwa wenzi wao. Hatupaswi kujiruhusu tuathiriwe na mtazamo huo. Yehova ameonyesha wazi kabisa kwamba anachukia uasherati na uzinzi. (Soma Waroma 12:9; Waebrania 10:31; 12:29) Tukifanya ngono na mtu ambaye si mume au mke wetu, tutakuwa tukiitia ndoa yetu unajisi. Tutaonyesha kwamba hatuheshimu viwango vya Yehova, na tutahatarisha uhusiano wetu na Mungu. Kwa hiyo, tunapaswa kuepuka kuchukua hatua ya kwanza inayoweza kutuongoza kwenye uzinzi. Hilo linatia ndani kuepuka mawazo yasiyofaa kuelekea mtu mwingine.—Ayubu 31:1.

18. (a) Kwa nini uzinzi ni sawa na kuabudu miungu ya uwongo? (b) Yehova ana maoni gani kuhusu uzinzi?

18 Katika taifa la kale la Israeli chini ya Sheria ya Musa, uzinzi ulikuwa dhambi nzito sana, sawa na kuabudu miungu ya uwongo. Adhabu iliyotolewa kwa dhambi zote mbili ilikuwa kifo. (Mambo ya Walawi 20:2, 10) Kulikuwa na ulinganifu gani kati ya kufanya uzinzi na kuabudu miungu ya uwongo? Mwisraeli alipoabudu miungu ya uwongo, alivunja ahadi yake ya kuwa mwaminifu kwa Yehova. Alipofanya uzinzi, alivunja ahadi yake ya kuwa mwaminifu kwa mwenzi wake. (Kutoka 19:5, 6; Kumbukumbu la Torati 5:9; soma Malaki 2:14.) Ni wazi kwamba tangu zamani Yehova aliuona uzinzi kuwa dhambi nzito sana.

19. Ni nini kitakachotusaidia kuazimia kutofanya uzinzi?

19 Vipi leo? Ingawa hatuko chini ya Sheria ya Musa, maoni ya Yehova kuhusu uzinzi hayajabadilika. Kama vile ambavyo hatuwezi kuabudu mungu wa uwongo, ndivyo hatupaswi kamwe kukosa kuwa waaminifu kwa mwenzi wetu. (Zaburi 51:1, 4; Wakolosai 3:5) Tukikosa kuwa waaminifu, tutaivunjia heshima ndoa yetu, na pia tutamvunjia heshima Mungu wetu, Yehova.—Soma Maelezo ya Ziada 26.

JINSI YA KUIMARISHA NDOA YAKO

20. Hekima inaweza kunufaishaje ndoa?

20 Unaweza kuimarishaje ndoa yako? Neno la Mungu linasema: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa utambuzi hufanywa iwe salama.” (Methali 24:3) Nyumba inaweza kuwa tupu na baridi au inaweza kuwa na joto, yenye kustarehesha, na salama. Ndoa inaweza kuwa hivyo pia. Mtu mwenye hekima atahakikisha kwamba ndoa yake ni salama, inapendeza, na kufurahisha.

21. Ujuzi unaweza kuimarishaje ndoa?

21 Biblia inaendelea kusema hivi kuhusu nyumba hiyo: “Kwa ujuzi vyumba hujazwa kila aina ya hazina zenye thamani na zinazopendeza.” (Methali 24:4) Mambo unayojifunza katika Neno la Mungu yanaweza kuboresha ndoa yako. (Waroma 12:2; Wafilipi 1:9) Mnaposoma Biblia na machapisho yetu mkiwa pamoja, zungumzieni jinsi mnavyoweza kutumia mambo mnayojifunza. Tafuteni njia za kuonyeshana upendo na heshima, pamoja na njia za kuonyeshana fadhili na ufikirio. Mwombeni Yehova awasaidie kusitawisha sifa ambazo zitaimarisha ndoa yenu na kufanya mwenzi wako akupende zaidi.—Methali 15:16, 17; 1 Petro 1:7.

Mtegemeeni Yehova awaongoze wakati wa ibada ya familia

22. Kwa nini tunapaswa kumwonyesha mwenzi wetu upendo, staha, na heshima?

22 Tunapaswa kufanya yote tuwezayo ili kumtendea mwenzi wetu kwa upendo, staha, na heshima. Ndoa yetu itaburudisha na kuimarika. Na jambo muhimu zaidi, tutamfanya Yehova afurahi.—Zaburi 147:11; Waroma 12:10.