Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA MBILI

Jinsi Unavyoweza Kuwa Rafiki ya Mungu

Jinsi Unavyoweza Kuwa Rafiki ya Mungu

1, 2. Taja baadhi ya watu waliokuwa rafiki za Yehova.

UNGEPENDA kuwa na rafiki wa aina gani? Bila shaka ni yule unayempenda na aliye tayari kushirikiana nawe. Mwenye fadhili na sifa nyingine bora unazopenda.

2 Yehova Mungu amewachagua baadhi ya wanadamu wawe rafiki zake. Kwa mfano, Abrahamu alikuwa rafiki wa Yehova. (Isaya 41:8; Yakobo 2:23) Yehova alimpenda pia Daudi. Alisema kwamba Daudi alikuwa ‘mtu anayeupendeza moyo wake.’ (Matendo 13:22) Nabii Danieli alikuwa “mtu mwenye thamani sana” kwa Yehova.—Danieli 9:23.

3. Kwa nini Abrahamu, Daudi, na Danieli walikuwa rafiki za Yehova?

3 Kwa nini Abrahamu, Daudi, na Danieli walikuwa rafiki za Yehova? Yehova alimwambia Abrahamu hivi: “Umeisikiliza sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Yehova ni rafiki ya wale wote wanaomtii kwa unyenyekevu. Hata watu wa taifa zima wanaweza kuwa rafiki za Yehova. Yehova aliliambia taifa la Israeli hivi: “Tiini sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu, nanyi mtakuwa watu wangu.” (Yeremia 7:23) Hivyo, unahitaji kumtii Yehova ikiwa unataka kuwa rafiki yake.

YEHOVA ANAWALINDA RAFIKI ZAKE

4, 5. Yehova anawalindaje rafiki zake?

4 Biblia inasema kwamba Yehova anatafuta nafasi “ili adhihirishe nguvu zake kwa niaba ya wale ambao moyo wao ni kamili kumwelekea yeye.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Katika Zaburi 32:8, Yehova anawaahidi rafiki zake hivi: “Nitakupa ufahamu na kukufundisha njia unayopaswa kufuata. Nitakupa ushauri jicho langu likikutazama.”

5 Adui mwenye nguvu anataka kutuzuia tusiwe rafiki za Mungu. Hata hivyo, Yehova anataka kutulinda dhidi ya adui huyo. (Soma Zaburi 55:22.) Tunamtumikia Yehova kwa moyo wote, kwa sababu ni rafiki yetu. Tunashikamana naye hata tukikabili hali ngumu. Nasi tuna uhakika kama wa mtunga zaburi, ambaye aliandika hivi kuhusu Yehova: “Kwa sababu yuko mkono wangu wa kulia, sitatikiswa kamwe.” (Zaburi 16:8; 63:8) Shetani hutuzuiaje tusiwe rafiki za Mungu?

MADAI YA SHETANI

6. Shetani anadai nini kuhusu wanadamu?

6 Katika Sura ya 11 tulijifunza kwamba Shetani alidai kuwa Yehova ni mwongo na hatendi haki kwa sababu aliwanyima Adamu na Hawa uhuru wa kujiamulia mema na mabaya. Kitabu cha Ayubu kinatuambia kwamba Shetani anawashutumu pia watu wote wanaotaka kuwa rafiki za Mungu. Anadai kwamba wanamtumikia Mungu kwa kuwa amewabariki, na si kwa sababu wanampenda. Pia, Shetani anadai kuwa anaweza kumgeuza mtu yeyote aache kumtumikia Mungu. Acheni tuchunguze mambo tunayojifunza kutoka kwa Ayubu na jinsi Yehova alivyomlinda.

7, 8. (a) Yehova alimwonaje Ayubu? (b) Shetani alidai nini kumhusu Ayubu?

7 Ayubu alikuwa nani? Alikuwa mtu mwaminifu aliyeishi miaka 3,600 iliyopita. Yehova alisema hakuna mwanadamu yeyote duniani aliyekuwa kama Ayubu. Ayubu alimheshimu sana Mungu, na alichukia mambo mabaya. (Ayubu 1:8) Naam, Ayubu alikuwa rafiki ya Yehova.

8 Shetani alidai kwamba Ayubu alimtumikia Mungu kwa sababu ya ubinafsi. Shetani alimwambia Yehova hivi: “Je, wewe hukuweka ukuta wa ulinzi [au, wigo] kumzunguka yeye na nyumba yake na kila kitu alicho nacho? Umeibariki kazi ya mikono yake, na mifugo yake imeenea nchini. Lakini, ili mambo yabadilike, nyoosha mkono wako na upige kila kitu alicho nacho, na kwa hakika atakutukana mbele za uso wako mwenyewe.”—Ayubu 1:10, 11.

9. Yehova alimruhusu Shetani afanye nini?

9 Shetani alidai kwamba Ayubu alimtumikia Yehova kwa sababu Mungu alimbariki. Shetani alidai kwamba angeweza kumgeuza Ayubu aache kumtumikia. Yehova alijua kwamba madai hayo yalikuwa ya uwongo, lakini alimruhusu Shetani amjaribu Ayubu ili athibitishe madai yake.

SHETANI AMSHAMBULIA AYUBU

10. Shetani alimshambuliaje Ayubu, na Ayubu alitendaje?

10 Kwanza, Shetani alisababisha mifugo yote ya Ayubu iibiwe au kuuawa. Halafu, aliwaua watumishi wengi wa Ayubu. Ayubu alipoteza kila kitu. Mwishowe, Shetani aliwaua watoto kumi wa Ayubu kwa kimbunga. Hata hivyo, Ayubu aliendelea kushikamana na Yehova. “Katika hayo yote, Ayubu hakutenda dhambi wala hakumlaumu Mungu kwa kutenda jambo lolote baya.”—Ayubu 1:12-19, 22.

Yehova alimbariki Ayubu kwa sababu ya ushikamanifu wake

11. (a) Ni mambo gani mengine ambayo Shetani alimsababishia Ayubu? (b) Ayubu alitendaje?

11 Shetani hakukata tamaa. Alimwambia Mungu hivi: “Upige mfupa na nyama yake, na kwa hakika atakutukana mbele za uso wako mwenyewe.” Hivyo, Shetani akamshambulia Ayubu kwa ugonjwa wenye maumivu makali. (Ayubu 2:5, 7) Lakini Ayubu aliendelea kushikamana na Yehova. Alisema hivi: “Mpaka nitakapokufa, sitaukana utimilifu wangu!”—Ayubu 27:5.

12. Ayubu alithibitishaje kwamba Shetani ni mwongo?

12 Ayubu hakujua chochote kuhusu madai ya Shetani au sababu za kuteseka. Alifikiri kwamba Yehova ndiye aliyesababisha matatizo aliyokabili. (Ayubu 6:4; 16:11-14) Licha ya hali hizo, Ayubu aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova. Bila shaka, Shetani alipata jibu la madai yake. Ayubu hakuwa mbinafsi. Alikuwa rafiki ya Yehova kwa sababu alimpenda. Madai ya Shetani yalithibitika kuwa ni ya uwongo!

13. Ayubu alipata matokeo gani kwa sababu ya ushikamanifu wake?

13 Ingawa Ayubu hakujua mambo yaliyotukia mbinguni, alikuwa mshikamanifu kwa Mungu na kuthibitisha kwamba Shetani ni mwovu. Yehova alimbariki Ayubu kwa ushikamanifu wake.—Ayubu 42:12-17.

JINSI UNAVYOHUSIKA

14, 15. Shetani anadai nini kuhusu watumishi wa Yehova?

14 Unaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na majaribu yaliyompata Ayubu. Shetani anadai kwamba tunamtumikia Yehova kwa sababu ametubariki. Katika Ayubu 2:4, Shetani alidai kwamba: “Mtu atatoa kila kitu alicho nacho ili aokoe uhai wake.” Kwa hiyo, Shetani anawashutumu watumishi wote wa Yehova kwamba ni wenye ubinafsi. Miaka mingi baada ya Ayubu kufa, Shetani aliendelea kumdhihaki Yehova na kuwashutumu watumishi wake. Kwa mfano, andiko la Methali 27:11, linasema hivi: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili niweze kumjibu yule anayenidhihaki [au, anayenitukana].”

15 Unaweza kuchagua kumtii Yehova na kuwa rafiki yake na hivyo uthibitishe kwamba Shetani ni mwongo. Kuchagua kuwa rafiki ya Mungu ni uamuzi bora sana hata kama utahitaji kufanya mabadiliko makubwa maishani mwako! Uamuzi huo ni jambo zito. Shetani anadai kwamba ukikabili matatizo, huwezi kuwa mshikamanifu kwa Mungu. Anajaribu kutupotosha tuache kushikamana na Mungu. Anatumia mbinu gani?

16. (a) Ni mbinu gani ambazo Shetani anatumia ili kuwazuia watu wasimtumikie Yehova? (b) Huenda Shetani akatumia mbinu gani ili kukuzuia kumtumikia Yehova?

16 Shetani anatumia mbinu mbalimbali ili kutuzuia tusiwe rafiki za Mungu. Anatushambulia “kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Usishangae rafiki zako, watu wa familia, au watu wengine wanapokuzuia kujifunza Biblia na kufanya mambo mazuri. Huenda ukahisi kana kwamba unashambuliwa. * (Yohana 15:19, 20) Pia, Shetani anaweza kujifanya “malaika wa nuru.” Hivyo, anaweza kutupotosha tusimtii Yehova. (2 Wakorintho 11:14) Mbinu nyingine ambayo Shetani anatumia kutuzuia tusimtumikie Yehova ni kutufanya tuhisi hatustahili kumtumikia Mungu.—Methali 24:10.

TII AMRI ZA YEHOVA

17. Kwa nini tunamtii Yehova?

17 Tunapomtii Yehova, tunathibitisha kwamba Shetani ni mwongo. Ni nini kitakachotusaidia kuwa watiifu? Biblia inasema hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Kumbukumbu la Torati 6:5) Tunamtii Yehova kwa sababu tunampenda. Upendo wetu kwa Yehova unapoongezeka, utatuchochea kufanya jambo lolote analotuambia. Mtume Yohana aliandika hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 Yohana 5:3.

18, 19. (a) Ni baadhi ya mambo gani ambayo yanamchukiza Yehova? (b) Tunajuaje kwamba Yehova hawezi kutuambia tufanye jambo linalopita uwezo wetu?

18 Ni baadhi ya mambo gani yanayomchukiza Yehova? Kuna mifano kadhaa katika sanduku “ Chukia Mambo Yanayomchukiza Yehova.” Huenda mwanzoni ukahisi kwamba baadhi ya mambo hayo si mabaya sana. Lakini unaposoma mistari hiyo ya Biblia na kuitafakari, utaelewa faida za kutii amri za Yehova. Pia, utagundua kwamba unahitaji kufanya mabadiliko fulani maishani mwako. Huenda ikawa vigumu kubadilika, hata hivyo ukifanya mabadiliko, utapata amani na furaha kwa sababu ya ushikamanifu wako kwa Mungu. (Isaya 48:17, 18) Je, inawezekana kufanya mabadiliko?

19 Yehova hawezi kutuagiza tufanye jambo lolote linalopita uwezo wetu. (Kumbukumbu la Torati 30:11-14) Akiwa Rafiki yetu wa karibu, anatujua vizuri kuliko tunavyojijua. Anajua uwezo na udhaifu wetu. (Zaburi 103:14) Mtume Paulo alitutia moyo hivi: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na majaribu hayo ataifanya pia njia ya kutokea ili mweze kuyavumilia.” (1 Wakorintho 10:13) Tuna uhakika kwamba Yehova atatupatia nguvu za kufanya mambo yanayofaa. Atakupatia “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili uvumilie hali ngumu. (2 Wakorintho 4:7) Mtume Paulo, aliyepata msaada wa Mungu alipokabili hali ngumu, alisema hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:13.

JIFUNZE KUPENDA MAMBO YANAYOMPENDEZA MUNGU

20. Unapaswa kuiga sifa gani za Mungu, na kwa nini?

20 Tukitaka kuwa rafiki za Yehova, tunapaswa kufanya mambo mengi zaidi ya kuchukia tu mambo mabaya. (Waroma 12:9) Rafiki za Yehova wanapenda mambo yanayompendeza. Mambo hayo yanatajwa katika Zaburi 15:1-5. (Soma.) Rafiki za Yehova wanaiga sifa zake, kama vile “upendo, shangwe, amani, subira, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.”—Wagalatia 5:22, 23.

21. Unawezaje kujifunza sifa zinazompendeza Mungu?

21 Unawezaje kuiga sifa hizo za Mungu? Unaweza kujua mambo yanayompendeza Yehova kwa kusoma na kujifunza Biblia kila siku. (Isaya 30:20, 21) Unapofanya hivyo, upendo wako kwa Yehova utaongezeka, nawe utachochewa kumtii zaidi.

22. Ukimtii Yehova utapata baraka gani?

22 Kufanya mabadiliko maishani ni sawa na kubadili nguo chafu na kuvaa nguo safi. Biblia inasema kwamba unahitaji kuvua “utu wa zamani” na kuvaa “utu mpya.” (Wakolosai 3:9, 10) Ingawa si rahisi, tukifanya mabadiliko na kumtii Yehova, anaahidi kutupatia “thawabu kubwa.” (Zaburi 19:11) Naam, chagua kumtii Yehova ili uthibitishe kwamba Shetani ni mwongo. Mtumikie Yehova kwa moyo wote na si kwa sababu ya baraka za wakati ujao. Hatimaye utakuwa rafiki wa karibu wa Mungu!

^ fu. 16 Hilo halimaanishi kwamba Shetani anawatuma watu wajaribu kukuzuia kujifunza Biblia. Hata hivyo, Shetani ni “mungu wa mfumo huu wa mambo,” na “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu [zake].” Hivyo, haishangazi kuona baadhi ya watu wakijaribu kutuzuia kumtumikia Yehova.—2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19.