Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 10

Ndoa​​—Zawadi Kutoka kwa Mungu

Ndoa​​—Zawadi Kutoka kwa Mungu

“Kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi.” —MHUBIRI 4:12.

1, 2. (a) Wenzi wapya wa ndoa wanakuwa na matarajio gani? (b) Tutazungumzia maswali gani katika sura hii?

WAZIA bwana na bibi-harusi ambao wana furaha siku ya harusi yao. Wana msisimko na wamejawa na matumaini wanapofikiria maisha yao ya wakati ujao pamoja. Wanatumaini kwamba ndoa yao itadumu na kuwa yenye furaha.

2 Hata hivyo, ndoa nyingi zinazoanza vizuri, haziendelei kuwa na furaha. Ili ndoa idumu na kuwa yenye furaha, wenzi wa ndoa wanahitaji mwongozo wa Mungu. Kwa hiyo, acheni tuzungumzie majibu ya Biblia kwa maswali haya: Ndoa ina faida zipi? Ukiamua kufunga ndoa, unaweza kuchaguaje mwenzi anayefaa? Unaweza kufanya nini ili uwe mume au mke bora? Na ni nini kinachoweza kusaidia ndoa idumu?—Soma Methali 3:5, 6.

JE, NIFUNGE NDOA?

3. Je, ni lazima mtu afunge ndoa ili awe na furaha? Fafanua.

3 Watu fulani wanaamini kwamba mtu hawezi kuwa na furaha ikiwa hajafunga ndoa. Lakini hilo si kweli. Yesu alisema kwamba useja unaweza kuwa zawadi. (Mathayo 19:11, 12) Na mtume Paulo alisema kwamba useja unaweza kuwa na faida. (1 Wakorintho 7:32-38) Kufunga ndoa ni uamuzi wa kibinafsi. Hupaswi kuruhusu rafiki zako, watu wa familia, au utamaduni wenu ukushinikize kufunga ndoa.

4. Taja baadhi ya faida za kuwa na ndoa yenye furaha.

4 Biblia pia inasema kwamba ndoa ni zawadi kutoka kwa Mungu na kwamba kuna faida za kufunga ndoa. Yehova alisema hivi kuhusu mwanamume wa kwanza, Adamu: “Si vema mwanamume huyu aendelee kuwa peke yake. Nitamuumbia msaidizi, awe kikamilisho chake.” (Mwanzo 2:18) Yehova alimuumba Hawa ili awe mke wa Adamu, nao wakawa familia ya kwanza ya wanadamu. Wenzi wa ndoa wakipata watoto, ndoa yao inapaswa kuandaa mazingira yanayofaa ya kuwalea. Hata hivyo, kusudi la ndoa si kupata watoto tu.—Zaburi 127:3; Waefeso 6:1-4.

5, 6. Ndoa inawezaje kuwa kama “kamba ya nyuzi tatu”?

5 Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja kwa sababu wanapata thawabu njema kwa kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, mwenzake anaweza kumwinua. Lakini itakuwaje kwa yule atakayeanguka naye hana mtu wa kumwinua? . . . Na kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi.”—Mhubiri 4:9-12.

6 Ndoa nzuri inaweza kuwa muungano wa marafiki wa karibu sana ambao wanasaidiana, kufarijiana, na kulindana. Upendo unaweza kufanya ndoa iwe imara, lakini itakuwa imara zaidi mume na mke wanapomwabudu Yehova. Kisha ndoa yao inaweza kuwa kama “kamba ya nyuzi tatu” zilizofumwa pamoja. Kamba hiyo ni imara kuliko kamba ya nyuzi mbili. Yehova anapohusishwa katika ndoa, itakuwa imara.

7, 8. Paulo alitoa ushauri gani kuhusu ndoa?

7 Baada ya wenzi kufunga ndoa, kila mmoja anaweza kutosheleza tamaa za kiasili za ngono za mwenzake. (Methali 5:18) Hata hivyo, ikiwa mtu atafunga ndoa ili tu atosheleze tamaa hizo, huenda asichague mwenzi kwa hekima. Hiyo ndiyo sababu Biblia inasema mtu anapaswa kufunga ndoa baada ya kupita “upeo wa ujana,” wakati ambapo tamaa za ngono huwa zenye nguvu. (1 Wakorintho 7:36) Ni bora kusubiri hadi tamaa hizo zitakapopungua kabla ya kufunga ndoa. Kisha, mtu anaweza kufikiri vizuri zaidi na kufanya uamuzi mzuri zaidi.—1 Wakorintho 7:9; Yakobo 1:15.

8 Ikiwa unafikiria kufunga ndoa, ni vema kuwa na usawaziko na kujua kwamba ndoa zote zina changamoto. Paulo alisema kwamba wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Hata ndoa bora zaidi, itapatwa na hali ngumu. Kwa hiyo, ukiamua kwamba unataka kufunga ndoa, hakikisha kwamba umechagua mwenzi wako kwa hekima.

KUCHAGUA MWENZI WA NDOA ANAYEFAA

9, 10. Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa tutafunga ndoa na mtu asiyemwabudu Yehova?

9 Ni muhimu kukumbuka kanuni hii ya Biblia mtu anapochagua mume au mke: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14) Mfano huo unatokana na maisha ya ukulima. Mkulima hawezi kuwafunga nira wanyama wawili wanaotofautiana sana kwa ukubwa na nguvu ili wakafanye kazi pamoja shambani. Halingekuwa jambo la fadhili kufanya hivyo kwa sababu wanyama wote wawili watateseka. Katika njia hiyohiyo, ndoa kati ya mtu anayemwabudu Yehova na mtu asiyemwabudu inaweza kuwa na matatizo mengi. Kwa hiyo, Biblia inatupa ushauri wa hekima kwamba tufunge ndoa “katika Bwana tu.”—1 Wakorintho 7:39.

10 Nyakati nyingine, Wakristo fulani wamehisi kwamba ni afadhali kufunga ndoa na mtu asiyemwabudu Yehova badala ya kuwa peke yao. Lakini tukipuuza shauri la Biblia, mara nyingi matokeo ni maumivu na kukosa furaha. Tukiwa waabudu wa Yehova, kumwabudu ndilo jambo muhimu zaidi maishani. Ungehisije ikiwa hungeweza kushiriki na mwenzi wako sehemu hiyo muhimu zaidi ya maisha yako? Watu wengi wameamua kubaki waseja badala ya kufunga ndoa na mtu asiyempenda au kumwabudu Yehova.—Soma Zaburi 32:8.

11. Unaweza kuchaguaje mwenzi wa ndoa anayefaa?

11 Hilo halimaanishi kwamba mtu yeyote anayemtumikia Yehova anaweza kuwa mume au mke anayekufaa. Ikiwa unafikiria kufunga ndoa, tafuta mtu unayempenda na mnayepatana katika masuala mengi. Subiri hadi upate mtu aliye na malengo kama yako na anayetanguliza kumtumikia Mungu. Tumia muda kusoma na kutafakari ushauri mzuri kuhusu ndoa unaoandaliwa katika machapisho ya mtumwa mwaminifu.—Soma Zaburi 119:105.

12. Tunaweza kujifunza nini katika Biblia kuhusu utamaduni wa kuchaguliwa mwenzi wa ndoa?

12 Katika tamaduni fulani, ni kawaida kwa wazazi kumchagulia mwana au binti yao mwenzi wa ndoa. Wanahisi kwamba wazazi wanajua mwenzi atakayemfaa zaidi mtoto wao. Zoea hilo lilikuwa la kawaida katika nyakati za Biblia pia. Hivyo, familia yenu ikiamua kufuata tamaduni hizo, Biblia inaweza kuwasaidia wazazi kujua sifa wanazopaswa kutafuta katika mwenzi huyo. Kwa mfano, Abrahamu alipomchagulia mwana wake Isaka mke, hakutanguliza pesa au umaarufu; alitafuta mke anayempenda Yehova.—Mwanzo 24:3, 67; soma Maelezo ya Ziada 25.

KUJITAYARISHA KWA AJILI YA NDOA

13-15. (a) Mwanamume anaweza kujitayarishaje kuwa mume mzuri? (b) Mwanamke anaweza kujitayarishaje kuwa mke mwema?

13 Ikiwa unafikiria kufunga ndoa, hakikisha kwamba uko tayari. Huenda ukafikiri kwamba uko tayari, lakini acheni tuzungumzie ni nini hasa kinachomaanishwa na kuwa tayari kwa ajili ya ndoa. Labda utashangazwa na mambo utakayojifunza.

Soma na utafakari mashauri ya Neno la Mungu kuhusu ndoa

14 Biblia inaonyesha kwamba waume na wake wana majukumu tofauti katika familia. Kwa hiyo, kila mmoja atajitayarisha kwa njia tofauti ikitegemea jinsia yake. Mwanamume anapofikiria kuoa, anahitaji kujiuliza ikiwa yuko tayari kuwa kichwa cha familia. Yehova anamtarajia mume amtunze mke na watoto wake kimwili na kihisia. Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba mume anahitaji kuongoza familia yake katika ibada. Biblia inamfafanua mwanamume ambaye haitunzi familia yake kuwa “mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Kwa hiyo, ikiwa wewe ni mwanamume anayefikiria kuoa, fikiria jinsi kanuni hii ya Biblia inavyoweza kutumika: “Tayarisha kazi yako ya nje, na utayarishe kila kitu shambani; kisha uijenge nyumba yako.” Kwa maneno mengine, kabla ya kufunga ndoa, hakikisha kwamba unaweza kuwa mume ambaye Yehova anataka uwe.—Methali 24:27.

15 Mwanamke anayefikiria kuolewa, anahitaji kujiuliza ikiwa yuko tayari kwa majukumu ya kuwa mke na huenda pia kuwa mama. Biblia inataja baadhi ya njia ambazo mke mwema anamtunza mume na watoto wake. (Methali 31:10-31) Leo, wanaume na wanawake wengi wanafikiria tu mambo ambayo mwenzi wao atawafanyia. Lakini Yehova anataka tufikirie kile ambacho sisi tunaweza kumfanyia mwenzi wetu.

16, 17. Ikiwa unafikiria kufunga ndoa, unapaswa kutafakari kuhusu mambo gani?

16 Kabla ya kufunga ndoa, tafakari mambo ambayo Yehova anasema kuhusu waume na wake. Kuwa kichwa cha familia, hakumaanishi kwamba mwanamume anaweza kumtendea mke wake vibaya kimwili au kihisia. Kichwa mzuri wa familia anamwiga Yesu, ambaye sikuzote anawapenda na kuwatendea kwa fadhili wale walio chini ya utunzaji wake. (Waefeso 5:23) Kwa upande wake, mwanamke anahitaji kufikiria inamaanisha nini kuunga mkono maamuzi ya mume wake na kushirikiana naye. (Waroma 7:2) Anahitaji kujiuliza ikiwa atakuwa na furaha akijitiisha chini ya mwanamume ambaye si mkamilifu. Ikiwa anafikiri kwamba hawezi kujitiisha, huenda akaamua kwamba inafaa aendelee kuwa mseja kwa sasa.

17 Waume na wake wanahitaji kujali faida za mwenzi wao kuliko kujifurahisha wao wenyewe. (Soma Wafilipi 2:4.) Paulo aliandika hivi: “Kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:21-33) Wanaume na wanawake wanahitaji kuhisi kwamba wanapendwa na kuheshimiwa. Lakini ili ndoa ifanikiwe, mwanamume anahitaji hasa kujua kwamba mke wake anamheshimu, na mke anahitaji hasa kujua kwamba mume wake anampenda.

18. Kwa nini watu wanaochumbiana wanahitaji kuwa waangalifu?

18 Kipindi cha uchumba kinapaswa kuwa kipindi cha furaha kwa watu wawili wanaoendelea kufahamiana vizuri zaidi. Pia, ni wakati unaofaa wa kuangalia mambo wakiwa na usawaziko na unyoofu ili waamue ikiwa kweli wanataka kuishi pamoja. Wakati wa uchumba, mwanamume na mwanamke wanajifunza kuwasiliana na wanajaribu kujua ni nini hasa kilicho moyoni mwa mwenzake. Wanapozidi kuwa na uhusiano wa karibu, ni jambo la kawaida kwa kila mmoja kuvutiwa kimwili na mwenzake. Lakini wanahitaji kudhibiti jinsi wanavyoonyesha hisia hizo kabla ya kufunga ndoa ili wasijiingize katika upotovu wa maadili. Upendo wa kweli utawasaidia kuwa na sifa ya kujizuia na utawazuia kufanya chochote ambacho kinaweza kudhuru uhusiano wao, na pia uhusiano wao na Yehova.—1 Wathesalonike 4:6.

Wakati wa uchumba, mwanamume na mwanamke wanaweza kujifunza kuwasiliana

SIRI YA KUDUMISHA NDOA

19, 20. Wakristo wana maoni gani kuhusu ndoa?

19 Vitabu na sinema nyingi humalizia kwa harusi kubwa yenye furaha. Katika maisha halisi, harusi ndio mwanzo tu. Yehova alikusudia ndoa iwe uhusiano unaodumu milele.—Mwanzo 2:24.

20 Leo, wengi wanaona ndoa kuwa mpango wa muda mfupi tu. Ni rahisi kufunga ndoa na ni rahisi kutalikiana. Wengine wanahisi kwamba matatizo yanapoanza, huo ndio wakati unaofaa wa kumwacha mwenzi wao na kuvunja ndoa hiyo. Lakini kumbuka ule mfano wa Biblia kuhusu kamba imara iliyofumwa kwa nyuzi tatu. Kamba hiyo haitakatika hata ikiwa chini ya mkazo. Tunapotafuta msaada wa Yehova, ndoa inaweza kudumu. Yesu alisema hivi: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:6.

21. Ni nini kitakachowasaidia mume na mke wapendane?

21 Sisi sote tuna sifa nzuri na tuna udhaifu pia. Ni rahisi sana kukazia fikira udhaifu wa wengine, hasa udhaifu wa mwenzi wetu. Tukifanya hivyo, hatutakuwa na furaha. Kwa upande mwingine, ikiwa tutakazia fikira sifa nzuri za mwenzi wetu, tunaweza kuwa na ndoa yenye furaha. Je, inafaa kuwa na maoni hayo kuelekea mwenzi wetu ambaye si mkamilifu? Ndiyo! Yehova anajua kwamba sisi si wakamilifu, hata hivyo, anakazia fikira sifa zetu nzuri. Ingekuwaje ikiwa hangefanya hivyo? Mtunga-zaburi alisema hivi: “Ikiwa ungekuwa unatazama tu makosa, Ee Yah, basi ni nani, Ee Yehova, angeweza kusimama?” (Zaburi 130:3) Waume na wake wanaweza kumwiga Yehova kwa kutafuta sifa nzuri za mwenzi wao na kwa kuwasamehe bila kukawia.—Soma Wakolosai 3:13.

22, 23. Abrahamu na Sara waliwawekea wenzi wa ndoa mfano gani mzuri?

22 Kadiri miaka inavyopita, ndivyo ndoa inavyoweza kuwa imara. Abrahamu na Sara waliishi pamoja kwa muda mrefu na ndoa yao ilikuwa yenye furaha. Yehova alipomwambia Abrahamu aondoke jiji la Uru, inawezekana Sara alikuwa na zaidi ya umri wa miaka 60. Wazia jinsi ilivyokuwa vigumu kwake kuacha nyumba yake yenye starehe na kuishi katika mahema. Lakini Sara alikuwa rafiki mzuri wa mume wake na alishirikiana naye na kumheshimu sana. Kwa hiyo, aliunga mkono maamuzi ya Abrahamu na alimsaidia kuyafanikisha.—Mwanzo 18:12; 1 Petro 3:6.

23 Bila shaka, kuwa na ndoa nzuri hakumaanishi kwamba mume na mke watakubaliana kuhusu kila jambo. Pindi moja, Abrahamu alipokataa maoni ya Sara, Yehova alimwambia hivi: “Msikilize.” Abrahamu alimsikiliza mke wake, na matokeo yakawa mazuri. (Mwanzo 21:9-13) Ikiwa nyakati fulani hukubaliani na mwenzi wako, usivunjike moyo. Jambo muhimu ni kwamba mnapokosa kukubaliana, endeleeni kutendeana kwa upendo na heshima.

Tumia Neno la Mungu tangu mwanzo wa ndoa yako

24. Ndoa zetu zinaweza kumleteaje Yehova heshima?

24 Katika kutaniko la Kikristo, kuna maelfu ya ndoa zenye furaha. Ukitaka kufunga ndoa, kumbuka kwamba kuchagua mwenzi wako ni mojawapo ya maamuzi muhimu zaidi utakayowahi kufanya. Uamuzi huo utaamua maisha yako yote yatakuwaje, kwa hiyo, tafuta mwongozo wa Yehova. Kisha utaweza kumchagua mwenzi kwa hekima, kujitayarisha vizuri kwa ajili ya ndoa, na kujitahidi kusitawisha kifungo imara na chenye upendo ambacho kitamletea Yehova heshima.