Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 16

Mpingeni Ibilisi

Mpingeni Ibilisi

“Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” —YAKOBO 4:7.

1, 2. Tunahitaji kujua nini kuhusu Shetani na roho waovu?

MAISHA katika ulimwengu mpya wa Yehova yatakuwa mazuri sana. Hatimaye, tutaishi kama Mungu alivyokusudia tuishi. Lakini sasa tunaishi katika ulimwengu unaoongozwa na Shetani na roho wake waovu. (2 Wakorintho 4:4) Ingawa hatuwezi kuwaona, wapo na wana nguvu nyingi sana.

2 Katika sura hii, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kukaa karibu na Yehova na kujilinda na Shetani. Yehova anaahidi kwamba atatusaidia. Lakini tunahitaji kuelewa njia ambazo Shetani na roho waovu wanatumia kutupotosha na kutushambulia.

“KAMA SIMBA ANAYENGURUMA”

3. Ibilisi anataka kutudhuru jinsi gani?

3 Shetani anadai kwamba wanadamu wanamwabudu Yehova kwa sababu za kichoyo na wataacha kumtumikia Yehova ikiwa hali zitakuwa ngumu. (Soma Ayubu 2:4, 5.) Mtu anapotaka kujifunza kumhusu Yehova, Shetani na roho waovu wanatambua jambo hilo na wanajaribu kumzuia. Wanakasirika mtu anapojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Biblia inamlinganisha Ibilisi na “simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Shetani anataka kuharibu uhusiano wetu na Yehova.—Zaburi 7:1, 2; 2 Timotheo 3:12.

Shetani anakasirika tunapojiweka wakfu kwa Yehova

4, 5. (a) Shetani hawezi kufanya nini? (b) Tunapaswa kufanya nini ili ‘kumpinga Ibilisi’?

4 Hatuhitaji kumwogopa Shetani na roho waovu. Yehova amedhibiti uwezo wao. Yehova anaahidi kwamba “umati mkubwa” wa Wakristo wa kweli utaokoka “dhiki kuu.” (Ufunuo 7:9, 14) Hakuna kitu ambacho Ibilisi anaweza kufanya ili kuzuia jambo hilo, kwa sababu Yehova anawalinda watu Wake.

5 Tukikaa karibu na Yehova, Shetani hawezi kuvunja uhusiano wetu na Yehova. Neno la Mungu linatuhakikishia: “Yehova yuko pamoja nanyi maadamu mnaendelea kuwa pamoja naye.” (2 Mambo ya Nyakati 15:2; soma 1 Wakorintho 10:13.) Wanaume na wanawake wengi wa kale ambao walikuwa waaminifu kama vile, Abeli, Enoko, Noa, Sara, na Musa, walimpinga Ibilisi kwa kukaa karibu na Yehova. (Waebrania 11:4-40) Tunaweza kufanya kama wao. Neno la Mungu linatuahidi hivi: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—Yakobo 4:7.

“TUNAPAMBANA”

6. Shetani anatushambulia jinsi gani?

6 Ingawa Shetani anajua kwamba Yehova amedhibiti uwezo wake, bado anajaribu kufanya chochote ili kudhoofisha uhusiano wetu na Mungu. Leo, Ibilisi anatushambulia kwa njia mbalimbali akitumia mbinu zilezile ambazo amekuwa akitumia kwa maelfu ya miaka. Tuzungumzie baadhi ya mbinu hizo.

7. Kwa nini Shetani anawashambulia watu wa Yehova?

7 Mtume Yohana aliandika hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Shetani anautawala ulimwengu huu uliopotoka na angependa kuwatawala watu wa Yehova pia. (Mika 4:1; Yohana 15:19; Ufunuo 12:12, 17) Ibilisi anajua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati, hivyo anajitahidi kutufanya tuache kuwa washikamanifu kwa Mungu. Nyakati nyingine Ibilisi anatumia mashambulizi ya moja kwa moja, lakini wakati mwingine anatushambulia kwa hila.

8. Kila Mkristo anapaswa kutambua nini?

8 Tunasoma hivi katika Waefeso 6:12: “Tunapambana [“tunapigana mweleka,” maelezo ya chini] . . . dhidi ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” Kila Mkristo anapambana kibinafsi dhidi ya Ibilisi na roho waovu. Tunapaswa kutambua kwamba wote waliojiweka wakfu kwa Yehova wako katika pambano hilo. Katika barua yake kwa Waefeso, mtume Paulo aliwasihi Wakristo mara tatu ‘wasimame imara.’—Waefeso 6:11, 13, 14.

9. Shetani na roho waovu wanajaribu kutufanya nini?

9 Shetani na roho waovu wanajaribu kutudanganya kwa njia mbalimbali. Kumpinga Shetani mara moja hakumaanishi kwamba hatuwezi kushindwa naye katika njia nyingine. Ibilisi anajaribu kutafuta udhaifu wetu ili atuwekee mtego. Hata hivyo, si lazima tunaswe kwa sababu Biblia inatufundisha kuhusu mitego ya Ibilisi. (2 Wakorintho 2:11; soma Maelezo ya Ziada 31.) Njia moja anayotumia ni kuwasiliana na roho waovu.

KAA MBALI NA ROHO WAOVU

10. (a) Kuwasiliana na roho waovu ni nini? (b) Yehova ana maoni gani kuhusu kuwasiliana na roho waovu?

10 Kuwasiliana na roho waovu kunahusisha mambo yote yanayomfanya mtu awe na uhusiano na roho waovu, kama vile kubashiri matukio ya wakati ujao, uchawi, au kujaribu kuzungumza na wafu. Biblia inatuambia kwamba kuwasiliana na roho waovu ni “chukizo” na kwamba hatuwezi kushirikiana na roho waovu na wakati huohuo tumwabudu Yehova. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Ufunuo 21:8) Wakristo wanapaswa kuepuka aina yoyote ya kuwasiliana na roho waovu.—Waroma 12:9.

11. Udadisi kuhusu mambo yanayohusiana na roho waovu unaweza kutuathirije?

11 Shetani anajua kwamba ikiwa tutavutiwa na mambo yanayohusiana na roho waovu, itakuwa rahisi kwake kutunasa. Aina yoyote ya kuwasiliana na roho waovu inaweza kuharibu uhusiano wetu na Yehova.

SHETANI ANAJARIBU KUTUPOTOSHA

12. Shetani anaweza kuvuruga kufikiri kwetu katika njia gani?

12 Shetani anajaribu kuvuruga kufikiri kwa watu. Anatokeza mashaka hatua kwa hatua hadi watu wanafikiri kwamba “wema ni uovu na uovu ni wema.” (Isaya 5:20) Ibilisi anaendeleza wazo la kwamba mashauri ya Biblia hayawezi kutusaidia na kwamba tunaweza kuwa na furaha zaidi tukipuuza viwango vya Mungu.

13. Shetani amekuwa akijaribu jinsi gani kutokeza mashaka?

13 Kueneza mashaka ni mbinu ambayo Shetani ametumia kwa mafanikio sana. Ametumia njia hiyo kwa muda mrefu sana. Katika bustani ya Edeni, alijaribu kutokeza shaka kwa kumuuliza Hawa hivi: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” (Mwanzo 3:1) Baadaye, wakati wa Ayubu, Shetani alimuuliza hivi Yehova mbele za malaika: “Je, Ayubu anamwogopa Mungu bure?” (Ayubu 1:9) Baada ya Yesu kubatizwa, Shetani alimjaribu kwa kumwambia: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, yaambie mawe haya yawe mikate.”—Mathayo 4:3.

14. Ni katika njia gani Shetani anaweza kuwafanya watu waone kwamba kuwasiliana na roho waovu si hatari?

14 Leo, Ibilisi anaendelea kutokeza mashaka. Anajaribu kufanya baadhi ya mazoea ya kuwasiliana na roho waovu yaonekane kuwa hayana madhara yoyote na hakuna ubaya wa kujihusisha nayo. Hata baadhi ya Wakristo wamepofushwa wasione hatari hiyo. (2 Wakorintho 11:3) Hivyo, tunaweza kufanya nini ili kujilinda? Tunaweza kuhakikishaje kwamba hatudanganywi na mbinu za Shetani? Acheni tuchunguze maeneo mawili ambayo tunaweza kupotoshwa: burudani na matibabu.

SHETANI ANATUMIA TAMAA ZETU KUTUNASA

15. Ni kwa njia gani tunaweza kuwasiliana na roho waovu kupitia burudani?

15 Leo, sinema nyingi, video, vipindi vya televisheni, michezo ya kompyuta na tovuti za Intaneti zinaonyesha mambo kuhusu roho waovu, uchawi, na nguvu zinazopita uwezo wa kibinadamu. Wengi wanaona mambo hayo kuwa burudani za kufurahisha zisizo na madhara yoyote na hawatambui hatari za kuwaruhusu roho waovu waingie katika maisha yao. Mtu anaweza kuwasiliana na roho waovu kwa kufanya uaguzi kwa kutumia nyota, kusoma kiganja, kusoma kadi za ubashiri, na matufe ya kubashiri. Ibilisi ameficha hatari ya kujihusisha na mambo hayo kwa kujaribu kuyafanya yaonekane kuwa yenye kusisimua, kuvutia, na kustaajabisha. Mtu anaweza kufikiri kwamba hakuna ubaya wa kutazama mambo yanayohusiana na roho waovu maadamu tu yeye mwenyewe hafanyi mambo hayo moja kwa moja. Kwa nini ni hatari kufikiri hivyo?—1 Wakorintho 10:12.

16. Kwa nini tunapaswa kuepuka burudani zinazohusiana na roho waovu?

16 Shetani na roho waovu hawawezi kusoma mawazo yetu. Lakini wanaweza kujua mambo tunayotamani na tunayofikiria kwa kuangalia uchaguzi tunaofanya kwa ajili yetu na familia yetu, kutia ndani burudani tunazochagua. Tunapochagua sinema, muziki, au vitabu vinavyohusu uaguzi, mambo ya uchawi, watu wanaonyonya wengine damu, au mambo kama hayo, Shetani na roho waovu wanaweza kujua kwamba tunataka kujua kuhusu mambo hayo. Wanaweza kujaribu kutufanya tujihusishe zaidi na roho waovu.—Soma Wagalatia 6:7.

17. Shetani anaweza kuitumiaje vibaya tamaa yetu ya kutaka kuwa na afya nzuri?

17 Pia, Shetani anaweza kutumia vibaya tamaa yetu ya kutaka kuwa na afya nzuri. Leo watu wengi wanasumbuliwa na matatizo ya afya. Mtu anaweza kujaribu matibabu ya kila aina bila mafanikio. (Marko 5:25, 26) Kwa sababu ya kutaka sana kupona anaweza kuamua kujaribu matibabu ya aina yoyote. Lakini tukiwa Wakristo tunapaswa kuwa waangalifu tusijihusishe na matibabu yanayohusiana na “nguvu za uchawi.”—Isaya 1:13.

Unapokuwa mgonjwa mtegemee Yehova

18. Wakristo wanapaswa kuepuka matibabu ya aina gani?

18 Katika Israeli la kale, kuna watu waliotumia “nguvu za uchawi.” Yehova aliwaambia hivi: “Mnaponyoosha mikono yenu, Mimi huficha macho yangu nisiwaone. Ingawa mnatoa sala nyingi, Mimi sisikilizi.” (Isaya 1:15) Hebu wazia hilo—Yehova alikataa kusikiliza sala zao! Hatungependa kufanya jambo lolote ambalo linaweza kuharibu uhusiano wetu na Yehova na kumfanya asitusaidie, hasa tunapokuwa wagonjwa. (Zaburi 41:3) Hivyo tunapaswa kuhakikisha ikiwa matibabu tunayotaka yanahusiana na roho waovu. (Mathayo 6:13) Ikiwa kuna uwezekano kwamba yanahusiana na roho waovu, tunapaswa kuyaepuka!—Soma Maelezo ya Ziada 32.

HADITHI KUHUSU ROHO WAOVU

19. Ibilisi amefanya nini ili watu wengi wamwogope?

19 Ingawa watu fulani wanafikiri kwamba Ibilisi na roho waovu si halisi, wengine wanajua kwamba ni viumbe halisi kutokana na mambo waliyojionea maishani. Watu wengi wanawaogopa sana roho waovu na ni watumwa wa ushirikina. Wengine wanawafanya watu wawaogope roho waovu kwa kuwasimulia hadithi za jinsi wanavyowaumiza wanadamu. Mara nyingi, watu wanastaajabishwa na hadithi hizo hivi kwamba wanazisimulia kwa msisimuko. Katika visa vingi, hadithi hizo huwafanya watu wamwogope Ibilisi.

20. Ni kwa njia gani tunaweza kueneza uwongo wa Shetani?

20 Zingatia jambo hili—Shetani anataka watu wamwogope. (2 Wathesalonike 2:9, 10) Yeye ni mwongo na anajua jinsi ya kuathiri akili za watu wanaovutiwa na roho waovu na kuwafanya waamini mambo ambayo si ya kweli. Watu hao wanaweza kusimulia mambo wanayofikiri wameona na kusikia. Kadiri watu wanavyosimulia hadithi hizo tena na tena, ndivyo zinavyotiwa chumvi. Hatungependa kumsaidia Shetani kueneza hofu kwa kusimulia hadithi hizo.—Yohana 8:44; 2 Timotheo 2:16.

21. Badala ya kusimulia hadithi kuhusu roho waovu, tunaweza kuzungumza kuhusu nini?

21 Ikiwa mtumishi wa Yehova aliwahi kuwasiliana na roho waovu zamani, hapaswi kurudia kusimulia hadithi hizo ili kuwatumbuiza wengine. Watu wa Yehova hawapaswi kuogopeshwa na kitu chochote ambacho Ibilisi na roho waovu wanaweza kufanya. Badala yake, tunapaswa kumkazia fikira Yesu, na nguvu ambazo amepewa na Yehova. (Waebrania 12:2) Yesu hakuwatumbuiza wafuasi wake kwa kuwasimulia hadithi kuhusu roho waovu. Alikazia fikira ujumbe wa Ufalme na “mambo makuu ya Mungu.”—Matendo 2:11; Luka 8:1; Waroma 1:11, 12.

22. Umeazimia kufanya nini?

22 Tusisahau kwamba lengo la Shetani ni kuharibu uhusiano wetu na Yehova. Anajaribu juu chini kutimiza lengo lake. Lakini tunazijua mbinu za Ibilisi na tumeazimia kuepuka aina zote za kuwasiliana na roho waovu. Hatutampa “Ibilisi nafasi” ya kudhoofisha azimio letu. (Soma Waefeso 4:27.) Naam, ikiwa tutampinga Ibilisi hatutanaswa na mitego yake na Yehova atatulinda.—Waefeso 6:11.