Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 17

Dumu Katika Upendo wa Mungu

Dumu Katika Upendo wa Mungu

“Jijengeni juu ya imani yenu takatifu zaidi . . . mwendelee kujitunza katika upendo wa Mungu.”—YUDA 20, 21.

1, 2. Tunaweza kufanya nini ili kudumu katika upendo wa Mungu?

SISI sote tunataka kuwa na nguvu na afya nzuri. Kwa hiyo, tunajitahidi kula chakula chenye lishe, kufanya mazoezi kwa ukawaida, na kutunza miili yetu. Ingawa jitihada inahitajika, tunafurahia faida za kufanya hivyo, kwa hiyo hatufi moyo. Vivyo hivyo, tunahitaji kuendelea kuwa na nguvu na afya nzuri katika njia nyingine pia.

2 Hata ingawa tumeanza kumjua Yehova, tunahitaji kuendelea kuimarisha uhusiano wetu pamoja naye. Yuda alipowatia moyo Wakristo ‘waendelee kujitunza katika upendo wa Mungu,’ alieleza jinsi wanavyoweza kufanya hivyo. Aliwaambia hivi: “Jijengeni juu ya imani yenu takatifu zaidi.” (Yuda 20, 21) Kwa hiyo, tunaweza kufanya nini ili tuwe na imani yenye nguvu?

ENDELEA KUJENGA IMANI YAKO

3-5. (a) Shetani angependa uhisije kuhusu viwango vya Yehova? (b) Wewe una maoni gani kuhusu sheria na kanuni za Yehova?

3 Ni muhimu kujisadikishia kwamba njia za Yehova ndizo bora. Shetani anataka ufikiri kwamba ni vigumu sana kuishi kupatana na viwango vya Mungu na kwamba utakuwa na furaha ukijiamulia mema na mabaya. Tangu bustani ya Edeni, Shetani amejaribu kuwafanya watu waamini hivyo. (Mwanzo 3:1-6) Naye bado anajaribu sana kufanya hivyo leo.

4 Je, Shetani anasema kweli? Je, viwango vya Yehova vinatubana sana? Hapana. Kwa mfano, jiwazie ukitembea katika bustani maridadi. Unaona kwamba kuna kizuizi kinachowazuia watu wasiingie eneo fulani. Huenda ukajiuliza kwa nini umezuiwa usiingie eneo hilo. Lakini ghafla unasikia simba akinguruma upande ule mwingine. Utahisije? Utafurahi kwamba kizuizi hicho kinakulinda usiliwe na simba, sivyo? Kanuni za Yehova ni kama kizuizi hicho, naye Ibilisi ni kama simba huyo. Neno la Mungu linatuonya hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni waangalifu! Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.”—1 Petro 5:8.

5 Yehova anataka tuwe na maisha bora zaidi. Hataki tudanganywe na Shetani. Hiyo ndiyo sababu ametupatia sheria na kanuni za kutulinda na kutufanya tuwe na furaha. (Waefeso 6:11) Yakobo aliandika hivi: “Anayechunguza sheria kamilifu ambayo ni ya uhuru na kudumu katika hiyo . . . atafurahia kile anachofanya.”—Yakobo 1:25.

6. Tunaweza kufanya nini ili tusadiki kwamba njia za Mungu ndizo bora?

6 Tunapofuata mwongozo wa Yehova, tunaboresha maisha yetu na urafiki wetu pamoja naye unaimarika. Kwa mfano, tunanufaika tunapokubali mwaliko anaotupa wa kusali kwake mara nyingi. (Mathayo 6:5-8; 1 Wathesalonike 5:17) Tunafurahi tunapotii mwongozo wake wa kukutana ili kumwabudu na kutiana moyo na pia tunaposhiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. (Mathayo 28:19, 20; Wagalatia 6:2; Waebrania 10:24, 25) Tunapofikiria jinsi ambavyo mambo hayo yametusaidia kudumisha imani yetu ikiwa imara, tunasadiki hata zaidi kwamba njia za Yehova ndizo bora.

7, 8. Ni nini kitakachotusaidia kuepuka wasiwasi kuhusu majaribu tunayoweza kukabili wakati ujao?

7 Huenda tukawa na wasiwasi kwamba wakati ujao tutakabili majaribu makali sana ya imani hivi kwamba tutashindwa kuidumisha. Ukihisi hivyo wakati wowote, kumbuka maneno haya ya Yehova: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Ninayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Ninayekuongoza katika njia unayopaswa kutembea. Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.”—Isaya 48:17, 18.

8 Tunapomtii Yehova, amani yetu itakuwa kama mto ambao haukauki na uadilifu wetu utakuwa kama mawimbi ya bahari ambayo kila wakati yanafika ufuoni. Hata tukabili nini maishani tunaweza kuwa waaminifu kwake. Biblia inaahidi hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye atakutegemeza. Hataruhusu kamwe mwadilifu aanguke.”—Zaburi 55:22.

“TUSONGE MBELE KUELEKEA UKOMAVU”

9, 10. Kukomaa kunamaanisha nini?

9 Unapoimarisha uhusiano wako na Yehova, ‘utasonga mbele kuelekea ukomavu.’ (Waebrania 6:1) Ni nini maana ya kuwa mkomavu?

10 Hatuwi Wakristo wakomavu kwa sababu tu ya kuzeeka. Ili tukomae, lazima tumfanye Yehova kuwa Rafiki yetu wa karibu zaidi na kujaribu kuwa na maoni kama yake. (Yohana 4:23) Paulo aliandika hivi: “Wale wanaoishi kulingana na mwili hukaza akili zao kwenye mambo ya mwili, lakini wale wanaoishi kulingana na roho kwenye mambo ya roho.” (Waroma 8:5) Mtu mkomavu hatangulizi raha au vitu vya kimwili maishani mwake. Badala yake, anakazia fikira kumtumikia Yehova na kufanya maamuzi yenye hekima maishani mwake. (Methali 27:11; soma Yakobo 1:2, 3.) Hajiruhusu ashawishiwe kutenda mabaya. Mkristo mkomavu anajua kilicho sawa na anaazimia kulifanya.

11, 12. (a) Paulo alisema nini kuhusu ‘nguvu za utambuzi’ za Mkristo? (b) Kuna ulinganifu gani kati ya kuwa Mkristo mkomavu na kuwa mkimbiaji?

11 Jitihada zinahitajika ili kufikia ukomavu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Lakini chakula kigumu ni cha watu wakomavu, ambao wamezoeza nguvu zao za utambuzi kwa kuzitumia ili kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.” (Waebrania 5:14) Neno “wamezoeza” linatufanya tufikirie kuhusu mazoezi ambayo mkimbiaji hufanya.

12 Tunapomwona mkimbiaji mwenye ustadi akikimbia, tunajua kwamba muda na mazoezi mengi yalihusika ili kusitawisha kipaji chake. Hakuzaliwa akiwa mkimbiaji. Mtoto anapozaliwa, hajui jinsi ya kutumia mikono na miguu yake. Lakini kadiri muda unavyopita anajifunza jinsi ya kushika vitu na jinsi ya kutembea. Ikiwa atazoezwa, huenda siku moja akawa mkimbiaji. Kwa njia kama hiyo, tunahitaji muda na mazoezi mengi ili tuwe Wakristo wakomavu.

13. Ni nini kitakachotusaidia kujifunza kufikiri kama Yehova anavyofikiri?

13 Katika kitabu hiki, tumechunguza jinsi ambavyo tunaweza kufikiri kama Yehova anavyofikiri na kuona mambo kama yeye anavyoyaona. Tumejifunza kuthamini na kupenda viwango vya Yehova. Tunapofanya maamuzi, tunajiuliza: ‘Ni sheria au kanuni gani za Biblia zinazohusika katika hali ninayokabili? Ninaweza kuzitumiaje? Yehova angependa nifanye nini?’—Soma Methali 3:5, 6; Yakobo 1:5.

14. Tunahitaji kufanya nini ili tuimarishe imani yetu?

14 Hatuachi kamwe kuimarisha imani yetu katika Yehova. Kama tu kula chakula kilicho na lishe kunavyojenga miili yetu, ndivyo kujifunza kumhusu Yehova kunavyotusaidia kujenga imani yenye nguvu. Tulipoanza kujifunza Biblia, tulijifunza kweli za msingi kumhusu Yehova na njia zake. Lakini kadiri muda unavyopita, tunahitaji kuelewa mambo yenye kina zaidi. Hilo ndilo jambo ambalo Paulo alimaanisha aliposema: “Chakula kigumu ni cha watu wakomavu.” Tunapotumia mambo tuliyojifunza, tunapata hekima. Biblia inatuambia hivi: “Hekima ndilo jambo muhimu zaidi.”—Methali 4:5-7; 1 Petro 2:2.

15. Ni muhimu kadiri gani kwamba tumpende Yehova na ndugu na dada zetu?

15 Mtu anaweza kuwa na nguvu na afya nzuri, lakini anajua kwamba ili aendelee hivyo lazima ajitunze. Katika njia hiyohiyo, mtu mkomavu anajua kwamba anahitaji kutia bidii ili kudumisha uhusiano wake pamoja na Yehova ukiwa imara. Paulo anatukumbusha hivi: “Endeleeni kujijaribu kama mko katika imani, endeleeni kuthibitisha jinsi ninyi wenyewe mlivyo.” (2 Wakorintho 13:5) Lakini haitoshi tu kuwa na imani yenye nguvu. Lazima tuongeze upendo wetu kwa Yehova na kwa ndugu na dada zetu. Paulo alisema hivi: “Ikiwa nina . . . ujuzi wote, na ikiwa nina imani yenye nguvu hata niweze kuhamisha milima, lakini sina upendo, mimi si kitu.”—1 Wakorintho 13:1-3.

KAZIA FIKIRA TUMAINI LAKO

16. Shetani angependa tuhisije?

16 Shetani anataka tufikiri kwamba hatuwezi kumpendeza Yehova kwa kiasi kinachofaa. Anataka tuvunjike moyo na tufikiri kwamba matatizo yetu hayawezi kusuluhishwa. Hataki tuwaamini Wakristo wenzetu, wala hataki tuwe na furaha. (Waefeso 2:2) Shetani anajua kwamba mawazo yasiyofaa yatatuathiri sisi na uhusiano wetu na Mungu. Lakini Yehova ametupa msaada wa kupambana na mawazo yasiyofaa. Ametupa tumaini.

17. Tumaini ni muhimu kadiri gani?

17 Kwenye 1 Wathesalonike 5:8, Biblia inalinganisha tumaini letu na kofia inayolinda kichwa cha mwanajeshi akiwa vitani. Inasema kofia hiyo ni “tumaini la wokovu.” Kutumaini ahadi za Yehova kunaweza kulinda akili zetu na kutusaidia kuepuka mawazo yasiyofaa.

18, 19. Tumaini lilimwimarishaje Yesu?

18 Tumaini la Yesu lilimwimarisha. Usiku kabla ya kifo chake, alikabili hali moja ngumu baada ya nyingine. Alisalitiwa na rafiki yake. Mwingine alimkana. Nao wengine walimwacha na kukimbia. Watu wa nchi yake mwenyewe walimkataa na kushinikiza kwamba ateswe na kuuawa. Ni nini kilichomsaidia kuvumilia mambo hayo yenye kuumiza? “Kwa sababu ya shangwe iliyowekwa mbele yake, alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.”—Waebrania 12:2.

19 Yesu alijua kwamba ikiwa angeendelea kuwa mwaminifu, angemletea Baba yake utukufu na kumthibitisha Shetani kuwa mwongo. Tumaini hilo lilimletea shangwe kubwa. Pia alijua kwamba baada ya muda mfupi angekuwa tena na Baba yake mbinguni. Tumaini hilo lilimsaidia kuvumilia. Kama Yesu, tunapaswa kukazia fikira tumaini letu. Litatusaidia kuvumilia hali ngumu ya aina yoyote ile.

20. Ni nini kitakachokusaidia uepuke mawazo yasiyofaa?

20 Yehova anaona imani na uvumilivu wako. (Isaya 30:18; soma Malaki 3:10.) Anaahidi “atatosheleza tamaa za moyo wako.” (Zaburi 37:4) Kwa hiyo, kazia fikira tumaini lako. Shetani anataka ukate tamaa na uhisi kwamba ahadi za Yehova hazitatimia. Lakini hupaswi kuwa na mawazo hayo yasiyofaa! Ukigundua kwamba tumaini lako limeanza kufifia, mwombe Yehova msaada. Kumbuka maneno ya Wafilipi 4:6, 7: “Msihangaike kuhusiana na jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu; na amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kupitia Kristo Yesu.”

21, 22. (a) Yehova ana kusudi gani kwa dunia? (b) Umeazimia kufanya nini?

21 Mara kwa mara, tenga wakati wa kutafakari jinsi wakati ujao utakavyokuwa wenye kusisimua. Hivi karibuni, kila mtu aliye hai atamwabudu Yehova. (Ufunuo 7:9, 14) Fikiria jinsi maisha yatakavyokuwa katika ulimwengu mpya. Yatakuwa mazuri kuliko tunavyoweza kuwazia! Shetani, roho wake waovu, na uovu wote hautakuwepo. Hutakuwa mgonjwa, wala hutakufa. Kila siku utakuwa na nguvu na furaha kuwa hai. Kila mtu atakuwa na chakula kizuri na mahali salama pa kuishi. Watu hawatatendeana kwa ukatili au jeuri, badala yake watatendeana kwa fadhili. Hatimaye, wanadamu wote duniani watafurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Waroma 8:21.

22 Yehova anataka umfanye kuwa Rafiki yako wa karibu zaidi. Kwa hiyo, fanya yote uwezayo kumtii Yehova na kumkaribia kila siku. Naam, sisi sote na tudumu katika upendo wa Mungu milele!—Yuda 21.