Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 15

Furahia Kazi Yako

Furahia Kazi Yako

“Kila mtu anapaswa . . . kufurahia kazi yake yote ngumu.”—MHUBIRI 3:13.

1-3. (a) Watu wengi wanahisije kuhusu kazi zao? (b) Tutachunguza maswali gani katika sura hii?

WATU ulimwenguni pote wanafanya kazi kwa bidii ili kujitegemeza na kuruzuku familia zao. Watu wengi hawapendi kazi zao, na wengine hata huogopa kwenda kazini kila siku. Ikiwa hivyo ndivyo unavyohisi, unaweza kufanya nini ili uwe na maoni yanayofaa kuhusu kazi yako na uifurahie?

2 Yehova anatuambia hivi: “Kila mtu anapaswa kula na kunywa na kufurahia kazi yake yote ngumu. Ni zawadi kutoka kwa Mungu.” (Mhubiri 3:13) Yehova alituumba tukiwa na uhitaji na tamaa ya kufanya kazi. Anataka tufurahie kazi yetu.—Soma Mhubiri 2:24; 5:18.

3 Kwa hiyo, ni nini kinachoweza kutusaidia kufurahia kazi yetu? Mkristo anapaswa kuepuka kufanya kazi za aina gani? Tunaweza kufanya nini ili kuwa na usawaziko kuhusu kazi ya kimwili na ibada yetu kwa Yehova? Na ni kazi gani muhimu zaidi ambayo tunaweza kufanya?

WAFANYAKAZI WAWILI WAKUU ZAIDI

4, 5. Yehova ana maoni gani kuhusu kazi?

4 Yehova anapenda kufanya kazi. Mwanzo 1:1 inasema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Baada ya Mungu kumaliza kuumba dunia na kila kitu ndani yake, alisema kwamba kila kitu alichoumba kilikuwa “chema sana.” (Mwanzo 1:31) Muumba aliridhishwa na kile alichokuwa ametengeneza.—1 Timotheo 1:11.

5 Hakuna wakati ambapo Yehova anaacha kufanya kazi. Yesu alisema: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa.” (Yohana 5:17) Ingawa hatuwezi kujua kuhusu mambo yote mazuri ambayo Yehova amekuwa akifanya, tunajua baadhi yake. Amekuwa akichagua wale watakaotawala na Mwana wake, Yesu Kristo, wakiwa sehemu ya Ufalme. (2 Wakorintho 5:17) Pia, Yehova anawaongoza na kuwatunza wanadamu. Kutokana na kazi ya kuhubiri inayofanywa ulimwenguni pote, mamilioni ya watu wanapata nafasi ya kumjua Yehova na wanakuwa na tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani.—Yohana 6:44; Waroma 6:23.

6, 7. Yesu alikuwa mfanyakazi wa aina gani?

6 Kama tu Baba yake, Yesu anapenda kufanya kazi. Kabla ya kuja duniani, Yesu alikuwa “mfanyakazi stadi” wa Mungu, akishiriki katika uumbaji wa kila kitu mbinguni na duniani. (Methali 8:22-31; Wakolosai 1:15-17) Alipokuwa duniani, Yesu aliendelea kufanya kazi kwa bidii. Alipokuwa kijana alijifunza kuwa seremala stadi, labda alitengeneza vifaa vya mbao na hata alijenga nyumba. Yesu alijifunza kufanya kazi hiyo kwa ustadi mwingi hivi kwamba alijulikana kama “yule seremala.”—Marko 6:3.

7 Hata hivyo, kazi muhimu zaidi ambayo Yesu alifanya alipokuwa duniani ni kuhubiri habari njema na kuwafundisha watu kumhusu Yehova. Alikuwa na muda wa miaka mitatu na nusu kukamilisha huduma yake, naye alifanya kazi kwa bidii kuanzia asubuhi hadi usiku sana. (Luka 21:37, 38; Yohana 3:2) Yesu alitembea mamia ya kilomita kwenye barabara zenye vumbi, ili kushiriki habari njema na watu wengi kadiri iwezekanavyo.—Luka 8:1.

8, 9. Kwa nini Yesu alifurahia kazi alizofanya?

8 Kwa maoni ya Yesu, kufanya kazi ya Mungu kulikuwa kama chakula. Kazi hiyo ilimpa nguvu. Kuna siku ambazo Yesu alifanya kazi kwa bidii sana hivi kwamba hata hakupata nafasi ya kula. (Yohana 4:31-38) Alitumia nafasi zote alizopata kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Baba yake. Hiyo ndiyo sababu angeweza kumwambia Yehova: “Nimekutukuza duniani, kwa kuwa nimemaliza kazi uliyonipa nifanye.”—Yohana 17:4.

9 Ni wazi kwamba Yehova na Yesu wanafanya kazi kwa bidii sana na wanafurahia na kuridhishwa na kazi yao. Tunataka kuwa “waigaji wa Mungu” na pia tunataka ‘kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu.’ (Waefeso 5:1; 1 Petro 2:21) Hiyo ndiyo sababu tunajaribu kufanya kazi kwa bidii na kuifanya kwa njia bora.

TUNAPASWA KUWA NA MAONI GANI KUHUSU KAZI YETU?

10, 11. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa na mtazamo mzuri kuhusu kazi tunayofanya?

10 Tukiwa watu wa Yehova, tunafanya kazi kwa bidii ili kujitegemeza na kuruzuku familia zetu. Ingawa tungependa kufurahia kazi yetu, inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo. Kwa hiyo, tunaweza kufanya nini ikiwa hatufurahii kazi yetu?

Kuwa na mtazamo unaofaa kunaweza kukusaidia kufurahia zaidi kazi yoyote unayofanya

11 Uwe na mtazamo unaofaa. Huenda tusiweze kubadili mahali ambapo tunafanya kazi au tunafanya kazi nyingi kadiri gani, lakini tunaweza kubadili mtazamo wetu. Kuelewa kile ambacho Yehova anatazamia tufanye kunaweza kutusaidia. Kwa mfano: Yehova anatazamia kichwa cha familia ashughulikie mahitaji ya familia yake kwa kadiri ya uwezo wake. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba mtu anayekosa kuandalia familia yake “ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Ikiwa wewe ni kichwa cha familia, unafanya kazi kwa bidii kuandalia familia yako. Iwe unaipenda kazi yako au la, unajua kwamba kwa kuiandalia familia yako, unamfurahisha Yehova.

12. Kufanya kazi kwa bidii na kwa unyoofu kunatunufaishaje?

12 Uwe mnyoofu na mwenye bidii. Ukifanya hivyo huenda ikawa rahisi zaidi kufurahia kazi yako. (Methali 12:24; 22:29) Sababu moja ni kwamba mwajiri wako atakuamini. Waajiri wanawathamini wafanyakazi wanyoofu kwa sababu hawaibi pesa, vifaa, au wakati. (Waefeso 4:28) Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba Yehova anajua unapofanya kazi kwa bidii na kwa unyoofu. Unaweza kuwa na “dhamiri nyoofu,” kwa sababu unajua unampendeza Mungu ambaye unampenda.—Waebrania 13:18; Wakolosai 3:22-24.

13. Kuna faida gani nyingine ya kuwa mnyoofu kazini?

13 Tambua kwamba mwenendo wako kazini unaweza kumletea Yehova sifa. Hilo linatupa sababu nyingine ya kufurahia kazi yetu. (Tito 2:9, 10) Huenda hata mfanyakazi mwenzako akataka kujifunza Biblia kwa sababu ya mfano wako mzuri.—Soma Methali 27:11; 1 Petro 2:12.

NIFANYE KAZI GANI?

14-16. Tunahitaji kufikiria nini tunapochagua kazi?

14 Biblia haina orodha ya kazi ambazo Mkristo anaweza kukubali na zile anazopaswa kukataa. Lakini ina kanuni ambazo zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayofaa kuhusu kazi. (Methali 2:6) Tukitumia kanuni za Biblia, tunaweza kujiuliza maswali yafuatayo.

Tafuta kazi ambayo haipingani na kanuni za Yehova

15 Je, nikikubali kazi hii nitafanya jambo ambalo Yehova anasema ni kosa? Tumejifunza kuhusu mazoea ambayo Yehova anachukia, kama vile kuiba na kusema uwongo. (Kutoka 20:4; Matendo 15:29; Waefeso 4:28; Ufunuo 21:8) Kwa hiyo, tunakuwa waangalifu kuepuka kazi yoyote ambayo inapinga viwango vya Yehova.—Soma 1 Yohana 5:3.

16 Je, kazi hii inaunga mkono zoea ambalo Yehova anashutumu? Kwa mfano, namna gani ukipata kazi kwenye mapokezi ya kliniki ya kutoa mimba? Hakuna ubaya kufanya kazi kwenye mapokezi. Lakini unajua jinsi Yehova anavyohisi kuhusu kutoa mimba. Kwa hiyo, ingawa wewe binafsi hufanyi kazi ya kutoa mimba, je, usingehisi kwamba kwa maoni ya Yehova wewe pia una hatia?—Kutoka 21:22-24.

17. Ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayompendeza Mungu?

17 Tunapotumia kanuni za Mungu, tunaweza kuwa aina ya watu wanaofafanuliwa kwenye Waebrania 5:14, “ambao wamezoeza nguvu zao za utambuzi kwa kuzitumia ili kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.” Jiulize: ‘Nikikubali kazi hii, je, nitawakwaza watu wengine? Je, nikifanya kazi hii nitalazimika kuhamia nchi nyingine na kumwacha mke wangu na watoto wangu kwa muda mrefu? Kufanya hivyo kutawaathirije?’

“MHAKIKISHE MAMBO MUHIMU ZAIDI”

18. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kutanguliza ibada yetu?

18 Inaweza kuwa vigumu kutanguliza ibada yetu kwa Yehova katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Huenda ikawa vigumu sana kupata kazi na kuidumisha. Tunahitaji kutunza familia yetu, lakini tunajua kwamba tunapaswa kutanguliza ibada yetu. Hatupaswi kuruhusu mambo ya kimwili yawe muhimu sana maishani mwetu. (1 Timotheo 6:9, 10) Kwa hiyo, tunaweza kufanya nini ili ‘kuhakikisha mambo muhimu zaidi’ na wakati uleule kuiandalia familia yetu mahitaji yake?—Wafilipi 1:10.

19. Kumtegemea Yehova kunaweza kutusaidiaje tuwe na usawaziko kuhusu kazi?

19 Mtegemee Yehova kabisa. (Soma Methali 3:5, 6.) Tunajua kwamba Mungu anajua tunachohitaji hasa na kwamba anatujali sana. (Zaburi 37:25; 1 Petro 5:7) Neno lake linatuambia hivi: “Njia yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu mlivyo navyo. Kwa maana [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa kamwe.’” (Waebrania 13:5) Yehova hataki tuwe na wasiwasi kupita kiasi kuhusu kuiandalia familia yetu. Ameonyesha mara nyingi sana kwamba anaweza kuwaandalia watu wake mahitaji yao. (Mathayo 6:25-32) Licha ya kazi tunayofanya, tunahakikisha kwamba tunajifunza Neno la Mungu kwa ukawaida, tunahubiri habari njema, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo.—Mathayo 24:14; Waebrania 10:24, 25.

20. Tunaweza kufanya nini ili kurahisisha maisha yetu?

20 Hakikisha jicho lako linakazia jambo hususa. (Soma Mathayo 6:22, 23.) Hilo linamaanisha kurahisisha maisha yako ili ukazie fikira kumtumikia Yehova. Tunajua kwamba ni upumbavu kuruhusu pesa, maisha ya starehe, au vifaa vya karibuni zaidi viwe muhimu zaidi kwetu kuliko urafiki wetu na Mungu. Kwa hiyo, ni nini kitakachotusaidia kutanguliza mambo ya kiroho? Tunapaswa kujitahidi kuepuka madeni. Ikiwa tayari una madeni, fanya mpango wa kuyapunguza au kuyalipa yote. Tusipokuwa waangalifu, vitu vya kimwili vinaweza kuchukua wakati na nguvu zetu nyingi, na huenda tusiwe na wakati wa kusali, kujifunza, au kuhubiri. Badala ya kuruhusu vitu vya kimwili vifanye maisha yetu kuwa magumu, tungependa kujifunza kuridhika na vitu vya msingi kama vile “chakula na mavazi.” (1 Timotheo 6:8) Hata tuwe tunakabili hali gani, ni vizuri kuchunguza hali yetu mara kwa mara ili kuona ni kwa njia gani tunaweza kumtumikia Yehova kikamili zaidi.

21. Kwa nini tunahitaji kuchagua mambo ya kutanguliza maishani mwetu?

21 Tambua mambo ya kutanguliza. Tunahitaji kutumia wakati, nguvu, na vitu vya kimwili kwa hekima. Tusipokuwa waangalifu, mambo yasiyo muhimu sana, kama vile elimu au pesa, yanaweza kuchukua wakati wetu wenye thamani. Yesu alisema: “Endeleeni kuutafuta kwanza Ufalme.” (Mathayo 6:33) Maamuzi tunayofanya, mazoea yetu, shughuli zetu za kila siku, na miradi yetu hufunua ni nini kilicho cha maana zaidi moyoni mwetu.

KAZI MUHIMU ZAIDI TUNAYOWEZA KUFANYA

22, 23. (a) Ni kazi gani muhimu zaidi tunayoweza kufanya tukiwa Wakristo? (b) Ni nini kitakachotusaidia kufurahia kazi yetu?

22 Kazi muhimu zaidi ni ile ya kumtumikia Yehova na kuwahubiria wengine habari njema. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kama Yesu, tunataka kufanya yote tuwezayo katika kazi hiyo. Wengine wamehamia maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Wengine wanajifunza lugha ya kigeni ili wawahubirie watu wanaozungumza lugha hiyo. Zungumza na wale ambao wamefanya hivyo na uwaulize walifauluje. Watakueleza jinsi wamekuwa na furaha zaidi maishani na jinsi maisha yao yamekuwa na maana zaidi.—Soma Methali 10:22.

Kumtumikia Yehova ndiyo kazi muhimu zaidi tunayoweza kufanya

23 Leo, wengi wetu wanalazimika kufanya kazi kwa muda mrefu au hata kufanya kazi kadhaa ili tu kuiandalia familia mahitaji ya msingi. Yehova anajua jambo hilo na anathamini kila kitu tunachofanya ili kutunza familia zetu. Sisi sote na tuendelee kumwiga Yehova na Yesu kwa kufanya kazi kwa bidii, hata iwe tunafanya kazi ya aina gani. Na tukumbuke kwamba kazi muhimu zaidi tunayoweza kufanya ni kumtumikia Yehova na kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Kufanya hivyo kunatuletea shangwe ya kweli.