Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 22

“Mapenzi ya Yehova na Yatendeke”

“Mapenzi ya Yehova na Yatendeke”

Akiwa ameazimia kufanya mapenzi ya Mungu, Paulo anaenda Yerusalemu

Matendo 21:1-17

1-4. Kwa nini Paulo anaenda Yerusalemu, na nini kinachomngojea huko?

 WATU wengi wamehuzunika baada ya Paulo kuondoka huko Mileto. Si rahisi kwa Paulo na Luka kuachana na wazee wa Efeso, waliowapenda sana! Wamishonari hao wawili wamesimama kwenye sitaha. Mizigo yao ina vitu wanavyohitaji kwa ajili ya safari. Pia wamebeba michango iliyokusanywa kwa ajili ya Wakristo wenye uhitaji huko Yudea nao wanakusudia kuwasilisha salama zawadi hizo.

2 Upepo mwanana unajaza matanga na meli yang’oa nanga. Wanaume hao wawili, na wengine saba wanaosafiri pamoja nao, wanawatazama ndugu zao wenye huzuni waliobaki ufuoni. (Mdo. 20:4, 14, 15) Wasafiri hao wanaendelea kupunga mikono mpaka wanapokuwa mbali wasiweze tena kuwaona rafiki zao.

3 Kwa miaka mitatu hivi, Paulo amekuwa akifanya kazi pamoja na wazee wa Efeso. Lakini sasa, akiongozwa na roho takatifu, anaelekea Yerusalemu. Kwa kiasi fulani, anajua yatakayompata. Awali, aliwaambia wazee hao hivi: “Nikiwa nimefungwa katika roho, ninasafiri kwenda Yerusalemu, ingawa sijui mambo yatakayonipata huko, isipokuwa kutoka jiji mpaka jiji roho takatifu inanitolea ushahidi tena na tena, ikisema kwamba nitafungwa gerezani na kupatwa na dhiki.” (Mdo. 20:22, 23) Licha ya hatari anazokabili, Paulo anahisi kwamba ‘amefungwa katika roho,’ yaani anawajibika na yuko tayari kufuata mwongozo wa roho wa kwenda Yerusalemu. Anathamini uhai wake, hata hivyo, kufanya mapenzi ya Mungu ndilo jambo kuu zaidi maishani mwake.

4 Je, unahisi hivyo? Tulipojiweka wakfu kwa Yehova, tuliahidi kwamba tutatanguliza mapenzi yake maishani mwetu. Tunaweza kunufaika kwa kuchunguza mfano mzuri wa mtume Paulo.

Kukiacha Nyuma “Kisiwa cha Kipro” (Mdo. 21:1-3)

5. Paulo na wenzake walipitia njia gani kwenda Tiro?

5 Meli ambayo Paulo na wenzake walipanda ‘ilienda moja kwa moja.’ Hilo linamaanisha kwamba kulikuwa na upepo mzuri uliovuma, na meli haikushusha matanga hadi walipofika Kosi siku hiyo. (Mdo. 21:1) Inaonekana kwamba meli hiyo ilitia nanga huko usiku kucha kabla ya kuelekea Rode na Patara. Walipofika Patara, katika pwani ya kusini ya Asia Ndogo, ndugu hao walipanda meli kubwa ya shehena, iliyowapeleka moja kwa moja hadi Tiro, Foinike. Wakiwa njiani, walikiacha nyuma “kisiwa cha Kipro . . . upande wa kushoto.” (Mdo. 21:3) Kwa nini Luka, aliyeandika kitabu cha Matendo, anataja jambo hilo?

6. (a) Kwa nini yawezekana kwamba Paulo alitiwa moyo alipokiona kisiwa cha Kipro? (b) Unapotafakari jinsi Yehova amekubariki na kukusaidia, unafikia mkataa gani?

6 Huenda Paulo aliwaonyesha wasafiri wenzake kisiwa hicho na kusimulia mambo aliyojionea alipokuwa huko. Katika safari yake ya kwanza ya umishonari, miaka tisa hivi iliyopita, Paulo, pamoja na Barnaba na Yohana Marko, walikutana na Elima mlozi, aliyepinga kazi yao ya kuhubiri. (Mdo. 13:4-12) Paulo aliimarishwa kukabiliana na mambo yaliyokuwa mbele yao baada ya kukiona kisiwa hicho na kutafakari yaliyotokea. Sisi pia tunaweza kunufaika kwa kutafakari jinsi Yehova ametubariki na kutusaidia kuvumilia majaribu. Tukitafakari kwa njia hiyo tunaweza kuchochewa kusema kama Daudi: “Mwadilifu ana matatizo mengi, lakini Yehova humwokoa kutoka katika matatizo hayo yote.”​—Zab. 34:19.

‘Tukawatafuta Wanafunzi na Tukawapata’ (Mdo. 21:4-9)

7. Paulo na wenzake walifanya nini walipofika Tiro?

7 Paulo alithamini sana ushirika wa Kikristo naye alipenda kuwa pamoja na waamini wenzake. Walipofika Tiro, Luka anaandika, ‘tukawatafuta wanafunzi na tukawapata.’ (Mdo. 21:4) Wakijua kwamba kuna Wakristo wenzao Tiro, wasafiri hao waliwatafuta na huenda walikaa pamoja nao. Mojawapo ya baraka kubwa za kujua kweli ni kwamba popote tunapoenda, tunaweza kupata waabudu wenzetu ambao watatukaribisha. Waabudu wa Mungu wa kweli wana marafiki ulimwenguni pote.

8. Andiko la Matendo 21:4 linamaanisha nini?

8 Akieleza kuhusu siku saba walizokaa Tiro, Luka anataja jambo ambalo mwanzoni linaonekana kuwa lenye kushangaza: “Kupitia roho [akina ndugu wa Tiro] wakamwambia Paulo tena na tena asikanyage Yerusalemu.” (Mdo. 21:4) Je, Yehova alikuwa amebadili nia yake? Je, sasa alikuwa akimzuia Paulo asiende Yerusalemu? Hapana. Roho ilionyesha kwamba Paulo angeteswa Yerusalemu, bali si kwamba asiende huko. Inaonekana kwamba kupitia roho takatifu, ndugu wa Tiro walikuwa sahihi kwamba Paulo angepatwa na matatizo Yerusalemu. Hivyo, wakimhangaikia Paulo, walimhimiza asiende huko. Hangaiko lao la kutaka kumlinda Paulo asipatwe na hatari zilizokuwa zikimngojea linaeleweka. Hata hivyo, akiwa ameazimia kufanya mapenzi ya Yehova, Paulo aliendelea na safari yake hadi Yerusalemu.​—Mdo. 21:12.

9, 10. (a) Aliposikia mahangaiko ya ndugu zake huko Tiro, inawezekana Paulo alikumbuka hali gani inayofanana na hiyo? (b) Ni maoni gani ambayo yameenea sana ulimwenguni leo, nayo yanatofautiana jinsi gani na maneno ya Yesu?

9 Aliposikia mahangaiko ya akina ndugu, huenda Paulo alikumbuka kwamba wanafunzi wa Yesu pia, walijaribu kumzuia alipowaambia ataenda Yerusalemu, ateswe, na kuuawa. Akisukumwa na hisia, Petro alimwambia Yesu: “Bwana jihurumie; hutapatwa kamwe na mambo hayo.” Yesu alimjibu: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu hufikirii mawazo ya Mungu, bali ya wanadamu.” (Mt. 16:21-23) Yesu aliazimia kuishi maisha ya kujidhabihu, jambo ambalo Mungu alikuwa amemtuma afanye. Paulo alihisi hivyo pia. Bila shaka, kama mtume Petro, ndugu wa Tiro walikuwa na nia nzuri, hata hivyo, hawakutambua mapenzi ya Mungu.

Ili kuwa mfuasi wa Yesu, lazima mtu awe na roho ya kujidhabihu

10 Watu wengi leo hupenda kujitendea kwa fadhili au kuishi maisha ya starehe. Kwa ujumla watu hutafuta dini ambayo haidai mengi ili wastarehe. Hata hivyo, Yesu aliwahimiza wafuasi wake wawe na maoni tofauti kabisa. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso na aendelee kunifuata.” (Mt. 16:24) Ni jambo la hekima na linalofaa kumfuata Yesu. Hata hivyo, si rahisi kufanya hivyo sikuzote.

11. Wanafunzi wa Tiro walionyesha jinsi gani upendo wao kwa Paulo na kwamba wanamuunga mkono?

11 Punde si punde, wakati wa Paulo, Luka, na wenzao kuondoka ukafika. Mambo yaliyotokea wanapoondoka yanagusa moyo sana. Yanaonyesha jinsi akina ndugu wa Tiro walivyompenda Paulo na walivyounga mkono kabisa huduma yake. Wanaume, wanawake, na watoto walimsindikiza Paulo na wenzake hadi ufuoni. Walipiga magoti na kusali pamoja kisha wakaagana. Baadaye, Paulo, Luka, na wenzao wakapanda meli na kuendelea na safari yao hadi Tolemai, ambako waliwakuta akina ndugu na kukaa pamoja nao kwa siku moja.​—Mdo. 21:5-7.

12, 13. (a) Filipo alikuwa na rekodi ya aina gani ya kutumikia kwa uaminifu? (b) Akina baba Wakristo leo, wanaweza kuiga jinsi gani mfano wa Filipo?

12 Kisha, Luka anaripoti kwamba Paulo na wasafiri wenzake wakaelekea Kaisaria. Walipofika huko, ‘wakaingia katika nyumba ya Filipo mweneza-injili.’ a (Mdo. 21:8) Lazima walifurahi sana kumwona Filipo. Miaka 20 hivi iliyopita huko Yerusalemu, Filipo alikuwa amewekwa rasmi na mitume asaidie kugawanya chakula katika kutaniko jipya la Kikristo. Filipo alikuwa mhubiri mwenye bidii kwa muda mrefu. Kumbuka kwamba wanafunzi walipotawanyika kwa sababu ya mateso, Filipo alienda Samaria na kuanza kuhubiri. Baadaye, alimhubiria na kumbatiza towashi Mwethiopia. (Mdo. 6:2-6; 8:4-13, 26-38) Alikuwa na rekodi nzuri sana ya kutumikia kwa uaminifu!

13 Filipo hakupunguza bidii yake katika huduma. Akiwa Kaisaria, bado alikuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri, kama Luka anavyoonyesha kwa kumwita “mweneza-injili.” Pia, tunaambiwa kwamba alikuwa na binti wanne waliokuwa wakitoa unabii, jambo linaloonyesha kwamba walifuata mfano wa baba yao. b (Mdo. 21:9) Hivyo, lazima Filipo alikuwa amefanya mengi ili kuijenga nyumba yake kiroho. Akina baba Wakristo wanapaswa kufuata mfano wake, kwa kuwa na bidii katika huduma na kuwasaidia watoto wao waipende kazi ya kuhubiri.

14. Ziara za Paulo zilitokeza nafasi ya nini, nasi tuna nafasi gani kama hizo leo?

14 Popote alipoenda, Paulo aliwatafuta waabudu wenzake na kukaa pamoja nao. Akina ndugu walikuwa tayari kumkaribisha mmishonari huyo na wenzake. Bila shaka, ziara hizo zilikuwa pindi za ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:11, 12) Kuna nafasi nyingi kama hizo leo. Unaweza kupata baraka nyingi kwa kumkaribisha mwangalizi wa mzunguko na mke wake nyumbani kwako, hata ikiwa hauna vitu vingi vya kimwili.​—Rom. 12:13.

“Niko Tayari . . . Kufa” (Mdo. 21:10-14)

15, 16. Agabo alileta habari gani, nazo zilikuwa na matokeo gani kwa wale waliozisikia?

15 Paulo alipokuwa akikaa na Filipo, mgeni mwingine aliyeheshimiwa akafika. Jina lake ni Agabo. Waliokuwa wamekusanyika nyumbani kwa Filipo walijua kwamba Agabo ni nabii; alikuwa ametabiri njaa kubwa wakati wa utawala wa Klaudio. (Mdo. 11:27, 28) Huenda walianza kujiuliza: ‘Kwa nini Agabo amekuja? Ana ujumbe gani?’ Walipokuwa wakimtazama kwa makini, alichukua mshipi wa Paulo—kitambaa kirefu ambacho kingeweza kubeba pesa na vitu vingine, nacho kilikuwa kikifungwa kiunoni. Agabo akafunga miguu na mikono yake. Kisha akaanza kuzungumza. Ujumbe wake ulikuwa mzito: “Hivi ndivyo roho takatifu inavyosema, ‘Wayahudi kule Yerusalemu watamfunga hivi mwanamume ambaye mshipi huu ni wake, nao watamtia mikononi mwa watu wa mataifa.’”​—Mdo. 21:11.

16 Kulingana na unabii huo, ni wazi kwamba Paulo angeenda Yerusalemu. Pia, unabii huo ulionyesha kwamba baadaye Wayahudi wangemtia “mikononi mwa watu wa mataifa.” Unabii huo uliwahangaisha sana wale waliokuwako. Luka anaandika: “Tuliposikia hayo, sisi na wale waliokuwa hapo tukaanza kumsihi Paulo asipande kwenda Yerusalemu. Kisha Paulo akasema: ‘Kwa nini mnalia na kujaribu kunivunja moyo? Muwe na hakika kwamba niko tayari si kufungwa tu bali pia kufa huko Yerusalemu kwa ajili ya jina la Bwana Yesu.’”​—Mdo. 21:12, 13.

17, 18. Paulo alionyesha azimio lake jinsi gani, na akina ndugu walitendaje?

17 Wazia hali hiyo. Akina ndugu, kutia ndani Luka, wanamsihi Paulo asiende. Baadhi yao wanalia. Akichochewa na hangaiko lao lenye upendo kwake, Paulo anasema kwa upole kwamba ‘wanajaribu kumvunja moyo,’ au kama tafsiri fulani zinavyosema, ‘wanaudhoofisha moyo wangu.’ Hata hivyo, azimio lake ni thabiti, na kama vile ilivyokuwa alipokutana na ndugu wa Tiro, hatakubali sihi zao au machozi yao yamfanye akengeuke. Badala yake, anawaeleza kwa nini lazima aende. Alikuwa ameazimia na alionyesha ujasiri! Kama alivyofanya Yesu, Paulo ameazimia kabisa kwenda Yerusalemu. (Ebr. 12:2) Paulo hakutaka kufa kimakusudi kwa sababu ya imani yake, lakini ikiwa angeuawa, angeona kuwa ni jambo la heshima kufa akiwa mfuasi wa Kristo Yesu.

18 Akina ndugu walitendaje? Waliheshimu msimamo wake. Tunasoma hivi: “Tuliposhindwa kumshawishi, tukaacha kumkataza, tukasema: ‘Mapenzi ya Yehova na yatendeke.’” (Mdo. 21:14) Waliojaribu kumshawishi Paulo asiende Yerusalemu hawakushikilia maoni yao. Walimsikiliza Paulo na kukubali maoni yake, wakitambua na kukubali mapenzi ya Yehova yatendeke, ingawa haikuwa rahisi kwao. Paulo alikuwa ameanza safari ambayo baadaye ingeweza kusababisha kifo chake. Mambo yangekuwa rahisi zaidi kwa Paulo ikiwa ndugu zake wapendwa wasingejaribu kumshawishi asiende.

19. Tunajifunza jambo gani muhimu kutokana na mambo yaliyompata Paulo?

19 Tunajifunza jambo muhimu kutokana na mambo yaliyompata Paulo: Hatupaswi kamwe kuwavunja moyo wengine wasiishi maisha ya kujidhabihu katika utumishi wao kwa Mungu. Tunaweza kutumia kanuni hiyo katika hali nyingi, si wakati tu ambapo uhai uko hatarini. Kwa mfano, ingawa wazazi wengi Wakristo huhuzunika watoto wao wanapoondoka nyumbani na kwenda kumtumikia Yehova katika nchi za kigeni, wameazimia kutowavunja moyo. Phyllis, anayeishi Uingereza, anakumbuka jinsi alivyolia sana wakati binti yake wa pekee alipoenda kutumikia akiwa mmishonari barani Afrika. Phyllis anasema hivi: “Nilihuzunika sana. Haikuwa rahisi kwangu kukubali kwamba atakuwa mbali sana. Nilihuzunika, lakini pia nilimwonea fahari. Nilisali sana. Hata hivyo, ulikuwa uamuzi wake, nami sikujaribu kamwe kuubadili. Sikuzote nilikuwa nimemfundisha kutanguliza Ufalme! Ametumikia katika nchi za kigeni kwa miaka 30, nami humshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya uaminifu wake.” Ni jambo zuri sana tunapowatia moyo waabudu wenzetu wanaojidhabihu!

Ni vizuri kuwatia moyo waabudu wenzetu wanaojidhabihu

“Akina Ndugu Wakatukaribisha kwa Furaha” (Mdo. 21:15-17)

20, 21. Tunajuaje kwamba Paulo alipenda kuwa pamoja na ndugu zake, na kwa nini alipenda kuwa pamoja na waabudu wenzake?

20 Matayarisho yalifanywa, naye Paulo akaendelea na safari yake, akisindikizwa na akina ndugu ambao kwa kufanya hivyo walimhakikishia kwamba wanamuunga mkono. Kila mahali walipopita katika safari yao kuelekea Yerusalemu, Paulo na wenzake walishirikiana na ndugu na dada zao Wakristo. Katika jiji la Tiro, walipata wanafunzi na kukaa nao siku saba. Walipokuwa Tolemai, waliwasalimu dada na ndugu zao na kukaa huko siku moja. Kaisaria, walikaa siku kadhaa katika nyumba ya Filipo. Kisha, baadhi ya wanafunzi kutoka Kaisaria wakamsindikiza Paulo na wenzake hadi Yerusalemu, ambapo walikaa kwa Mnasoni, mwanafunzi wa awali. Hatimaye, wasafiri hao walipofika Yerusalemu, Luka anaripoti kwamba ‘akina ndugu waliwakaribisha kwa furaha.’​—Mdo. 21:17.

21 Ni wazi kwamba Paulo alipenda kuwa pamoja na waabudu wenzake. Mtume huyo alitiwa moyo na ndugu na dada zake, kama ilivyo leo. Bila shaka, baada ya Paulo kutiwa moyo na kuimarishwa na akina ndugu, angeweza kukabiliana na wapinzani wenye hasira waliotaka kumuua.

a Ona sanduku lenye kichwa “ Kaisaria—Jiji Kuu la Mkoa wa Yudea.”

b Ona sanduku lenye kichwa “ Je, Wanawake Wanaweza Kuwa Wahudumu Wakristo?.”