Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 13

Je, Sherehe Zote Zinampendeza Mungu?

Je, Sherehe Zote Zinampendeza Mungu?

“Endeleeni kuhakikisha jambo linalokubalika kwa Bwana.”—WAEFESO 5:10.

1. Tunahitaji kufanya nini ili tuhakikishe kwamba ibada yetu inampendeza Yehova, na kwa nini?

YESU alisema hivi: “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.” (Yohana 4:23; 6:44) Ni lazima kila mmoja wetu “[aendelee] kuhakikisha jambo linalokubalika kwa Bwana.” (Waefeso 5:10) Si rahisi kufanya hivyo sikuzote. Shetani anajaribu kutupotosha tufanye mambo ambayo hayampendezi Yehova.—Ufunuo 12:9.

2. Eleza mambo yaliyotokea karibu na Mlima Sinai.

2 Shetani anajaribu kutupotosha jinsi gani? Njia moja ni kwa kutufanya tushindwe kutofautisha kati ya lililo sawa na lililo kosa. Fikiria kilichotokea Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi karibu na Mlima Sinai. Musa alikuwa ameenda juu mlimani, na watu walikuwa wakimsubiri arudi kambini. Mwishowe walichoka kusubiri na wakamwomba Haruni awatengenezee mungu. Alitengeneza sanamu ya dhahabu yenye umbo la ndama. Kisha watu wakapanga kuwe na sherehe. Walicheza dansi mbele ya sanamu hiyo ya ndama na kuiinamia. Waliamini kwamba kwa kuiinamia sanamu hiyo, walikuwa wakimwabudu Yehova. Lakini hata ikiwa watu waliona tukio hilo kuwa “sherehe kwa ajili ya Yehova,” maoni yao hayakufanya sherehe hiyo ikubalike kwa Yehova. Aliiona kuwa ibada ya sanamu, na akawaangamiza watu wengi. (Kutoka 32:1-6, 10, 28) Tunajifunza nini kutokana na hilo? Usidanganyike. “[Usiguse] kitu chochote kichafu,” na umruhusu Yehova akufundishe kutofautisha kati ya mema na mabaya.—Isaya 52:11; Ezekieli 44:23; Wagalatia 5:9.

3, 4. Kwa nini inafaa kuchunguza vyanzo vya sherehe zinazopendwa na watu wengi?

3 Yesu alipokuwa duniani, aliwazoeza mitume wake waweke kielelezo kuhusiana na ibada safi. Baada ya kifo chake, mitume waliendelea kuwafundisha wanafunzi wapya kanuni za Yehova. Lakini baada ya mitume kufa, walimu wa uwongo walianza kuingiza kutanikoni mafundisho ya uwongo, desturi, na sherehe za kipagani. Hata walibadili majina ya baadhi ya sherehe za kipagani ili kuzifanya zionekane za Kikristo. (2 Wathesalonike 2:7, 10; 2 Yohana 6, 7) Sherehe nyingi kati ya hizo bado zinapendwa leo, na bado zinaendeleza mafundisho ya uwongo na mambo yanayohusiana na uchawi. *Ufunuo 18:2-4, 23.

4 Ulimwenguni pote, sherehe na sikukuu ni sehemu muhimu ya maisha ya watu. Hata hivyo, unapoendelea kujifunza maoni ya Yehova kuhusu mambo, huenda ukaona uhitaji wa kubadili mawazo yako kuhusu sherehe fulani. Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo, lakini unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakusaidia. Acheni tuchunguze vyanzo vya baadhi ya sherehe zinazopendwa na watu wengi ili tuelewe maoni ya Yehova kuhusiana nazo.

KRISMASI ILIANZAJE?

5. Kuna uthibitisho gani kwamba Yesu hakuzaliwa Desemba 25?

5 Katika sehemu nyingi duniani, watu wanasherehekea Krismasi Desemba 25, tarehe ambayo watu wengi wanafikiri Yesu alizaliwa. Biblia haionyeshi siku au mwezi ambao Yesu alizaliwa, lakini inatuambia Yesu alizaliwa katika kipindi gani cha mwaka. Luka aliandika kwamba Yesu alipozaliwa huko Bethlehemu, “wachungaji [walikuwa wakiishi] nje,” wakitunza mifugo yao. (Luka 2:8-11) Katika mwezi wa Desemba, kunakuwa na baridi, mvua, na theluji katika Bethlehemu, kwa hiyo wachungaji hawangeweza kuwa nje na mifugo yao usiku. Tunajifunza nini kutokana na hilo? Yesu hakuzaliwa Desemba. Uthibitisho wa Biblia na historia unaonyesha alizaliwa katika miezi ya Septemba au Oktoba katika kalenda ya sasa, wakati hali ya hewa ilikuwa nzuri.

6, 7. (a) Desturi nyingi za Krismasi zilianzaje? (b) Ni nini kinachopaswa kutuchochea kutoa zawadi?

6 Kwa hiyo, Krismasi ilianzaje? Ilitokana na sherehe za kipagani, kama vile sherehe ya Waroma ya Saturnalia, iliyofanywa kwa ajili ya Saturn, mungu wa kilimo. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Saturnalia ni sherehe ya Kiroma iliyofanywa katikati ya Desemba, na desturi nyingi zinazofanywa wakati wa Krismasi zilitokana nayo. Kwa mfano, wakati wa sherehe hiyo watu walikuwa na karamu kubwa, walipeana zawadi, na kuwasha mishumaa.” (The Encyclopedia Americana) Pia, Waajemi walisherehekea sikukuu ya kuzaliwa kwa mungu-jua anayeitwa Mithra Desemba 25.

7 Hata hivyo, watu wengi wanaosherehekea Krismasi leo hawafikirii vyanzo vyake vya kipagani. Wanatazamia kwa hamu kuwa pamoja na familia zao, kula chakula kizuri, na kutoa zawadi wakati wa Krismasi. Bila shaka, tunapenda familia zetu na marafiki wetu, na Yehova anataka watumishi wake waonyeshane ukarimu. Andiko la 2 Wakorintho 9:7 linatuambia, “Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” Yehova hataki tuonyeshe ukarimu katika pindi za pekee tu. Watu wa Yehova wanafurahia kutoa zawadi na kuwa pamoja na marafiki wao na familia zao wakati wowote katika mwaka, bila kutarajia kupata chochote. Wanatoa kwa sababu wanawapenda wengine.—Luka 14:12-14.

Kujua chanzo cha sherehe mbalimbali kunaweza kujua kile tunachopaswa kuepuka

8. Je, wanajimu walimpa Yesu zawadi alipokuwa mtoto mchanga baada tu ya kuzaliwa? Eleza.

8 Ili kuunga mkono wazo la kutoa zawadi wakati wa Krismasi, watu wengi wanasema kwamba Yesu alipozaliwa wanaume watatu wenye hekima walimletea zawadi akiwa amelazwa kwenye hori. Ni kweli kwamba wanaume fulani walimtembelea Yesu na kumletea zawadi. Katika nyakati za Biblia, lilikuwa jambo la kawaida kumletea zawadi mtu muhimu. (1 Wafalme 10:1, 2, 10, 13) Lakini je, ulijua kwamba Biblia inasema wanaume hao walikuwa wanajimu, watu waliofanya mazingaombwe na ambao hawakuwa waabudu wa Yehova? Zaidi ya hilo, hawakumtembelea Yesu akiwa mtoto mchanga aliyelazwa kwenye hori. Walimtembelea baadaye, alipokuwa akiishi ndani ya nyumba. Isitoshe, huenda wanajimu hao walisafiri kwa miezi kadhaa kutoka Mashariki. Kwa hiyo, kufikia wakati walipofika, Yesu hakuwa tena mtoto mchanga aliyetoka tu kuzaliwa.—Mathayo 2:1, 2, 11.

BIBLIA INASEMA NINI KUHUSU SIKUKUU ZA KUZALIWA?

9. Ni sikukuu zipi za kuzaliwa zinazotajwa katika Biblia?

9 Siku ambayo mtoto anazaliwa ni siku ya furaha. (Zaburi 127:3) Lakini hilo halimaanishi kwamba tunapaswa kusherehekea sikukuu za kuzaliwa. Fikiria hili: Ni sherehe mbili tu za sikukuu ya kuzaliwa zinazotajwa katika Biblia. Moja ilikuwa sikukuu ya kuzaliwa kwa Farao wa Misri, na nyingine ilikuwa sikukuu ya kuzaliwa kwa Mfalme Herode Antipa. (Soma Mwanzo 40:20-22; Marko 6:21-29.) Hakuna yeyote kati ya watawala hao aliyekuwa mtumishi wa Yehova. Kwa hakika, hakuna sehemu yoyote katika Biblia inayoonyesha kwamba mwabudu wa Yehova alisherehekea sikukuu ya kuzaliwa.

10. Wakristo wa mapema walikuwa na maoni gani kuhusu sikukuu za kuzaliwa?

10 Kitabu kimoja kinasema kwamba Wakristo wa mapema “waliona kusherehekea siku ya kuzaliwa ya mtu yeyote kuwa desturi ya kipagani.” (The World Book Encyclopedia) Desturi kama hizo zilitokana na mafundisho ya uwongo. Kwa mfano, Wagiriki wa zamani waliamini kwamba kila mtu analindwa na roho fulani iliyokuwepo mtu huyo alipokuwa akizaliwa. Na walifikiri kwamba roho hiyo ilikuwa na uhusiano na mungu ambaye siku ya kuzaliwa kwake ililingana na siku ya kuzaliwa kwa mtu huyo. Mbali na hilo, sikukuu za kuzaliwa zinahusiana na unajimu na uaguzi.

11. Kwa maoni ya Yehova tunapaswa kuonyesha ukarimu wakati gani?

11 Watu wengi huhisi kwamba siku ya kuzaliwa ni ya pekee na wanapaswa kuthaminiwa na kuonyeshwa upendo. Lakini tunaweza kuwaonyesha upendo marafiki na watu wa familia wakati wowote katika mwaka, badala ya kufanya hivyo siku moja tu. Yehova anataka tuwe wenye fadhili na wakarimu kila wakati. (Soma Matendo 20:35.) Kila siku tunamshukuru kwa zawadi yenye thamani ya uhai, na si katika siku tuliyozaliwa tu.—Zaburi 8:3, 4; 36:9.

Upendo huwachochea Wakristo wa kweli kutoa zawadi

12. Ni kwa njia gani siku ya kufa inaweza kuwa bora kuliko siku ya kuzaliwa?

12 Mhubiri 7:1 inasema hivi: “Jina zuri ni bora kuliko mafuta mazuri, na siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa.” Siku ya kufa inawezaje kuwa bora kuliko siku yetu ya kuzaliwa? Wakati ambapo mtu anazaliwa, hajatimiza jambo lolote maishani iwe ni zuri au baya. Lakini tunapotumia maisha yetu kumtumikia Yehova na kuwatendea wengine mema, tunasitawisha “jina zuri,” au sifa nzuri, na Yehova atatukumbuka hata baada ya kufa. (Ayubu 14:14, 15) Waabudu wa Yehova hawasherehekei siku yao ya kuzaliwa au ya Yesu. Kwa hakika, tukio pekee ambalo Yesu alituamuru tuadhimishe ni Ukumbusho wa kifo chake.—Luka 22:17-20; Waebrania 1:3, 4.

CHANZO CHA ISTA

13, 14. Sherehe za Ista zinahusianishwa na nini?

13 Watu wengi wanaamini kwamba wanaposherehekea Ista wanasherehekea ufufuo wa Yesu. Lakini je, Kristo aliamuru tusherehekee ufufuo wake? Hapana, hakufanya hivyo. Vitabu vya kihistoria vinasema kwamba Wakristo wa mapema hawakusherehekea Ista na kwamba inatokana na desturi za zamani za kipagani. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Hakuna popote katika Agano Jipya ambapo panaashiria kwamba Wakristo waliadhimisha sikukuu ya Ista . . . Wakristo hawakuwa hata na wazo la sikukuu za aina hiyo zilizotukuzwa.” (The Encyclopædia Britannica) Ni wazi kwamba Ista haihusiani na ufufuo wa Yesu.

14 Je, Yehova anafurahi anapoona watu wakichanganya desturi za dini za uwongo na ufufuo wa Mwana wake? La hasha. (2 Wakorintho 6:17, 18) Kwa kweli, Yehova hajawahi kutuagiza tusherehekee ufufuo wa Yesu.

DESTURI ZINAZOHUSIANA NA KIFO

15. Kwa nini Wakristo wa kweli huepuka desturi fulani zinazohusiana na kifo?

15 Wakristo wa kweli huepuka desturi nyingi zinazohusiana na kifo. Mtu anapokufa ni kawaida kwa waombolezaji kukesha usiku wote. Wakati wa mazishi, watu wa karibu wa familia hutupa mchanga au maua katika kaburi kabla ya kulifunika. Desturi nyingine pia hufanywa siku chache, miezi, au miaka baada ya mtu kufa. Mambo hayo yote hufanywa kwa sababu watu wanaamini kwamba wafu wanaweza kuwasaidia au kuwadhuru walio hai. Lakini Biblia inafundisha waliokufa “hawajui lolote kamwe.” Kwa hiyo, wale wanaotaka kudumu katika upendo wa Mungu hawawezi kushiriki katika desturi zozote zinazohusiana na kuabudu wafu. —Mhubiri 9:5, 10.

HARUSI ZINAZOMPENDEZA MUNGU

16, 17. Tunapaswa kufikiria nini tunapopanga harusi?

16 Siku ya harusi ni siku ya furaha. Watu husherehekea harusi kwa njia tofauti-tofauti duniani pote. Mara nyingi, watu hawafikirii chanzo cha desturi za sherehe za harusi, hivyo huenda wasijue kwamba baadhi ya desturi hizo zilitokana na mafundisho ya dini za kipagani. Wakristo wanaopanga harusi yao wanahitaji kuhakikisha kwamba itampendeza Yehova. Wakielewa chanzo cha desturi za harusi, wataweza kufanya uamuzi unaofaa.—Marko 10:6-9.

17 Inaaminiwa kwamba kusudi la desturi fulani za harusi ni kuwaletea ‘bahati njema’ wenzi wapya wa ndoa. (Isaya 65:11) Kwa mfano, katika maeneo fulani watu huwatupia maharusi mchele au vitu vingine. Wanaamini kwamba kufanya hivyo kutawapa wenzi hao wapya watoto, furaha, maisha marefu, na kutawalinda kutokana na maovu. Lakini Wakristo wanajitahidi kuepuka desturi zozote zinazohusiana na ibada ya uwongo.—Soma 2 Wakorintho 6:14-18.

18. Ni kanuni zipi nyingine za Biblia zinazotumika katika ndoa?

18 Wakristo wanaofunga ndoa wanataka harusi yao iwe na shangwe na yenye heshima na kuwafurahisha watakaohudhuria. Wageni wanapopewa nafasi ya kuzungumza katika harusi ya Kikristo hawapaswi kuzungumza bila fadhili, kuzungumzia mambo yanayoamsha hamu ya ngono, au yanayowavunjia maharusi heshima. (Methali 26:18, 19; Luka 6:31; 10:27) Mkristo anapofanya harusi anaepuka “kujionyesha mali zake maishani.” (1 Yohana 2:16) Ikiwa unapanga harusi, hakikisha kwamba baadaye hutakuwa na sababu yoyote ya kuhuzunika unapoikumbuka.—Soma Maelezo ya Ziada 28.

CHANZO CHA KUMTAKIA MTU HERI KWA GLASI YA KINYWAJI

19, 20. Ni nini chanzo cha kutakiana heri kwa glasi ya kinywaji?

19 Zoea moja ambalo limeenea sana katika harusi na sherehe nyingine ni lile la kuwatakia watu heri kwa glasi ya kinywaji. Katika pindi hizo, mtu mmoja anawatakia wengine heri wakiwa wameinua glasi zao. Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu desturi hiyo?

20 Kitabu kimoja kinatusaidia kuelewa mahali ambapo huenda desturi ya kuwatakia wengine heri kwa glasi ya kinywaji ilitoka. Kinasema kwamba wakati wa desturi fulani ya zamani ya kipagani “kinywaji fulani kitakatifu kilitolewa kwa miungu.” (International Handbook on Alcohol and Culture) Mtu alifanya hivyo “ili ombi lake lijibiwe. Sala yake ilikuwa tu na maneno ‘maisha marefu!’ au ‘afya njema!’” Zamani, watu waliinua vikombe ili kuomba miungu yao baraka. Lakini Yehova hatumii njia hiyo kutoa baraka.—Yohana 14:6; 16:23.

“ENYI MNAOMPENDA YEHOVA, CHUKIENI MAOVU”

21. Ni sherehe zipi nyingine ambazo Wakristo wanapaswa kuepuka?

21 Unapotaka kuamua ikiwa utashiriki sherehe fulani au la, jiulize sherehe hiyo inachochea watu wawe na mtazamo na tabia gani? Kwa mfano, sherehe fulani zinahusisha dansi chafu, kunywa kupita kiasi, na hata maadili mapotovu. Huenda pia lengo la sherehe hizo likawa kutukuza maisha ya mashoga na wasagaji au kuunga mkono utaifa. Tukishiriki katika sherehe za aina hiyo, je, kweli tunachukia kile ambacho Yehova anachukia?—Zaburi 1:1, 2; 97:10; 119:37.

22. Ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo kuamua ikiwa atashiriki katika sherehe fulani?

22 Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu sana kuepuka sherehe yoyote inayomvunjia Mungu heshima. Mtume Paulo aliandika hivi: “Iwe mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31; soma Maelezo ya Ziada 29.) Ni kweli kwamba si sherehe zote zinazohusisha maadili mapotovu, dini ya uwongo, au utaifa. Ikiwa sherehe fulani haivunji kanuni za Biblia, tunahitaji kufanya uamuzi wa kibinafsi ikiwa tutashiriki au la. Pia, tunapaswa kufikiria jinsi uamuzi wetu utakavyowaathiri wengine.

MTUKUZE YEHOVA KWA MANENO NA MATENDO YAKO

23, 24. Tunaweza kuwaelezaje washiriki wa familia maamuzi yetu kuhusu sherehe fulani?

23 Huenda umeacha kushiriki sherehe zinazomvunjia Yehova heshima. Lakini huenda baadhi ya watu wa familia yako ambao si Mashahidi wa Yehova wakafikiri kwamba huwapendi au hutaki kushirikiana nao tena. Wanaweza kuhisi kwamba wakati wa sikukuu ndizo pindi pekee ambapo familia inakuwa pamoja. Basi, unaweza kufanya nini? Kuna njia nyingi unazoweza kuwahakikishia kwamba unawapenda na kwamba wao ni wenye thamani kwako. (Methali 11:25; Mhubiri 3:12, 13) Unaweza kuwaalika katika pindi nyingine.

24 Ikiwa watu wako wa ukoo wanataka kujua kwa nini huwezi kusherehekea sikukuu fulani, unaweza kutafuta habari katika machapisho yetu na kwenye tovuti ya jw.org zitakazokusaidia kuwajibu. Usiwafanye wahisi kwamba unajaribu kushinda mabishano au kuwalazimisha wafikiri kama wewe. Wasaidie watu wa familia waone kwamba ulizingatia mambo mengi kabla ya kufanya uamuzi wa kibinafsi. Uwe mtulivu, na “maneno [yako] yawe yenye neema sikuzote, yaliyokolezwa chumvi.”—Wakolosai 4:6.

25, 26. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao kupenda kanuni za Yehova?

25 Ni muhimu kwamba sisi sote tuelewe kabisa sababu zetu za kibinafsi za kutoshiriki sherehe fulani. (Waebrania 5:14) Lengo letu ni kumpendeza Yehova. Na ikiwa sisi ni wazazi, tunapaswa kujitahidi kuwasaidia watoto wetu waelewe na kupenda kanuni za Biblia. Yehova anapokuwa halisi kwao, wao pia watataka kumpendeza.—Isaya 48:17, 18; 1 Petro 3:15.

26 Yehova anafurahi kutuona tukifanya yote tuwezayo ili kumwabudu kwa unyoofu na kwa njia inayokubalika. (Yohana 4:23) Lakini watu wengi wanafikiri kwamba mtu hawezi kuwa mnyoofu katika ulimwengu huu usio na unyoofu. Je, hilo ni kweli? Acheni tuzungumzie hilo katika sura inayofuata.

^ fu. 3 Unaweza kupata habari kuhusu sherehe hususa katika Fahirisi, Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova, na jw.org.