Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 3

Chagua Marafiki Wanaompenda Mungu

Chagua Marafiki Wanaompenda Mungu

“Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima.” —METHALI 13:20.

1-3. (a) Methali 13:20 inatufundisha nini? (b) Kwa nini tunahitaji kuchagua marafiki kwa hekima?

JE, UMEWAHI kuona jinsi mtoto mdogo anavyowatazama wazazi wake? Hata kabla ya kujifunza kuongea, anajifunza kutokana na mambo anayotazama na kusikiliza. Anapoendelea kukua, anaanza kuwaiga wazazi wake hata bila kujua. Hiyo ndiyo sababu hata watu wazima huanza kufikiri na kutenda kama watu wanaoshirikiana nao kwa ukawaida.

2 Kwenye Methali 13:20, tunajifunza jambo hili: “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima.” Wazo linalotajwa hapo la ‘kutembea na’ mtu fulani linahusisha kuchagua kutumia wakati mwingi pamoja na mtu huyo. Hilo linahusisha mengi zaidi ya kuwa katika eneo moja na mtu huyo. Msomi mmoja wa Biblia alisema kwamba kutembea na mtu kunatia ndani wazo la kumpenda na kuwa na uhusiano wa karibu naye. Tunaathiriwa sana na watu tunaotumia wakati mwingi pamoja nao, hasa ikiwa tunahisi kuwa tuna uhusiano wa karibu nao.

3 Rafiki zetu wanaweza kuwa na uvutano juu yetu kwa njia nzuri au mbaya. Methali 13:20 inaendelea kusema: “Anayeshirikiana na wapumbavu ataumia.” Katika Kiebrania, ‘kushirikiana na’ mtu kunaweza kumaanisha ‘kuwa mwandamani’ wa mtu huyo, yaani, kuwa na urafiki naye. (Methali 22:24; Waamuzi 14:20) Marafiki wanaompenda Mungu watatutia moyo tuendelee kuwa waaminifu kwake. Ili tufaulu kuchagua marafiki kwa hekima, acheni tuzungumzie watu ambao Yehova anachagua wawe rafiki zake.

NI NANI RAFIKI ZA MUNGU?

4. Kwa nini ni heshima kubwa kuwa rafiki ya Mungu? Kwa nini Yehova alimwita Abrahamu “rafiki yangu”?

4 Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, anatupatia nafasi ya kuwa rafiki zake. Hiyo ni heshima kubwa. Yehova anawachagua rafiki zake kwa uangalifu. Anawachagua watu wanaompenda na wanaomwamini. Mfikirie Abrahamu. Alikuwa tayari kufanya chochote kwa ajili ya Mungu. Tena na tena, Abrahamu alionyesha kwamba alikuwa mwaminifu na mtiifu. Hata alikuwa tayari kumdhabihu mwana wake Isaka. Abrahamu alikuwa na imani kwamba “Mungu angeweza kumfufua hata kutoka kwa wafu.” (Waebrania 11:17-19; Mwanzo 22:1, 2, 9-13) Abrahamu alikuwa mwaminifu na mtiifu, na Yehova alimwita “rafiki yangu.”—Isaya 41:8; Yakobo 2:21-23.

5. Yehova anahisije kuhusu wale ambao ni washikamanifu kwake?

5 Yehova anawaona rafiki zake kuwa wenye thamani. Rafiki zake wanatanguliza kuwa washikamanifu kwake mbele ya kitu kingine chochote. (Soma 2 Samweli 22:26) Wao ni washikamanifu na watiifu kwa sababu wanampenda. Biblia inasema kwamba Mungu “ana urafiki wa karibu na watu wanyoofu,” yaani, wale ambao wanamtii. (Methali 3:32) Yehova anawakaribisha rafiki zake wawe wageni katika “hema” lake. Anawakaribisha wamwabudu na kusali kwake wakati wowote.—Zaburi 15:1-5.

6. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunampenda Yesu?

6 Yesu alisema: “Ikiwa yeyote ananipenda, atalishika neno langu, naye Baba yangu atampenda.” (Yohana 14:23) Kwa hiyo, ili tuwe marafiki wa Yehova, tunahitaji pia kumpenda Yesu na kufanya mambo ambayo alifundisha. Kwa mfano, tunatii maagizo ya Yesu ya kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20; Yohana 14:15, 21) Kwa sababu tunampenda Yesu, ‘tunafuata hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Petro 2:21) Yehova anafurahi anapoona tukifanya yote tunayoweza ili kumwiga Mwana wake kwa maneno na matendo.

7. Kwa nini tunapaswa kuhakikisha kwamba rafiki zetu ni rafiki za Yehova?

7 Marafiki wa Yehova ni waaminifu, washikamanifu, na watiifu, nao wanampenda Mwana wake. Je, tunachagua marafiki ambao Yehova anachagua? Rafiki zako wakimwiga Yesu na kuwa na bidii kuwafundisha wengine kuhusu Ufalme wa Mungu, wanaweza kukusaidia uwe na sifa nzuri na uendelee kuwa mshikamanifu kwa Yehova.

KUJIFUNZA KUTOKANA NA MIFANO YA BIBLIA

8. Ni nini kinachokupendeza kuhusu urafiki wa Ruthu na Naomi?

8 Katika Biblia, tunasoma kuhusu urafiki kati ya watu mbalimbali, kama vile Ruthu na mama-mkwe wake, Naomi. Wanawake hao walitoka katika nchi na malezi tofauti. Pia, Naomi alikuwa na umri mkubwa kuliko Ruthu. Walikuwa marafiki wa karibu kwa sababu wote wawili walimpenda Yehova. Naomi alipotaka kuondoka nchi ya Moabu na kurudi Israeli, ‘Ruthu alishikamana naye.’ Alimwambia Naomi hivi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:14, 16) Ruthu alimwonyesha Naomi fadhili nyingi. Walipofika Israeli, Ruthu alifanya kazi kwa bidii ili kumtegemeza rafiki yake. Naomi alimpenda sana Ruthu na akampa ushauri mzuri. Ruthu akamsikiliza, na kwa sababu hiyo, wote wawili walipata baraka nyingi.—Ruthu 3:6.

9. Ni nini kinachokupendeza kuhusu urafiki wa Daudi na Yonathani?

9 Urafiki wa Daudi na Yonathani ni mfano mwingine wa marafiki ambao walikuwa washikamanifu kwa Yehova. Yonathani alimzidi Daudi kwa umri wa miaka 30 hivi, naye Yonathani ndiye aliyepaswa kuwa mfalme anayefuata wa Israeli. (1 Samweli 17:33; 31:2; 2 Samweli 5:4) Hata hivyo, alipofahamu kwamba Yehova alikuwa amemchagua Daudi kuwa mfalme, hakumwonea wivu wala kushindana naye. Badala yake, Yonathani alifanya yote aliyoweza ili kumtegemeza Daudi. Kwa mfano, Daudi alipokuwa hatarini, Yonathani alimsaidia “kupata nguvu katika Yehova.” Hata alihatarisha uhai wake kwa ajili ya Daudi. (1 Samweli 23:16, 17) Daudi pia alikuwa rafiki mshikamanifu. Aliahidi kuitunza familia ya Yonathani, naye alitimiza ahadi hiyo hata baada ya Yonathani kufa.—1 Samweli 18:1; 20:15-17, 30-34; 2 Samweli 9:1-7.

10. Unajifunza nini kuhusu urafiki kutokana na mfano wa wale Waebrania watatu?

10 Shadraki, Meshaki, na Abednego walikuwa vijana watatu Waebrania ambao walikuwa marafiki. Walipelekwa utekwani walipokuwa wangali watoto. Ingawa walikuwa mbali na familia zao, walisaidiana kudumisha uaminifu wao kwa Yehova. Baadaye, walipokuwa watu wazima, imani yao ilijaribiwa Mfalme Nebukadneza alipowaamuru waabudu sanamu ya dhahabu. Shadraki, Meshaki na Abednego walikataa kuiabudu sanamu hiyo na wakamwambia mfalme hivi: “Hatutaiabudu miungu yako wala kuabudu sanamu ya dhahabu uliyosimamisha.” Imani yao ilipojaribiwa, marafiki hao watatu walidumisha ushikamanifu kwa Mungu wao.—Danieli 1:1-17; 3:12, 16-28.

11. Tunajuaje kwamba Paulo na Timotheo walikuwa marafiki wa karibu?

11 Mtume Paulo alipokutana na kijana Timotheo, aliona kwamba Timotheo alimpenda Yehova na alilijali sana kutaniko. Kwa hiyo, Paulo alimzoeza Timotheo kuwasaidia ndugu na dada walioishi katika maeneo mengi tofauti. (Matendo 16:1-8; 17:10-14) Timotheo alifanya kazi kwa bidii hivi kwamba Paulo akasema: “Alitumikia pamoja nami katika kuendeleza habari njema.” Paulo alijua kwamba Timotheo ‘angewajali kwa unyoofu’ akina ndugu na dada. Kadiri Paulo na Timotheo walivyoendelea kumtumikia Yehova kwa bidii pamoja, ndivyo walivyokuwa marafiki wa karibu.—Wafilipi 2:20-22; 1 Wakorintho 4:17.

JINSI YA KUCHAGUA MARAFIKI

12, 13. (a) Kwa nini tunahitaji kuchagua marafiki wetu kwa uangalifu hata kutanikoni? (b) Kwa nini mtume Paulo alitoa onyo lililo kwenye 1 Wakorintho 15:33?

12 Katika kutaniko, tunaweza kujifunza kutoka kwa ndugu na dada zetu na kusaidiana kudumisha uaminifu. (Soma Waroma 1:11, 12.) Lakini hata katika kutaniko, tunahitaji kuwa waangalifu tunapochagua marafiki wa karibu. Inapendeza kwamba tuna ndugu na dada wa aina tofauti ambao wanatoka katika utamaduni na malezi mbalimbali. Baadhi yao ni wapya kutanikoni, na wengine wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa miaka mingi. Muda unahitajika kwa uhusiano wa mtu na Yehova kukua, kama tu inavyochukua muda mrefu kwa matunda kuiva. Kwa hiyo, tunahitaji kuwa na subira na upendo, na sikuzote tuchague marafiki kwa hekima.—Waroma 14:1; 15:1; Waebrania 5:12–6:3.

13 Nyakati nyingine, hali inaweza kutokea kutanikoni inayohitaji tuwe waangalifu sana. Huenda ndugu au dada akafanya mambo ambayo Biblia inakataza. Au huenda mtu akawa na mtazamo wa kulalamika ambao unaweza kutokeza madhara kutanikoni. Hilo halitushangazi, kwa kuwa hata katika karne ya kwanza, nyakati nyingine kulikuwa na matatizo kutanikoni. Mtume Paulo aliwaonya Wakristo walioishi wakati huo hivi: “Msipotoshwe. Kushirikiana na watu wabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:12, 33) Pia, Paulo alimwonya Timotheo kwamba anapaswa kuwa mwangalifu anapochagua rafiki zake wa karibu. Sisi pia tunapaswa kuwa waangalifu.—Soma 2 Timotheo 2:20-22.

14. Uhusiano wetu na Yehova unaweza kuathiriwaje na watu tunaowachagua kuwa marafiki?

14 Lazima tulinde uhusiano wetu na Yehova. Hicho ndicho kitu chenye thamani zaidi kwetu. Kwa hiyo, tunaepuka kuwa marafiki wa karibu na mtu yeyote anayeweza kudhoofisha imani yetu na kuharibu uhusiano wetu na Yehova. Kama vile unapotumbukiza pamba ndani ya mafuta huwezi kutazamia ijae maji, hatuwezi kushirikiana na marafiki wanaotenda mabaya na kutazamia kwamba itakuwa rahisi kwetu kutenda mema. Tunahitaji kuwa waangalifu tunapochagua marafiki wa karibu.—1 Wakorintho 5:6; 2 Wathesalonike 3:6, 7, 14.

Unaweza kupata marafiki wanaompenda Yehova

15. Unaweza kufanya nini ili upate marafiki wazuri kutanikoni?

15 Katika kutaniko, unaweza kupata watu wanaompenda Yehova kikweli. Wanaweza kuwa rafiki zako wa karibu. (Zaburi 133:1) Usitafute marafiki wa umri au malezi yako tu. Kumbuka kwamba Yonathani alikuwa mwenye umri mkubwa sana kuliko Daudi, na Ruthu alikuwa na umri mdogo kuliko Naomi. Tunataka kutii shauri hili la Biblia: “Fungueni kabisa mioyo yenu.” (2 Wakorintho 6:13; soma 1 Petro 2:17.) Kadiri unavyomwiga Yehova, ndivyo wengine watakavyotaka kuwa marafiki wako.

MATATIZO YANAPOTOKEA

16, 17. Mtu kutanikoni akitukasirisha, tunapaswa kuepuka kufanya nini?

16 Katika kila familia, kuna watu wenye nyutu, maoni, na njia mbalimbali za kufanya mambo. Hilo ni kweli pia katika kutaniko. Tofauti hizo hufanya maisha yapendeze, na kila mtu anaweza kujifunza mengi kutoka kwa mwenzake. Lakini nyakati nyingine tofauti zetu zinaweza kutufanya tukose kumwelewa ndugu au dada na hivyo tumkasirikie. Pindi fulani tunaweza kuchukizwa au tukaumizwa hisia. (Methali 12:18) Je, turuhusu matatizo kama hayo yatuvunje moyo au yatufanye tuache kushirikiana na kutaniko?

17 Hapana. Hata mtu anapotuvunja moyo kwa njia fulani, hatupaswi kuacha kushirikiana na kutaniko. Si Yehova aliyetukasirisha. Yehova ametupa uhai na vitu vingine vyote. Anastahili upendo na ushikamanifu wetu. (Ufunuo 4:11) Kutaniko ni zawadi kutoka kwa Yehova inayotusaidia kuimarisha imani yetu. (Waebrania 13:17) Hatuwezi kukataa zawadi hiyo kutoka kwa Yehova eti kwa sababu tu mtu alituvunja moyo.—Soma Zaburi 119:165.

18. (a) Ni nini kinachoweza kutusaidia tuishi kwa amani na ndugu na dada zetu? (b) Kwa nini tunapaswa kuwasamehe wengine?

18 Tunawapenda ndugu na dada zetu na tunataka kuishi kwa amani pamoja nao. Yehova hatazamii mwanadamu yeyote awe mkamilifu, nasi pia hatupaswi kutazamia ukamilifu kutoka kwa yeyote. (Methali 17:9; 1 Petro 4:8) Sisi sote hukosea, lakini upendo utatusaidia tuendelee “kusameheana kwa hiari.” (Wakolosai 3:13) Tunapokosana kidogo, upendo utatuzuia tusifanye jambo hilo dogo liwe tatizo kubwa. Ni kweli kwamba mtu anapotukasirisha, huenda isiwe rahisi kuacha kufikiria kuhusu jambo hilo. Ni rahisi kukasirika na kuwa na kinyongo. Lakini hilo litatufanya tusiwe na furaha na kutuletea uchungu. Kwa upande mwingine, tunapomsamehe mtu ambaye alitukasirisha, tunaweza kuwa na amani ya akili, umoja kutanikoni, na muhimu zaidi, tutakuwa na uhusiano mzuri na Yehova.—Mathayo 6:14, 15; Luka 17:3, 4; Waroma 14:19.

MTU ANAPOTENGWA NA USHIRIKA

19. Ni wakati gani ambapo tunapaswa kuacha kushirikiana na mtu kutanikoni?

19 Katika familia yenye upendo, kila mtu hutimiza sehemu yake ili kuhakikisha wengine wana furaha. Lakini wazia kwamba mtu mmoja anaasi. Kila mtu katika familia anajaribu tena na tena kumsaidia, lakini anapuuza. Anaweza kuamua kuondoka nyumbani, au huenda kichwa cha familia akalazimika kumwambia aondoke. Jambo kama hilo linaweza kutokea kutanikoni. Huenda mtu akachagua kuendelea kufanya mambo yanayomchukiza Yehova na yanayolidhuru kutaniko. Anakataa msaada na kuonyesha kwa matendo yake kwamba hataki tena kuwa sehemu ya kutaniko. Huenda yeye mwenyewe akaamua kuliacha kutaniko, au huenda ikaamuliwa kwamba anapaswa kutengwa na ushirika. Hilo linapotokea, Biblia inasema waziwazi kwamba tunapaswa ‘kuacha kushirikiana’ naye. (Soma 1 Wakorintho 5:11-13; 2 Yohana 9-11) Inaweza kuwa vigumu sana kufanya hivyo ikiwa yeye ni rafiki yetu au mtu wa familia. Lakini katika hali kama hiyo, ushikamanifu wetu kwa Yehova unapaswa kuwa muhimu zaidi kuliko ushikamanifu wetu kwa mtu mwingine yeyote.—Soma Maelezo ya Ziada 8.

20, 21. (a) Mpango wa kutenga na ushirika unaonyeshaje upendo? (b) Kwa nini ni muhimu kwetu kuchagua marafiki kwa hekima?

20 Mpango wa kutenga na ushirika ni uandalizi wenye upendo kutoka kwa Yehova. Unahakikisha kwamba kutaniko linalindwa kutokana na watu ambao hawapendi viwango vya Yehova. (1 Wakorintho 5:7; Waebrania 12:15, 16) Unatusaidia kuonyesha jinsi tunavyolipenda jina takatifu la Yehova, viwango vyake vya juu, na tunavyompenda Yehova. (1 Petro 1:15, 16) Na mpango wa kutenga na ushirika ni njia ya kumwonyesha upendo mtu huyo ambaye si mshiriki wa kutaniko tena. Nidhamu hiyo kali inaweza kumsaidia kutambua kwamba anachofanya ni kosa na kumchochea kubadilika. Watu wengi ambao walikuwa wametengwa na ushirika walimrudia Yehova baadaye na wakakaribishwa tena kutanikoni kwa uchangamfu.—Waebrania 12:11.

21 Marafiki wetu hutuathiri, kwa njia moja au nyingine. Kwa hiyo, ni muhimu kuwachagua kwa uangalifu. Ikiwa tunawapenda wale ambao Yehova anawapenda, tutashirikiana na watu ambao watatusaidia kudumisha uaminifu wetu kwa Mungu milele.