Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 9

“Ukimbieni Uasherati!”

“Ukimbieni Uasherati!”

“Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kuhusiana na uasherati, uchafu, hamu isiyodhibitiwa ya ngono, tamaa yenye madhara, na pupa, ambayo ni ibada ya sanamu.”—WAKOLOSAI 3:5.

1, 2. Balaamu alitumia mbinu gani kujaribu kuwadhuru watu wa Yehova?

MVUVI huenda hadi mahali ambapo kuna aina ya samaki anaotaka kuvua. Anachagua chambo atakachotumia, kisha anatupa ndoana majini. Anangoja kwa subira, na samaki anapouma ndoana, mvuvi huhakikisha ndoana imenasa vizuri, kisha anamvuta samaki.

2 Watu wanaweza kunaswa katika njia hiyohiyo. Kwa mfano, Waisraeli walikuwa karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi walipopiga kambi katika Nyanda za Moabu. Mfalme wa Moabu alimwahidi mwanamume aliyeitwa Balaamu pesa nyingi ikiwa angewalaani Waisraeli. Hatimaye, Balaamu alipata njia ya kuwafanya Waisraeli wajilaani wenyewe. Alichagua chambo kwa uangalifu. Aliwatuma wanawake vijana Wamoabu waende kwenye kambi ya Waisraeli ili kuwashawishi wanaume.—Hesabu 22:1-7; 31:15, 16; Ufunuo 2:14.

3. Waisraeli walinaswa jinsi gani na chambo cha Balaamu?

3 Je, chambo cha Balaamu kilifanya kazi? Ndiyo. Maelfu ya wanaume Waisraeli walifanya “uasherati na mabinti wa Moabu.” Pia, wakaanza kuabudu miungu ya uwongo, kutia ndani Baali wa Peori, aliyekuwa mungu wa ngono mwenye kuchukiza. Kwa sababu hiyo, Waisraeli 24,000 walikufa wakiwa kwenye mpaka wa Nchi ya Ahadi.—Hesabu 25:1-9.

4. Kwa nini maelfu ya Waisraeli walifanya uasherati?

4 Kwa nini Waisraeli wengi sana walinaswa na mbinu ya Balaamu? Walikuwa wakifikiria tu kutosheleza tamaa zao za ubinafsi, na wakasahau mambo yote ambayo Yehova alikuwa amewafanyia. Waisraeli walikuwa na sababu nyingi za kuwa washikamanifu kwa Mungu. Alikuwa amewakomboa kutoka utumwani Misri, akawalisha walipokuwa jangwani, na akawaleta salama hadi kwenye mpaka wa Nchi ya Ahadi. (Waebrania 3:12) Hata hivyo, walishawishiwa wakafanya uasherati. Mtume Paulo aliandika hivi: “Wala tusifanye uasherati, kama baadhi yao walivyofanya uasherati, na . . . wakaanguka.”—1 Wakorintho 10:8.

5, 6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyotendeka kwenye Nyanda za Moabu?

5 Ulimwengu mpya uko karibu sana. Kwa hiyo, kwa njia fulani tuko katika hali kama ya Waisraeli walipokuwa kwenye mpaka wa Nchi ya Ahadi. (1 Wakorintho 10:11) Watu katika ulimwengu huu tunamoishi wanapendezwa kupita kiasi na ngono hata kuliko Wamoabu. Mtazamo huo unaweza kuwaathiri watu wa Yehova kwa urahisi. Kwa kweli, uasherati ndicho chambo ambacho Ibilisi hutumia kuwanasa watu wengi zaidi leo.—Hesabu 25:6, 14; 2 Wakorintho 2:11; Yuda 4.

6 Jiulize, ‘Je, nichague kwa ubinafsi kutosheleza tamaa fulani kwa muda mfupi tu, au afadhali niishi milele nikifurahia maisha katika ulimwengu mpya?’ Je, si jambo lenye faida kubwa sana kufanya jitihada zote ili kutii amri hii ya Yehova: “Ukimbieni uasherati”?—1 Wakorintho 6:18.

UASHERATI NI NINI?

7, 8. Uasherati ni nini? Kwa nini ni jambo zito?

7 Watu wengi leo wana mtazamo mpotovu na wanashushia heshima sheria za Mungu kuhusu ngono. Katika Biblia, uasherati unarejelea matendo ya ngono kati ya watu ambao hawajaoana Kimaandiko. Inatia ndani matendo ya ngono kati ya watu wa jinsia moja na ngono kati ya wanadamu na wanyama. Matendo ya ngono yanahusisha pia ngono ya kinywa, ngono ya mkundu, au kugusa viungo vya uzazi vya mtu mwingine kwa njia inayosisimua hamu ya ngono.—Soma Maelezo ya Ziada 23.

8 Biblia inaonyesha wazi kwamba mtu akiendelea kufanya uasherati, hawezi kuendelea kuwa sehemu ya kutaniko. (1 Wakorintho 6:9; Ufunuo 22:15) Isitoshe, mtu aliye na maadili mapotovu huacha kujiheshimu na wengine wanaacha kumwamini. Sikuzote maadili mapotovu hutokeza matatizo. Kwa kawaida, maadili mapotovu humfanya mtu awe na dhamiri chafu na mara nyingi yanatokeza mimba zisizotakiwa, matatizo ya ndoa, magonjwa, au hata kifo. (Soma Wagalatia 6:7, 8.) Ikiwa mtu angetua na kufikiria madhara ambayo hutokezwa na maadili mapotovu, huenda hangetaka kujihusisha nayo. Lakini mara nyingi mtu hufikiria tu kutosheleza tamaa zake mwenyewe anapochukua hatua ya kwanza kuelekea uasherati. Mara nyingi, hatua hiyo ya kwanza huhusisha ponografia.

PONOGRAFIA—HATUA YA KWANZA

9. Kwa nini ponografia ni hatari?

9 Ponografia imekusudiwa kuchochea tamaa zetu za ngono. Leo, ponografia inapatikana kila mahali—katika magazeti, vitabu, muziki, na vipindi vya televisheni, kutia ndani kwenye Intaneti. Watu wengi huhisi kwamba ponografia haina madhara, lakini kwa kweli ni hatari sana. Inaweza kumfanya mtu apende sana kufanya ngono na kusitawisha tamaa zilizopotoka. Mara tu mtu anapojihusisha na ponografia, anaanza kufuata njia inayoweza kumwongoza kwenye tabia ya kupiga punyeto, matatizo ya ndoa, na hata talaka.—Waroma 1:24-27; Waefeso 4:19; soma Maelezo ya Ziada 24.

Ni jambo la hekima kuwa mwangalifu unapotumia Intaneti

10. Kanuni iliyo kwenye Yakobo 1:14, 15 inawezaje kutusaidia kuepuka maadili mapotovu?

10 Ni muhimu tuelewe jinsi uasherati unavyoweza kuonekana kuwa wenye kutuvutia. Ona onyo hili linalopatikana kwenye Yakobo 1:14, 15: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, baada ya kufanywa, huleta kifo.” Kwa hiyo, mawazo mabaya yanapoingia akilini mwako, yaondoe mara moja. Ukiona bila kukusudia picha zenye kuamsha hamu ya ngono, angalia kando! Zima kompyuta, au ubadili stesheni ya televisheni. Usiruhusu tamaa mbaya maishani mwako. Usipofanya hivyo, tamaa zako mbaya zinaweza kuwa zenye nguvu sana hivi kwamba itakuwa vigumu sana kuzidhibiti.—Soma Mathayo 5:29, 30.

11. Yehova anaweza kutusaidiaje tunapokuwa na mawazo yasiyofaa?

11 Yehova anatujua vizuri zaidi kuliko tunavyojijua. Kwa hiyo, anajua tumepungukiwa kwa kadiri gani. Lakini anajua pia kwamba tunaweza kushinda tamaa mbaya. Yehova anatuambia hivi: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kuhusiana na uasherati, uchafu, hamu isiyodhibitiwa ya ngono, tamaa yenye madhara, na pupa, ambayo ni ibada ya sanamu.” (Wakolosai 3:5) Hata ingawa si rahisi kufanya hivyo, Yehova anatuonyesha subira, naye atatusaidia. (Zaburi 68:19) Ndugu mmoja kijana alinaswa na zoea la kutazama ponografia na kupiga punyeto. Rafiki zake shuleni walihisi kwamba hayo ni mambo ya kawaida ya ukuzi, lakini yeye alisema hivi: “Kufanya hivyo kulichafua dhamiri yangu, na nikaanza kuishi maisha mapotovu.” Alitambua kwamba alihitaji kudhibiti tamaa zake, na kwa msaada wa Yehova, akafaulu kuacha zoea hilo. Ikiwa una mawazo mapotovu, mwombe Yehova akupe “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili uendelee kuwa na mawazo safi.—2 Wakorintho 4:7; 1 Wakorintho 9:27.

12. Kwa nini tunahitaji ‘kulinda moyo wetu’?

12 Sulemani aliandika hivi: “Ulinde moyo wako kuliko vitu vyote unavyolinda, kwa maana humo ndimo zinamotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) “Moyo” wetu unawakilisha yule mtu tuliye kwa ndani, utu ambao Yehova anaona. Mambo tunayotazama yanaweza kutuathiri kwa njia kubwa. Mwanamume mwaminifu Ayubu alisema hivi: “Nimefanya agano na macho yangu. Basi ninawezaje kumtazama bikira kwa njia isiyofaa?” (Ayubu 31:1) Kama Ayubu, tunahitaji kudhibiti mambo tunayotazama na kufikiria. Na kama mtunga-zaburi, tunasali hivi: “Yageuzie mbali macho yangu yasitazame mambo yasiyofaa.”—Zaburi 119:37.

DINA ALIFANYA UAMUZI USIO NA HEKIMA

13. Dina alichagua marafiki wa aina gani?

13 Rafiki zetu wanaweza kutuathiri kwa njia kubwa, iwe ni kwa njia nzuri au mbaya. Ukichagua marafiki wanaofuata viwango vya Mungu, wanaweza kukusaidia kufanya hivyo pia. (Methali 13:20; soma 1 Wakorintho 15:33.) Tunapofikiria kilichompata Dina, tunaweza kuona jinsi marafiki tunaochagua wanavyotuathiri. Alikuwa mmoja kati ya binti za Yakobo, kwa hiyo alilelewa katika familia iliyomwabudu Yehova. Dina hakuwa mtu mwenye maadili mapotovu, lakini akaanzisha urafiki wa karibu na wasichana Wakanaani ambao hawakumwabudu Yehova. Maoni ya Wakanaani kuhusu ngono yalikuwa tofauti sana na ya watu wa Mungu, hata walijulikana sana kwa maadili yao mapotovu. (Mambo ya Walawi 18:6-25) Dina alipokuwa na rafiki zake, alikutana na kijana Mkanaani anayeitwa Shekemu, ambaye alivutiwa na Dina. Shekemu alikuwa kijana ‘aliyeheshimiwa kuliko watu wote’ wa familia yao. Lakini hakumpenda Yehova.—Mwanzo 34:18, 19.

14. Ni nini kilichompata Dina?

14 Shekemu alifanya jambo ambalo lilionekana kuwa la kawaida kwake na lililompendeza. Kwa kuwa alivutiwa na Dina, “alimchukua na kumbaka.” (Soma Mwanzo 34:1-4.) Jambo hilo lilianzisha mfululizo wa matukio ambayo yalitokeza matatizo kwa Dina na familia yote ya Yakobo.—Mwanzo 34:7, 25-31; Wagalatia 6:7, 8.

15, 16. Tunaweza kufanya nini ili tuwe na hekima?

15 Hatungependa kufanya makosa kama yale ambayo Dina alifanya ili tujifunze kwamba viwango vya maadili vya Yehova ndivyo vinavyotufaa. “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wapumbavu ataumia.” (Methali 13:20) Lifanye liwe lengo lako kuelewa “njia yote ya lililo jema,” nawe utaepuka matatizo na maumivu yasiyo ya lazima.—Methali 2:6-9; Zaburi 1:1-3.

16 Tunaweza kuwa na hekima kwa kujifunza Neno la Mungu, kusali kabla ya kufanya maamuzi, na kufuata mashauri mazuri yanayotoka kwa mtumwa mwaminifu na mwenye busara. (Mathayo 24:45; Yakobo 1:5) Bila shaka, unajua kwamba sisi sote ni dhaifu na si wakamilifu. (Yeremia 17:9) Lakini ungetendaje ikiwa mtu angekuonya kwamba unakabili hatari ya kujihusisha katika uasherati? Je, ungekasirika, au ungekubali msaada huo kwa unyenyekevu?—2 Wafalme 22:18, 19.

17. Toa mfano wa jinsi shauri kutoka kwa Mkristo mwenzetu linavyoweza kutusaidia.

17 Kwa mfano, wazia hali hii. Dada akiwa kazini, mwanamume fulani anaanza kumwonyesha upendezi na kumwalika waende matembezi pamoja. Mwanamume huyo si mtumishi wa Yehova, lakini anaonekana kuwa mtu mwema na mwenye fadhili. Dada mwingine anawaona pamoja na baadaye anajaribu kumwonya kuhusu jambo hilo. Yule dada wa kwanza atatendaje? Je, atajitetea, au ataona hekima ya kutii onyo hilo? Huenda dada huyo akawa anampenda Yehova na anataka kufanya lililo sawa. Lakini akiendelea kwenda matembezi na mwanamume huyo, je, ‘anaukimbia uasherati’ au ‘anautumaini moyo wake mwenyewe’?—Methali 22:3; 28:26; Mathayo 6:13; 26:41.

JIFUNZE KUTOKANA NA MFANO WA YOSEFU

18, 19. Eleza jinsi Yosefu alivyoukimbia uasherati.

18 Alipokuwa kijana, Yosefu alikuwa mtumwa kule Misri. Siku baada ya siku, mke wa bwana wake alimwomba wafanye ngono, lakini Yosefu alijua kwamba lingekuwa kosa kufanya hivyo. Yosefu alimpenda Yehova na alitaka kumfurahisha. Kwa hiyo, kila mara mwanamke huyo alipojaribu kumshawishi, Yosefu alikataa. Kwa kuwa alikuwa mtumwa, hangeweza kuondoka kwa bwana wake. Siku moja, mke wa bwana wake alipojaribu kumlazimisha wafanye ngono, ‘alikimbilia nje.’—Soma Mwanzo 39:7-12.

19 Hali ingekuwa tofauti sana ikiwa Yosefu angejiruhusu kufikiria mambo mapotovu kiadili au ikiwa angekuwa akiota ndoto za mchana kumhusu mwanamke huyo. Yosefu aliona uhusiano wake na Yehova kuwa muhimu zaidi kuliko kitu kingine chochote. Alimwambia mwanamke huyo hivi: “Bwana wangu . . . hajanikataza kitu chochote isipokuwa wewe, kwa sababu wewe ni mke wake. Basi ninawezaje kufanya uovu huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?”—Mwanzo 39:8, 9.

20. Tunajuaje kwamba Yehova alifurahishwa na Yosefu?

20 Ingawa Yosefu alikuwa mbali na familia yao, sikuzote alikuwa mshikamanifu kwa Mungu, na Yehova alimbariki. (Mwanzo 41:39-49) Yehova alifurahishwa na ushikamanifu wa Yosefu. (Methali 27:11) Inaweza kuwa vigumu kuepuka maadili mapotovu. Lakini kumbuka maneno haya: “Enyi mnaompenda Yehova, chukieni maovu. Anaulinda uhai wa washikamanifu wake; huwaokoa kutoka katika mkono wa mwovu.”—Zaburi 97:10.

21. Ndugu mmoja kijana alimwigaje Yosefu?

21 Kila siku, watu wa Yehova huonyesha kwa ujasiri kwamba ‘wanachukia maovu’ na kwamba ‘wanapenda mema.’ (Amosi 5:15) Hata uwe na umri gani, unaweza kuwa mwaminifu kwa Yehova. Imani ya ndugu mmoja kijana ilijaribiwa alipokuwa shuleni. Msichana mmoja alimwambia kwamba angefanya ngono naye ikiwa kijana huyo angemsaidia kufaulu katika mtihani wa hesabu. Ndugu huyo alifanya nini? Alitenda kama Yosefu. Anasema hivi: “Nilikataa papo hapo. Kuendelea kuwa mtimilifu kumeniwezesha kuheshimiwa na kujiheshimu.” Ingawa mtu anaweza “kufurahia dhambi kwa muda,” mara nyingi raha hizo za muda mfupi huleta maumivu mengi ya kimwili na moyoni. (Waebrania 11:25) Sikuzote kumtii Yehova hutokeza furaha ya kudumu.—Methali 10:22.

KUBALI MSAADA WA YEHOVA

22, 23. Yehova anaweza kutusaidiaje hata tunapotenda dhambi nzito?

22 Shetani atajaribu kutumia uasherati kutunasa, na hilo linaweza kutokeza changamoto. Huenda sisi sote tukapatwa na mawazo mabaya mara kwa mara. (Waroma 7:21-25) Yehova anaelewa jambo hilo na anakumbuka kwamba “sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Kwa hiyo, namna gani Mkristo akitenda dhambi nzito ya uasherati? Je, hilo linamaanisha kwamba hana tumaini? Hapana. Ikiwa mtu huyo anatubu kikweli, Yehova atamsaidia. Mungu yuko “tayari kusamehe.”—Zaburi 86:5; Yakobo 5:16; soma Methali 28:13.

23 Pia, Yehova ametupatia “wanaume kuwa zawadi,” yaani, wazee wenye upendo na wanaotujali. (Waefeso 4:8, 12; Yakobo 5:14, 15) Ametupatia wazee ili watusaidie kurekebisha uhusiano wetu pamoja naye.—Methali 15:32.

TUMIA “BUSARA”

24, 25. “Busara” inaweza kutusaidiaje kuepuka uasherati?

24 Ili tufanye maamuzi mazuri, tunahitaji kuelewa jinsi sheria za Yehova zinavyotunufaisha. Hatutaki kuwa kama kijana anayefafanuliwa kwenye Methali 7:6-23. Hakuwa na “busara,” kwa hiyo alinaswa na chambo cha uasherati. Kuwa na busara hakumaanishi tu kuwa mwerevu. Tunapokuwa na busara tunajaribu kuelewa jinsi Mungu anavyofikiri na kutumia mawazo ya Mungu maishani mwetu. Kumbuka maneno haya yenye hekima: “Yeyote anayepata busara anajipenda mwenyewe. Yeyote anayethamini utambuzi kama hazina atapata mafanikio.”—Methali 19:8.

25 Je, unasadiki kabisa kwamba viwango vya Mungu vinafaa? Je, kweli unaamini kwamba kuvifuata kutakuletea furaha? (Zaburi 19:7-10; Isaya 48:17, 18) Ikiwa bado huna uhakika, kumbuka mambo yote mazuri ambayo Yehova amekufanyia. ‘Onja uone kwamba Yehova ni mwema.’ (Zaburi 34:8) Utaona kwamba kadiri unavyoendelea kufanya hivyo, ndivyo utakavyompenda Mungu zaidi. Penda mambo anayopenda, na uchukie anayochukia. Jaza akili yako mawazo yanayofaa—mambo yaliyo ya kweli, ya uadilifu, yaliyo safi kiadili, yanayopendeka, na mema kiadili. (Wafilipi 4:8, 9) Tunaweza kuwa kama Yosefu ambaye alifaidika kutokana na hekima ya Yehova.—Isaya 64:8.

26. Tutazungumzia nini katika sura zinazofuata?

26 Iwe wewe ni mseja au umefunga ndoa, Yehova anataka ufurahie maisha na uwe na furaha. Sura mbili zinazofuata zina habari zitakazotusaidia tufanikiwe katika ndoa zetu.