Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 5

Jinsi ya Kujitenga na Ulimwengu

Jinsi ya Kujitenga na Ulimwengu

“Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” —YOHANA 15:19.

1. Yesu alihangaikia nini usiku kabla ya kifo chake?

ULIKUWA usiku wa mwisho kabla ya kifo cha Yesu. Alijua kwamba alikuwa karibu kuwaacha wanafunzi wake, na alihangaikia wakati wao ujao. Aliwaambia hivi: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Baadaye, alisali kwa Baba yake kuwahusu, akisema hivi: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:15, 16) Yesu alimaanisha nini?

2. Yesu alizungumza kuhusu “ulimwengu” gani?

2 Neno “ulimwengu” kama linavyotumiwa hapa linarejelea watu wasiomjua Mungu na wanaotawaliwa na Shetani. (Yohana 14:30; Waefeso 2:2; Yakobo 4:4; 1 Yohana 5:19) Tunawezaje kuepuka kuwa “sehemu ya ulimwengu”? Katika sura hii, tutachunguza njia kadhaa: Kwanza, tunaendelea kuwa washikamanifu kwa Ufalme wa Mungu na hatuungi mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. Pili, tunaipinga roho ya ulimwengu. Tatu, tunahakikisha mavazi na mapambo yetu hayavuki mipaka, na tuna maoni yenye usawaziko kuhusu pesa. Pia, tunavaa “mavazi . . . ya silaha” ambayo Mungu anatuandalia.—Soma Maelezo ya Ziada 16.

UWE MSHIKAMANIFU KWA UFALME WA MUNGU

3. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu siasa?

3 Yesu alipokuwa duniani, aliona kwamba watu walikuwa na matatizo mengi na maisha yao hayakuwa rahisi. Aliwajali sana na alitaka kuwasaidia. Je, aliamua kuwa kiongozi wa kisiasa? Hapana. Alijua kwamba watu walihitaji hasa Ufalme au serikali ya Mungu. Yesu angekuwa Mfalme wa Ufalme huo, na Ufalme ulikuwa kichwa kikuu cha mahubiri yake. (Danieli 7:13, 14; Luka 4:43; 17:20, 21) Yesu hakujihusisha na siasa, na hakuunga mkono upande wowote. Alipokuwa mbele ya Gavana Mroma Pontio Pilato, alisema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Wanafunzi wake pia hawakuunga mkono upande wowote. Kitabu kimoja kilisema kwamba Wakristo wa mapema “hawakukubali vyeo vya kisiasa.” (On the Road to Civilization) Leo, Wakristo wa kweli wana maoni hayohayo. Tunaunga mkono kwa ushikamanifu Ufalme wa Mungu na hatuungi mkono siasa za ulimwengu huu.—Mathayo 24:14.

Unaweza kueleza ni kwa nini unaunga mkono kwa ushikamanifu Ufalme wa Mungu?

4. Wakristo wa kweli wanaungaje mkono Ufalme wa Mungu?

4 Mabalozi huwakilisha serikali yao katika nchi ya kigeni na hawajihusishi na siasa za nchi hiyo. Hali hiyo inalingana na ya watiwa-mafuta, ambao wana tumaini la kutawala na Kristo mbinguni. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo watiwa-mafuta: “Sisi ni mabalozi walio badala ya Kristo.” (2 Wakorintho 5:20) Watiwa-mafuta wanawakilisha serikali ya Mungu. Hawajihusishi na masuala ya kisiasa na ya serikali za ulimwengu huu. (Wafilipi 3:20) Badala yake, watiwa-mafuta wanawasaidia mamilioni ya watu kujifunza kuhusu serikali ya Mungu. “Kondoo wengine,” ambao wana tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu, wanawaunga mkono watiwa-mafuta. Wao pia hawaungi mkono upande wowote. (Yohana 10:16; Mathayo 25:31-40) Ni wazi kwamba hakuna Mkristo wa kweli ambaye angetaka kujihusisha na siasa za ulimwengu huu.—Soma Isaya 2:2-4.

5. Ni sababu gani inayofanya Wakristo wasijihusishe katika vita?

5 Wakristo wa kweli huwaona waabudu wenzao kuwa familia yao na wana umoja hata iwe wanatoka nchi gani au wana malezi gani. (1 Wakorintho 1:10) Ikiwa tungeenda kupigana vitani, tungekuwa tunapigana na familia yetu wenyewe, yaani, waabudu wenzetu, ambao Yesu alituamuru tuwapende. (Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:10-12) Isitoshe, Yesu aliwaambia wanafunzi wake wawapende hata adui zao.—Mathayo 5:44; 26:52.

6. Watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu wana maoni gani kuhusu serikali?

6 Hata ingawa tukiwa Wakristo tunadumisha msimamo wa kutounga mkono upande wowote, tunajitahidi sana kuwa raia wema. Kwa mfano, tunaheshimu serikali kwa kutii sheria zake na kulipa kodi. Hata hivyo, sikuzote tunahakikisha tunampa “Mungu vitu vya Mungu.” (Marko 12:17; Waroma 13:1-7; 1 Wakorintho 6:19, 20) “Vitu vya Mungu” vinatia ndani upendo wetu, ibada yetu na utii wetu kwake. Tuko tayari kupoteza uhai badala ya kukosa kumtii Yehova.—Luka 4:8; 10:27; soma Matendo 5:29; Waroma 14:8.

PINGA “ROHO YA ULIMWENGU”

7, 8. “Roho ya ulimwengu” ni nini, na inawaathiri watu jinsi gani?

7 Kujitenga na ulimwengu wa Shetani kunamaanisha kwamba hatupaswi kuruhusu “roho ya ulimwengu” ituongoze. Roho hiyo ni njia ya kufikiri na kutenda inayotoka kwa Shetani na inayowaongoza wale wasiomwabudu Yehova. Lakini Wakristo wanapinga mtazamo huo. Kama Paulo alivyosema, “hatukupokea roho ya ulimwengu, bali tulipokea roho inayotoka kwa Mungu.”—1 Wakorintho 2:12; Waefeso 2:2, 3; soma Maelezo ya Ziada 17.

8 Roho ya ulimwengu huwafanya watu wawe na ubinafsi, kiburi, na kuwa waasi. Inawafanya wafikiri kwamba hawahitaji kumtii Mungu. Shetani anataka watu wafanye wanachotaka bila kufikiria matokeo. Angependa watu waamini kwamba “tamaa ya mwili na tamaa ya macho” ndiyo mambo muhimu zaidi maishani. (1 Yohana 2:16; 1 Timotheo 6:9, 10) Ibilisi anajaribu sana kuwapotosha watumishi wa Yehova na kutufanya tufikiri kama yeye anavyofikiri.—Yohana 8:44; Matendo 13:10; 1 Yohana 3:8.

9. Roho ya ulimwengu inaweza kutuathiri jinsi gani?

9 Kama hewa tunayopumua, roho ya ulimwengu inatuzunguka pande zote. Ikiwa hatutajitahidi kuipinga roho hiyo, itatuathiri. (Soma Methali 4:23.) Tunaweza kuanza kuipumua kwa kufanya mambo yanayoonekana kuwa hayana madhara, kama vile, kujiruhusu tuathiriwe na fikira na mtazamo wa watu wasiomwabudu Yehova. (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Au tunaweza kuathiriwa na mambo kama vile ponografia, uasi-imani, au michezo inayochochea sana roho ya mashindano.—Soma Maelezo ya Ziada 18.

10. Tunaweza kuipingaje roho ya ulimwengu?

10 Hivyo basi, tunaweza kuipingaje roho ya ulimwengu? Tunahitaji kudumisha uhusiano wa karibu na Yehova na kuruhusu hekima yake ituongoze. Pia, tunapaswa kusali bila kuacha ili tupate roho takatifu na kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kumtumikia. Yehova ndiye mwenye nguvu zaidi ulimwenguni. Tuna uhakika kwamba anaweza kutusaidia kupinga roho ya ulimwengu.—1 Yohana 4:4.

VALIA KWA NJIA INAYOMLETEA MUNGU HESHIMA

11. Roho ya ulimwengu imeathirije jinsi watu wanavyovalia?

11 Tunaonyesha kwamba sisi si sehemu ya ulimwengu kupitia mavazi na mapambo yetu. Watu wengi ulimwenguni huvalia kwa njia itakayowaelekezea fikira, inayochochea wengine wawe na mawazo mapotovu, inayoonyesha kwamba wao ni waasi, au inayoonyesha wana pesa nyingi sana. Watu wengine hawajali jinsi wanavyoonekana. Wanajiacha wakiwa wachafu au kuvalia ovyoovyo. Hatupaswi kuruhusu mitazamo hiyo iathiri jinsi tunavyovalia na kujipamba.

Je, ninamletea Yehova heshima kwa jinsi ninavyovalia?

12, 13. Ni kanuni zipi zinazopaswa kutusaidia kuamua jinsi tutakavyovalia?

12 Tukiwa watumishi wa Yehova, tunataka sikuzote kuvalia mavazi nadhifu, safi, yasiyoudhi, na yanayofaana na hali. Tunavalia kwa “kiasi na utimamu wa akili,” ili kuonyesha kwamba ‘tunamtumikia Mungu.’—1 Timotheo 2:9, 10; Yuda 21.

13 Mavazi yetu yanaweza kuathiri maoni ya watu kumhusu Yehova na watu wake. Tunataka kufanya “mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31) Kuwa na kiasi kunahusisha kuheshimu hisia na maoni ya wengine. Hivyo, tunapochagua mavazi au kuamua jinsi tunavyotaka kuonekana, tunakumbuka kwamba maamuzi yetu yanawaathiri watu wengine.—1 Wakorintho 4:9; 2 Wakorintho 6:3, 4; 7:1.

14. Tunapaswa kufikiria nini tunapochagua mavazi tutakayovaa katika shughuli za Kikristo?

14 Tunavaliaje tunapokuwa kwenye mikutano au huduma ya shambani? Je, mavazi yetu yanatufanya tukaziwe sana fikira? Je, yanawaaibisha wengine? Je, tunahisi kwamba hakuna mtu anayepaswa kuingilia haki yetu ya kuamua jinsi tunavyovalia? (Wafilipi 4:5; 1 Petro 5:6) Bila shaka, sote tunataka kupendeza, lakini sifa zetu za Kikristo ndizo hasa zinazofanya tupendeze. Hizo ndizo sifa ambazo Yehova anaona anapotutazama. Zinaonyesha jinsi tulivyo kwa ndani, ‘yule mtu wa siri wa moyoni ambaye ni wa thamani kubwa machoni pa Mungu.’—1 Petro 3:3, 4.

15. Kwa nini Yehova hatuamulii jinsi tunavyopaswa kuvalia na kujipamba?

15 Yehova hajatupatia orodha ya sheria za mavazi tunayopaswa au tusiyopaswa kuvaa. Badala yake, ametuandalia kanuni za Biblia ambazo zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayofaa. (Waebrania 5:14) Anataka maamuzi yetu, makubwa kwa madogo, yaonyeshe upendo wetu kwake na kwa wengine. (Soma Marko 12:30, 31.) Ulimwenguni pote, watu wa Yehova wanavalia kwa njia tofauti-tofauti ikitegemea utamaduni wao na mapendezi yao. Tofauti hizo zinapendeza na kuburudisha.

MAONI YENYE USAWAZIKO KUHUSU PESA

16. Maoni ya ulimwengu kuhusu pesa yanapingana na mafundisho ya Yesu katika njia gani? Tunapaswa kujiuliza maswali gani?

16 Shetani anataka watu wafikiri kwamba pesa na vitu vya kimwili ndivyo vitakavyowaletea furaha, lakini watumishi wa Yehova wanajua kuwa hilo si kweli. Tunaamini maneno haya ya Yesu: “Hata mtu anapokuwa na vitu vingi, uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Pesa haziwezi kutuletea furaha ya kweli, wala haziwezi kutupa marafiki wa kweli, amani ya akili, au uzima wa milele. Bila shaka, tunahitaji vitu fulani vya kimwili, na tunataka kufurahia maisha. Lakini Yesu alitufundisha kwamba tutakuwa na furaha ikiwa tutakuwa na uhusiano mzuri na Mungu na ikiwa ibada yetu ndiyo jambo muhimu zaidi maishani mwetu. (Mathayo 5:3; 6:22, maelezo ya chini) Jiulize hivi: ‘Je, maoni ya ulimwengu kuhusu pesa yameniathiri? Je, ninafikiria na kuzungumza kuhusu pesa kila wakati?’—Luka 6:45; 21:34-36; 2 Yohana 6.

17. Maisha yako yataboreshwaje ukipinga maoni ya ulimwengu kuhusu pesa?

17 Ikiwa tutakazia fikira kumtumikia Yehova na kupinga maoni ya ulimwengu kuhusu pesa, maisha yetu yatakuwa yenye kusudi. (Mathayo 11:29, 30) Tutaridhika na tutakuwa na amani akilini na moyoni. (Mathayo 6:31, 32; Waroma 15:13) Hatutakuwa na mahangaiko mengi kuhusu vitu vya kimwili. (Soma 1 Timotheo 6:9, 10.) Tutapata furaha inayotokana na kutoa. (Matendo 20:35) Na maisha yetu yatatuwezesha kuwa na muda mwingi pamoja na wale tunaowapenda. Huenda hata tukalala vizuri zaidi.—Mhubiri 5:12.

“MAVAZI KAMILI YA SILAHA”

18. Shetani anajaribu kutufanya nini?

18 Shetani anajaribu kuharibu uhusiano wetu na Yehova, hivyo, tunapaswa kufanya yote tuwezayo kuulinda. Tunapambana “dhidi ya majeshi ya roho waovu.” (Waefeso 6:12) Shetani na majeshi yake ya roho waovu hawataki tuwe na furaha au tuishi milele. (1 Petro 5:8) Maadui hao wenye nguvu wanapigana nasi, lakini kwa msaada wa Yehova tunaweza kushinda!

19. Andiko la Waefeso 6:14-18 linafafanuaje ‘mavazi ya silaha’ ya Mkristo?

19 Katika nyakati za kale, wanajeshi walivalia mavazi ya kujilinda walipokuwa vitani. Katika njia hiyohiyo, tunapaswa kuvaa “mavazi . . . ya silaha” ambayo Yehova ametuandalia. (Waefeso 6:13) Mavazi hayo yatatulinda. Tunasoma hivi kuhusu mavazi hayo ya silaha kwenye Waefeso 6:14-18: “Kwa hiyo, simameni imara, mkiwa mmejifunga kiunoni mshipi wa ile kweli, mkiwa mmevaa bamba la kifuani la uadilifu, na mkiwa mmevaa viatu miguuni tayari kutangaza habari njema ya amani. Mbali na mambo hayo, chukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwa kuitumia mtaizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu. Pia, pokeeni kofia ya chuma ya wokovu, na upanga wa roho, yaani, neno la Mungu, na kwa kila namna ya sala na dua mkiendelea kusali kila wakati katika roho.”

20. Tunapaswa kufanya nini ili ‘mavazi ya silaha’ yatusaidie?

20 Mwanajeshi akisahau sehemu yoyote ya mavazi ya silaha na kuacha sehemu ya mwili wake bila ulinzi, hapo ndipo adui yake atamshambulia. Tukitaka ‘mavazi yetu ya silaha’ yatulinde, hatupaswi kusahau kufunika sehemu yoyote. Tunahitaji kuyavaa wakati wote na kuyadumisha yakiwa katika hali nzuri. Tutaendelea kupambana hadi ulimwengu wa Shetani utakapoangamizwa na yeye pamoja na roho wake waovu watakapoondolewa duniani. (Ufunuo 12:17; 20:1-3) Kwa hiyo, ikiwa tunapambana na udhaifu fulani au tamaa zisizofaa, hatupaswi kukata tamaa!—1 Wakorintho 9:27.

21. Tunaweza kushinda pambano letu jinsi gani?

21 Kwa nguvu zetu wenyewe, hatuwezi kumshinda nguvu Ibilisi. Lakini kwa msaada wa Yehova, tunaweza kumshinda! Ili tuendelee kuwa waaminifu, tunahitaji kusali kwa Yehova, kujifunza Neno lake, na kushirikiana na ndugu na dada zetu. (Waebrania 10:24, 25) Mambo hayo yatatusaidia kuwa washikamanifu kwa Mungu na kuwa tayari kutetea imani yetu.

UWE TAYARI KUTETEA IMANI YAKO

22, 23. (a) Tunaweza kufanya nini ili tuwe tayari sikuzote kutetea imani yetu? (b) Tutachunguza nini katika sura inayofuata?

22 Tunahitaji kuwa tayari kutetea imani yetu nyakati zote. (Yohana 15:19) Katika masuala fulani, Mashahidi wa Yehova wanakuwa na msimamo tofauti sana na watu wengi. Jiulize hivi: ‘Je, ninaelewa kabisa kwa nini tunachukua msimamo fulani? Je, nina uhakika kwamba kile ambacho Biblia na mtumwa mwaminifu anasema ni sahihi? Je, ninajivunia kuwa Shahidi wa Yehova? (Zaburi 34:2; Mathayo 10:32, 33) Je, ninaweza kuwaeleza wengine mambo ninayoamini?’—Mathayo 24:45; Yohana 17:17; soma 1 Petro 3:15.

23 Katika hali nyingi, ni rahisi kujua tunachopaswa kufanya ili tusiwe sehemu ya ulimwengu. Lakini katika hali nyingine, si rahisi kujua tunapaswa kufanya nini. Shetani anajaribu kututega katika njia mbalimbali. Mtego mmoja anaotumia ni burudani. Tunaweza kuchaguaje burudani kwa hekima? Tutaona hilo katika sura inayofuata.