Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 1

Upendo wa Mungu Unadumu Milele

Upendo wa Mungu Unadumu Milele

“Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”​—1 YOHANA 5:3.

1, 2. Kwa nini unampenda Yehova Mungu?

JE, UNAMPENDA Mungu? Huenda ikawa unampenda sana hivi kwamba umejiweka wakfu kwake. Huenda ukahisi kwamba yeye ndiye Rafiki yako wa karibu zaidi. Yehova alikupenda hata kabla wewe hujampenda. Tunasoma hivi katika Biblia: “Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.”—1 Yohana 4:19.

2 Fikiria njia zote ambazo Yehova ameonyesha kwamba anatupenda. Ametupa dunia maridadi iwe makao yetu na akatupa kila kitu tunachohitaji ili kufurahia maisha. (Mathayo 5:43-48; Ufunuo 4:11) Anataka tuwe na uhusiano mzuri pamoja naye, na amefanya iwezekane kwetu kujifunza kumhusu. Tunaposoma Biblia, tunamsikiliza Yehova. Na tunaposali, yeye anatusikiliza. (Zaburi 65:2) Anatuongoza na kutuimarisha kwa roho yake takatifu iliyo na nguvu. (Luka 11:13) Hata alimtuma mwana wake wa pekee duniani ili atuweke huru kutokana na dhambi na kifo.—Soma Yohana 3:16; Waroma 5:8.

3. Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuwa na uhusiano mzuri na Yehova?

3 Fikiria kidogo kuhusu rafiki yako wa karibu, ambaye hajawahi kukuacha hata ulipokabili hali mbaya. Jitihada zinahitajika ili kuendeleza urafiki wa karibu kama huo. Jitihada pia zinahitajika ili kuendeleza urafiki wetu na Yehova. Yeye ndiye Rafiki wa karibu zaidi tunayeweza kumpata. Urafiki wetu pamoja na Yehova unaweza kudumu milele. Kwa hiyo, Biblia inatueleza hivi: “Mwendelee kujitunza katika upendo wa Mungu.” (Yuda 21) Tunawezaje kufanya hivyo? Biblia inajibu hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 Yohana 5:3.

“KUMPENDA MUNGU HUMAANISHA HIVI”

4, 5. (a) “Kumpenda Mungu” kunamaanisha nini? (b) Upendo wako kwa Yehova uliongezekaje?

4 Biblia inamaanisha nini inaposema “kumpenda Mungu”? Inaeleza jinsi kila mmoja wetu anavyohisi kumwelekea Mungu. Je, unakumbuka ulipoanza kumpenda Yehova?

Unapojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa unaonyesha kwamba unampenda na unataka kumtii milele

5 Kumbuka ulivyohisi ulipojifunza kwa mara ya kwanza kwamba Yehova anataka uishi milele katika ulimwengu wake mpya. Ulijifunza kuhusu mambo yote ambayo amefanya ili hilo liwezekane na pia ukajifunza kuhusu zawadi yenye thamani sana ambayo Yehova alitupa alipomtuma Mwana wake duniani. (Mathayo 20:28; Yohana 8:29; Waroma 5:12, 18) Ulipojifunza jinsi Yehova anavyokupenda sana, ulichochewa sana, nawe ukaanza kumpenda.—Soma 1 Yohana 4:9, 10.

6. Kumpenda mtu kunahusisha nini? Upendo wako kwa Mungu umekuchochea kufanya nini?

6 Lakini kuwa na hisia hizo za kumpenda Yehova ni mwanzo tu. Kwa mfano, ikiwa unampenda mtu humwambii tu “ninakupenda.” Upendo unakuchochea utake kufanya mambo yatakayomfurahisha mtu huyo. Katika njia hiyohiyo, upendo wako kwa Yehova ulikuchochea utake kuishi kwa njia itakayompendeza. Upendo huo ulipoongezeka, huenda ulijiweka wakfu kwake na ukabatizwa. Kwa kufanya hivyo, uliahidi kumtumikia Yehova milele. (Soma Waroma 14:7, 8.) Unaweza kufanya nini ili kutimiza ahadi yako?

“TUZISHIKE AMRI ZAKE”

7. Ikiwa tunampenda Yehova, tutafanya nini? Taja baadhi ya amri zake.

7 Kwa sababu tunampenda Yehova, ‘tunashika amri zake.’ Tunafanyaje hivyo? Kwa kumtii. Katika Biblia tunajifunza jinsi Yehova anavyotaka tuishi. Kwa mfano, anatuambia kwamba ni kosa kulewa, kuiba, kusema uwongo, kufanya ngono na mtu ambaye si mwenzi wetu wa ndoa, au kumwabudu mtu au kitu kingine chochote isipokuwa Yehova.—1 Wakorintho 5:11; 6:18; 10:14; Waefeso 4:28; Wakolosai 3:9.

8, 9. Tutajuaje kile ambacho Yehova anataka tufanye ikiwa hakuna sheria hususa katika Biblia? Toa mfano.

8 Lakini ili kumpendeza Yehova, tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kutii amri zake. Yehova hajaweka orodha ndefu ya sheria kuhusu kila hali maishani. Kwa hiyo, huenda kukawa na pindi ambazo hakuna sheria hususa katika Biblia inayotuambia tunachopaswa kufanya. Tutafanyaje maamuzi mazuri? (Waefeso 5:17) Katika Biblia kuna kanuni, ambazo ni kweli za msingi zinazotufundisha jinsi Yehova anavyoona mambo. Tunaposoma Biblia, tunajifunza jinsi Yehova alivyo. Tunajifunza jinsi anavyofikiri, kutia ndani mambo anayopenda na yale anayochukia.—Soma Zaburi 97:10; Methali 6:16-19; soma Maelezo ya Ziada 1.

9 Kwa mfano, tunaamuaje kile ambacho tutatazama kwenye televisheni au kwenye Intaneti? Yehova hajatuambia kihususa kile ambacho tunapaswa kufanya. Lakini kanuni anazotupa zinatusaidia kufanya maamuzi mazuri. Burudani nyingi leo zimejaa ukatili na ngono. Katika Biblia, Yehova anatuambia kwamba yeye “humchukia mtu yeyote anayependa ukatili” na kwamba “atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Zaburi 11:5; Waebrania 13:4) Kanuni hizo zinaweza kutusaidiaje kufanya maamuzi mazuri? Tunapojua tu kwamba Yehova anachukia jambo fulani au analiona kuwa linakiuka maadili, tunapaswa kuliepuka.

10, 11. Kwa nini tunamtii Yehova?

10 Kwa nini tunamtii Yehova? Si ili tu kuepuka kuadhibiwa au kuepuka madhara yanayotokana na kufanya uamuzi mbaya. (Wagalatia 6:7) Badala yake, tunamtii Yehova kwa sababu tunampenda. Kama tu watoto wanavyotaka kumfurahisha baba yao, tunataka pia kumfurahisha Baba yetu wa mbinguni. Hakuna jambo bora kuliko kujua kwamba Yehova anapendezwa nasi!—Zaburi 5:12; Methali 12:2; soma Maelezo ya Ziada 2.

11 Hatumtii Yehova wakati tu ni rahisi kufanya hivyo au kwa sababu hali zinatulazimisha tufanye hivyo. Wala hatuchagui ni sheria au viwango gani tutakavyofuata na ni gani hatutafuata. (Kumbukumbu la Torati 12:32) Badala yake, tunamtii kikamili, kama mtunga-zaburi aliyesema hivi: “Ninazipenda sana amri zako, naam, ninazipenda.” (Zaburi 119:47; Waroma 6:17) Tunataka kuwa kama Noa, ambaye alionyesha kwamba anampenda Yehova kwa kufanya mambo yote ambayo Yehova alimwamuru afanye. Biblia inasema kwamba “hivyo ndivyo [Noa] alivyofanya.” (Mwanzo 6:22) Je, ungependa Yehova aseme hivyo kukuhusu?

12. Tunaweza kufanya nini ili kumfurahisha Yehova?

12 Yehova anahisije tunapomtii? Tunafanya ‘moyo wake ushangilie.’ (Methali 11:20; 27:11) Hebu fikiria jambo hilo! Tunamfanya Muumba wa ulimwengu wote afurahi tunapomtii. Lakini yeye hatulazimishi tumtii. Badala yake, ametupa uhuru wa kuchagua. Hilo linamaanisha kwamba tuna uhuru wa kuchagua kufanya mema au mabaya. Yehova anataka upendo wetu kwake utuchochee kufanya maamuzi mazuri ili tuishi maisha bora zaidi.—Kumbukumbu la Torati 30:15, 16, 19, 20; soma Maelezo ya Ziada 3.

“AMRI ZAKE SI MZIGO MZITO”

13, 14. Tunajuaje kwamba si vigumu sana kutii amri za Mungu? Toa mfano.

13 Namna gani tukifikiri kwamba ni vigumu kutii amri za Yehova au kwamba zitatunyima uhuru? Biblia inasema hivi waziwazi: “Amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Katika maandiko mengine, neno “mzigo” linatumiwa kufafanua sheria kali au watu wanaojaribu kuwadhibiti na kuwaumiza wengine. (Mathayo 23:4; Matendo 20:29, 30) Tafsiri ya Biblia ya Neno—Agano Jipya, inasema: “Amri zake hazitulemei.” Amri za Yehova si “nzito,” yaani, si vigumu sana kwetu kuzitii. Hakuna wakati ambapo anadai tufanye jambo linalopita uwezo wetu.

14 Kwa mfano, tuseme kwamba unamsaidia rafiki yako kuhama. Amepakia kila kitu katika masanduku. Masanduku fulani ni mepesi na rahisi kubeba, lakini mengine ni mazito sana hivi kwamba lazima yabebwe na watu wawili. Je, rafiki yako anaweza kukuomba ubebe sanduku zito sana peke yako? Hawezi kufanya hivyo! Kwa nini? Kwa sababu hataki uumie. Kama rafiki huyo, Yehova hatazamii tufanye kitu ambacho ni vigumu sana kwetu kufanya. (Kumbukumbu la Torati 30:11-14) Yehova anatuelewa vizuri. “Anajua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”—Zaburi 103:14.

15. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba amri za Yehova zimekusudiwa kutufaidi?

15 Musa aliliambia taifa la Israeli kwamba amri za Yehova zingewasaidia ‘wafanikiwe daima’ na kwamba ikiwa wangeendelea kuzitii ‘wangeendelea kuishi.’ (Kumbukumbu la Torati 5:28-33; 6:24) Ndivyo ilivyo leo. Chochote ambacho Yehova anatuagiza tufanye kitaboresha maisha yetu. (Soma Isaya 48:17.) Sikuzote Baba yetu, Yehova, anajua kinachotufaa zaidi. (Waroma 11:33) Biblia inatuambia: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Hilo linamaanisha kwamba kila kitu ambacho Yehova anasema na kufanya kinachochewa na upendo.

16. Tunajuaje kwamba tunaweza kutii hata ingawa sisi si wakamilifu na tunaishi katika ulimwengu mwovu?

16 Si rahisi kumtii Mungu nyakati zote. Tunaishi katika ulimwengu mwovu unaotawaliwa na Ibilisi. Anajaribu kuwachochea watu watende mabaya. (1 Yohana 5:19) Pia, kwa kuwa sisi si wakamilifu, lazima tupambane na mawazo na hisia zetu ambazo zinaweza kutufanya tusimtii Mungu. (Waroma 7:21-25) Upendo wetu kwa Yehova unatupa nguvu za kufanya kilicho sawa. Anaona jitihada zetu za kumtii, naye anatusaidia kwa kutupa roho yake takatifu yenye nguvu. (1 Samweli 15:22, 23; Matendo 5:32) Roho takatifu inatusaidia kusitawisha sifa ambazo zinafanya iwe rahisi kwetu kumtii.—Wagalatia 5:22, 23.

17, 18. (a) Tutajifunza nini katika kitabu hiki? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?

17 Katika kitabu hiki, tutajifunza jinsi ya kuishi kwa njia inayompendeza Yehova. Tutajifunza jinsi ya kutumia kanuni na viwango vyake vya maadili maishani mwetu. Kumbuka kwamba Yehova hatulazimishi kamwe tumtii. Tunapochagua kumtii, maisha yetu yanaboreshwa, nasi tutakuwa na wakati ujao mzuri. Jambo muhimu zaidi ni kwamba kumtii Mungu kutaonyesha kina cha upendo wetu kwake.—Soma Maelezo ya Ziada 4.

18 Ili kutusaidia kutofautisha kati ya mema na mabaya, Yehova ametupa sisi sote dhamiri. Tukiizoeza dhamiri yetu vizuri, inaweza kutusaidia ‘kushika amri zake.’ Kwa hiyo, dhamiri ni nini, na tunaweza kuizoeza jinsi gani? Acheni tuone.