Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 2

Dhamiri Njema Mbele za Mungu

Dhamiri Njema Mbele za Mungu

“Iweni na dhamiri njema.” —1 PETRO 3:16.

1, 2. Kwa nini unahitaji kuongozwa unapokuwa katika eneo usilolifahamu? Yehova ametupa nini ili kutuongoza?

WAZIA kwamba unatembea katika jangwa kubwa sana. Kila wakati ambapo upepo mkali unavuma unahamisha mchanga na hivyo mandhari inabadilika-badilika. Unaweza kupotea kwa urahisi. Utajuaje upande wa kuelekea? Unahitaji kuongozwa na mtu au kitu fulani. Huenda ukatumia dira, ramani, mfumo wa satelaiti (GPS), jua na nyota, au labda uongozwe na mtu anayefahamu jangwa hilo vizuri sana. Ni muhimu kuongozwa kwa sababu uhai wako unategemea kujua mahali unapopaswa kwenda.

2 Sisi sote tunakabili hali ngumu maishani, na nyakati fulani tunaweza kuhisi kwamba tumepotea. Lakini Yehova ametupa sisi sote dhamiri ya kutuongoza. (Yakobo 1:17) Acheni tujifunze dhamiri ni nini na jinsi inavyofanya kazi. Kisha tutajifunza jinsi tunavyoweza kuizoeza dhamiri yetu, jinsi ya kujali dhamiri za watu wengine, na jinsi kuwa na dhamiri safi kunavyoweza kutusaidia kuishi maisha mazuri.

DHAMIRI NI NINI NA INAFANYAJE KAZI?

3. Dhamiri ni nini?

3 Dhamiri yetu ni zawadi nzuri kutoka kwa Yehova. Ni uwezo ulio ndani yetu unaotusaidia kutofautisha mema na mabaya. Katika Biblia, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “dhamiri” linamaanisha “kujijua.” Dhamiri yetu inapofanya kazi vizuri, inatusaidia kuchunguza sisi ni watu wa aina gani. Inaweza kutusaidia tuchunguze mawazo na hisia zetu za ndani kwa unyoofu. Inaweza kutuongoza tufanye mema na tuepuke kufanya mabaya. Inaweza kutufanya tuwe na furaha tunapofanya uamuzi wenye hekima au tujihisi tuna hatia tunapofanya uamuzi mbaya.—Soma Maelezo ya Ziada 5.

4, 5. (a) Ni nini kilichotukia Adamu na Hawa walipopuuza dhamiri yao? (b) Kuna mifano gani ya Biblia inayoonyesha jinsi dhamiri inavyofanya kazi?

4 Kila mmoja wetu anaweza kuchagua ikiwa ataisikiliza dhamiri yake au la. Adamu na Hawa waliamua hawatasikiliza dhamiri zao, na kwa sababu hiyo wakatenda dhambi. Baadaye walijihisi wakiwa na hatia, lakini ilikuwa kuchelewa mno. Tayari walikuwa wamemwasi Mungu. (Mwanzo 3:7, 8) Hata ingawa kila mmoja wao alikuwa na dhamiri kamilifu na alijua ni kosa kumwasi Mungu, wote wawili waliamua kupuuza dhamiri zao.

5 Kwa upande mwingine, wanadamu wengi wasio wakamilifu wametii dhamiri zao. Ayubu ni mfano mzuri. Alisikiliza dhamiri yake na kufanya maamuzi mazuri, hivyo angeweza kusema hivi: “Moyo wangu hautanihukumu maadamu ninaishi.” (Ayubu 27:6) Ayubu alipotaja “moyo” wake, alikuwa akimaanisha dhamiri yake, uwezo wake wa kutofautisha mema na mabaya. Pindi fulani Daudi alipuuza dhamiri yake, hivyo akakosa kumtii Yehova. Baadaye, alijihisi kuwa mwenye hatia sana kana kwamba moyo wake ulikuwa ‘ukimchoma.’ (1 Samweli 24:5) Dhamiri ya Daudi ndiyo iliyokuwa ikimwambia amekosea. Kwa kusikiliza dhamiri yake, angeweza kuepuka kurudia kosa hilo.

6. Kwa nini tunaweza kusema kwamba dhamiri yetu ni zawadi kutoka kwa Mungu?

6 Kwa kawaida hata watu ambao hawamjui Yehova wanatambua kwamba mambo fulani ni mema na mengine ni mabaya. Biblia inasema hivi: “Kwa fikira zao wenyewe wanashtakiwa au hata kutetewa.” (Waroma 2:14, 15) Kwa mfano, watu wengi wanajua kwamba ni vibaya kuua au kuiba. Ingawa huenda wasitambue, wanasikiliza dhamiri zao, yaani, uwezo wa kutofautisha mema na mabaya ambao Yehova aliweka ndani yao. Pia wanafuata kanuni za Mungu, au kweli za msingi ambazo Yehova ametupatia ili kutusaidia kufanya maamuzi mazuri maishani.

7. Ni nini kinachoweza kufanya dhamiri yetu ituongoze vibaya?

7 Lakini pindi fulani dhamiri yetu inaweza kutuongoza vibaya. Kwa mfano, inaweza kupotoshwa na mawazo na hisia zetu zenye dhambi na kutuongoza kwa njia isiyofaa. Dhamiri nzuri haijitokezi tu yenyewe. (Mwanzo 39:1, 2, 7-12) Inahitaji kuzoezwa. Yehova ametupatia roho takatifu na kanuni za Biblia ili kutusaidia. (Waroma 9:1) Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuzoeza dhamiri yetu.

TUNAWEZA KUFANYA NINI ILI KUIZOEZA DHAMIRI?

8. (a) Hisia zetu zinaweza kuiathiri dhamiri yetu jinsi gani? (b) Tunapaswa kujiuliza swali gani kabla ya kufanya uamuzi?

8 Watu fulani wanafikiri kwamba kuisikiliza dhamiri kunamaanisha tu kufuata hisia zao. Wanafikiri kwamba wanaweza kufanya chochote wanachotaka maadamu jambo wanalofanya haliwasumbui. Lakini hisia zetu si kamilifu, na zinaweza kutuongoza vibaya. Hisia zetu zinaweza kuwa na nguvu sana hivi kwamba zikaathiri dhamiri yetu. Biblia inasema: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” (Yeremia 17:9) Kwa hiyo, tunaweza kufikiri kwamba kitu fulani ni sawa hata ikiwa ni kibaya. Kwa mfano, kabla ya Paulo kuwa Mkristo, aliwatesa vikali watu wa Mungu naye aliamini kwamba anafanya jambo zuri. Kwa maoni yake, alikuwa na dhamiri njema. Lakini baadaye alisema hivi: “Anayenichunguza ni Yehova.” (1 Wakorintho 4:4; Matendo 23:1; 2 Timotheo 1:3) Paulo alipojifunza jinsi Yehova alivyohisi kuhusu matendo yake, alitambua kwamba alihitaji kubadilika. Ni wazi kwamba kabla ya kufanya jambo fulani, tunahitaji kujiuliza, ‘Yehova anataka nifanye nini?’

9. Ni nini maana ya kumwogopa Mungu?

9 Unapompenda mtu, hutaki kumkosea. Kwa kuwa tunampenda Yehova, hatutaki kufanya jambo lolote litakalomkasirisha. Tunapaswa kuogopa sana kufanya jambo lolote litakalomchukiza Yehova. Fikiria mfano wa Nehemia. Alikataa kutumia cheo chake akiwa gavana kujipatia utajiri. Kwa nini? Alisema ni kwa sababu ‘alimwogopa Mungu.’ (Nehemia 5:15) Nehemia hakutaka kufanya jambo lolote ambalo lingemchukiza Yehova. Kama Nehemia, sisi pia tunaogopa kumkasirisha Yehova kwa kufanya jambo baya. Tunaposoma Biblia tunaweza kujifunza mambo yanayompendeza.—Soma Maelezo ya Ziada 6.

10, 11. Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kutusaidia kufanya maamuzi mazuri kuhusu kileo?

10 Kwa mfano, huenda Mkristo akahitaji kuamua ikiwa atatumia kileo au la. Ni kanuni gani zitakazomsaidia kufanya uamuzi mzuri? Zifuatazo ni baadhi yake: Biblia haikatazi kunywa kileo. Hata inasema kwamba divai ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Zaburi 104:14, 15) Hata hivyo, Yesu aliwaambia wafuasi wake ‘wasinywe kupita kiasi.’ (Luka 21:34) Na Paulo aliwaambia Wakristo waepuke “karamu zenye vurugu na ulevi.” (Waroma 13:13) Pia alisema kwamba walevi “hawataurithi Ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10.

11 Huenda ikafaa Mkristo ajiulize hivi: ‘Kileo ni muhimu kwangu kadiri gani? Je, ninaihitaji ili nijitulize? Je, ninakunywa kileo ili nijiamini zaidi? Je, ninaweza kudhibiti kiasi ninachokunywa na mara ambazo ninakunywa? * Je, ninaweza kufurahia ushirika na marafiki hata ikiwa hakuna kileo?’ Ni muhimu sana pia kumwomba Yehova atusaidie kufanya maamuzi yenye hekima. (Soma Zaburi 139:23, 24.) Tunapotafakari kanuni za Biblia na kujichunguza kwa unyoofu, tunaizoeza dhamiri yetu kutambua kanuni za Biblia. Lakini mengi zaidi yanahusika, kama tutakavyoona.

KWA NINI TUNAJALI DHAMIRI ZA WENGINE?

12, 13. Kwa nini huenda dhamiri yako ikatofautiana na ya mtu mwingine? Unaweza kushughulikiaje tofauti hizo?

12 Dhamiri zinatofautiana. Huenda dhamiri yako ikakuruhusu kufanya jambo ambalo dhamiri ya mtu mwingine haimruhusu. Kwa mfano, huenda ukaamua kunywa kileo, na mwingine akahisi kwamba hapaswi kunywa. Kwa nini huenda watu wawili wakawa na maoni tofauti kuhusu hilo?

Dhamiri iliyozoezwa inaweza kukusaidia kuamua ikiwa utakunywa kileo au la

13 Mara nyingi, hisia za mtu kuhusu jambo fulani zinaweza kuathiriwa na eneo ambalo alilelewa, jinsi familia yake ilivyoona jambo hilo, mambo aliyojionea maishani, na hali nyingine. Inapohusu kileo, huenda mtu ambaye zamani alikuwa na tatizo la kunywa kupita kiasi akaamua kutokunywa kabisa. (1 Wafalme 8:38, 39) Kwa hiyo, ukimpa mtu kileo naye akatae, utatendaje? Je, utakasirika? Je, utasisitiza anywe? Je, utamlazimisha akueleze sababu yake ya kukataa? Hapana. Hutafanya hivyo kwa sababu unaheshimu dhamiri yake.

14, 15. Ni hali gani iliyokuwepo katika siku za Paulo? Paulo alitoa ushauri gani mzuri?

14 Katika siku za mtume Paulo, hali fulani ilitokea ambayo ilionyesha jinsi dhamiri zinavyoweza kutofautiana. Nyama fulani zilizouzwa sokoni zilikuwa zimetumiwa katika ibada ya uwongo na kutolewa dhabihu kwa sanamu. (1 Wakorintho 10:25) Paulo hakuona kwamba kuna ubaya kununua na kula nyama hizo. Kwa maoni yake, chakula chote kilitoka kwa Yehova. Lakini ndugu fulani ambao zamani walikuwa waabudu wa sanamu walikuwa na maoni tofauti. Walihisi kwamba lilikuwa kosa kula nyama hizo. Unafikiri Paulo alijiambia kwamba kwa sababu haisumbui dhamiri yake, alikuwa na haki ya kula chochote alichotaka?

15 Paulo hakufikiri kwa njia hiyo. Hisia zake kuwaelekea ndugu zake zilikuwa muhimu sana hivi kwamba alikuwa tayari kudhabihu haki zake. Paulo alisema kwamba hatupaswi kuwa “tukijipendeza wenyewe.” Aliongezea hivi: “Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.” (Waroma 15:1, 3) Kama Yesu, Paulo aliwajali wengine kuliko alivyojijali.—Soma 1 Wakorintho 8:13; 10:23, 24, 31-33.

16. Kwa nini hatupaswi kumhukumu ndugu yetu kwa sababu ya mambo ambayo dhamiri yake inamruhusu kufanya?

16 Lakini namna gani dhamiri ya mtu fulani ikimruhusu kufanya jambo linaloonekana kuwa baya kwa maoni yetu? Tunahitaji kuwa waangalifu sana tusimchambue au kusisitiza kwamba amekosea. (Soma Waroma 14:10.) Yehova alitupatia dhamiri itusadie kujihukumu, si kuwahukumu wengine. (Mathayo 7:1) Tusingependa maamuzi yetu yasababishe mgawanyiko kutanikoni. Badala yake, tunatafuta njia za kuchochea upendo na umoja.—Waroma 14:19.

KUWA NA DHAMIRI NJEMA KUNAWEZA KUTUNUFAISHA

17. Dhamiri za watu fulani zimepatwa na nini?

17 Mtume Petro aliandika hivi: “Iweni na dhamiri njema.” (1 Petro 3:16) Kwa kusikitisha, watu wanapoendelea kupuuza kanuni za Yehova, hatimaye dhamiri zao zinaacha kuwaonya. Paulo alisema kwamba dhamiri kama hizo “zimetiwa alama kama kwa chuma cha moto.” (1 Timotheo 4:2) Je, umewahi kuungua sana? Mtu anapoungua, ngozi inakuwa na kovu baya ambalo haliwezi kuhisi chochote. Mtu anapoendelea kufanya mambo mabaya, ni kana kwamba dhamiri yake inaungua na kupatwa na kovu baya, na hatimaye inaacha kufanya kazi.

Dhamiri njema inaweza kutuongoza maishani na kutuletea shangwe na amani ya akili

18, 19. (a) Hisia za hatia au aibu zinatufundisha nini? (b) Tunaweza kufanya nini ikiwa tunahisi tuna hatia ya dhambi ambazo tayari tumetubu?

18 Tunapohisi kwamba tuna hatia, huenda dhamiri ikawa inatuambia tumekosea. Hilo linaweza kutusaidia tutambue kosa letu na tuache kulifanya. Tunapaswa kujifunza kutokana na makosa yetu ili tusiyarudie. Kwa mfano, ingawa Mfalme Daudi alitenda dhambi, dhamiri yake ilimchochea kutubu. Alichukia jambo alilokuwa amefanya naye akaazimia kwamba wakati ujao atamtii Yehova. Kutokana na mambo aliyojionea, Daudi angeweza kusema kwamba Yehova “ni mwema na [yuko] tayari kusamehe.”—Zaburi 51:1-19; 86:5; soma Maelezo ya Ziada 7.

19 Muda mrefu baada ya mtu kutubu dhambi aliyofanya, huenda bado akajihisi ana hatia. Hisia hizo zinaweza kumuumiza na kumfanya mtu ajihisi hafai. Ikiwa nyakati nyingine unahisi hivyo, kumbuka kwamba huwezi kubadili mambo yaliyotokea zamani. Iwe wakati huo ulijua au hukujua tofauti kati ya mema na mabaya, Yehova alikusamehe, na dhambi hizo zikafutwa. Uko safi mbele za Yehova na unajua kwamba sasa unafanya lililo sawa. Ingawa huenda bado moyo wako unakuhukumu, Biblia inasema hivi: “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu.” (Soma 1 Yohana 3:19, 20.) Hilo linamaanisha kwamba upendo na msamaha wake unaweza kutusaidia kushinda hisia zozote za hatia au za aibu tunazoweza kuwa nazo. Unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova amekusamehe. Mtu anapokubali kwamba Yehova amemsamehe, dhamiri yake inatulia naye anaweza kuwa na furaha anapomtumikia Mungu.—1 Wakorintho 6:11; Waebrania 10:22.

20, 21. (a) Kitabu hiki kimekusudiwa kukusaidia kufanya nini? (b) Yehova ametupatia uhuru gani? Tunapaswa kuutumiaje uhuru huo?

20 Kitabu hiki kimekusudiwa kukusaidia kuizoeza dhamiri yako ili ikuonye na kukulinda katika siku hizi za mwisho zilizo ngumu kushughulika nazo. Pia, kitakusaidia kufuata kanuni za Biblia unapokabili hali mbalimbali maishani. Bila shaka, kitabu hiki hakitatuonyesha orodha ya sheria tunazopaswa kufuata katika hali zote. Tunaishi kupatana na “sheria ya Kristo,” inayotegemea kanuni za Mungu. (Wagalatia 6:2) Hatufikiri kwamba kwa kuwa hakuna sheria hususa kuhusu jambo fulani basi huo ni udhuru wa kutenda mabaya. (2 Wakorintho 4:1, 2; Waebrania 4:13; 1 Petro 2:16) Badala yake, tunatumia uhuru wetu kuonyesha kwamba tunampenda Yehova.

21 Tunapotafakari kanuni za Biblia na kuzitumia, tunajifunza kutumia ‘nguvu zetu za utambuzi’ na kufikiri kama Yehova anavyofikiri. (Waebrania 5:14) Matokeo ni kwamba tutakuwa na dhamiri iliyozoezwa itakayotuongoza maishani na kutusaidia kudumu katika upendo wa Mungu.

^ fu. 11 Madaktari wengi wanasema kwamba ni vigumu zaidi kwa waraibu wa kileo kudhibiti kiasi wanachokunywa. Madaktari wanapendekeza kwamba waraibu wasinywe kileo kabisa.