Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 8

Yehova Anataka Watu Wake Wawe Safi

Yehova Anataka Watu Wake Wawe Safi

“Kwa walio safi unajidhihirisha mwenyewe kuwa safi.”—ZABURI 18:26.

1-3. (a) Kwa nini mama anahakikisha kwamba mtoto wake ni safi? (b) Kwa nini Yehova anataka watu wake wawe safi?

WAZIA mama akimtayarisha mtoto wake aende shule. Anahakikisha kwamba mtoto wake ameoga na nguo zake ni safi na nadhifu. Hilo litamsaidia mtoto awe na afya nzuri na wengine wataona kwamba wazazi wake wanamtunza.

2 Baba yetu, Yehova anataka tuwe safi. (Zaburi 18:26) Anajua kwamba kuwa safi kutatunufaisha. Na tunapokuwa safi, tunafanya aheshimiwe.—Ezekieli 36:22; soma 1 Petro 2:12.

3 Kuwa safi kunamaanisha nini? Kuna faida gani za kuwa safi? Tunapochunguza maswali hayo, huenda tukaona mabadiliko tunayopaswa kufanya.

KWA NINI TUNAPASWA KUWA SAFI?

4, 5. (a) Kwa nini tunapaswa kuwa safi? (b) Uumbaji unatufundisha nini kuhusu jinsi Yehova anavyoona usafi?

4 Tunajifunza kuwa safi kutokana na mfano wa Yehova mwenyewe. (Mambo ya Walawi 11:44, 45) Kwa hiyo, sababu kuu ya kuwa safi ni kwamba tunataka ‘kumwiga Mungu.’—Waefeso 5:1.

5 Uumbaji unatufundisha mambo mengi kuhusu jinsi Yehova anavyouona usafi. Yehova aliumba mizunguko ya asili ambayo inafanya hewa na maji yawe safi. (Yeremia 10:12) Fikiria njia nyingi ambazo dunia inajisafisha, hata baada ya wanadamu kuichafua. Kwa mfano, Yehova aliumba vijidudu vidogo sana ambavyo vinaweza kuonekana tu kwa kutumia hadubini. Vijidudu hivyo vinaweza kugeuza takataka zenye sumu kuwa vitu visivyo na madhara. Huo ni uwezo wa ajabu sana. Wanasayansi hata wametumia baadhi ya vijidudu hivyo kurekebisha madhara ya uchafuzi.—Waroma 1:20.

6, 7. Sheria ya Musa ilionyeshaje kwamba wale wanaomwabudu Yehova wanapaswa kuwa safi?

6 Pia, Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli kupitia Musa inatuonyesha umuhimu wa kuwa safi. Kwa mfano, watu walihitaji kuwa safi kimwili ili Yehova akubali ibada yao. Katika Siku ya Kufunika Dhambi, kuhani mkuu alipaswa kuoga mara mbili. (Mambo ya Walawi 16:4, 23, 24) Na kabla ya kutoa dhabihu, makuhani walipaswa kunawa mikono na miguu. (Kutoka 30:17-21; 2 Mambo ya Nyakati 4:6) Katika visa fulani, hukumu ya kutotii sheria ya usafi ilikuwa kifo.—Mambo ya Walawi 15:31; Hesabu 19:17-20.

7 Vipi kuhusu wakati wetu? Tunaweza kujifunza mambo mengi kuhusu viwango vya Yehova kupitia Sheria. (Malaki 3:6) Ilionyesha waziwazi kwamba waabudu wa Yehova wanapaswa kuwa safi. Viwango vya Yehova havijabadilika. Leo, bado anatarajia waabudu wake wawe safi.—Yakobo 1:27.

KUWA SAFI KUNAMAANISHA NINI?

8. Tunapaswa kuwa safi katika njia zipi?

8 Kwa maoni ya Yehova, kuwa safi kunamaanisha mambo mengi zaidi ya usafi wa mwili, mavazi, na nyumba zetu. Usafi unahusisha sehemu zote za maisha yetu. Unatia ndani ibada, mwenendo, na mawazo yetu. Naam, ili Yehova atuone sisi ni safi, tunapaswa kuwa safi katika kila sehemu ya maisha yetu.

9, 10. Tunapaswa kufanya nini ili ibada yetu iwe safi?

9 Ibada safi. Hatupaswi kujihusisha na ibada ya uwongo katika njia yoyote ile. Waisraeli walipokuwa wafungwa kule Babiloni walizungukwa na watu ambao walishirikiana na dini za kipagani zenye maadili mapotovu. Isaya alitabiri kwamba Waisraeli wangerudi nyumbani Israeli na kurudisha upya ibada safi. Yehova aliwaambia hivi: “Tokeni humo, msiguse kitu chochote kichafu! Tokeni kati yake, iweni safi.” Ibada yao kwa Mungu haikupaswa kuchanganywa na mafundisho, tabia, au desturi za dini ya uwongo ya Babiloni.—Isaya 52:11.

10 Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli leo wanaepuka dini ya uwongo. (Soma 1 Wakorintho 10:21.) Ulimwenguni pote, utamaduni, desturi, na imani zinazopendwa na watu wengi zinategemea mafundisho ya dini za uwongo. Kwa mfano, katika tamaduni nyingi, watu wanaamini kwamba kuna kitu fulani ndani ya mwili wa mwanadamu ambacho kinaendelea kuishi baada ya mtu kufa, na kuna desturi nyingi zinazotokana na imani hiyo. (Mhubiri 9:5, 6, 10) Wakristo wanahitaji kuepuka desturi hizo. Washiriki wa familia zetu wanaweza kutushinikiza tushiriki katika desturi hizo. Hata hivyo, kwa kuwa tunataka Yehova atuone kuwa safi, hatukubali kushinikizwa.—Matendo 5:29.

11. Inamaanisha nini kuwa na mwenendo safi?

11 Mwenendo safi. Ili Yehova atuone sisi ni safi, tunapaswa kuepuka kila aina ya upotovu wa maadili kingono. (Soma Waefeso 5:5.) Katika Biblia, Yehova anatuambia ‘tuukimbie uasherati.’ Ameeleza waziwazi kwamba waasherati ambao hawatubu “hawataurithi Ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10, 18; soma Maelezo ya Ziada 22.

12, 13. Kwa nini tunahitaji kuwa safi katika mawazo yetu?

12 Mawazo safi. Mara nyingi mawazo huongoza kwenye matendo. (Mathayo 5:28; 15:18, 19) Mawazo safi yatatuchochea tutende kwa njia safi. Bila shaka, sisi si wakamilifu na mara kwa mara tutakuwa na mawazo mabaya. Mawazo mabaya yanapoingia akilini, tunapaswa kuyaondoa mara moja. Tusipofanya hivyo, baada ya muda moyo wetu utachafuliwa na mawazo mabaya. Tunaweza kuanza kutamani kufanya mambo tunayofikiria kuyahusu. Badala yake, tunapaswa kujaza mawazo safi katika akili zetu. (Soma Wafilipi 4:8.) Kwa hiyo, tunaepuka burudani zinazoonyesha maadili mapotovu au jeuri. Tunachagua kwa uangalifu mambo tunayosoma, tunayotazama, na tunayozungumzia.—Zaburi 19:8, 9.

13 Ili tudumu katika upendo wa Mungu, ibada yetu, mwenendo wetu, na mawazo yetu yanapaswa kuwa safi. Lakini mbali na hilo ni jambo la maana kwa Yehova kwamba tuwe safi kimwili.

NI KWA NJIA GANI TUNAWEZA KUWA SAFI KIMWILI?

14. Kwa nini ni muhimu kuwa safi kimwili?

14 Tunaposafisha mazingira yetu na mwili wetu tunajinufaisha sisi wenyewe na watu wanaotuzunguka. Tutajihisi vizuri na watu watafurahi kuwa pamoja nasi. Zaidi ya hilo, kuna sababu muhimu zaidi ya kuwa safi kimwili. Kuwa safi kunamletea Yehova heshima. Fikiria jambo hili: Ukimwona mtoto ambaye kila siku ni mchafu, unaweza kuwa na maoni yasiyofaa kuwaelekea wazazi wake. Vivyo hivyo, ikiwa hatujitunzi na kudumisha usafi, huenda watu wakawa na maoni yasiyofaa kumhusu Yehova. Paulo alisema hivi: “Hatutoi sababu yoyote ya kukwaza, ili kosa lolote lisipatikane katika huduma yetu; bali katika kila njia tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu.”—2 Wakorintho 6:3, 4.

Tukiwa watu wa Yehova, tunapaswa kuwa safi na kuhakikisha mazingira yetu ni safi

15, 16. Tunaweza kufanya nini ili tuwe safi?

15 Mwili wetu na mavazi yetu. Usafi unapaswa kuwa sehemu ya maisha yetu ya kila siku. Kwa mfano, tunaoga kwa ukawaida, ikiwezekana kila siku. Tunanawa mikono kwa sabuni na maji, hasa kabla ya kupika au kula na kila baada ya kutumia choo au kushika kitu kichafu. Huenda kunawa mikono kukaonekana kuwa jambo dogo, lakini ni muhimu sana ili kuua bakteria na kuzuia kuenea kwa magonjwa. Kufanya hivyo kunaweza hata kuokoa uhai. Ikiwa hatuna choo, tunaweza kutafuta njia inayofaa ya kuondoa uchafu. Waisraeli wa kale hawakuwa na vyoo, kwa hiyo walifukia uchafu wao ardhini, mbali na makazi ya watu na vyanzo vya maji.—Kumbukumbu la Torati 23:12, 13.

16 Si lazima mavazi yetu yawe yenye madoido, ya gharama ya juu, au mtindo wa karibuni. Lakini yanapaswa kuwa safi na nadhifu. (Soma 1 Timotheo 2:9, 10.) Sikuzote tunataka kumletea Yehova heshima kwa jinsi tunavyoonekana.—Tito 2:10.

17. Kwa nini tunahitaji kudumisha nyumba zetu na mazingira yakiwa safi?

17 Nyumba zetu na mazingira. Hata iwe tunaishi wapi, nyumba zetu zinapaswa kuwa safi. Pia, tunahakikisha kwamba magari yetu, pikipiki, baiskeli, au chombo chochote tunachotumia kwa usafiri ni safi, hasa ikiwa tunakitumia kwenda mikutanoni au katika kazi ya kuhubiri. Kwa kweli, tunapohubiri tunawaeleza wengine kwamba watu wataishi katika dunia paradiso itakayokuwa safi. (Luka 23:43; Ufunuo 11:18) Nyumba zetu na mazingira yetu yanapaswa kuonyesha kwamba tunajitayarisha kuishi katika ulimwengu huo mpya.

18. Kwa nini tunataka mahali petu pa ibada pawe safi?

18 Mahali petu pa ibada. Tunaonyesha kwamba usafi ni muhimu kwa kuendelea kudumisha mahali petu pa ibada pakiwa safi, iwe ni Jumba la Ufalme au mahali tunapofanyia makusanyiko. Watu wanapokuja kwenye Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza, mara nyingi wanagundua jinsi lilivyo safi. Jambo hilo humtukuza Yehova. Tukiwa washiriki wa kutaniko, sisi sote tuna nafasi ya kusaidia kusafisha Jumba letu la Ufalme na kulidumisha likiwa katika hali nzuri.—2 Mambo ya Nyakati 34:10.

KUONDOLEA MBALI MAZOEA MACHAFU

19. Tunahitaji kuepuka nini?

19 Ingawa Biblia haina orodha ya mazoea yote tunayopaswa kuepuka, ina kanuni zinazoweza kutusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyohisi kuhusiana na mazoea hayo. Hataki tuvute sigara, kutumia kileo kupita kiasi, au kutumia dawa za kulevya. Ikiwa sisi ni rafiki za Mungu, tutaepuka kufanya mambo hayo. Kwa nini? Kwa sababu tunaheshimu sana zawadi ya uhai. Tabia kama hizo zinaweza kufupisha uhai wetu, kudhuru afya yetu, na kuwadhuru watu walio karibu nasi. Watu wengi hujaribu kuacha mazoea hayo ili walinde afya zao. Hata hivyo, tukiwa rafiki za Yehova, tunaacha mazoea hayo kwa sababu tunampenda. Mwanamke mmoja kijana alisema hivi: “Kwa msaada wa Yehova, nilisafisha maisha yangu na kuacha uraibu wangu. . . . Ninafikiri isingekuwa rahisi kwangu kufanya mabadiliko hayo kwa nguvu zangu mwenyewe.” Acheni tuzungumzie kanuni tano za Biblia ambazo zitamsaidia mtu kuacha mazoea yenye kudhuru.

20, 21. Ni mazoea gani ambayo Yehova anataka tuwe huru kutokana nayo?

20 “Wapendwa, kwa kuwa tuna ahadi hizi, acheni tujisafishe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Yehova anataka tuwe huru kutokana na mazoea yasiyo safi ambayo yanaweza kuchafua akili au mwili wetu.

21 Sababu kuu ya ‘kujisafisha kila unajisi’ inaelezwa kwenye 2 Wakorintho 6:17, 18. Yehova anatuambia: “Mwache kugusa kitu kichafu.” Kisha anatuahidi hivi: “Nitawakaribisha ndani. Nami nitakuwa baba kwenu, nanyi mtakuwa wana na mabinti kwangu.” Naam, kama vile baba anavyowapenda watoto wake ndivyo Yehova atakavyotupenda ikiwa tutaepuka kitu chochote kinachoweza kutufanya tusiwe safi mbele zake.

22-25. Ni kanuni gani za Kimaandiko zinazoweza kutusaidia kuepuka mazoea yasiyo safi?

22 “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Hii ndiyo amri muhimu zaidi kuliko zote. (Mathayo 22:38) Yehova anastahili upendo wetu kamili. Tunawezaje kudai kwamba tunampenda kikamili ikiwa tunaamua kufanya jambo linaloweza kufupisha uhai wetu au kuharibu ubongo wetu? Badala yake, tunafanya chochote tunachoweza ili kuonyesha kwamba tunaheshimu uhai ambao ametupatia.

23 “[Yehova] huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:24, 25) Rafiki yako akikupa zawadi ya pekee, je, unaweza kuitupa au kuiharibu? Uhai ni zawadi ya pekee sana kutoka kwa Yehova. Tunaithamini sana zawadi hiyo. Kwa hiyo, tunataka kuutumia uhai wetu kwa njia ambayo itamletea utukufu.— Zaburi 36:9.

24 “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.” (Mathayo 22:39) Mazoea yasiyo safi hayatudhuru sisi tu. Yanaweza kuwadhuru watu wengine pia, na mara nyingi yanawadhuru watu tunaowapenda sana. Kwa mfano, mtu anayeishi na mvutaji wa sigara anaweza kupata ugonjwa mbaya kwa sababu tu ya moshi wa sigara. Lakini tunapoacha mazoea hayo, tunawaonyesha watu walio karibu nasi kwamba tunawapenda.—1 Yohana 4:20, 21.

25 “Endelea kuwakumbusha wajitiishe na kuzitii serikali na mamlaka.” (Tito 3:1) Katika maeneo mengi ni kosa kisheria kutumia au kuwa na dawa za kulevya. Kwa kuwa Yehova anatuamuru tuheshimu serikali, tunatii sheria hizo.—Waroma 13:1.

Tunapoendelea kuwa safi, tunamletea Yehova heshima

26. (a) Tunahitaji kufanya nini ili Yehova akubali ibada yetu? (b) Kwa nini kuwa safi machoni pa Mungu ndiyo njia bora ya maisha?

26 Ikiwa tunataka kuwa rafiki za Yehova, huenda tukatambua kwamba tunahitaji kufanya mabadiliko fulani. Ikiwa ndivyo, tunapaswa kufanya hivyo mara moja. Kwa kawaida, si rahisi kuacha mazoea machafu, lakini tunaweza kuyaacha! Yehova anaahidi kutusaidia. Anasema hivi: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Ninayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Ninayekuongoza katika njia unayopaswa kutembea.” (Isaya 48:17) Tunapojitahidi kuwa safi, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tunamletea Mungu wetu heshima.