Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA  6

Jinsi ya Kuchagua Burudani

Jinsi ya Kuchagua Burudani

“Fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” —1 WAKORINTHO 10:31.

1, 2. Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu tunapochagua burudani?

WAZIA unataka kula tunda halafu unagundua kwamba sehemu fulani imeoza. Utafanya nini? Je, utakula tunda hilo? Utalitupa? Au utakata sehemu iliyooza halafu ule sehemu nzuri?

2 Kwa njia fulani, burudani ni kama tunda hilo. Burudani fulani zinafurahisha, lakini nyingi zimeoza kwa sababu zinahusisha mambo mapotovu kiadili, ukatili, au mambo yanayohusiana na uchawi. Hivyo, unapochagua burudani, je, unasema: “Kwa sababu uamuzi ni wangu ninaweza kuchagua burudani yoyote ninayotaka”? Au labda unaona kwamba burudani zote ni mbaya? Au je, unachagua kwa uangalifu, ukiepuka burudani mbaya na kufurahia nzuri?

3. Tunapaswa kufikiria nini tunapochagua burudani?

3 Sisi sote tunahitaji kuwa na pindi za tafrija na burudani, na tunataka kuchagua vizuri. Hivyo basi, tunahitaji kufikiria jinsi burudani tunazochagua zinavyoweza kuathiri ibada yetu kwa Yehova.

“FANYENI MAMBO YOTE KWA UTUKUFU WA MUNGU”

4. Ni kanuni gani ya Biblia inayoweza kutusaidia tunapochagua burudani?

4 Tunapojiweka wakfu kwa Yehova, tunamwahidi kwamba tutatumia maisha yetu kumtumikia. (Soma Mhubiri 5:4.) Tunaahidi kwamba “[tutafanya] mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31) Hilo linamaanisha kwamba tumejiweka wakfu kwa Mungu hata tunapopumzika au kufurahia burudani, si tu tunapokuwa kwenye mikutano au utumishi wa shambani.

5. Tunapaswa kumtolea Yehova ibada ya aina gani?

5 Kila kitu tunachofanya maishani kinahusiana na ibada yetu kwa Yehova. Paulo alifafanua hilo aliposema hivi: “Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, na yenye kukubalika kwa Mungu.” (Waroma 12:1) Yesu alisema hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Sikuzote tunataka kumpa Yehova kilicho bora. Katika Israeli la kale, watu walipomtolea Yehova dhabihu, walitarajiwa kutoa mnyama mwenye afya. Ikiwa dhabihu ilikuwa na kasoro, Mungu hakuikubali. (Mambo ya Walawi 22:18-20) Vivyo hivyo, ibada yetu inaweza kukataliwa na Yehova. Jinsi gani?

6, 7. Burudani tunazochagua zinaweza kuathiri ibada yetu kwa Yehova jinsi gani?

6 Yehova anatuambia hivi: “Lazima muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.” (1 Petro 1:14-16; 2 Petro 3:11) Yehova atakubali ibada yetu ikiwa tu ni takatifu, au safi. (Kumbukumbu la Torati 15:21) Ibada yetu haiwezi kuwa safi ikiwa tunafanya mambo ambayo Yehova anachukia, kama vile upotovu wa maadili, ukatili, au mambo yanayohusiana na uchawi. (Waroma 6:12-14; 8:13) Pia, Yehova hatafurahi ikiwa tutajiruhusu kuburudishwa na mambo kama hayo. Hilo linaweza kufanya ibada yetu isiwe safi na isikubalike machoni pa Yehova na kuharibu uhusiano wetu pamoja naye.

7 Kwa hiyo, tunaweza kuchaguaje burudani kwa hekima? Ni kanuni zipi zinazoweza kutusaidia kutambua burudani zinazofaa na zisizofaa?

CHUKIA MABAYA

8, 9. Tunapaswa kuepuka burudani za aina gani? Kwa nini tuziepuke?

8 Kuna aina nyingi za burudani zinazopatikana leo. Baadhi ya burudani zinakubalika kwa Wakristo, lakini nyingi hazikubaliki. Kwanza, tuzungumzie aina za burudani tunazohitaji kuepuka.

9 Sinema nyingi, tovuti, vipindi vya televisheni, michezo ya video, na muziki unahusisha mambo mapotovu kiadili, ukatili, na mambo yanayohusiana na uchawi. Mara nyingi mambo mabaya yanaonyeshwa kana kwamba hayana madhara au hata kuwa yenye kuchekesha. Lakini Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu kukataa burudani ambazo hazipatani na viwango safi vya Yehova. (Matendo 15:28, 29; 1 Wakorintho 6:9, 10) Tunapokataa burudani kama hizo, tunamwonyesha Yehova kwamba tunachukia mabaya.—Zaburi 34:14; Waroma 12:9.

10. Kunaweza kuwa na madhara gani tunapofanya maamuzi mabaya kuhusu burudani?

10 Watu fulani wanahisi kwamba hakuna ubaya kusikiliza, kutazama, au kushiriki burudani zenye jeuri, maadili mapotovu, au mambo yanayohusiana na uchawi. Wanajiambia hivi: ‘Kuna ubaya gani? Siwezi kamwe kufanya mambo hayo.’ Ikiwa tunafikiri kwa njia hiyo, tunajidanganya. Biblia inasema hivi: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Ikiwa tunaburudishwa na mambo ambayo hayakubaliki machoni pa Yehova, tunawezaje kusema kwamba tunayachukia? Kadiri tunavyoendelea kuburudishwa nayo, ndivyo tutakavyoanza kuyaona kuwa ya kawaida. Baada ya muda, dhamiri yetu itadhoofika na kuacha kutuonya tunapokaribia kufanya uamuzi mbaya.—Zaburi 119:70; 1 Timotheo 4:1, 2.

11. Andiko la Wagalatia 6:7 litatusaidiaje kuchagua burudani inayofaa?

11 Neno la Mungu linatuambia hivi: “Lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.” (Wagalatia 6:7) Ni wazi kwamba tukijiruhusu tufurahishwe na mambo mabaya, baada ya muda huenda tukayafanya. Kwa mfano, watu fulani waliathiriwa sana na burudani zenye upotovu wa maadili hivi kwamba wakafanya uasherati. Lakini Yehova anatuandalia msaada tunaohitaji ili tuchague burudani kwa hekima.

TUMIA KANUNI ZA BIBLIA UNAPOFANYA MAAMUZI

12. Ni nini kitakachotusaidia kufanya maamuzi mazuri kuhusu burudani?

12 Burudani fulani hazikubaliwi na Yehova, na tunajua kwamba tunahitaji kuziepuka. Lakini namna gani ikiwa hazijashutumiwa waziwazi? Yehova hajatupatia orodha ya sheria kuhusu mambo tunayoweza na tusiyoweza kutazama, kusikiliza, au kusoma. Badala yake, anataka tutumie dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia. (Soma Wagalatia 6:5.) Yehova anatupatia kanuni, yaani, kweli za msingi zinazotufundisha maoni yake. Kanuni hizo zinaweza kutusaidia kuzoeza dhamiri yetu. Zinatusaidia kufahamu “mapenzi ya Yehova” ili tufanye maamuzi yatakayompendeza.—Waefeso 5:17.

Kanuni za Biblia zinatusaidia kuchagua burudani

13. Kwa nini Wakristo hufanya maamuzi yanayotofautiana kuhusu burudani? Lakini jambo muhimu ni nini kwa Wakristo wote?

13 Mara nyingi Mkristo mmoja atachagua burudani tofauti na Mkristo mwingine. Kwa nini? Kwa sababu tuna mapendezi tofauti. Pia, mambo yanayokubalika kwa mtu mmoja huenda yasikubalike kwa mwingine. Hata hivyo, ili kufanya maamuzi mazuri, Wakristo wote wanapaswa kuongozwa na kanuni za Biblia. (Wafilipi 1:9) Hilo litatusaidia kuchagua burudani inayokubalika machoni pa Mungu.—Zaburi 119:11, 129; 1 Petro 2:16.

14. (a) Ni jambo gani muhimu tunalohitaji kuzingatia kuhusu jinsi tunavyotumia wakati? (b) Paulo aliwapa Wakristo shauri gani?

14 Jambo lingine tunalopaswa kuzingatia ni muda tunaotumia kwa ajili ya burudani. Hilo linaweza kuonyesha burudani ni muhimu kadiri gani kwetu. Tukiwa Wakristo, utumishi wetu kwa Yehova ndilo jambo muhimu zaidi maishani. (Soma Mathayo 6:33.) Lakini bila kugundua, tunaweza kuruhusu burudani ichukue muda wetu mwingi. Paulo aliwashauri Wakristo hivi: “Endeleeni kuangalia sana jinsi mnavyotembea, si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkiutumia vizuri kabisa wakati wenu.” (Waefeso 5:15, 16) Kwa hiyo, tunahitaji kuweka mipaka ya muda tutakaotumia kufuatilia burudani na kuhakikisha sikuzote kwamba tunatanguliza utumishi wetu kwa Mungu.—Wafilipi 1:10.

15. Tunaweza kujilinda jinsi gani na burudani ambazo zinaweza kudhuru uhusiano wetu na Yehova?

15 Ni wazi kwamba tunapaswa kukataa burudani tunazojua hazikubaliki kwa Yehova. Lakini namna gani ikiwa hatuna uhakika kuhusu burudani fulani? Je, bado tunahitaji kuwa waangalifu? Fikiria hili. Tuseme unatembea kwenye njia ya mlimani iliyo kando ya bonde, je, utatembea karibu kabisa na ukingo wa njia hiyo? Hapana. Ikiwa unajali uhai wako, utajiepusha na hatari. Unapaswa kuzingatia hilo unapochagua burudani. Neno la Mungu linatuambia hivi: “Iepushe miguu yako na lililo ovu.” (Methali 4:25-27) Hivyo, hatuepuki tu burudani tunazojua kuwa ni mbaya, bali pia tunaepuka burudani ambazo tunashuku kwamba si nzuri na zinaweza kudhuru uhusiano wetu na Yehova.

KUPATA MAONI YA YEHOVA

16. (a) Ni baadhi ya mambo gani ambayo Yehova anachukia? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunachukia kile ambacho Yehova anachukia?

16 Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Enyi mnaompenda Yehova, chukieni maovu.” (Zaburi 97:10) Biblia inatufundisha jinsi ambavyo Yehova anafikiri na kuhisi. Jiulize jinsi mambo unayojifunza yanavyoweza kukusaidia uwe na maoni kama ya Yehova. Kwa mfano, tunajifunza kwamba Yehova anachukia “ulimi wa uwongo, na mikono inayomwaga damu isiyo na hatia, moyo unaopanga njama za uovu, na miguu inayokimbilia haraka uovu.” (Methali 6:16-19) Tunajifunza kwamba tunapaswa kuepuka “uasherati, . . . ibada ya sanamu, kuwasiliana na roho, . . . wivu, milipuko ya hasira, . . . husuda, ulevi, karamu zenye vurugu, na mambo kama hayo.” (Wagalatia 5:19-21) Je, unaona jinsi kanuni hizo za Biblia zinavyoweza kukusaidia kuchagua burudani? Tunataka kufuata viwango vya Yehova katika mambo yote maishani mwetu, iwe kuna watu wengine karibu au tuko peke yetu. (2 Wakorintho 3:18) Kwa kweli, mambo tunayochagua tukiwa peke yetu yanaonyesha kihalisi jinsi tulivyo.—Zaburi 11:4; 16:8.

17. Unapaswa kujiuliza maswali gani unapochagua burudani?

17 Hivyo, unapochagua burudani, jiulize hivi: ‘Burudani ninayochagua itaathirije uhusiano wangu na Yehova? Itaathirije dhamiri yangu?’ Acheni tuchunguze kanuni nyingine zinazoweza kutusaidia tunapochagua burudani.

18, 19. (a) Paulo aliwapa Wakristo ushauri gani? (b) Ni kanuni zipi zinazoweza kutusaidia tunapochagua burudani?

18 Tunapochagua burudani, tunachagua kile kitakachojaza akili zetu. Paulo aliandika hivi: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yanayopendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, mambo yoyote ya wema wa adili, na mambo yoyote yanayostahili sifa, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.” (Wafilipi 4:8) Tunapojaza akili zetu mambo mazuri kama hayo, tunaweza kusema hivi: “Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yakupendeze wewe, Ee Yehova.”—Zaburi 19:14.

19 Jiulize: ‘Ninajaza akili yangu mambo gani? Baada ya kutazama sinema au kipindi fulani, je, ninakuwa na mawazo mazuri, yenye kuburudisha? Je, ninahisi kwamba nina amani na kwamba nina dhamiri safi? (Waefeso 5:5; 1 Timotheo 1:5, 19) Je, ninajihisi huru kusali kwa Yehova? Au je, ninajihisi vibaya? Je, burudani hiyo ilinifanya nifikiri kuhusu ukatili au mambo mapotovu kiadili? (Mathayo 12:33; Marko 7:20-23) Je, burudani ninayochagua inanifinyanga kulingana na “mfumo huu wa mambo”?’ (Waroma 12:2) Majibu yetu ya unyoofu yanaweza kutusaidia kuona tunachohitaji kufanya ili kudumisha uhusiano mzuri na Yehova. Tungependa kusali kama mtunga-zaburi aliyesali hivi: “Yageuzie mbali macho yangu yasitazame mambo yasiyofaa.” *​—Zaburi 119:37.

MAAMUZI YETU YANAWAATHIRI WENGINE

20, 21. Kwa nini tunahitaji kuzingatia hisia za wengine tunapochagua burudani?

20 Kanuni nyingine muhimu tunayopaswa kukumbuka ni hii: “Mambo yote ni halali, lakini si mambo yote yanayojenga. Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:23, 24) Hatupaswi kufanya jambo kwa sababu tu tuna uhuru wa kulifanya. Tunapaswa kufikiria kwa uzito jinsi maamuzi yetu yanavyoathiri ndugu na dada zetu.

21 Dhamiri zinatofautiana. Kwa mfano, dhamiri yako inaweza kukuruhusu kutazama kipindi fulani cha televisheni. Lakini unagundua kwamba kipindi hicho kinasumbua dhamiri ya ndugu au dada yako. Utafanya nini? Hata ingawa una haki ya kukitazama, huenda ukaamua kwamba hutafanya hivyo. Kwa nini? Kwa sababu hutaki ‘kuwatendea dhambi ndugu zako’—au hata ‘kumtendea dhambi Kristo.’ (1 Wakorintho 8:12) Hatutaki kufanya chochote ambacho kitamkwaza Mkristo mwenzetu.—Waroma 14:1; 15:1; 1 Wakorintho 10:32.

22. Utaonyeshaje kwamba una usawaziko kuhusiana na maamuzi yanayofanywa na Wakristo wengine?

22 Kwa upande mwingine, namna gani ikiwa dhamiri yako haikuruhusu kutazama, kusoma, au kufanya jambo ambalo mwingine anahisi ni sawa kulifanya? Kwa sababu unampenda na kumheshimu ndugu yako, hutamshinikiza achague burudani zilezile unazochagua. Kwa mfano, mtu anayeendesha gari anajua kwamba watu wengine huenda wakaendesha kwa kasi au polepole kuliko yeye lakini bado ni madereva wazuri. Katika njia hiyohiyo, wewe na ndugu mwingine mnaweza kuwa mnatumia kanuni za Biblia lakini muwe na maoni yanayotofautiana kuhusu burudani zinazokubalika.—Mhubiri 7:16; Wafilipi 4:5.

23. Ni nini kitakachotusaidia kuchagua burudani kwa njia inayofaa?

23 Kwa hiyo, ni nini kitakachotusaidia kuchagua burudani vizuri? Tukitumia dhamiri yetu iliyozoezwa na kanuni za Biblia na ikiwa tunawajali kikweli ndugu na dada zetu, tutachagua kwa hekima. Na tutafurahi kwamba tunafanya “mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”

^ fu. 19 Tunaweza kupata kanuni zaidi za kutusaidia kuchagua burudani katika Methali 3:31; 13:20; Waefeso 5:3, 4; na Wakolosai 3:5, 8, 20.