Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maelezo ya Ziada

Maelezo ya Ziada

 1 KANUNI

Sheria za Mungu zinategemea kanuni zake. Kanuni hizo ni kweli za msingi tunazopata katika Biblia. Zinatusaidia kuelewa jinsi Mungu anavyofikiri na kuhisi kuhusu mambo mbalimbali. Kanuni zinatusaidia kufanya maamuzi mazuri maishani na kutenda kwa njia inayofaa. Zinatusaidia hasa chini ya hali ambazo hakuna sheria hususa za Mungu.

Sura ya 1, fungu la 8

 2 UTII

Kumtii Yehova kunamaanisha kwamba kwa hiari tunafanya anachotuambia tufanye. Yehova anataka tumtii kwa sababu tunampenda. (1 Yohana 5:3) Ikiwa tunampenda Mungu na kumtumaini, tutafuata mashauri yake hata iwe tunakabili hali gani. Tutamtii hata inapokuwa vigumu kwetu kufanya hivyo. Ni vizuri kwetu kumtii Yehova, kwa sababu anatufundisha jinsi ya kuwa na maisha mazuri sasa na anatuahidi kwamba tutafurahia baraka nyingi wakati ujao.—Isaya 48:17.

Sura ya 1, fungu la 10

 3 UHURU WA KUCHAGUA

Yehova amempa kila mtu uhuru wa kuchagua, au uwezo wa kufanya maamuzi. Hakutuumba tukiwa kama roboti. (Kumbukumbu la Torati 30:19; Yoshua 24:15) Tunaweza kutumia uhuru wetu kufanya maamuzi mazuri. Lakini tusipokuwa waangalifu, tunaweza kufanya maamuzi yasiyo na hekima. Kuwa na uhuru wa kuchagua kunamaanisha kwamba tunapaswa kuamua ikiwa tunataka kuwa washikamanifu kwa Yehova na kuthibitisha kwamba tunampenda kikweli.

Sura ya 1, fungu la 12

 4 VIWANGO VYA MAADILI

Yehova anaweka viwango vya maadili, au miongozo, ya jinsi tunavyopaswa kujiendesha na kutenda. Katika Biblia, tunaweza kujifunza viwango hivyo na jinsi vinavyoweza kutusaidia kuishi kwa njia nzuri. (Methali 6:16-19; 1 Wakorintho 6:9-11) Miongozo hiyo inatusaidia kujua maoni ya Mungu kuhusu mema na mabaya. Pia, vinatusaidia kujua jinsi ya kutenda kwa upendo, jinsi ya kufanya maamuzi mazuri, na jinsi ya kuwatendea wengine kwa fadhili. Ingawa viwango vya ulimwengu vinazidi kushuka, viwango vya Yehova havibadiliki. (Kumbukumbu la Torati 32:4-6; Malaki 3:6) Kufuata viwango hivyo kunatulinda tusipatwe na madhara kimwili na kihisia.

Sura ya 1, fungu la 17

 5 DHAMIRI

Dhamiri yetu ni hisi yetu ya ndani inayotofautisha mema na mabaya. Yehova amempa kila mmoja wetu dhamiri. (Waroma 2:14, 15) Ili dhamiri yetu ifanye kazi vizuri, lazima tuizoeze kulingana na viwango vya maadili vya Yehova. Hivyo dhamiri yetu inaweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayompendeza Mungu. (1 Petro 3:16) Dhamiri yetu inaweza kutuonya tunapokuwa karibu kufanya uamuzi mbaya, au inaweza kutuumiza sana baada ya kufanya jambo baya. Dhamiri yetu inaweza kudhoofika, lakini kwa msaada wa Yehova, tunaweza kuiimarisha tena. Dhamiri nzuri hutusaidia tuwe na amani ya akili na tujiheshimu.

Sura ya 2, fungu la 3

 6 KUMWOGOPA MUNGU

Kumwogopa Mungu kunamaanisha kwamba tunampenda na kumheshimu sana hivi kwamba hatungependa kufanya jambo lolote litakalomchukiza. Kumwogopa Mungu kunatusaidia kutenda mema na kuepuka kutenda mabaya. (Zaburi 111:10) Kunatuchochea kusikiliza kwa makini mambo yote ambayo Yehova anasema. Pia, kunatusaidia tutimize ahadi zote tunazomtolea kwa sababu tunamheshimu sana. Kumwogopa Mungu kunaathiri jinsi tunavyofikiri, jinsi tunavyowatendea wengine, na maamuzi tunayofanya kila siku.

Sura ya 2, fungu la 9

 7 TOBA

Toba inatia ndani huzuni nyingi ambayo mtu huhisi kwa sababu amefanya jambo baya. Wale wanaompenda Mungu wanasikitika sana wanapotambua wametenda jambo linalokiuka viwango vyake. Tukifanya jambo baya, tunapaswa kumsihi Yehova atusamehe kwa msingi wa dhabihu ya Yesu. (Mathayo 26:28; 1 Yohana 2:1, 2) Tunapotubu kikweli na kuacha kutenda mabaya, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusamehe. Hatuhitaji kuendelea kuhisi tuna hatia kwa sababu ya mambo tuliyofanya zamani. (Zaburi 103:10-14; 1 Yohana 1:9; 3:19-22) Tunapaswa kutia jitihada nyingi ili kujifunza kutokana na makosa yetu, tuache kufikiri kwa njia isiyofaa, na kuishi kupatana na viwango vya Yehova.

Sura ya 2, fungu la 18

 8 KUTENGA NA USHIRIKA

Mtu aliyetenda dhambi nzito asipotubu na akatae kufuata viwango vya Yehova, hawezi tena kuendelea kuwa mshiriki wa kutaniko. Anapaswa kutengwa na ushirika. Mtu anapotengwa na ushirika, hatushirikiani tena naye na tunaacha kuzungumza naye. (1 Wakorintho 5:11; 2 Yohana 9-11) Mpango wa kutenga na ushirika hulinda jina la Yehova na kutaniko. (1 Wakorintho 5:6) Pia, kumtenga mtu na ushirika ni nidhamu inayoweza kumsaidia mtenda-dhambi kutubu ili amrudie Yehova.—Luka 15:17.

Sura ya 3, fungu la 19

 9 MWONGOZO, MWELEKEZO, NA MASHAURI

Yehova anatupenda na anataka kutusaidia. Hiyo ndiyo sababu anatupa mwongozo, mwelekezo, na mashauri kupitia Biblia na kupitia watu wanaompenda Mungu. Tukiwa wanadamu ambao si wakamilifu, tunahitaji sana msaada huo. (Yeremia 17:9) Tunapowasikiliza kwa heshima wale ambao Yehova anawatumia kutuelekeza, tunaonyesha kwamba tunamheshimu na tunataka kumtii.—Waebrania 13:7.

Sura ya 4, fungu la 2

 10 KIBURI NA UNYENYEKEVU

Kwa kuwa sisi si wakamilifu, ni rahisi kwetu kuwa na ubinafsi na kiburi. Lakini Yehova anataka tuwe wanyenyekevu. Mara nyingi, sisi huanza kujifunza jinsi ya kuwa wanyenyekevu tunapojilinganisha na Yehova na kutambua jinsi tulivyo duni sana. (Ayubu 38:1-4) Pia, njia nyingine muhimu ni kujifunza kufikiria zaidi kuwahusu wengine na kitakachowafaa badala ya kujifikiria tu. Mara nyingi, kiburi humfanya mtu aamini kwamba yeye ni bora kuliko wengine. Mtu mnyenyekevu hujichunguza kwa unyoofu na kuona sifa zake nzuri na udhaifu wake pia. Haogopi kukubali makosa yake, kuomba msamaha, na kukubali mapendekezo na mashauri. Mtu mnyenyekevu anamtegemea Yehova na kufuata mwongozo wake.—1 Petro 5:5.

Sura ya 4, fungu la 4

 11 MAMLAKA

Mamlaka ni haki ya kutoa maagizo na kufanya maamuzi. Yehova ndiye mwenye mamlaka kuu zaidi mbinguni na duniani. Kwa sababu aliumba vitu vyote, yeye ndiye mwenye nguvu zaidi ulimwenguni. Sikuzote anatumia mamlaka yake kuwanufaisha wengine. Yehova amewapa wanadamu fulani mamlaka ya kututunza, kama vile, wazazi, wazee wa kutaniko, na serikali. Wote hao wana mamlaka, na Yehova anataka tushirikiane nao. (Waroma 13:1-5; 1 Timotheo 5:17) Lakini sheria za wanadamu zinapopingana na sheria za Mungu, lazima tumtii Mungu badala ya wanadamu. (Matendo 5:29) Tunapokubali mamlaka ya wale ambao Yehova anawatumia, tunamwonyesha Yehova kwamba tunaheshimu maamuzi yake.

Sura ya 4, fungu la 7

 12 WAZEE

Yehova anawatumia wazee, ambao ni ndugu wenye uzoefu, ili kulitunza kutaniko. (Kumbukumbu la Torati 1:13; Matendo 20:28) Wanaume hao hutusaidia kudumisha uhusiano wetu na Yehova ukiwa na nguvu na kumwabudu kwa amani na kwa utaratibu. (1 Wakorintho 14:33, 40) Ili wazee wawekwe rasmi kwa roho takatifu, lazima wafikie sifa zinazopatikana katika Biblia. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9; 1 Petro 5:2, 3) Tunalitumaini na kulitegemeza tengenezo la Mungu, kwa hiyo tunafurahi kushirikiana na wazee.—Zaburi 138:6; Waebrania 13:17.

Sura ya 4, fungu la 8

 13 KICHWA CHA FAMILIA

Yehova amewapa wazazi daraka la kuwatunza watoto wao na nyumba yao. Hata hivyo, Biblia inaeleza kwamba mume ndiye kichwa cha familia. Ikiwa familia haina baba, mama ndiye anayekuwa kichwa cha familia. Madaraka ya kichwa cha familia yanatia ndani kuiandalia familia chakula, mavazi, na makao. Ni muhimu sana kwamba kichwa cha familia aongoze katika kuisaidia familia imwabudu Yehova. Kwa mfano, anahakikisha kwamba wanahudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida, wanashiriki katika huduma ya shambani, na kujifunza Biblia pamoja. Pia, kichwa cha familia anaongoza katika kufanya maamuzi. Sikuzote anajaribu kumwiga Yesu kwa kuwa mwenye fadhili na usawaziko, bila kuwa mkatili au mkali. Hali inapokuwa hivyo familia inakuwa na roho ya upendo, hivi kwamba wote wanajihisi salama na wanaendelea kukuza uhusiano wao na Yehova.

Sura ya 4, fungu la 12

 14 BARAZA LINALOONGOZA

Baraza Linaloongoza ni kikundi cha wanaume walio na tumaini la kwenda mbinguni ambao wanatumiwa na Mungu kuelekeza kazi ya watu wake. Katika karne ya kwanza, Yehova alitumia baraza linaloongoza kuelekeza ibada na kazi ya kuhubiri ya kutaniko la Kikristo la mapema. (Mdo 15:2) Leo, kikundi cha ndugu wanaotumikia wakiwa Baraza Linaloongoza wanafanya kazi ya kuelekeza, kuongoza, na kulinda watu wa Mungu. Ndugu hao wanapofanya maamuzi, wanategemea mwongozo wa Neno la Mungu na roho yake takatifu. Yesu alisema kuwa kikundi hicho cha wanaume waliotiwa mafuta ndio “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt 24:45-47.

Sura ya 4, fungu la 15

 15 KUFUNIKA KICHWA

Huenda kuna pindi ambazo dada anaombwa afanye jambo fulani kutanikoni ambalo kwa kawaida linafanywa na ndugu. Anapofanya kazi hiyo, anaonyesha kwamba anaheshimu mpango wa Yehova kwa kufunika kichwa. Lakini atafunika kichwa chake chini ya hali fulani tu. Kwa mfano, dada atafunika kichwa chake anapoongoza funzo la Biblia mume wake au ndugu aliyebatizwa akiwepo.—1 Wakorintho 11:11-15.

Sura ya 4, fungu la 17

 16 KUTOUNGA MKONO UPANDE WOWOTE

Hilo linamaanisha hatuungi mkono upande wowote wa mambo ya kisiasa. (Yohana 17:16) Watu wa Yehova wanaunga mkono Ufalme wake. Kama Yesu, sisi pia hatuungi mkono upande wowote wa mambo ya ulimwengu.

Yehova anatuamuru ‘tutii serikali na mamlaka.’ (Tito 3:1, 2; Waroma 13:1-7) Lakini sheria ya Mungu pia inasema kwamba hatupaswi kuua. Kwa hiyo, dhamiri ya Mkristo haiwezi kumruhusu aende vitani. Ikiwa Mkristo ana uchaguzi wa kufanya utumishi wa kiraia badala ya utumishi wa kijeshi, ataamua ikiwa dhamiri yake inamruhusu kufanya hivyo.

Tunamwabudu Yehova peke yake, kwa sababu yeye ndiye Muumba wetu. Ingawa tunaheshimu nembo za kitaifa, hatusalimu bendera wala hatuimbi wimbo wa taifa. (Isaya 43:11; Danieli 3:1-30; 1 Wakorintho 10:14) Pia, watu wa Yehova wanafanya uamuzi wa kibinafsi wa kutopiga kura wakati wa uchaguzi wa kisiasa. Hiyo ni kwa sababu tayari tumechagua kuwa upande wa serikali ya Mungu.—Mathayo 22:21; Yohana 15:19; 18:36.

Sura ya 5, fungu la 2

 17 ROHO YA ULIMWENGU

Ulimwengu unaendeleza njia ya kufikiri ya Shetani. Njia hiyo ya kufikiri imeenea sana kati ya watu ambao hawampendi Yehova na ambao hawamwigi na wanapuuza viwango vyake. (1 Yohana 5:19) Biblia inapozungumza kuhusu roho ya ulimwengu inarejelea kufikiri huko pamoja na matendo yanayotokana na kufikiri huko. (Waefeso 2:2) Watu wa Yehova wanajitahidi kuhakikisha kwamba hawaathiriwi na roho hiyo. (Waefeso 6:10-18) Badala yake, tunapenda njia za Yehova na tunajitahidi sana kushikamana na njia yake ya kufikiri.

Sura ya 5, fungu la 7

 18 UASI-IMANI

Uasi-imani ni kuchukua msimamo dhidi ya kweli ya Biblia. Waasi-imani humpinga Yehova na Yesu, Mfalme aliyewekwa rasmi juu ya Ufalme wa Mungu. Wao hujaribu kuwachochea watu wengine wajiunge nao. (Waroma 1:25) Wanataka kupanda mashaka katika akili za wale wanaomwabudu Yehova. Watu fulani katika kutaniko la Kikristo la mapema waligeuka na kuwa waasi-imani, na wengine katika siku zetu wamefanya hivyo pia. (2 Wathesalonike 2:3) Wale ambao ni washikamanifu kwa Yehova hawashirikiani hata kidogo na waasi-imani. Hatupaswi kujiruhusu tushinikizwe na wengine au udadisi wetu utufanye tusome au kusikiliza maoni ya waasi-imani. Sisi ni washikamanifu kwa Yehova na tunamwabudu yeye peke yake.

Sura ya 5, fungu la 9

 19 KUFUNIKA DHAMBI

Chini ya Sheria ya Musa, taifa la Israeli lilimwomba Yehova asamehe dhambi zao. Walipeleka dhabihu za kufunika dhambi za nafaka, mafuta, na wanyama hekaluni. Kwa njia hiyo, Waisraeli walikumbushwa kwamba Yehova alikuwa tayari kuwasamehe dhambi zao, wakiwa taifa na mtu mmojammoja. Baadaye, Yesu alipotoa uhai wake ili kufunika dhambi zetu, dhabihu hizo za kufunika dhambi hazikuhitajiwa tena. Yesu alitoa dhabihu kamilifu “mara moja kwa wakati wote.”—Waebrania 10:1, 4, 10.

Sura ya 7, fungu la 6

 20 KUHESHIMU UHAI WA WANYAMA

Chini ya Sheria ya Musa, watu waliruhusiwa kula wanyama. Pia waliamriwa watoe dhabihu za wanyama. (Mambo ya Walawi 1:5, 6) Lakini Yehova hakuwaruhusu watu wake wawatendee wanyama kwa ukatili. (Methali 12:10) Sheria ilikuwa na maagizo yaliyowalinda wanyama dhidi ya ukatili. Waisraeli waliamriwa wawatunze wanyama vizuri.—Kumbukumbu la Torati 22:6, 7.

Sura ya 7, fungu la 6

 21 VISEHEMU VYA DAMU NA MBINU ZA MATIBABU

Visehemu vya damu. Damu imefanyizwa kwa sehemu nne kuu—chembe nyekundu, chembe nyeupe, chembelele (platelets), na utegili (plasma). Sehemu hizo kuu za damu zinaweza kugawanywa katika visehemu vidogo. *

Wakristo hawakubali kutiwa damu nzima mishipani au yoyote kati ya sehemu nne kuu za damu. Lakini je, wanaweza kukubali visehemu vya damu? Biblia haitoi habari hususa. Kwa hiyo, kila Mkristo anapaswa kufanya uamuzi wake mwenyewe kwa kutegemea dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia.

Wakristo fulani huamua kukataa visehemu vyote vya damu. Huenda wakasema Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilidai kwamba damu iliyotolewa kwa mnyama imwagwe “ardhini.”—Kumbukumbu la Torati 12:22-24.

Wengine hufanya uamuzi tofauti. Dhamiri yao inawaruhusu kukubali visehemu fulani vya damu. Huenda wakasema kwamba visehemu hivyo vidogo haviwakilishi tena uhai wa kiumbe ambaye damu hiyo ilitolewa.

Unapofanya maamuzi kuhusu visehemu vya damu, fikiria maswali yafuatayo:

  • Je, ninatambua kwamba kwa kukataa visehemu vyote vya damu ninakataa dawa fulani zinazotibu magonjwa au zinazoweza kusaidia kugandisha damu?

  • Ninaweza kumwelezaje daktari sababu yangu ya kukataa au kukubali kisehemu chochote cha damu?

Mbinu za matibabu. Tukiwa Wakristo, hatuchangii damu, wala hatuhifadhi damu yetu wenyewe majuma kadhaa kabla ya kufanyiwa upasuaji. Hata hivyo, kuna mbinu nyingine zinazohusisha matumizi ya damu ya mgonjwa. Kila Mkristo anapaswa kujiamulia jinsi damu yake itakavyotumiwa wakati wa upasuaji, upimaji damu, au tiba inayotumika wakati huo. Wakati mbinu hizo za matibabu zinapotumiwa, huenda damu ya mgonjwa ikaondolewa kutoka kwenye mwili wa mgonjwa kwa muda fulani.—Kwa habari zaidi, ona Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 2000, ukurasa wa 30-31.

Kwa mfano, kuna mbinu ya matibabu inayoitwa uzimuaji wa damu (hemodilution). Katika mbinu hiyo, damu ya mgonjwa hutolewa mwilini kabla ya upasuaji na badala yake mgonjwa hutiwa umajimaji fulani mwilini. Baadaye, damu hurudishwa tena katika mwili wa mgonjwa kabla ya upasuaji kukamilika au muda mfupi baada ya upasuaji kukamilika.

Mbinu nyingine inaitwa uokoaji wa chembe za damu (cell salvage). Katika mbinu hiyo, damu inayovuja wakati wa upasuaji hukusanywa, inasafishwa au kuchujwa, kisha inarudishwa katika mwili wa mgonjwa wakati wa upasuaji au muda mfupi tu baada ya upasuaji.

Huenda kila daktari akatumia mbinu hizi kwa njia tofauti kidogo. Kwa hiyo, kabla ya kukubali tiba, vipimo, au mbinu yoyote ya kitiba, Mkristo anahitaji kujua damu yake itatumiwa jinsi gani.

Tunapofanya maamuzi kuhusu mbinu za matibabu zinazohusisha matumizi ya damu yetu wenyewe, tunapaswa kuzingatia maswali yafuatayo:

  • Ikiwa kiasi fulani cha damu yangu kitaelekezwa nje ya mwili na huenda mzunguko wa damu ukatizwe kwa muda fulani, je, dhamiri yangu itaniruhusu kuona damu hiyo kuwa sehemu ya mwili wangu bado, bila kuwa na uhitaji wa “kuimwaga ardhini”?—Kumbukumbu la Torati 12:23, 24.

  • Je, dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia ingenisumbua ikiwa wakati wa matibabu kiasi fulani cha damu yangu kingetolewa, kuboreshwa, na kurudishwa tena mwilini?

  • Je, ninatambua kwamba kukataa matibabu yote yanayohusisha damu yangu kunamaanisha kwamba ninakataa damu yangu ipimwe, na pia ninakataa matibabu kama utenganishaji wa koloidi (hemodialysis), au mashine ya kusaidia moyo au mapafu kufanya kazi (heart-lung bypass machine)?

Kabla ya kufanya maamuzi kuhusu visehemu vya damu na mbinu za matibabu zinazohusisha damu yetu wenyewe, tunapaswa kusali tupate mwongozo wa Yehova kisha tufanye utafiti. (Yakobo 1:5, 6) Baada ya kufanya hivyo, lazima tutumie dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia kufanya uamuzi. Hatupaswi kuwauliza wengine wangefanya nini ikiwa wangekabili hali kama yetu, wala wengine hawapaswi kutushinikiza tufanye uamuzi fulani.—Waroma 14:12; Wagalatia 6:5.

Sura ya 7, fungu la 11

 22 USAFI WA MAADILI

Kuwa na maadili safi kunamaanisha kwamba mwenendo na matendo yetu ni safi machoni pa Mungu. Usafi wa maadili unahusisha kile tunachofikiria, kusema, na kutenda. Yehova anatuamuru tuepuke aina yoyote ya uchafu wa kingono au maadili mapotovu. (Methali 1:10; 3:1) Lazima tuazimie kwamba tutafuata viwango safi vya Yehova hata kabla ya kuingia katika hali inayoweza kutushawishi kufanya jambo baya. Tunahitaji kusali kwa ukawaida kuomba msaada wa Mungu ili tudumishe akili zetu zikiwa safi, na tunapaswa kuazimia kukataa vishawishi vya kujihusisha katika maadili mapotovu.—1 Wakorintho 6:9, 10, 18; Waefeso 5:5.

Sura ya 8, fungu la 11

 23 MWENENDO MPOTOVU NA UCHAFU

Mwenendo mpotovu unahusisha kuzungumza au kutenda kwa njia ambayo inavunja kabisa viwango vya Mungu na inayoonyesha mtazamo wa kutokuwa na aibu au wa ukaidi. Mtu anayetenda kwa njia hiyo anaonyesha kwamba haheshimu sheria za Mungu. Mtu anapokuwa na hatia ya mwenendo mpotovu, atashughulikiwa na halmashauri ya hukumu. Uchafu unatia ndani aina mbalimbali za matendo mabaya. Kwa kutegemea uzito wa jambo lenyewe, huenda mambo fulani yanayohusisha uchafu yakahitaji kushughulikiwa na halmashauri ya hukumu kutanikoni.​—Wagalatia 5:19-21; Waefeso 4:19; kwa habari zaidi, ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2006.

Sura ya 9, fungu la 7; Sura ya 12, fungu la 10

 24 KUPIGA PUNYETO

Yehova alikusudia ngono kuwa njia safi ya kuonyesha upendo kati ya mume na mke. Lakini mtu anapopiga punyeto, au anapotumia vibaya viungo vyake vya uzazi ili kuona raha ya ngono, anajipatia raha ya ngono kwa njia isiyo safi. Zoea hilo linaweza kudhuru uhusiano wa mtu na Yehova. Linaweza kutokeza tamaa potovu na kumfanya mtu awe na maoni yaliyopotoka kuhusu ngono. (Wakolosai 3:5) Mtu hapaswi kukata tamaa ikiwa anapata ugumu wa kuacha zoea hilo chafu. (Zaburi 86:5; 1 Yohana 3:20) Ikiwa uko katika hali hiyo, sali kwa unyoofu na umwombe Yehova akusaidie. Epuka mambo kama vile ponografia, ambayo itakufanya ufikirie mambo machafu. Zungumza na mzazi Mkristo au na rafiki mkomavu ambaye anaheshimu sheria za Yehova. (Methali 1:8, 9; 1 Wathesalonike 5:14; Tito 2:3-5) Unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaona na kuthamini jitihada zako za kuendelea kuwa safi kiroho.​—Zaburi 51:17; Isaya 1:18.

Sura ya 9, fungu la 9

 25 NDOA YA WAKE WENGI

Yehova alikusudia ndoa iwe kati ya mwanamume mmoja na mwanamke mmoja. Katika Israeli la kale, Mungu aliwaruhusu wanaume kuwa na zaidi ya mke mmoja, lakini hilo halikuwa kusudi lake la awali. Leo, Yehova haruhusu watu wake wawe katika ndoa ya wake wengi. Mume anaweza kuwa na mke mmoja tu, na mke anaweza kuwa na mume mmoja tu.​—Mathayo 19:9; 1 Timotheo 3:2.

Sura ya 10, fungu la 12

 26 TALAKA NA KUTENGANA

Yehova alikusudia mume na mke waishi pamoja maisha yao yote. (Mwanzo 2:24; Malaki 2:15, 16; Mathayo 19:3-6; 1 Wakorintho 7:39) Anakubali talaka itolewe wakati tu mwenzi mmoja anapofanya uzinzi. Chini ya hali kama hiyo, Yehova anampa mwenzi asiye na hatia haki ya kuamua ikiwa atatoa talaka au la.​—Mathayo 19:9.

Nyakati nyingine, Wakristo fulani wameamua kutengana na mwenzi wao hata ingawa hakuna aliyefanya uzinzi. (1 Wakorintho 7:11) Katika hali zifuatazo Mkristo anaweza kufikiria ikiwa atatengana na mwenzi wake.

  • Kutotegemeza familia kimakusudi: Mume anakataa kuiandalia familia yake kimwili, hivi kwamba familia inakosa pesa au chakula.​—1 Timotheo 5:8.

  • Kuumizwa kimwili kupita kiasi: Kuumizwa kimwili kufikia hatua ambayo mwenzi anayetendewa hivyo anahisi afya au uhai wake uko hatarini.​—Wagalatia 5:19-21.

  • Kuhatarishwa kabisa kwa uhusiano wa mtu na Yehova: Mume au mke anamzuia kabisa mwenzi wake asimtumikie Yehova.​—Matendo 5:29.

Sura ya 11, fungu la 19

 27 KUPONGEZANA NA KUTIANA MOYO

Sisi sote tunahitaji kupongezwa na kutiwa moyo. (Methali 12:25; 16:24) Tunaweza kuimarishana na kufarijiana kwa maneno yenye upendo na fadhili. Maneno kama hayo yanaweza kuwasaidia ndugu na dada zetu kuvumilia na kuendelea kumtumikia Yehova licha ya hali ngumu sana. (Methali 12:18; Wafilipi 2:1-4) Mtu anapovunjika moyo sana, tunapaswa kumsikiliza kwa heshima na kujaribu kuelewa jinsi anavyohisi. Hilo linaweza kutusaidia kujua jambo la kumwambia au la kufanya ili kumsaidia. (Yakobo 1:19) Lifanye liwe lengo lako kuwafahamu ndugu na dada zako vizuri ili uelewe kikweli kile wanachohitaji. Kisha unaweza kuwasaidia kumfikia Chanzo cha faraja yote na kitia-moyo, na hapo watapata burudisho la kweli.​—2 Wakorintho 1:3, 4; 1 Wathesalonike 5:11.

Sura ya 12, fungu la 16

 28 HARUSI

Biblia haitoi sheria hususa kuhusu harusi. Desturi za eneo na matakwa ya kisheria hutofautiana kutoka sehemu moja hadi nyingine. (Mwanzo 24:67; Mathayo 1:24; 25:10; Luka 14:8) Sehemu muhimu zaidi ya harusi ni ile nadhiri ambayo wenzi wa ndoa hutoa mbele za Yehova. Wenzi wengi wa ndoa huchagua kuwa na watu wa familia na marafiki wa karibu wanaposema nadhiri zao, nao hupenda mzee wa kutaniko atoe hotuba inayotegemea Biblia. Wanaofunga ndoa ndio huamua ikiwa watafanya karamu ya harusi, na itakuwa ya aina gani. (Luka 14:28; Yohana 2:1-11) Wanapaswa kuhakikisha kwamba uamuzi wowote wanaofanya kuhusu harusi yao utamtukuza Yehova. (Mwanzo 2:18-24; Mathayo 19:5, 6) Kanuni za Biblia zinaweza kuwasaidia kufanya maamuzi mazuri. (1 Yohana 2:16, 17) Wenzi hao wakiamua kuwe na kileo kwenye karamu yao, wanapaswa kuhakikisha kwamba karamu hiyo imesimamiwa vizuri. (Methali 20:1; Waefeso 5:18) Wakiamua kuwe na muziki au burudani, wanapaswa kuhakikisha kwamba mambo hayo yatamtukuza Yehova. Wenzi wa ndoa Wakristo wanapaswa kukazia fikira uhusiano wao na Mungu na kati yao wenyewe badala ya kukazia tu fikira siku yao ya harusi.​—Methali 18:22; ili upate mapendekezo zaidi, ona Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 2006, ukurasa wa 18-31.

Sura ya 13, fungu la 18

 29 KUFANYA MAAMUZI YENYE HEKIMA

Tunataka kufanya maamuzi mazuri yanayotegemea kanuni za Neno la Mungu. Kwa mfano, Mkristo anaweza kualikwa na mwenzi wake wa ndoa ambaye si Shahidi wa Yehova akale mlo na watu wa ukoo wakati wa sikukuu ya kilimwengu. Ukikabili hali hiyo utafanya nini? Ikiwa dhamiri yako inakuruhusu kwenda, unaweza kumweleza mwenzi wako kwamba ikiwa desturi za kipagani ni sehemu ya mlo huo, hutashiriki. Pia, unapaswa kufikiria ikiwa wengine watakwazwa ikiwa utaenda kwenye mlo huo.​—1 Wakorintho 8:9; 10:23, 24.

Au ikiwa mwajiri wako anakupa bakshishi wakati wa msimu wa sikukuu. Je, ukatae bakshishi hiyo? Si lazima. Uamuzi wako wa kukubali au kukataa huenda ukategemea kwa kadiri fulani maoni ya mwajiri wako. Je, anaona bakshishi hiyo kuwa sehemu ya sikukuu hiyo? Au ni njia tu ya kuonyesha shukrani zake? Baada ya kutafakari sababu hizo na nyingine nyingi, utahitaji kuamua ikiwa utakubali bakshishi hiyo.

Katika hali nyingine, huenda mtu akakupa zawadi wakati wa sikukuu na kukuambia: “Najua wewe husherehekei sikukuu hii, lakini nilitaka tu kukupa zawadi hii.” Labda mtu huyo anakuonyesha fadhili tu. Kwa upande mwingine, je, kuna sababu ya kufikiri kwamba anajaribu imani yako au anajaribu kukuhusisha katika kusherehekea sikukuu hiyo? Baada ya kufikiria jambo hilo, wewe utahitaji kuamua ikiwa utakubali zawadi hiyo au la. Tunapaswa kuhakikisha kuwa uamuzi wowote tutakaofanya utatuacha tukiwa na dhamiri njema na kwamba tutaendelea kuwa waaminifu kwa Yehova.​—Matendo 23:1.

Sura ya 13, fungu la 22

 30 MAMBO YA KIBIASHARA NA YA KISHERIA

Katika visa vingi, kutoelewana kunaposhughulikiwa haraka na kwa amani, hakuhitaji kuwa jambo kubwa. (Mathayo 5:23-26) Jambo kuu zaidi kwa Wakristo linapaswa kuwa kumletea Yehova utukufu na kudumisha umoja wa kutaniko.​—Yohana 13:34, 35; 1 Wakorintho 13:4, 5.

Wakristo wanapokosa kuelewana katika suala la kibiashara, wanapaswa kujaribu kulisuluhisha bila kupelekana mahakamani. Andiko la 1 Wakorintho 6:1-8 linaonyesha shauri ambalo mtume Paulo alitoa kuhusu Wakristo kupelekana mahakamani. Kumpeleka ndugu mahakamani kunaweza kumvunjia Yehova heshima na kulishushia kutaniko heshima. Kwenye Mathayo 18:15-17, hatua tatu zinaorodheshwa ambazo Wakristo wanapaswa kufuata ili kutatua mashtaka makubwa kama vile uchongezi au upunjaji: (1) Kwanza wanapaswa kujaribu kutatua jambo hilo kati yao wenyewe. (2) Ikiwa hatua hiyo haitafanikiwa, wanaweza kuomba msaada kutoka kwa mshiriki mmoja au wawili wakomavu kutanikoni. (3) Halafu, ikihitajika, wanaweza kuliomba baraza la wazee lishughulikie jambo hilo. Hali ikifikia hapo, wazee watatumia kanuni za Biblia kujaribu kuwasaidia wote wanaohusika watatue mambo kwa amani.  Ikiwa yeyote hayuko tayari kufuata viwango vya Biblia, huenda wazee wakahitaji kuchukua hatua ya kihukumu.

Huenda kukawa na visa ambavyo vinamlazimu mtu kwenda mahakamani kuchukua hatua za kisheria, labda hali zinazohusu talaka, malezi ya watoto, malipo ya talaka, malipo ya bima, kufilisika, au wosia. Mkristo akitumia hatua hizo za kisheria kutatua jambo hilo kwa amani, hatakuwa akikiuka shauri la Paulo.

Mkristo akiripoti uhalifu mkubwa kwa wenye mamlaka kama vile, ubakaji, kumtendea mtoto vibaya, kushambuliwa kimwili, wizi mkubwa, au uuaji, hatakuwa akikiuka shauri la Paulo.

Sura ya 14, fungu la 14

 31 UWONGO WA SHETANI

Tangu bustani ya Edeni, Shetani amekuwa akijaribu kuwadanganya wanadamu. (Mwanzo 3:1-6; Ufunuo 12:9) Anajua kwamba ikiwa atapotosha kufikiri kwetu, anaweza kutuchochea tutende jambo lisilofaa. (2 Wakorintho 4:4; Yakobo 1:14, 15) Anatumia siasa, dini, biashara, burudani, elimu, na mambo mengine mengi ili kuendeleza njia yake ya kufikiri na kuifanya ionekane kuwa sawa.​—Yohana 14:30; 1 Yohana 5:19.

Shetani anajua kwamba hana wakati mwingi uliobaki wa kuwapotosha watu. Kwa hiyo, anafanya yote anayoweza ili kuwapotosha watu wengi kadiri anavyoweza. Jambo kuu analotaka ni kuwapotosha watu wanaomtumikia Yehova. (Ufunuo 12:12) Tusipokuwa waangalifu, Ibilisi anaweza kupotosha kufikiri kwetu hatua kwa hatua. (1 Wakorintho 10:12) Kwa mfano, Yehova anataka ndoa zidumu. (Mathayo 19:5, 6, 9) Lakini watu wengi leo wanaona ndoa kuwa makubaliano ya kawaida tu yanayoweza kuvunjwa kwa urahisi. Sinema nyingi na programu za televisheni zinaendeleza wazo hilo pia. Lazima tuwe waangalifu tusiruhusu maoni ya ulimwengu kuhusu ndoa yatuathiri.

Njia nyingine ambayo Shetani anatumia kujaribu kutupotosha ni kwa kuchochea mtazamo wa kujitegemea. (2 Timotheo 3:4) Tusipokuwa waangalifu, tunaweza kuacha kuheshimu mamlaka ya wale waliowekwa rasmi na Yehova. Kwa mfano, huenda ndugu akaanza kupinga mwongozo wa wazee wa kutaniko. (Waebrania 12:5) Au dada anaweza kuanza kutilia shaka mpango wa Yehova wa ukichwa katika familia.​—1 Wakorintho 11:3.

Lazima tuazimie kwamba hatutamruhusu Ibilisi aathiri kufikiri kwetu. Badala yake, tunataka kuiga kufikiri kwa Yehova na ‘kukaza akili zetu kwenye mambo yaliyo juu, si kwenye mambo yaliyo duniani.’​—Wakolosai 3:2; 2 Wakorintho 2:11.

Sura ya 16, fungu la 9

 32 MATIBABU

Sisi sote tunataka kuwa na afya na kupata matibabu bora kabisa tunapokuwa wagonjwa. (Isaya 38:21; Marko 5:25, 26; Luka 10:34) Leo, kuna mbinu nyingi za kitiba na matibabu ya aina nyingi yanayotolewa na madaktari na watu wengine. Tunapoamua ni matibabu ya aina gani tutakayokubali, ni muhimu kwamba tufuate kanuni za Biblia. Tunakumbuka kwamba ni Ufalme wa Mungu tu utakaotuponya kikamili. Hatutaki kukazia fikira afya yetu sana na kupuuza ibada yetu kwa Yehova.​—Isaya 33:24; 1 Timotheo 4:16.

Tunapaswa kuwa waangalifu kuepuka matibabu yoyote ambayo huenda yakawa yanategemea nguvu za roho waovu. (Kumbukumbu la Torati 18:​10-12; Isaya 1:13) Kwa hiyo, kabla ya kukubali matibabu au dawa za aina yoyote, tunapaswa kuchunguza kikamili chanzo chake na mawazo yanayoendelezwa nayo. (Methali 14:15) Hatupaswi kusahau kwamba Shetani angependa kutudanganya tujihusishe katika mambo yanayohusiana na roho waovu. Hata ikiwa tu tunahisi kwamba matibabu fulani yanahusiana na roho waovu, ni vizuri kuyaepuka.​—1 Petro 5:8.

Sura ya 16, fungu la 18

^ fu. 98 Madaktari fulani huona sehemu hizo nne kuu kuwa visehemu vya damu. Kwa hiyo, huenda ukahitaji kueleza uamuzi wako binafsi wa kutokubali kutiwa mishipani damu nzima au sehemu nne kuu za damu, yaani, chembe nyekundu, chembe nyeupe, chembelele, na utegili.