Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 14

Uwe Mnyoofu Katika Mambo Yote

Uwe Mnyoofu Katika Mambo Yote

“Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—WAEBRANIA 13:18.

1, 2. Yehova anahisije tunapojitahidi kuwa wanyoofu?

MVULANA akiwa njiani kutoka shuleni anaokota mfuko ulio na pesa. Atafanya nini? Anaweza kujiwekea pesa hizo. Lakini badala ya kufanya hivyo anamrudishia mwenyewe mfuko wake. Mama ya mvulana huyo anaposikia kuhusu hilo, anafurahi sana.

2 Wazazi wengi wanafurahi watoto wao wanapokuwa wanyoofu. Baba yetu wa mbinguni, Yehova, ndiye “Mungu wa ukweli,” naye anafurahi tunapokuwa wanyoofu. (Zaburi 31:5) Tunataka kumfurahisha kwa “kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Tuzungumzie maeneo manne ambayo huenda ikawa vigumu kwetu kuwa wanyoofu. Kisha tutachunguza faida tunazopata kwa kuwa wanyoofu.

KUJICHUNGUZA KWA UNYOOFU

3-5. (a) Tunaweza kujidanganyaje? (b) Ni nini kitakachotusaidia kujichunguza kwa unyoofu?

3 Ili tuweze kushughulika na wengine kwa unyoofu, lazima kwanza tujichunguze kwa unyoofu. Si rahisi kufanya hivyo. Katika karne ya kwanza, akina ndugu katika kutaniko la Laodikia walijidanganya kwamba walikuwa wakimpendeza Mungu lakini kwa kweli hawakuwa wakifanya hivyo. (Ufunuo 3:17) Sisi pia tunaweza kujidanganya kwamba tunampendeza Mungu.

4 Mwanafunzi Yakobo alieleza hivi: “Ikiwa mtu yeyote anafikiri yeye ni mwabudu wa Mungu lakini haudhibiti kabisa ulimi wake, anaudanganya moyo wake, na ibada yake ni ubatili.” (Yakobo 1:26) Tunaweza kuwa tukijidanganya ikiwa tunafikiri kwamba maadamu tunafanya mambo fulani mazuri, Mungu hajali sana ikiwa sisi ni wakaidi, tunawakejeli wengine, au tunasema uwongo. Ni nini kinachoweza kutusaidia tusijidanganye?

5 Tunapotazama kioo, tunaweza kuona jinsi tulivyo kwa nje. Tunaposoma Biblia, tunaona jinsi tulivyo kwa ndani. Hivyo, Biblia inaweza kutusaidia tujue mambo tunayofanya vizuri na udhaifu wetu pia. Inatuonyesha marekebisho tunayopaswa kufanya katika kufikiri, kutenda, na kusema. (Soma Yakobo 1:23-25.) Lakini tukijiambia kwamba hatuna kasoro yoyote, hatuwezi kufanya maendeleo yoyote. Kwa hiyo, tunapaswa kutumia Biblia kujichunguza kwa unyoofu. (Maombolezo 3:40; Hagai 1:5) Pia, sala inatusaidia tujichunguze jinsi tulivyo kwa kweli. Tunaweza kumwomba Yehova katika sala atuchunguze na kutusaidia kuona kasoro zetu ili tuzirekebishe. (Zaburi 139:23, 24) Tunakumbuka kwamba “Yehova humchukia mtu mwenye hila, lakini ana urafiki wa karibu na watu wanyoofu.”—Methali 3:32.

UNYOOFU KATIKA FAMILIA

6. Kwa nini mume na mke wanapaswa kuwa wanyoofu?

6 Unyoofu ni jambo muhimu sana katika familia. Mume na mke wanapoelezana mambo waziwazi, wanajihisi wakiwa salama na wanaweza kuaminiana kabisa. Kuna njia nyingi ambazo mtu anaweza kuonyesha kwamba yeye si mnyoofu katika ndoa. Baadhi ya njia hizo ni kwa kumchezea kimapenzi mtu mwingine, au kutazama ponografia, au kuwa na uhusiano wa siri wa kimahaba na mtu mwingine. Ona kile ambacho mtunga-zaburi alisema: “Sishirikiani na watu wadanganyifu, nami huwaepuka wale wanaoficha jinsi walivyo.” (Zaburi 26:4) Ikiwa wewe si mnyoofu kwa mwenzi wako hata katika mawazo yako, utaidhuru ndoa yako.

Tenda upesi kuepuka chochote kitakachodhoofisha ndoa yako

7, 8. Unaweza kuitumiaje Biblia kuwafundisha watoto umuhimu wa kuwa wanyoofu?

7 Vilevile watoto wanahitaji kujifunza kwamba ni muhimu kuwa wanyoofu. Wazazi wanaweza kutumia Biblia kuwafundisha jambo hilo. Biblia ina mifano mibaya ya watu ambao hawakuwa wanyoofu: Akani, aliyekuwa mwizi; Gehazi, ambaye alisema uwongo ili apate pesa; na Yuda, ambaye alikuwa akiiba pesa na baadaye akamsaliti Yesu kwa sarafu 30 za fedha.—Yoshua 6:17-19; 7:11-25; 2 Wafalme 5:14-16, 20-27; Mathayo 26:14, 15; Yohana 12:6.

8 Biblia pia ina mifano mingi mizuri ya watu ambao walikuwa wanyoofu: Yakobo, ambaye aliwasihi watoto wake warudishe pesa walizokuwa wamepata; Yeftha na binti yake, ambao walitimiza ahadi yao kwa Mungu; na Yesu, ambaye alikuwa mnyoofu hata hali zilipokuwa ngumu. (Mwanzo 43:12; Waamuzi 11:30-40; Yohana 18:3-11) Mifano hiyo inaweza kuwasaidia watoto waelewe umuhimu wa kuwa wanyoofu.

9. Watoto watafaidikaje wazazi wao wanapokuwa wanyoofu?

9 Wazazi wanaweza kujifunza kanuni hii muhimu ya Biblia: “Hata hivyo, je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe unayehubiri, ‘Usiibe,’ je, wewe huiba?” (Waroma 2:21) Watoto wanajua wakati ambapo wazazi wao wanasema jambo fulani lakini wanatenda tofauti na wanavyosema. Tukiwaambia watoto wetu wawe wanyoofu lakini sisi si wanyoofu, watachanganyikiwa. Watoto wakitambua kwamba wazazi wao wanasema uwongo hata kuhusu mambo madogo, huenda wakafanya vivyo hivyo. (Soma Luka 16:10.) Kwa upande mwingine, watoto wakiona kwamba wazazi wao ni wanyoofu, huenda hilo likawasaidia baadaye kuwa wazazi wanaotegemeka watakapopata watoto wao wenyewe.—Methali 22:6; Waefeso 6:4.

UNYOOFU KUTANIKONI

10. Tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba sisi ni wanyoofu tunapozungumza na Wakristo wenzetu?

10 Tunapaswa pia kuwa wanyoofu tunaposhughulika na Wakristo wenzetu. Ni rahisi kwa mazungumzo kugeuka na kuwa porojo, au hata uchongezi. Tukirudia kusema jambo tulilosikia bila kuchunguza ikiwa ni la kweli, huenda tukawa tukieneza uwongo. Ni afadhali ‘kudhibiti midomo yetu.’ (Methali 10:19) Kuwa wanyoofu hakumaanishi kwamba tunapaswa kusema kila kitu tunachofikiria, tunachojua, au tulichosikia. Hata ikiwa jambo tunalosema ni kweli, huenda halituhusu, au huenda hakuna haja ya kulisema na linaweza kumuumiza mtu mwingine. (1 Wathesalonike 4:11) Watu fulani hutetea ukaidi wao kwa kudai kwamba wao ni wanyoofu. Lakini tukiwa watu wa Yehova, sikuzote tunataka maneno yetu yawe yenye neema na fadhili.—Soma Wakolosai 4:6.

11, 12. (a) Mtu ambaye ametenda dhambi anaweza kufanyaje mambo yawe mabaya zaidi kwa kutokuwa mnyoofu? (b) Tunaweza kujiuliza maswali gani? (c) Ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba sisi ni wanyoofu kwa tengenezo la Yehova?

11 Yehova amewapa wazee jukumu la kusaidia kutaniko. Ni rahisi kwa wazee kutusaidia tunapokuwa wanyoofu. Kwa nini? Ukienda kumwona daktari akusaidie kwa sababu wewe ni mgonjwa, je, utaficha baadhi ya dalili za ugonjwa wako? Ukificha atakusaidiaje? Vivyo hivyo, tunapofanya kosa, hatupaswi kusema uwongo. Badala yake, tunapaswa kuwafikia wazee na kuwaeleza kosa hilo kwa unyoofu. (Zaburi 12:2; Matendo 5:1-11) Wazia hali nyingine tofauti: Namna gani ukigundua kwamba rafiki yako amefanya kosa zito? (Mambo ya Walawi 5:1) Je, utajiambia kwamba unapaswa kuficha jambo hilo kwa kuwa wewe ni rafiki yake? Au utakumbuka kwamba wazee wako tayari kumpa msaada anaohitaji ili arekebishe na kuimarisha uhusiano wake na Yehova?—Waebrania 13:17; Yakobo 5:14, 15.

12 Pia tunapaswa kuwa wanyoofu kwa tengenezo la Yehova tunapojaza ripoti, kama vile tunaporipoti utendaji wetu katika huduma. Na tunakuwa wanyoofu tunapojaza fomu ya kuwa mapainia au tunapoomba kushiriki katika aina fulani ya utumishi.—Soma Methali 6:16-19.

13. Tunapofanya biashara na Mkristo mwenzetu, tunawezaje kuhakikisha kwamba tunadumisha unyoofu?

13 Ndugu na dada Wakristo hawapaswi kuchanganya biashara na ibada. Kwa mfano, hatufanyi biashara tunapokuwa kwenye Jumba la Ufalme au katika huduma. Na hatuwatendei ndugu na dada zetu kwa njia isiyo ya haki ili kujifaidi wenyewe katika mambo ya kibiashara. Ukiwaajiri Mashahidi, walipe kwa wakati, wape kiasi cha pesa mlichokubaliana, na uwape marupurupu ambayo sheria inaagiza. Huenda hilo likatia ndani bima ya afya au kuwalipa mshahara hata wanapokuwa likizo. (1 Timotheo 5:18; Yakobo 5:1-4) Na ikiwa umeajiriwa na Shahidi mwenzako, usitazamie kutendewa kwa njia ya pekee. (Waefeso 6:5-8) Hakikisha kwamba unafanya kazi kwa muda mliokubaliana na unafanya kazi ambayo umelipwa kuifanya.—2 Wathesalonike 3:10.

14. Wakristo wanapaswa kufanya nini kabla ya kuanzisha biashara pamoja?

14 Namna gani tukianzisha biashara na ndugu au dada? Huenda hilo likahusisha kuwekeza au kutoa mkopo. Katika hali kama hizo, kuna kanuni muhimu sana ya Biblia: Andikeni mambo yote! Nabii Yeremia aliponunua shamba, aliandika nakala mbili za mkataba huo, akahakikisha mashahidi wametia sahihi nakala moja, kisha akahifadhi hati zote mbili kwa matumizi ya wakati ujao. (Yeremia 32:9-12; ona pia Mwanzo 23:16-20.) Huenda wengine wakahisi kwamba kuandika mkataba kutawafanya waonekane hawamwamini ndugu yao. Lakini kwa kweli, kuandika mkataba kunaweza kuzuia mizozo mingi, kuvunjika moyo, na kukosana. Hata katika mambo ya kibiashara, kumbuka kwamba amani ya kutaniko ni muhimu zaidi kuliko biashara yoyote.—1 Wakorintho 6:1-8; soma Maelezo ya Ziada 30.

UNYOOFU KATIKA SHUGHULI ZA KIMWILI

15. Yehova anahisije kuhusu ukosefu wa unyoofu katika biashara?

15 Tunapaswa kuwa wanyoofu tunaposhughulika na kila mtu, kutia ndani wale ambao si Mashahidi wa Yehova. Kwa maoni ya Yehova ni jambo muhimu sana kwamba tuwe wanyoofu. “Mizani ya uwongo humchukiza Yehova, lakini kipimo sahihi humfurahisha.” (Methali 11:1; 20:10, 23) Katika nyakati za Biblia, mizani ilitumiwa katika shughuli za kibiashara. Lakini wafanyabiashara fulani waliwadanganya wateja wao kwa kuwapa kipimo cha chini kuliko walichokubaliana au kwa kuwafanya walipe pesa nyingi kuliko walivyopaswa. Kama tu ilivyokuwa katika nyakati za Biblia, ni kawaida kwa watu leo kukosa kuwa wanyoofu katika biashara. Kama tu Yehova alivyouchukia ukosefu wa unyoofu wakati huo, ndivyo anavyouchukia leo.

16, 17. Ni mambo gani ya kawaida ya ukosefu wa unyoofu ambayo tunapaswa kuepuka?

16 Sisi sote tunajikuta katika hali ambazo tunaweza kukosa kuwa wanyoofu—kama vile tunapojaza ombi la kutafuta kazi, tunapojaza fomu za serikali, au tunapofanya mitihani shuleni. Wengi huamini kwamba hakuna ubaya kusema uwongo, kutia chumvi, au kutoa majibu yenye kupotosha. Hilo halitushangazi. Biblia ilitabiri kwamba katika siku za mwisho za mfumo huu, watu watakuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiopenda wema.”—2 Timotheo 3:1-5.

17 Nyakati nyingine huenda ikaonekana kwamba watu wasio wanyoofu ndio wanaofanikiwa katika ulimwengu wa leo. (Zaburi 73:1-8) Huenda Mkristo akapoteza kazi, akaibiwa pesa, au akatendewa vibaya kazini kwa sababu ya kuwa mnyoofu. Lakini unyoofu ni muhimu hata hali iweje. Kwa nini?

BARAKA ZA KUWA MNYOOFU

18. Kwa nini ni muhimu kuwa na sifa nzuri?

18 Kuwa mnyoofu, mwenye kuaminika, na mwenye kutegemeka ni sifa zenye thamani sana katika ulimwengu huu lakini si wengi walio nazo. Kila mmoja wetu anaweza kuwa na sifa hizo. (Mika 7:2) Ni kweli kwamba huenda watu fulani wakakudhihaki kwa kuwa mnyoofu na kusema kwamba wewe ni mjinga. Lakini wengine watathamini unyoofu wako na kukuamini. Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa unyoofu wao. Waajiri fulani wanapenda kuwaajiri Mashahidi kwa sababu wanajua wao ni wanyoofu. Na katika pindi ambazo wafanyakazi wengine wamefutwa kazi kwa sababu ya kutokuwa wanyoofu, mara nyingi Mashahidi wamedumisha kazi zao.

Tunaweza kumtukuza Yehova kwa kufanya kazi kwa bidii

19. Kuwa mnyoofu kutaathirije urafiki wako na Yehova?

19 Kuwa mnyoofu katika mambo yote kutakusaidia kuwa na dhamiri njema na amani ya akili. Tunaweza kuwa kama Paulo ambaye aliandika hivi: “Tuna hakika kwamba tuna dhamiri nyoofu.” (Waebrania 13:18) Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba Baba yako wa mbinguni mwenye upendo, Yehova, atatambua na kuthamini jitihada zako za kuwa mnyoofu katika mambo yote.—Soma Zaburi 15:1, 2; Methali 22:1.