Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 7

Je, Una Maoni Kama ya Mungu Kuhusu Uhai?

Je, Una Maoni Kama ya Mungu Kuhusu Uhai?

“Wewe ndiye chanzo cha uhai.”—ZABURI 36:9.

1, 2. (a) Yehova ametupatia zawadi gani yenye thamani kubwa? (b) Yehova ametupatia nini ili kutusaidia tuwe na maisha bora?

YEHOVA amempa kila mmoja wetu zawadi ya pekee sana. Ni zawadi ya uhai. (Mwanzo 1:27) Anataka tuwe na maisha bora sana. Kwa hiyo, ametupatia kanuni ambazo zinatufundisha jinsi ya kufanya maamuzi mazuri. Tunapaswa kutumia kanuni hizo ili “kutofautisha” kati ya “mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.” (Waebrania 5:14) Tunapofanya hivyo, tunamruhusu Yehova atuzoeze kufikiri vizuri. Tunapoishi kulingana na kanuni za Mungu na kuona jinsi zinavyoboresha maisha yetu, tunaelewa thamani yake.

2 Maisha yana changamoto nyingi. Mara nyingi, tunahitaji kufanya maamuzi kuhusu mambo ambayo hakuna sheria hususa katika Biblia. Kwa mfano, huenda tukahitaji kufanya uamuzi kuhusu matibabu yanayohusisha damu. Tunaweza kufanyaje maamuzi ambayo yatampendeza Yehova? Biblia ina kanuni ambazo zinatufundisha maoni ya Yehova kuhusu uhai na damu. Ikiwa tutaelewa kanuni hizo, tutakuwa na uwezo wa kufanya maamuzi ya hekima na kudumisha dhamiri safi. (Methali 2:6-11) Tuchunguze baadhi ya kanuni hizo.

YEHOVA ANA MAONI GANI KUHUSU UHAI NA DAMU?

3, 4. (a) Mungu alifunuaje maoni yake kuhusu damu? (b) Damu inawakilisha nini?

3 Biblia inatufundisha kwamba damu ni takatifu kwa sababu inawakilisha uhai. Na uhai una thamani kubwa kwa Yehova. Kaini alipomuua ndugu yake, Yehova alimwambia hivi: “Damu ya ndugu yako inanililia kwa sauti kutoka ardhini.” (Mwanzo 4:10) Damu ya Abeli iliwakilisha uhai wake; Yehova alipozungumza kuhusu damu ya Abeli, alikuwa akirejelea uhai wake.

4 Baada ya Gharika ya siku za Noa, Mungu aliwaambia wanadamu kwamba wanaweza kula nyama. Lakini alisema hivi moja kwa moja: “Nyama pamoja na uhai wake—damu yake—hampaswi kula.” (Mwanzo 9:4) Amri hii inatumika kwa wazao wote wa Noa, kutia ndani sisi. Ni wazi kwamba kwa maoni ya Yehova, damu inawakilisha uhai. Nasi tunapaswa kuwa na maoni kama hayo kuhusu damu.—Zaburi 36:9.

5, 6. Sheria ya Musa ilionyeshaje maoni ya Yehova kuhusu uhai na damu?

5 Katika sheria ambayo Yehova alimpa Musa, alisema hivi: “Yeyote . . . akila damu yoyote ile, kwa hakika nitamkataa mtu anayekula damu, nami nitamwangamiza atoke miongoni mwa watu wake. Kwa maana uhai wa kiumbe umo katika damu.”—Mambo ya Walawi 17:10, 11.

6 Sheria ya Musa ilisema kwamba mtu akimuua mnyama kwa ajili ya chakula, alipaswa kumwaga damu yake ardhini. Jambo hilo lingeonyesha kwamba uhai wa mnyama huyo ulikuwa mtakatifu na ulikuwa mali ya Muumba wake, Yehova. (Kumbukumbu la Torati 12:16; Ezekieli 18:4) Lakini Yehova hakutarajia Waisraeli waondoe kila tone la damu walipomchinja mnyama. Maadamu wangefanya yote wawezayo kuondoa damu ya mnyama huyo, wangeweza kula nyama hiyo wakiwa na dhamiri safi. Kwa kuheshimu damu ya mnyama, wangeonyesha kwamba wanamheshimu Mpaji wa uhai, Yehova. Pia, Sheria iliwaamuru Waisraeli watoe wanyama kuwa dhabihu ya kufunika dhambi.—Soma Maelezo ya Ziada 19 na 20.

7. Daudi alionyeshaje kwamba anaheshimu damu?

7 Tunaweza kuona thamani ya damu kutokana na jambo ambalo Daudi alifanya alipokuwa akipigana na Wafilisti. Wanaume wa Daudi waliona kwamba alikuwa na kiu sana, hivyo wakaingia katika eneo hatari la maadui na kuhatarisha uhai wao ili wamletee maji. Lakini walipompelekea Daudi, alikataa kuyanywa na “akayamwaga mbele za Yehova.” Daudi akasema: “Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia, Ee Yehova, kufanya hivyo! Je, ninywe damu ya wanaume walioenda kuhatarisha uhai wao?” Daudi alielewa kwamba uhai na damu ni zenye thamani sana kwa Mungu.—2 Samweli 23:15-17.

8, 9. Wakristo leo wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu damu?

8 Kufikia wakati wa Wakristo wa mapema, watu wa Mungu hawakuhitaji kutoa dhabihu za wanyama. Lakini bado walihitaji kuwa na maoni yanayofaa kuhusu damu. Sehemu moja ya sheria ambayo Yehova alitaka Wakristo waendelee kushika ni “kujiepusha . . . na damu.” Kufanya hivyo kulikuwa muhimu kama tu kujiepusha na uasherati au ibada ya sanamu.—Matendo 15:28, 29.

Ninaweza kuelezaje uamuzi wangu kuhusu matumizi ya visehemu vya damu?

9 Hilo halijabadilika. Tukiwa Wakristo, tunajua kwamba Yehova ndiye Chanzo cha uhai na kila kitu kilicho na uhai ni mali yake. Pia, tunatambua kwamba damu ni takatifu na inawakilisha uhai. Hivyo, tunahakikisha kwamba tunazingatia kanuni za Biblia tunapofanya uamuzi wowote unaohusu matibabu yanayohusisha damu.

MATUMIZI YA DAMU KATIKA MATIBABU

10, 11. (a) Mashahidi wa Yehova wana maoni gani kuhusu kutia damu mishipani iwe ni damu nzima au sehemu nne kuu za damu? (b) Ni maamuzi gani ya kibinafsi ambayo kila Mkristo anahitaji kufanya?

10 Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba “kujiepusha . . . na damu” hakuhusishi tu kula au kunywa damu. Kunamaanisha kwamba hatukubali kutiwa damu mishipani, kuchangia damu, au kuhifadhi damu yetu wenyewe kwa ajili ya kutiwa mishipani. Pia, kunamaanisha kwamba hatukubali kutiwa mishipani sehemu yoyote kati ya zile sehemu nne kuu za damu—chembe nyekundu, chembe nyeupe, chembelele (platelets), na utegili (plasma).

11 Sehemu hizo nne kuu zinaweza kutenganishwa kitaalamu na kutokeza sehemu nyingine ndogondogo ambazo zinaitwa visehemu vya damu. Kila Mkristo anapaswa kuamua ikiwa atakubali au kukataa visehemu hivyo vya damu. Pia, kila Mkristo anapaswa kuamua ikiwa atakubali au kukataa mbinu za matibabu zinazohusisha matumizi ya damu yake mwenyewe. Kila mtu lazima ajiamulie jinsi damu yake itakavyoshughulikiwa wakati wa upasuaji, vipimo vinapochukuliwa, au mbinu ya kisasa ya matibabu inapotumiwa.—Soma Maelezo ya Ziada 21.

12. (a) Kwa nini maamuzi tunayofanya kwa kutegemea dhamiri ni muhimu machoni pa Yehova? (b) Tunaweza kufanyaje maamuzi yenye hekima kuhusiana na matibabu?

12 Je, kweli maamuzi tunayofanya kwa kutegemea dhamiri ni muhimu machoni pa Yehova? Ndiyo. Kwa nini? Kwa sababu yanaonyesha kilicho moyoni mwetu, na Yehova anapendezwa sana kujua mawazo na hisia zetu. (Soma Methali 17:3; 24:12.) Kwa sababu hiyo, tunapofanya maamuzi yanayohusu matibabu, tunahitaji kusali ili tupate mwongozo wa Yehova na kufanya utafiti kuhusu matibabu hayo. Baada ya hapo tunahitaji kutumia dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia kujifanyia uamuzi. Hatupaswi kuwauliza wengine wangefanya nini ikiwa wangekabili hali kama yetu, wala wengine hawapaswi kutushawishi tufanye uamuzi kwa kutegemea maoni yao. Kila Mkristo “ataubeba mzigo wake mwenyewe.”—Wagalatia 6:5; Waroma 14:12.

SHERIA ZA YEHOVA ZINAONYESHA KWAMBA ANATUPENDA

13. Tunajifunza nini kumhusu Yehova kutokana na sheria na kanuni zake kuhusu damu?

13 Kila kitu ambacho Yehova anatuagiza tufanye ni kwa ajili ya faida yetu na kinaonyesha kwamba anatupenda. (Zaburi 19:7-11) Hata hivyo, hatumtii tu kwa sababu amri zake zinatunufaisha. Tunamtii kwa sababu tunampenda. Upendo wetu kwa Yehova unatuchochea kuepuka kutiwa damu mishipani. (Matendo 15:20) Kufanya hivyo pia kunalinda afya yetu. Watu wengi leo wanajua hatari za kutiwa damu mishipani, na madaktari wengi wanaamini kwamba kufanya upasuaji bila kumtia mtu damu kuna faida kubwa kwa afya ya mgonjwa. Ni wazi kwamba njia za Yehova zinaonyesha hekima na upendo wake.—Soma Isaya 55:9; Yohana 14:21, 23.

14, 15. (a) Yehova aliwapa watu wake sheria zipi ili kuwalinda? (b) Unaweza kutumiaje kanuni zinazotegemea sheria hizo?

14 Sikuzote sheria za Mungu zimewafaidi watu wake. Yehova aliwapa Waisraeli wa kale sheria ili kuwalinda wasipate madhara. Kwa mfano, sheria moja ilisema kwamba mwenye nyumba alipaswa kujenga ukuta mdogo kuzunguka paa ambazo zilikuwa tambarare ili mtu asianguke kutoka juu. (Kumbukumbu la Torati 22:8) Sheria nyingine ilihusu kushughulika na wanyama. Ikiwa mtu alikuwa na ng’ombe dume mwenye vurugu, alikuwa na wajibu wa kumdhibiti ili asimshambulie au kumuua mtu yeyote. (Kutoka 21:28, 29) Mwisraeli ambaye hakutii sheria hizo, angekuwa na hatia ikiwa mtu angekufa kutokana na kutotii kwake.

15 Sheria hizo zinatuonyesha kwamba uhai ni wenye thamani sana kwa Yehova. Kujua jambo hilo kunapaswa kutuchocheaje? Tunapaswa kuonyesha kwamba tunaheshimu uhai kwa jinsi tunavyotunza nyumba na magari yetu, jinsi tunavyoendesha gari, na burudani tunazochagua. Baadhi ya watu, hasa vijana, huhisi kwamba hakuna jambo baya linaloweza kuwapata, hivyo wanahatarisha uhai wao na kupuuza uwezekano wa hatari kutokea. Lakini Yehova hataki tujiendeshe kwa njia hiyo. Anataka tuone uhai wote kuwa muhimu—uhai wetu na uhai wa watu wengine.—Mhubiri 11:9, 10.

16. Yehova ana maoni gani kuhusu kutoa mimba?

16 Uhai wa kila mwanadamu ni wenye thamani machoni pa Yehova. Hata mtoto ambaye hajazaliwa ni mwenye thamani machoni pa Yehova. Chini ya Sheria ya Musa, ikiwa mtu angemuumiza mwanamke mwenye mimba bila kukusudia na mwanamke huyo au mtoto wake afe, Yehova alimwona mtu huyo kuwa na hatia ya kuua. Hilo linamaanisha kwamba hata kama haikuwa makusudi, kwa kuwa mtu alikuwa ameuawa, uhai huo ulipaswa kufidiwa. (Soma Kutoka 21:22, 23.) Kwa maoni ya Mungu, mtoto ambaye bado hajazaliwa ni mtu aliye hai. Ukiwa na wazo hilo, unafikiri anahisije kuhusu kutoa mimba? Unafikiri Yehova anahisije anapoona mamilioni ya watoto ambao bado hawajazaliwa wakiuawa kila mwaka?

17. Ni jambo gani linaloweza kumfariji mwanamke ambaye alitoa mimba kabla ya kujifunza kumhusu Yehova?

17 Vipi ikiwa mwanamke alitoa mimba kabla ya kujifunza maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo? Anaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaweza kumsamehe kwa msingi wa dhabihu ya Yesu. (Luka 5:32; Waefeso 1:7) Mwanamke ambaye alifanya kosa kama hilo zamani hahitaji kuendelea kuhisi ana hatia ikiwa alitubu kwa unyoofu. “Yehova ni mwenye rehema na mwenye huruma . . . Kama mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali sana na sisi.”—Zaburi 103:8-14.

EPUKA CHUKI

18. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kadiri tuwezavyo kuondoa mawazo ya chuki?

18 Kuheshimu zawadi ya uhai ambayo Mungu ametupatia huanzia moyoni. Inatia ndani jinsi tunavyohisi kuwahusu wengine. Mtume Yohana aliandika hivi: “Kila mtu anayemchukia ndugu yake ni muuaji.” (1 Yohana 3:15) Bila sisi kutambua, ikiwa hatumpendi mtu fulani tunaweza kuanza kumchukia. Chuki inaweza kumfanya mtu asiwaheshimu wengine, atoe shutuma za uwongo kuwahusu, au hata atamani wafe. Yehova anajua jinsi tunavyohisi kuelekea watu wengine. (Mambo ya Walawi 19:16; Kumbukumbu la Torati 19:18-21; Mathayo 5:22) Tukitambua kwamba tuna mawazo ya chuki kuelekea mtu fulani, tunapaswa kujitahidi kuyaondoa.—Yakobo 1:14, 15; 4:1-3.

19. Maoni ya Yehova kuhusu ukatili yanapaswa kutuchochea kufanya nini?

19 Kuna njia nyingine ambayo tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini uhai. Katika Zaburi 11:5, tunajifunza kwamba Yehova “humchukia mtu yeyote anayependa ukatili.” Tukichagua burudani zenye ukatili, tunaweza kuonyesha kwamba tunapenda ukatili. Kwa nini tuingize maneno, mawazo, na picha zenye ukatili akilini mwetu? Badala yake, tunataka kujaza mawazo safi na yenye amani akilini mwetu.—Soma Wafilipi 4:8, 9.

USIWE SEHEMU YA MASHIRIKA YASIYOHESHIMU UHAI

20-22. (a) Yehova ana maoni gani kuhusu ulimwengu wa Shetani? (b) Watu wa Mungu wanaweza kuonyeshaje kwamba wao “si sehemu ya ulimwengu”?

20 Ulimwengu wa Shetani hauheshimu uhai. Yehova anauona kuwa una hatia ya damu. Kwa karne nyingi, wenye mamlaka wa kisiasa wamesababisha vifo vya watu wengi, kutia ndani watumishi wengi wa Yehova. Katika Biblia, mamlaka, au serikali hizo zinatajwa kuwa kama wanyama wakali na wenye ukatili. (Danieli 8:3, 4, 20-22; Ufunuo 13:1, 2, 7, 8) Leo, biashara ya silaha ni biashara kubwa sana. Watu wanapata faida kubwa kwa kuuza silaha hatari. Ni wazi, “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”—1 Yohana 5:19.

21 Lakini Wakristo wa kweli “si sehemu ya ulimwengu.” Watu wa Yehova hawaungi mkono upande wowote wa kisiasa na katika vita. Kama tu ambavyo hawaui mtu yeyote, hawaungi mkono shirika lolote ambalo linawaua watu. (Yohana 15:19; 17:16) Wakristo wanapoteswa, hawalipizi kisasi. Yesu alifundisha kwamba tunapaswa kuwapenda hata adui zetu.—Mathayo 5:44; Waroma 12:17-21.

22 Dini zimesababisha vifo vya mamilioni ya watu. Inapozungumza kuhusu Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo, Biblia inasema hivi: “Ndani yake ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wale wote ambao wameuawa duniani.” Sasa unaweza kuelewa sababu iliyofanya Yehova atoe amri hii: “Tokeni kwake, watu wangu.” Wote wanaomwabudu Yehova hawashirikiani na dini ya uwongo.—Ufunuo 17:6; 18:2, 4, 24.

23. ‘Kutoka’ katika Babiloni Mkubwa kunahusisha nini?

23 ‘Kutoka’ katika Babiloni Mkubwa kunatia ndani kuonyesha wazi kabisa kwamba hatushirikiani hata kidogo na dini ya uwongo. Kwa mfano, tunapaswa kuhakikisha kwamba jina letu limeondolewa kutoka katika orodha ya washiriki wa dini tuliyokuwa tukishirikiana nayo. Hata hivyo, mengi zaidi yanahitajika. Tunapaswa pia kuchukia na kuepuka mambo yote mabaya ambayo dini ya uwongo inafanya. Dini ya uwongo inaruhusu na kuendeleza maadili mapotovu, siasa, na pupa. (Soma Zaburi 97:10; Ufunuo 18:7, 9, 11-17) Matokeo ni kwamba kwa miaka mingi mamilioni ya watu wamekufa.

24, 25. Kumjua Yehova kunaweza kutupatiaje amani na dhamiri njema?

24 Kabla ya kumjua Yehova, kila mmoja wetu aliunga mkono kwa njia fulani mambo mabaya ya ulimwengu wa Shetani. Lakini sasa tumebadilika. Tumeikubali fidia na kuweka maisha yetu wakfu kwa Mungu. Tunafurahia “majira yenye kuburudisha . . . kutoka kwa Yehova mwenyewe.” Tuna amani na dhamiri njema, kwa sababu tunajua kwamba tunampendeza Mungu.—Matendo 3:19; Isaya 1:18.

25 Hata kama tulikuwa sehemu ya shirika ambalo haliheshimu uhai, Yehova anaweza kutusamehe kwa msingi wa fidia. Tunathamini sana zawadi ya uhai kutoka kwa Yehova. Tunaonyesha shukrani zetu kwa kufanya yote tuwezayo kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova, kuuacha ulimwengu wa Shetani, na kufurahia urafiki wa karibu na Mungu.—2 Wakorintho 6:1, 2.

WAAMBIE WENGINE KUHUSU UFALME

26-28. (a) Ni kazi gani ya pekee ambayo Yehova alimpa Ezekieli? (b) Yehova anatuagiza tufanye nini leo?

26 Katika taifa la kale la Israeli, Yehova alimwambia nabii Ezekieli awaonye watu kwamba Yerusalemu lilikuwa karibu kuharibiwa na awafundishe mambo waliyohitaji kufanya ili waokoke. Ikiwa Ezekieli hangewaonya watu, angekuwa na hatia kwa sababu ya vifo vya watu hao. (Ezekieli 33:7-9) Ezekieli alionyesha kwamba anatambua uhai ni wenye thamani kwa kufanya yote aliyoweza ili kutangaza ujumbe huo muhimu.

27 Yehova ametuagiza tuwaonye watu kwamba ulimwengu wa Shetani karibuni utaharibiwa na kuwasaidia kumjua Yehova ili waokoke na kuingia katika ulimwengu mpya. (Isaya 61:2; Mathayo 24:14) Tungependa kufanya yote tuwezayo ili kuwahubiria wengine ujumbe huo. Tunatumaini kwamba tutaweza kusema kama Paulo alivyosema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote, kwa maana sikukosa kuwaambia mashauri yote ya Mungu.”—Matendo 20:26, 27.

28 Bila shaka, ili tudumu katika upendo wa Mungu haitoshi tu kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu uhai na damu. Tunahitaji pia kuendelea kuwa safi machoni pake. Tutachunguza hilo katika sura inayofuata.