Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 20

Neno la Yehova ‘Lilikua na Kusitawi’ Licha ya Upinzani

Neno la Yehova ‘Lilikua na Kusitawi’ Licha ya Upinzani

Licha ya Upinzani Jinsi Apolo na Paulo walivyochangia ukuzi wa habari njema

Matendo 18:23–19:41

1, 2. (a) Paulo na wenzake wanakabili hatari gani Efeso? (b) Tutazungumzia nini katika sura hii?

 WATU jijini Efeso wanapiga kelele na kukimbia mitaani. Umati wa watu unakusanyika, ghasia inatokea! Baadhi ya watu wanawakamata wanaume wawili waliosafiri pamoja na Paulo na kuwaburuta. Watu wamejaa kwenye barabara pana yenye maduka kandokando. Wanajiunga na umati huo wenye hasira, na wote wanaelekea kwenye uwanja wa michezo wa jiji hilo. Uwanja huo ulikuwa mkubwa sana na mashabiki 25,000 wangeweza kukusanyika hapo. Wengi kati ya watu wanaokusanyika hapo hawajui kwa nini ghasia hiyo imetokea, lakini wanahisi kwamba hekalu lao na mungu wao wa kike Artemi yumo hatarini. Hivyo, wote wanaanza kupaaza sauti kwa pamoja kwa kurudia-rudia wakisema: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!”​—Mdo. 19:34.

2 Kwa mara nyingine tena, Shetani anajaribu kutumia umati wenye hasira kuzuia habari njema ya Ufalme wa Mungu. Bila shaka, jeuri ni mojawapo tu ya njia anazotumia Shetani. Katika sura hii, tutazungumzia mbinu mbalimbali ambazo Shetani alitumia ili kudhoofisha kazi na umoja wa Wakristo hao wa karne ya kwanza. Lakini, tutaona jinsi ambavyo mbinu zake zote zilishindwa, kwa sababu ‘kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova lilizidi kukua na kusitawi.’ (Mdo. 19:20) Ni nini kilichowasaidia Wakristo hao kusimama imara? Ni kilekile kinachotusaidia leo. Bila shaka, hatutegemei nguvu zetu wenyewe, bali tunamtegemea Yehova. Hata hivyo, kama Wakristo wa karne ya kwanza, lazima tutimize sehemu yetu. Roho takatifu ya Yehova inaweza kutusaidia kukuza sifa zitakazotuwezesha kutimiza huduma yetu kwa mafanikio. Kwanza, acheni tuzungumzie mfano wa Apolo.

“Alikuwa . . . na Ujuzi Mwingi wa Maandiko” (Mdo. 18:24-28)

3, 4. Akila na Prisila walitambua nini kuhusu Apolo, nao walimsaidiaje?

3 Paulo alipoelekea Efeso, katika safari ya tatu ya umishonari, Myahudi anayeitwa Apolo aliwasili jijini humo. Alitoka katika jiji maarufu la Aleksandria, nchini Misri. Apolo alikuwa na sifa za pekee. Alikuwa mwenye ufasaha wa kuzungumza. Isitoshe, “alikuwa . . . na ujuzi mwingi wa Maandiko.” Pia, ‘alikuwa amewaka roho.’ Akiwa mwenye bidii, Apolo alizungumza kwa ujasiri mbele za Wayahudi waliokuwa katika sinagogi.​—Mdo. 18:24, 25.

4 Akila na Prisila walimsikia Apolo akizungumza. Bila shaka walifurahi walipomwona ‘akifundisha kwa usahihi kumhusu Yesu.’ Mambo aliyosema kumhusu Yesu yalikuwa sahihi. Lakini, baada ya muda mfupi Akila na Prisila wakatambua kwamba kuna jambo muhimu ambalo Apolo haelewi. “Alifahamu ubatizo wa Yohana tu.” Wenzi hao, waliokuwa watengenezaji wa mahema, hawakumwogopa Apolo kwa sababu ya ufasaha na elimu yake. Badala yake, “wakamchukua na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.” (Mdo. 18:25, 26) Mtu huyo mwenye ufasaha na elimu aliitikiaje? Alionyesha mojawapo ya sifa muhimu zaidi ambazo Mkristo anapaswa kusitawisha—sifa ya unyenyekevu.

5, 6. Ni nini kilichomsaidia Apolo kupata matokeo mazuri katika utumishi wa Yehova, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Apolo?

5 Kwa kuwa Apolo alikubali msaada wa Akila na Prisila, alipata matokeo mazuri katika utumishi wa Yehova. Alisafiri kwenda Akaya, na akiwa huko, “akawasaidia sana” waabudu wenzake. Pia, aliwahubiria Wayahudi waliokuwa katika eneo hilo ambao walidai kwamba Yesu si Masihi aliyeahidiwa. Luka anasema hivi: “Alithibitisha kikamili . . . kwa juhudi nyingi kwamba Wayahudi walikuwa wamekosea, na kuwaonyesha kwa Maandiko kuwa Yesu ndiye Kristo.” (Mdo. 18:27, 28) Apolo alisaidia sana kutaniko! Kwa kweli, alichangia kusitawi kwa “neno la Yehova.” Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Apolo?

6 Lazima Wakristo wasitawishe sifa ya unyenyekevu. Kila mmoja wetu ana vipawa mbalimbali—iwe ni uwezo wa asili, uzoefu, au ujuzi ambao tumepata. Hata hivyo, tunapaswa kutambuliwa kwa sababu ya unyenyekevu bali si vipawa vyetu. La sivyo, huenda vipawa vyetu vikatusababishia matatizo. Tunaweza kuanza kuwa na kiburi. (1 Kor. 4:7; Yak. 4:6) Ikiwa kwa kweli sisi ni wanyenyekevu, tutajitahidi kuwaona wengine kuwa bora kuliko sisi. (Flp. 2:3) Hatutakasirika tunaporekebishwa au kukataa tunapofundishwa na wengine. Hatutaendelea kushikilia maoni yetu kwa ushupavu tukijua kwamba hayapatani na mwongozo wa sasa wa roho takatifu. Tukiendelea kuwa wanyenyekevu, Yehova na Mwana wake wataendelea kututumia.​—Luka 1:51, 52.

7. Paulo na Apolo walionyeshaje sifa ya unyenyekevu, na tunaweza kuwaiga kwa njia gani?

7 Pia, unyenyekevu huzuia roho ya mashindano. Bila shaka Shetani angependa Wakristo wa karne ya kwanza wawe na migawanyiko. Angefurahi sana ikiwa watu wawili mashuhuri kama vile Apolo na mtume Paulo wangeanza kushindana, huenda hata kuoneana wivu na kujaribu kutafuta wafuasi katika makutaniko! Jambo hilo lingeweza kutokea. Katika jiji la Korintho, Wakristo fulani walianza kusema, “Mimi ni wa Paulo,” huku wengine wakisema, “Lakini mimi ni wa Apolo.” Je, Paulo na Apolo walitaka ndugu na dada wawe na mgawanyiko? Hapana! Badala yake, Paulo alionyesha unyenyekevu kwa kutambua mchango wa Apolo katika kazi ya kuhubiri, na kumpa mapendeleo ya utumishi. Na Apolo alifuata maagizo ya Paulo. (1 Kor. 1:10-12; 3:6, 9; Tito 3:12, 13) Ndugu hao wawili walituwekea mfano mzuri sana wa kufanya kazi bega kwa bega!

“Kujadiliana kwa Ushawishi Kuhusu Ufalme” (Mdo. 18:23; 19:1-10)

8. Paulo alipitia njia gani ili kufika Efeso, na kwa nini?

8 Paulo aliahidi atarudi Efeso, naye alitimiza ahadi hiyo. a (Mdo. 18:20, 21) Hata hivyo, alirudi jinsi gani? Kwa kuwa alikuwa Antiokia ya Siria, angeweza kwenda Seleukia, apande meli, na kusafiri baharini hadi Efeso. Badala yake, alimua ‘kupitia bara.’ Inakadiriwa kwamba, safari ya Paulo inayozungumziwa katika Matendo 18:23 na 19:1, ilikuwa na urefu wa kilomita 1,600 hivi! Kwa nini Paulo aliamua kuzunguka? Kwa sababu lengo lake lilikuwa ‘kuwaimarisha wanafunzi wote.’ (Mdo. 18:23) Safari yake ya tatu ya umishonari, kama zile safari mbili za kwanza, haikuwa rahisi, hata hivyo, hakujuta. Waangalizi wa mzunguko na wake zao leo wanaonyesha roho hiyohiyo. Tunauthamini sana upendo wao wa kujidhabihu!

9. Kwa nini wanafunzi fulani walihitaji kubatizwa tena, na tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa chao?

9 Alipofika Efeso, Paulo alikuta kikundi cha watu kumi na wawili hivi waliokuwa wanafunzi wa Yohana Mbatizaji. Walikuwa wamebatizwa ubatizo wa Yohana ambao haukuwa na maana tena. Isitoshe, hawakuelewa vizuri kazi ya roho takatifu. Paulo aliwasaidia kuelewa ni kwa nini wanapaswa kubatizwa katika jina la Yesu. Kama Apolo, walikuwa wanyenyekevu na wenye hamu ya kujifunza. Baada ya kubatizwa katika jina la Yesu, walipokea roho takatifu na zawadi fulani za kufanya miujiza. Kwa kweli, Yehova huwabariki wale ambao wako tayari kufuata mwongozo mpya unatolewa na tengenezo lake.​—Mdo. 19:1-7.

10. Kwa nini Paulo alihama kutoka katika sinagogi na kwenda katika ukumbi wa shule, na tunawezaje kumwiga katika huduma yetu?

10 Si hao tu, wengine pia walifanya maendeleo. Paulo alihubiri kwa ujasiri katika sinagogi kwa miezi mitatu. Ingawa “[alijadiliana] kwa ushawishi kuhusu Ufalme wa Mungu,” baadhi ya wasikilizaji wake walikataa kumsikiliza na kuanza kumpinga. Paulo aliamua kutoa hotuba katika ukumbi wa shule badala ya kupoteza wakati akizungumza na watu waliokuwa “wakizungumza vibaya kuhusu Ile Njia.” (Mdo. 19:8, 9) Watu waliotaka kufanya maendeleo ya kiroho walihitaji kutoka katika sinagogi na kwenda katika ukumbi huo. Kama Paulo, tunaweza kukatisha mazungumzo tunapotambua kwamba mwenye nyumba hataki kusikiliza au anataka tu kubishana. Bado kuna watu wengi walio mfano wa kondoo wanaohitaji kusikiliza ujumbe wetu wenye kutia moyo!

11, 12. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo alikuwa na bidii na alibadilika kulingana na hali? (b) Mashahidi wa Yehova wanaonyeshaje kwamba wana bidii na wako tayari kubadilika kulingana na hali wanapohubiri?

11 Inawezekana Paulo alizungumza katika ukumbi huo kuanzia saa tano asubuhi hadi saa kumi jioni. (Mdo. 19:9) Inaonekana kulikuwa na joto kali muda huo na watu wengi waliacha kazi zao ili wale chakula na kupumzika. Ikiwa Paulo alifanya hivyo kwa miaka miwili, basi alitumia zaidi ya saa 3,000 akifundisha. b Hiyo ni sababu nyingine iliyofanya neno la Yehova lizidi kukua na kusitawi. Paulo alikuwa mwenye bidii naye alibadilika kulingana na hali. Alibadili ratiba ya kuhubiri ili aweze kuwasaidia watu wengi zaidi. Alipata matokeo gani? “Wote walioishi katika mkoa wa Asia wakasikia neno la Bwana, Wayahudi na Wagiriki pia.” (Mdo. 19:10) Bila shaka alitoa ushahidi kikamili.

Sisi hujitahidi kuwahubiria watu popote wanapopatikana

12 Mashahidi wa Yehova leo huhubiri kwa bidii na kubadilika kulingana na hali. Tunajitahidi kuwafikia watu popote walipo na wakati wowote wanapoweza kupatikana. Tunawahubiria barabarani, sokoni, na katika maegesho ya magari. Tunawasiliana na watu kupitia simu au barua. Na tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunajitahidi kufanya hivyo wakati ambapo kuna uwezekano mkubwa wa kuwapata nyumbani.

Neno la Yehova ‘Lilikua na Kusitawi’ Licha ya Roho Waovu (Mdo. 19:11-22)

13, 14. (a) Yehova alimwezesha Paulo kufanya nini? (b) Wana wa Skewa walifanya kosa gani, na watu wengi leo katika dini zinazodai kuwa za Kikristo wanafanyaje kosa kama hilo?

13 Luka anatujulisha kwamba kwa muda fulani mambo yalikuwa shwari, na Yehova alimwezesha Paulo kufanya “matendo yenye nguvu yasiyo ya kawaida.” Hata nguo na vitambaa ambavyo Paulo alivaa vilichukuliwa na kupelekwa kwa wagonjwa, nao wakapona. Roho waovu walitolewa kwa njia hiyo pia. c (Mdo. 19:11, 12) Ushindi huo dhidi ya majeshi ya Shetani uliwashangaza watu wengi. Hata hivyo si watu wote waliofurahia jambo hilo.

14 “Baadhi ya Wayahudi waliosafiri huku na huku wakifukuza roho waovu” walijaribu kuiga miujiza ya Paulo. Baadhi yao walijaribu kufukuza roho waovu kwa kutumia jina la Yesu na Paulo. Luka anasema kwamba wana saba wa Skewa—kutoka katika familia ya kikuhani—walijaribu kufanya hivyo. Roho mwovu aliwaambia: “Ninamjua Yesu nami ninamfahamu Paulo; lakini ninyi ni nani?” Kisha mtu huyo aliyekuwa na roho mwovu, akawarukia na kuwashambulia matapeli hao kama mnyama mwitu, akawajeruhi na kuwatimua wakiwa uchi. (Mdo. 19:13-16) Huo ulikuwa ushindi mkubwa wa “neno la Yehova,” kwa sababu ilionekana wazi kwamba Yehova alimpatia Paulo nguvu nyingi lakini wale wafuasi wa dini za uwongo hawakuwa na nguvu kutoka kwa Yehova. Leo, mamilioni ya watu hufikiri kwamba kuliitia tu jina la Yesu, au kujiita “Mkristo” kunatosha. Hata hivyo, kama Yesu alivyosema, wale wanaofanya mapenzi ya Baba yake ndio tu walio na tumaini hakika la wakati ujao.​—Mt. 7:21-23.

15. Tunawezaje kuwaiga Waefeso kuhusiana na mazoea ya kuwasiliana na roho, au vitu vinavyohusiana na mazoea hayo?

15 Ilipojulikana wazi kwamba wana wa Skewa hawana nguvu, watu wengi waliamua kuwa Wakristo na kuacha mazoea ya kuwasiliana na roho. Waefeso wengi waliamini mambo ya uchawi. Watu walifanya mambo ya uchawi na walikuwa na vitu na vitabu vingi vilivyohusiana na mambo hayo. Hivyo, Waefeso wengi walichochewa kutoa vitabu vyao vya uchawi na kuviteketeza hadharani. Kulingana na viwango vya leo, vitabu hivyo vilikuwa na thamani ya pesa nyingi sana. d Luka anasema: “Hivyo kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova likazidi kukua na kusitawi.” (Mdo. 19:17-20) Ulikuwa ushindi mkubwa wa ile kweli dhidi ya uwongo na roho waovu! Watu hao waaminifu walituwekea mfano mzuri tunaoweza kuiga leo. Sisi pia tunaishi katika ulimwengu ambao watu wengi wana mazoea ya kuwasiliana na roho. Tukigundua kwamba tuna kitu fulani kinachohusiana na mazoea hayo, tunapaswa kufanya kama walivyofanya Waefeso—kukiharibu kabisa! Na tuepuke kabisa mazoea hayo yenye kuchukiza, hata ikiwa ni vigumu kufanya hivyo.

“Kukatokea Mvurugo Mkubwa” (Mdo. 19:23-41)

“Wanaume, mnajua vema kwamba tunapata mafanikio yetu kutokana na biashara hii.”—Matendo 19:25

16, 17. (a) Eleza jinsi Demetrio alivyoanzisha vurugu jijini Efeso. (b) Waefeso walionyeshaje wanashikilia kupita kiasi maoni ya dini yao?

16 Sasa, hila ya Shetani inaonekana wazi Luka anaposema kwamba “kukatokea mvurugo mkubwa kuhusu Ile Njia.” Ilikuwa hali ya hatari sana. e (Mdo. 19:23) Fundi fulani wa fedha anayeitwa Demetrio ndiye aliyeanzisha vurugu hizo. Aliwachochea mafundi wenzake kwa kuwakumbusha kwamba utajiri wao unatokana na kazi ya kuuza sanamu. Alidai kwamba ujumbe ambao Paulo alihubiri ungeharibu kazi yao, kwa sababu Wakristo hawaabudu sanamu. Kisha akijua kwamba Waefeso hao walijivunia jiji na taifa lao, akawaonya kwamba ikiwa watu watamsikiliza Paulo, mungu wao wa kike Artemi, na hekalu lao linalojulikana ulimwenguni pote, “litaonwa kuwa si kitu.”​—Mdo. 19:24-27.

17 Njama ya Demetrio ilifanikiwa. Mafundi hao walikasirika na kuanza kupiga kelele “Artemi wa Waefeso ni mkuu!” Kisha vurugu ikatokea katika jiji hilo kama ilivyosimuliwa mwanzoni mwa sura hii. f Paulo alikuwa jasiri sana na alitaka kwenda kwenye uwanja huo ili azungumze na watu hao, lakini wanafunzi wakasisitiza asijihatarishe. Mtu fulani anayeitwa Aleksanda akasimama mbele ya umati huo na kujaribu kuzungumza. Kwa kuwa alikuwa Myahudi, huenda alitaka kueleza tofauti kati ya Wayahudi na Wakristo hao. Lakini watu hao hawakumsikiliza. Walipotambua kwamba ni Myahudi, walianza kumzomea, na kurudia tena na tena maneno yao “Artemi wa Waefeso ni mkuu!” kwa muda wa saa mbili hivi. Leo pia kuna watu wanaoshikilia sana maoni au itikadi zao za kidini, na si rahisi kuwafundisha.​—Mdo. 19:28-34.

18, 19. (a) Karani wa jiji aliunyamazisha jinsi gani umati jijini Efeso? (b) Watu wa Yehova wamelindwa jinsi gani na wenye mamlaka, na wakati mwingine ulinzi huo unategemea nini?

18 Mwishowe, karani wa jiji akaunyamazisha umati huo. Ofisa huyo alikuwa na usawaziko. Kwanza aliwaambia watu hao wenye hasira kwamba Wakristo hawangeweza kuhatarisha hekalu lao na mungu wao wa kike. Pia aliwaambia kwamba Paulo na wenzake hawajafanya kosa lolote dhidi ya hekalu la Artemi. Na pia aliwaeleza kwamba kuna njia rasmi za kushughulikia mambo kama hayo. Huenda walinyamaza kabisa karani huyo alipowaambia kwamba wasipotulia, watashtakiwa chini ya sheria za Roma kwa kukusanyika kinyume cha sheria na kuanzisha vurugu. Kisha, akawaagiza waondoke. Maneno yenye usawaziko ya ofisa huyo yalituliza hasira za watu hao.​—Mdo. 19:35-41.

19 Hiyo haikuwa mara ya kwanza kwa ofisa wa serikali mwenye usawaziko kuingilia kati na kuwalinda wafuasi wa Yesu, na wala haikuwa ya mwisho. Mtume Yohana aliona katika maono kwamba katika siku za mwisho, wenye mamlaka katika ulimwengu huu, wanaofananishwa na dunia, wangemeza maji ya mafuriko ya mateso ya Shetani dhidi ya wafuasi wa Yesu. (Ufu. 12:15, 16) Ndivyo ilivyo leo. Katika visa vingi, mahakimu wenye usawaziko wamelinda haki za Mashahidi wa Yehova za kukutana kwa ajili ya ibada na kuwahubiria wengine habari njema. Bila shaka, nyakati nyingine mwenendo wetu huchangia matokeo mazuri tunayopata. Mwenendo wa Paulo ulifanya apendwe na kuheshimiwa na maofisa fulani wa serikali huko Efeso, nao walitaka awe salama. (Mdo. 19:31) Sikuzote na tujiendeshe kwa unyoofu na heshima. Kufanya hivyo kunaweza kuwa na matokeo mazuri.

20. (a) Unahisije unapotafakari jinsi neno la Yehova lilivyositawi katika karne ya kwanza na linavyositawi leo? (b) Umeazimia kufanya nini kuhusiana na ushindi wa Yehova katika siku zetu?

20 Inasisimua kutafakari jinsi ‘neno la Yehova lilivyozidi kukua na kusitawi’ katika karne ya kwanza. Leo, pia, inasisimua kuona jinsi Yehova ametusaidia kupata ushindi mbalimbali. Je, ungependa kushiriki katika ushindi huo hata ikiwa ni kwa kiwango kidogo? Basi jifunze kutokana na mifano ambayo imezungumziwa. Endelea kuwa mnyenyekevu. Mwongozo wa tengenezo la Yehova unapotolewa, ufuate bila kukawia. Endelea kuwa na bidii. Epuka kabisa mazoea ya kuwasiliana na roho. Fanya kila uwezalo ili kutoa ushahidi kamili kupitia mwenendo wako wa unyoofu na heshima.

a Ona sanduku lenye kichwa “ Efeso—Jiji Kuu la Asia.”

b Akiwa Efeso, Paulo aliandika barua ya kwanza kwa Wakorintho.

c Huenda “nguo” zinazotajwa ni vitambaa vya mkononi ambavyo Paulo alijifunga kichwani ili kuzuia jasho lisiingie machoni. Na “vitambaa” alivyojifunga vinadokeza kwamba alikuwa akiendelea na kazi yake ya kutengeneza mahema wakati ambapo hakuwa akihubiri, labda mapema asubuhi.​—Mdo. 20:34, 35.

d Kulingana na Luka, vitabu hivyo viligharimu vipande 50,000 vya fedha. Ikiwa alikuwa akizungumzia dinari, basi mfanyakazi wa nyakati hizo angehitaji kufanya kazi kila siku kwa siku 50,000—miaka 137 hivi ili kupata pesa hizo.

e Watu fulani husema kwamba Paulo alikuwa akirejelea tukio hili alipowaambia Wakorintho “hatukuwa na uhakika hata kuhusu uhai wetu.” (2 Kor. 1:8) Hata hivyo, huenda alikuwa akizungumzia pindi nyingine iliyokuwa hatari zaidi. Paulo alipoandika kwamba ‘alipigana na wanyama wa mwituni huko Efeso,’ huenda alikuwa akizungumzia wanyama wakali katika uwanja fulani wa michezo au wanadamu wapinzani. (1 Kor. 15:32) Inawezekana alikabili hali hizo kihalisi au kwa njia ya mfano.

f Vyama au mashirika kama hayo ya wafanyakazi yanaweza kuwa na nguvu sana. Kwa mfano, karne moja hivi baadaye, chama cha waokaji kilichochea vurugu kama hizo jijini Efeso.