Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 4

Kwa Nini Unapaswa Kuheshimu Mamlaka?

Kwa Nini Unapaswa Kuheshimu Mamlaka?

“Waheshimuni watu wa namna zote, upendeni ushirika mzima wa akina ndugu, mwogopeni Mungu, mheshimuni mfalme.”—1 PETRO 2:17.

1, 2. (a) Tunahitaji kufuata mwongozo wa nani? (b) Tutazungumzia maswali gani katika sura hii?

ULIPOKUWA mtoto, huenda kuna pindi ambazo wazazi wako walikuambia ufanye jambo ambalo hukupenda kufanya. Uliwapenda wazazi wako na ulijua kwamba unapaswa kuwatii. Hata hivyo, huenda kuna pindi ambazo hukutaka kuwatii.

2 Tunajua kwamba Baba yetu, Yehova, anatupenda. Anatutunza na kuhakikisha kwamba tuna kila kitu tunachohitaji ili kufurahia maisha. Anatupatia mwongozo tunaohitaji ili tufanikiwe. Nyakati fulani anatumia watu wengine kutupatia mwongozo. Tunahitaji kuheshimu mamlaka ya Yehova. (Methali 24:21) Lakini kwa nini nyakati nyingine ni vigumu kukubali mwongozo? Kwa nini Yehova anatuambia tufuate mwongozo? Na tunaonyeshaje kwamba tunaheshimu mamlaka yake?—Soma Maelezo ya Ziada 9.

KWA NINI NI VIGUMU?

3, 4. Wanadamu walipataje dhambi? Kwa nini inaweza kuwa vigumu kwetu kukubali kuongozwa na wengine?

3 Tukiwa wanadamu tuna mwelekeo wa kuasi. Hali imekuwa hivyo tangu mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, walipoasi. Hata ingawa waliumbwa wakiwa wakamilifu, waliasi mamlaka ya Mungu. Tangu wakati huo, wanadamu wote wamezaliwa wakiwa na dhambi. Kutokamilika kwetu ni sababu moja inayofanya iwe vigumu kukubali mwongozo kutoka kwa Yehova na kwa wanadamu. Sababu nyingine ni kwamba wale ambao Yehova anawatumia kutupa mwongozo si wakamilifu pia.—Mwanzo 2:15-17; 3:1-7; Zaburi 51:5; Waroma 5:12.

4 Kwa kuwa sisi si wakamilifu, tuna mwelekeo wa kuwa na kiburi. Kiburi hufanya iwe vigumu kwetu kukubali mwongozo. Kwa mfano, katika Israeli la kale, Yehova alimchagua Musa awaongoze watu Wake. Mwanamume aliyeitwa Kora, ambaye alikuwa amemtumikia Yehova kwa miaka mingi, aliruhusu kiburi kimfanye amdharau Musa. Ingawa Musa alikuwa akiwaongoza watu wa Mungu, hakuwa na kiburi. Hata Biblia inasema alikuwa mtu mnyenyekevu zaidi duniani wakati huo. Lakini Kora hakukubali kuongozwa na Musa. Hata alisadikisha umati mkubwa wa watu wamwunge mkono na kumwasi Musa. Ni nini kilichompata Kora na waasi wenzake? Waliuawa. (Hesabu 12:3; 16:1-3, 31-35) Katika Biblia, tunasoma mifano mingi inayotufundisha kwamba ni hatari kuwa na kiburi.—2 Mambo ya Nyakati 26:16-21; soma Maelezo ya Ziada 10.

5. Wanadamu fulani wametumiaje mamlaka yao vibaya?

5 Huenda umesikia watu wakisema kwamba mamlaka huwafanya watu wawe na kiburi. Katika historia, wanadamu wengi wametumia mamlaka vibaya. (Soma Mhubiri 8:9.) Kwa mfano, Sauli alipochaguliwa na Yehova kuwa mfalme wa Israeli alikuwa mwema na myenyekevu. Lakini aliruhusu kiburi na wivu visitawi moyoni mwake, na hilo likamfanya amtese Daudi, ambaye hakuwa na hatia. (1 Samweli 9:20, 21; 10:20-22; 18:7-11) Baadaye, Daudi akawa mfalme, naye alikuwa mmoja kati ya wafalme bora zaidi wa Israeli. Hata hivyo, Daudi pia alitumia mamlaka yake vibaya. Alifanya uzinzi na Bath-sheba, mke wa mwanamume aliyeitwa Uria, kisha akajaribu kuficha dhambi yake kwa kuagiza Uria akauawe vitani.—2 Samweli 11:1-17.

KWA NINI TUNAHESHIMU MAMLAKA YA YEHOVA?

6, 7. (a) Upendo wetu kwa Yehova unatuchochea kufanya nini? (b) Ni nini kitakachotusaidia kuwa watiifu hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo?

6 Tunaheshimu mwongozo ambao Yehova anatupa kwa sababu tunampenda. Kwa sababu tunampenda Yehova zaidi ya kitu au mtu mwingine yeyote, tunataka kumfurahisha. (Soma Methali 27:11; Marko 12:29, 30.) Tangu wanadamu wawili wa kwanza walipoanza kuishi katika bustani ya Edeni, Shetani amekuwa akijaribu kuwafanya watu wapinge mamlaka ya Yehova. Ibilisi anataka tufikiri kwamba Yehova hana haki ya kutuambia tunachopaswa kufanya. Lakini tunajua huo ni uwongo. Tunakubaliana na maneno haya: “Unastahili, Ee Yehova Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote.”—Ufunuo 4:11.

7 Ulipokuwa mtoto, huenda ulifundishwa kuwatii wazazi wako hata wakati ambapo hukutaka kufanya hivyo. Kwa njia hiyohiyo, tukiwa watumishi wa Yehova, huenda kuna pindi ambazo ni vigumu kutii. Lakini kwa kuwa tunampenda Yehova na kumheshimu, tunafanya yote tuwezayo kumtii. Yesu alituwekea kielelezo. Alimtii Yehova hata wakati ambapo hali ilikuwa ngumu au alipokabili hali zisizofaa. Hiyo ndiyo sababu angeweza kumwambia Baba yake hivi: “Si kama ninavyopenda, bali mapenzi yako na yatendeke.”—Luka 22:42; soma Maelezo ya Ziada 11.

8. Taja baadhi ya njia ambazo Yehova anatumia kutuongoza. (Ona sanduku “ Sikiliza Mashauri.”)

8 Leo, Yehova anatuongoza kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, ametupatia Biblia. Pia ametupatia wazee wa kutaniko. Tunaonyesha kwamba tunaheshimu mamlaka ya Yehova tunapowaheshimu wale anaowatumia kutuongoza. Tukikataa msaada wao, ni kana kwamba tunampinga Yehova. Waisraeli walipomkataa Musa, Yehova aliona hilo kuwa jambo zito sana. Aliona ni kana kwamba wanampinga yeye.—Hesabu 14:26, 27; soma Maelezo ya Ziada 12.

9. Upendo utatuchocheaje kufuata mwongozo?

9 Tunapoheshimu mamlaka, tunaonyesha kwamba tunawapenda ndugu na dada zetu pia. Fikiria mfano huu. Kunapokuwa na majanga ya asili, mara nyingi kikundi cha wanaotoa msaada hushirikiana ili kuokoa watu wengi kadiri iwezekanavyo. Ili kikundi hicho kiwe na matokeo, lazima mtu mmoja asimamie mambo na wengine wote wanahitaji kufuata mwongozo wake. Lakini namna gani mmoja kati ya wale wanaotoa msaada akiamua kupuuza mwongozo huo na kufanya kile anachotaka? Hata ikiwa ana nia njema, kukataa kwake kutii mwongozo unaotolewa kunaweza kuwasababishia wenzake matatizo, na labda hata kuwafanya wajeruhiwe vibaya. Kwa njia kama hiyo, tusipofuata mwongozo wa Yehova na wale ambao amewapa mamlaka, huenda wengine wakaumia. Lakini tunapomtii Yehova, tunaonyesha kwamba tunawapenda ndugu zetu na tunaheshimu mpango wa Yehova.—1 Wakorintho 12:14, 25, 26.

10, 11. Tutazungumzia nini?

10 Chochote ambacho Yehova anatuagiza tufanye ni kwa faida yetu. Tunapoheshimu mamlaka katika familia, kutanikoni, na tunaposhughulika na maofisa wa serikali, kila mtu anafaidika.—Kumbukumbu la Torati 5:16; Waroma 13:4; Waefeso 6:2, 3; Waebrania 13:17.

11 Tunaweza kuwaonyesha wengine heshima ikiwa tunaelewa kwa nini Yehova anataka tufanye hivyo. Tuzungumzie kwa kina zaidi jinsi tunavyoweza kuonyesha heshima katika maeneo matatu maishani.

HESHIMA KATIKA FAMILIA

12. Mume anaweza kuonyeshaje kwamba anaheshimu mamlaka?

12 Yehova alianzisha familia na akampa kila mtu katika familia jukumu lake. Kila mshiriki anapofanya mambo ambayo Yehova anamtazamia afanye, mpango wa familia utafanikiwa na familia yote itanufaika. (1 Wakorintho 14:33) Yehova amemweka mume kuwa kichwa cha familia. Hilo linamaanisha kwamba Yehova anamtazamia amtunze na kumwongoza mke wake na watoto wake kwa upendo. Kwa hiyo, lazima mume awajibike kwa Yehova kuhusu anavyoitunza familia yake. Mume Mkristo ni mwenye fadhili na upendo na anaitendea familia yake kwa njia ileile ambayo Yesu analitendea kutaniko. Mume anapofanya hivyo, anaonyesha anamheshimu Yehova.—Waefeso 5:23; soma Maelezo ya Ziada 13.

Anapoitunza familia yake, baba Mkristo anamwiga Kristo

13. Mke anaweza kuonyeshaje kwamba anaheshimu mamlaka?

13 Pia mke Mkristo ana jukumu muhimu na lenye heshima. Anamuunga mkono mume wake anapojitahidi kutumia ukichwa wake vizuri. Ana daraka la kuwazoeza watoto akishirikiana na mume wake. Njia moja anayowafundisha watoto wake kuwa na heshima ni kupitia mfano wake mwenyewe. (Methali 1:8) Anamheshimu mume wake na kuunga mkono maamuzi yake. Hata wakati ambapo hakubaliani naye kuhusu jambo fulani, kwa fadhili na heshima anamweleza jinsi anavyohisi. Mwanamke Mkristo ambaye mume wake si Shahidi wa Yehova, anakabili changamoto za pekee. Lakini akiendelea kumtendea kwa upendo na heshima, huenda siku moja mume wake pia akataka kumjua Yehova na kumwabudu.—Soma 1 Petro 3:1.

14. Watoto wanaweza kuonyeshaje kwamba wanaheshimu mamlaka?

14 Watoto ni wenye thamani kwa Yehova, na wanahitaji sana kulindwa na kuongozwa. Watoto wanapotii wazazi wao, wanawafanya wafurahi. Jambo muhimu hata zaidi, wanapokuwa watiifu wanamwonyesha Yehova heshima na kumfurahisha. (Methali 10:1) Katika familia nyingi, watoto wanalelewa na mzazi mmoja. Huenda hali hiyo ikawa ngumu kwa mzazi na watoto pia. Lakini watoto wanapotii na kumuunga mkono mama au baba yao, maisha ya familia yao yanakuwa mazuri. Hata hali iweje, hakuna familia kamilifu. Lakini familia zote zinaweza kuwa na furaha zaidi kila mshiriki anapofuata mwongozo wa Yehova. Kufanya hivyo humletea Yehova utukufu ambaye ndiye Muumba wa familia zote.—Waefeso 3:14, 15.

HESHIMA KATIKA KUTANIKO

15. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaheshimu mamlaka kutanikoni?

15 Yehova anatuongoza kupitia kutaniko la Kikristo, naye amempa Yesu mamlaka kamili ya kuliongoza. (Wakolosai 1:18) Naye Yesu amempa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” daraka la kuwatunza watu wa Mungu duniani. (Mathayo 24:45-47) Leo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ni Baraza Linaloongoza. Baraza Linaloongoza linatupatia tunachohitaji kwa wakati unaofaa ili kutusaidia tudumishe imani yetu ikiwa na nguvu. Wazee, watumishi wa huduma, na waangalizi wa mzunguko hutegemeza makutaniko ulimwenguni pote na wanapokea mwongozo kutoka kwa Baraza Linaloongoza. Ndugu hao wote wana daraka la kututunza. Watatoa hesabu kwa Yehova kuhusiana na wanavyoshughulikia daraka hilo. Kwa hiyo, tunapowaheshimu wanaume hao, tunamheshimu Yehova.—Soma 1 Wathesalonike 5:12; Waebrania 13:17; soma Maelezo ya Ziada 14.

16. Kwa nini tunaweza kusema kwamba wazee na watumishi wa huduma huwekwa rasmi na roho takatifu?

16 Wazee na watumishi wa huduma hulisaidia kutaniko kuendelea kuwa na uaminifu na umoja. Bila shaka, wao ni wanadamu wasio wakamilifu kama sisi tu. Wanachaguliwaje? Lazima ndugu hao wajitahidi kuwa na sifa za kustahili zinazopatikana katika Biblia. (1 Timotheo 3:1-7, 12; Tito 1:5-9) Yehova alitumia roho takatifu kuwasaidia waandikaji wa Biblia kufafanua sifa hizo za kustahili. Wazee wa kutaniko husali kwa Yehova wakiomba roho yake takatifu wanapozungumzia ni nani anayepaswa kuwekwa rasmi kuwa mzee au mtumishi wa huduma. Ni wazi kwamba makutaniko yanaongozwa na Yehova na Yesu. (Matendo 20:28) Wanaume waliowekwa rasmi kututegemeza na kututunza ni zawadi kutoka kwa Mungu.—Waefeso 4:8.

17. Ili kuonyesha heshima, huenda pindi fulani dada akalazimika kufanya nini?

17 Nyakati nyingine huenda wazee na watumishi wa huduma wasiwepo ili kutimiza mgawo fulani kutanikoni. Chini ya hali hizo, ndugu waliobatizwa ndio husaidia, lakini ikiwa hawapo, huenda dada akalazimika kutimiza mgawo ambao kwa kawaida unapaswa kushughulikiwa na ndugu aliyebatizwa. Inapokuwa hivyo, atafunika kichwa chake, labda kwa kitambaa au kofia. (1 Wakorintho 11:3-10) Kwa njia hiyo, anaonyesha kwamba anaheshimu mpango wa ukichwa ambao Yehova ameweka katika familia na kutanikoni.—Soma Maelezo ya Ziada 15.

KUWAHESHIMU MAOFISA WA SERIKALI

18, 19. (a) Tunajifunza nini kutokana na Waroma 13:1-7? (b) Tunaonyeshaje kwamba tunaheshimu serikali?

18 Leo, Yehova ameruhusu serikali ziwe na mamlaka fulani, nasi tunapaswa kuziheshimu. Zinafanya mipango katika nchi na jamii ili shughuli ziendeshwe kwa njia inayofaa na watu wapate huduma za lazima. Wakristo wanatii agizo lililo katika Waroma 13:1-7. (Soma.) Tunaheshimu “mamlaka zilizo kubwa” na kutii sheria za nchi au jamii tunamoishi. Huenda sheria hizo zikaathiri familia yetu, biashara yetu, au mali zetu. Kwa mfano, tunalipa kodi na kutoa habari ambayo serikali inahitaji. Lakini tutatendaje ikiwa serikali inatuomba tufanye jambo ambalo linapinga sheria ya Mungu? Mtume Petro alisema hivi: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.”—Matendo 5:28, 29.

19 Ikiwa lazima tushughulike na ofisa wa serikali, kama vile hakimu au polisi, sikuzote tunapaswa kuwa na heshima. Vijana Wakristo wanawaonyesha heshima walimu na wafanyakazi wengine wa shule. Katika maeneo yetu ya kazi, tunamwonyesha mwajiri wetu heshima, hata ikiwa wafanyakazi wengine hawafanyi hivyo. Tunapofanya hivyo, tunamwiga mtume Paulo, ambaye aliwaheshimu maofisa ingawa nyakati fulani ilikuwa vigumu kufanya hivyo. (Matendo 26:2, 25) Hata wengine wasipotutendea vizuri, tunaendelea kuwaheshimu.—Soma Waroma 12:17, 18; 1 Petro 3:15.

20, 21. Ni mambo gani mazuri yanayotimizwa tunapowaonyesha wengine heshima?

20 Ulimwenguni pote, watu wanazidi kuacha kuheshimiana. Lakini watu wa Yehova ni tofauti. Tunaazimia kumheshimu kila mtu. Tunafuata mwongozo wa mtume Petro: “Waheshimuni watu wa namna zote.” (1 Petro 2:17) Tunapowaheshimu wengine, wanatambua hilo. Yesu alituambia hivi: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili waone matendo yenu mema na kumtukuza Baba yenu.”—Mathayo 5:16.

21 Tunapoonyesha heshima katika familia, kutanikoni, na katika maeneo mengine maishani, tunaweza kuwafanya wengine watake kujifunza mengi zaidi kumhusu Yehova. Na tunapowaonyesha wengine heshima, tunamheshimu Yehova mwenyewe. Hilo linamfurahisha Yehova na kumwonyesha kwamba tunampenda.