Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 12

Sema Lililo “Jema kwa Ajili ya Kujenga”

Sema Lililo “Jema kwa Ajili ya Kujenga”

Neno lililooza lisitoke kinywani mwenu, bali neno jema kwa ajili ya kujenga.”​—WAEFESO 4:29.

1-3. (a) Yehova ametupatia zawadi gani njema? Ni katika njia gani inaweza kutumiwa vibaya? (b) Tunapaswa kuitumiaje zawadi yetu ya usemi?

BABA anampa mwana wake baiskeli. Anafurahi kumpa mwana wake zawadi ya pekee hivyo. Lakini namna gani mwana huyo akiendesha baiskeli hiyo ovyoovyo, amgonge mtu, na kumjeruhi? Baba atahisije?

2 Yehova ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yakobo 1:17) Mojawapo ya zawadi zake njema ni uwezo wetu wa kusema. Zawadi ya usemi inaturuhusu kueleza mambo tunayofikiria na kuhisi. Tunaweza kusema mambo yanayowatia moyo watu na kuwafanya wajihisi vizuri. Lakini mambo tunayosema yanaweza pia kuwadhuru wengine na kuwaumiza.

3 Maneno yana nguvu sana, na Yehova anatufundisha jinsi ya kutumia zawadi ya usemi vizuri. Anatuambia hivi: “Neno lililooza lisitoke kinywani mwenu, bali neno jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwanufaishe wale wanaolisikia.” (Waefeso 4:29) Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kutumia zawadi hii kutoka kwa Mungu katika njia itakayompendeza na itakayowatia moyo wengine.

UWE MWANGALIFU KUHUSU YALE UNAYOSEMA

4, 5. Methali za Biblia zinatufundisha maneno yana nguvu za kufanya nini?

4 Maneno yana nguvu, kwa hiyo tunahitaji kuwa waangalifu kuhusu kile tunachosema na jinsi tunavyokisema. Methali 15:4 inasema hivi: “Ulimi mtulivu ni mti wa uzima, lakini maneno yaliyopotoka hukatisha tamaa.” Kama tu mti unavyoburudisha na kuendeleza uhai, maneno yenye fadhili humburudisha msikilizaji. Kwa upande mwingine, maneno makali huwaumiza wengine na kuwafanya wajihisi vibaya.—Methali 18:21.

Maneno matulivu yanaburudisha

5 “Maneno yanayosemwa bila kufikiri huchoma kama upanga,” inasema Methali 12:18. Maneno yasiyo na fadhili yanaweza kusababisha maumivu ya kihisia na kuharibu mahusiano. Huenda unakumbuka wakati ambapo mtu fulani alizungumza bila fadhili na kukuumiza sana. Hata hivyo, methali hiyo inaendelea kusema: “Ulimi wa mwenye hekima huponya.” Maneno yenye ufikirio yanaweza kuponya moyo wenye maumivu na kurudisha uhusiano kati ya marafiki waliokosana. (Soma Methali 16:24.) Tukikumbuka kwamba maneno yetu yanawaathiri wengine, tutakuwa waangalifu tunapozungumza.

6. Kwa nini ni vigumu kudhibiti mambo tunayosema?

6 Sababu nyingine ya kuwa waangalifu kuhusu maneno yetu ni kwamba sisi sote si wakamilifu. “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya,” na mara nyingi maneno yetu hufunua kile kilicho moyoni mwetu. (Mwanzo 8:21; Luka 6:45) Inaweza kuwa vigumu sana kudhibiti maneno yetu. (Soma Yakobo 3:2-4.) Lakini tunahitaji kuendelea kujitahidi kuboresha jinsi tunavyozungumza na wengine.

7, 8. Maneno yetu yanaweza kuathirije uhusiano wetu na Yehova?

7 Pia tunahitaji kuwa waangalifu kuhusu maneno yetu kwa kuwa tunawajibika kwa Yehova kuhusu yale tunayosema na jinsi tunavyoyasema. Yakobo 1:26 inasema: “Ikiwa mtu yeyote anafikiri yeye ni mwabudu wa Mungu lakini haudhibiti kabisa ulimi wake, anaudanganya moyo wake, na ibada yake ni ubatili.” Neno la awali linalotafsiriwa “ubatili” linaweza pia kumaanisha “bure.” (1 Wakorintho 15:17) Kwa hiyo, ikiwa tunazungumza ovyoovyo tunaweza kuharibu au hata kupoteza uhusiano wetu na Yehova.—Yakobo 3:8-10.

8 Ni wazi kwamba tuna sababu nzuri za kuwa waangalifu tunasema nini na jinsi tunavyozungumza. Ili tutumie zawadi yetu ya usemi kwa njia ambayo Yehova anataka, tunahitaji kujua usemi ambao tunapaswa kuepuka.

MANENO YANAYOBOMOA

9, 10. (a) Ni usemi gani ambao ni wa kawaida sana katika ulimwengu leo? (b) Kwa nini tunaepuka kutumia maneno machafu?

9 Ni kawaida sana kwa watu leo kutumia maneno machafu. Wengi hufikiri wanahitaji kutumia matusi au maneno machafu ili wanachosema kieleweke. Mara nyingi, watumbuizaji hutumia mzaha mchafu ili kuwachekesha watu. Hata hivyo, mtume Paulo alisema hivi: “Lazima myaondoe mambo haya yote kutoka kwenu: ghadhabu, hasira, ubaya, matusi, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu.” (Wakolosai 3:8) Pia, alisema kwamba “mizaha michafu” haipaswi ‘kutajwa kamwe miongoni’ mwa Wakristo wa kweli.—Waefeso 5:3, 4.

10 Maneno machafu yanamchukiza Yehova na wale ambao wanampenda. Huo ni uchafu. Katika Biblia, “uchafu” unaorodheshwa kati ya “matendo ya mwili.” (Wagalatia 5:19-21) “Uchafu” unaweza kutia ndani dhambi mbalimbali, na zoea moja chafu linaweza kuongoza kwenye zoea lingine. Ikiwa mtu ana zoea la kutumia maneno machafu sana, na anakataa kuacha, hilo linaweza kuonyesha kwamba hapaswi kuendelea kuwa sehemu ya kutaniko.—2 Wakorintho 12:21; Waefeso 4:19; soma Maelezo ya Ziada 23.

11, 12. (a) Porojo yenye kuumiza ni nini? (b) Kwa nini tunapaswa kuepuka kumchongea mtu mwingine?

11 Pia tunahitaji kuepuka porojo yenye kuumiza. Ni kawaida kupendezwa na wengine na kueleza habari kuhusu marafiki na watu wa familia. Hata katika karne ya kwanza, Wakristo wa mapema walitaka kujua jinsi ndugu na dada zao walivyokuwa wakiendelea na wangeweza kufanya nini ili kuwasaidia. (Waefeso 6:21, 22; Wakolosai 4:8, 9) Lakini ni rahisi kwa mazungumzo kuwahusu wengine kubadilika na kuwa porojo yenye kuumiza. Tukimweleza mtu mwingine porojo tuliyosikia, huenda tukasema mambo ambayo si ya kweli au tukazungumzia mambo ya siri. Tusipokuwa waangalifu, mazungumzo hayo yasiyofaa yanaweza kubadilika na kuwa mashtaka yasiyo ya kweli, au uchongezi. Mafarisayo walimchongea Yesu walipomshtaki kwa mambo ambayo hakuwa amefanya. (Mathayo 9:32-34; 12:22-24) Uchongezi huharibu sifa nzuri za mtu mwingine, unasababisha ugomvi na maumivu, na kuharibu urafiki.—Methali 26:20.

12 Yehova anataka tutumie maneno yetu kuwasaidia na kuwatia moyo wengine, si kuwafanya marafiki wawe maadui. Yehova anamchukia yeyote “anayepanda ugomvi miongoni mwa ndugu.” (Methali 6:16-19) Mchongezi wa kwanza alikuwa Shetani Ibilisi, ambaye alimchongea Mungu. (Ufunuo 12:9, 10) Katika ulimwengu wa leo, ni jambo la kawaida kwa watu kusema uwongo kuhusu wengine. Lakini haipaswi kuwa hivyo katika kutaniko la Kikristo. (Wagalatia 5:19-21) Kwa hiyo, tunapaswa kuwa waangalifu tunasema nini na sikuzote tufikiri kabla ya kusema. Kabla ya kurudia kusema jambo ulilosikia kumhusu mtu mwingine, jiulize: ‘Je, jambo ninalotaka kusema ni kweli? Je, ni lenye fadhili? Je, lina faida? Je, ningependa mtu ninayezungumza kumhusu asikie ninalosema? Ningehisije ikiwa mtu angesema jambo hilo kunihusu?’—Soma 1 Wathesalonike 4:11.

13, 14. (a) Maneno machafu yanaweza kuwaathirije wengine? (b) Kwa nini Mkristo anapaswa kuepuka zoea la kuwatukana wengine?

13 Nyakati nyingine, sisi sote husema mambo ambayo tunajutia baadaye. Lakini hatutaki kuwa na zoea la kuwachambua wengine au kusema mambo yasiyo na fadhili au yenye kuumiza. Hatupaswi kamwe kutumia matusi. Paulo alisema hivi: “Acheni kabisa kila aina ya chuki yenye uhasama, hasira, ghadhabu, kufoka, [na] matusi.” (Waefeso 4:31) Biblia nyingine zinatafsiri neno “matusi” kuwa “maneno maovu,” “usemi wenye kuumiza,” na “lugha chafu.” Matusi huwashushia wengine heshima na kuwafanya wajihisi hawafai. Watoto hasa ndio wanaoweza kuumia kwa urahisi, kwa hiyo tungependa kuwa waangalifu sana tusiwaumize kwa maneno yetu.—Wakolosai 3:21.

14 Biblia inatuonya kuhusu kuwa na zoea la kuwatukana wengine tukiwa na lengo la kuwaumiza. Ni jambo lenye kuhuzunisha sana kwa mtu kumtendea mke wake au watoto wake kwa njia hiyo. Kwa kweli, mtu ambaye anakataa kuacha kuwatukana wengine kwa njia hiyo hawezi kustahili kuwa sehemu ya kutaniko. (1 Wakorintho 5:11-13; 6:9, 10) Kama tulivyojifunza, tukisema maneno machafu, yasiyo ya kweli, au yasiyo na fadhili, tutaharibu uhusiano wetu na Yehova na pamoja na wengine.

MANENO YANAYOJENGA

15. Ni usemi wa aina gani unaoimarisha mahusiano?

15 Tunaweza kutumiaje zawadi ya usemi kwa njia ambayo Yehova anataka? Hata ingawa Biblia haituambii kihususa kile tunachopaswa au tusichopaswa kusema, inatuambia tuseme “neno jema kwa ajili ya kujenga.” (Waefeso 4:29) Maneno yenye kujenga ni safi, yenye fadhili, na ya kweli. Yehova anataka tutumie maneno yetu kuwatia moyo na kuwasaidia wengine. Inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo. Ni vigumu zaidi kusema mambo mazuri kuliko kusema mambo yenye kuumiza bila kufikiri. (Tito 2:8) Acheni tuzungumzie njia mbalimbali tunazoweza kuwajenga wengine kupitia maneno yetu.

16, 17. (a) Kwa nini tunapaswa kuwapongeza wengine? (b) Tunaweza kuwapongeza nani?

16 Yehova na Yesu hutoa pongezi kwa wingi. Tunataka kuwaiga. (Mathayo 3:17; 25:19-23; Yohana 1:47) Ili kutoa pongezi ambayo kwa kweli itamtia moyo mtu tunapaswa kumfikiria na kumwonyesha upendezi wa kibinafsi. Methali 15:23 inasema hivi: “Neno linalosemwa wakati unaofaa—ni jema sana!” Tunatiwa moyo mtu anapotupongeza kwa unyoofu kwa sababu ya kazi yetu ngumu au anapotushukuru kwa jambo ambalo tumefanya.—Soma Mathayo 7:12; soma Maelezo ya Ziada 27.

17 Unapokuwa na zoea la kutafuta sifa nzuri za wengine, itakuwa rahisi kuwapongeza kwa unyoofu. Kwa mfano, labda unatambua kwamba kwa kawaida mtu fulani katika kutaniko lenu hutayarisha hotuba zake vizuri au anajitahidi kutoa maelezo mikutanoni. Kijana anaweza kuwa anaitetea kweli shuleni, au mtu mwenye umri mkubwa anaweza kuwa akishiriki kwa ukawaida katika huduma. Watafurahi sana kusikia ukiwapongeza. Ni muhimu sana pia kwa mume kumwambia mke wake kwamba anampenda na kumthamini sana. (Methali 31:10, 28) Kama tu mimea inavyohitaji mwangaza na maji, ndivyo watu wanavyohitaji kuhisi kwamba wanathaminiwa. Hilo ni kweli hasa kwa watoto. Tafuta nafasi za kuwapongeza kwa sifa zao nzuri na jitihada wanazofanya. Pongezi inaweza kuwafanya wawe na ujasiri na wajiamini, na pia inaweza kuwafanya watie bidii hata zaidi kufanya yaliyo mema.

Tunaweza kuwatia moyo na kuwafariji watu kupitia maneno tunayosema na jinsi tunavyoyasema

18, 19. Kwa nini tunapaswa kufanya yote tuwezayo kuwatia moyo na kuwafariji wengine? Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

18 Tunapowatia moyo na kuwafariji wengine, tunaiga mfano wa Yehova. Yeye anawajali sana “watu wa hali ya chini” na “wale wanaopondwa.” (Isaya 57:15) Yehova anataka ‘tuendelee kutiana moyo’ na ‘tuwafariji wale walioshuka moyo.’ (1 Wathesalonike 5:11, 14) Tunapojaribu kufanya hivyo, anaona jitihada zetu na kuzithamini.

19 Huenda ukatambua kwamba mtu kutanikoni amevunjika moyo au kushuka moyo. Unaweza kumwambia nini ili kumsaidia? Huenda usiweze kutatua tatizo lake, lakini unaweza kumwonyesha kwamba unajali. Kwa mfano, unaweza kupanga kutumia wakati pamoja naye. Unaweza kumsomea mstari fulani wa Biblia au hata kutoa sala pamoja naye. (Zaburi 34:18; Mathayo 10:29-31) Mhakikishie kwamba ndugu na dada zake kutanikoni wanampenda. (1 Wakorintho 12:12-26; Yakobo 5:14, 15) Na uzungumze katika njia inayoonyesha kwamba unaamini na kumaanisha unachosema.—Soma Methali 12:25.

20, 21. Ni nini kinachofanya iwe rahisi kwa watu kukubali mashauri?

20 Pia, tunawajenga wengine tunapowapa mashauri mazuri. Kwa kuwa sisi si wakamilifu, sote tunahitaji mashauri mara kwa mara. Methali 19:20 inasema: “Sikiliza mashauri na ukubali nidhamu, ili uwe na hekima wakati wako ujao.” Si wazee tu wanaoweza kutoa mashauri. Wazazi wanahitaji kuwapa watoto wao mwongozo. (Waefeso 6:4) Na akina dada wanaweza kuwashauri akina dada wenzao kwa njia nzuri. (Tito 2:3-5) Kwa sababu tunawapenda ndugu na dada zetu, tunataka kuhakikisha kwamba tunawashauri kwa njia ambayo haitawafanya wajihisi vibaya. Ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya hivyo?

21 Labda unakumbuka wakati ambapo mtu alikupa mashauri mazuri katika njia ambayo ilikuwa rahisi kukubali. Ni nini kilichofanya shauri hilo liwe na matokeo? Huenda ulihisi kwamba mtu huyo alikujali sana. Au labda alizungumza nawe kwa fadhili na upendo. (Wakolosai 4:6) Huenda shauri lake lilitegemea Biblia. (2 Timotheo 3:16) Iwe tunanukuu moja kwa moja kutoka kwenye Biblia au la, lazima kuwe na msingi wa Kimaandiko kwa shauri tunalotoa. Hakuna mtu anayepaswa kuwalazimisha wengine wafuate maoni yake au kutumia maandiko vibaya ili kuunga mkono maoni yake. Kukumbuka jinsi wewe ulivyoshauriwa kunaweza kukusaidia unapowashauri wengine.

22. Wewe ungependa kutumia zawadi yako ya usemi kwa njia gani?

22 Uwezo wa kusema ni zawadi kutoka kwa Mungu. Upendo wetu kwake unapaswa kutuchochea kutumia zawadi hiyo vizuri. Kumbuka kwamba maneno yana nguvu za kubomoa au kujenga. Kwa hiyo, na tufanye yote tunayoweza kutumia maneno yetu kuwaimarisha na kuwatia moyo wengine.