Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 21

“Mimi Sina Hatia ya Damu ya Mtu Yeyote”

“Mimi Sina Hatia ya Damu ya Mtu Yeyote”

Bidii ya Paulo katika huduma na ushauri wake kwa wazee

Matendo 20:1-38

1-3. (a) Eleza matukio ya siku ambayo Eutiko alikufa. (b) Paulo afanya nini, na tukio hilo laonyesha nini kumhusu Paulo?

 PAULO yuko katika chumba cha juu huko Troa. Chumba hicho kimejaa watu. Ana mazungumzo marefu pamoja na akina ndugu, kwa kuwa huu ndio usiku wa mwisho atakaokuwa pamoja nao. Ni usiku wa manane. Kuna taa nyingi zinazowaka chumbani, na kwa hiyo kuna joto jingi na moshi pia. Kijana mmoja anayeitwa Eutiko ameketi dirishani. Paulo anapozungumza, Eutiko analala usingizi mzito na kuanguka nje ya chumba hicho kilicho katika ghorofa ya tatu!

2 Kwa kuwa ni daktari, huenda Luka ndiye wa kwanza kufika nje ili kuona hali ya kijana huyo. Eutiko ‘anaokotwa akiwa amekufa.’ (Mdo. 20:9) Hata hivyo, muujiza watokea. Paulo akajitupa juu ya kijana huyo na kuuambia umati: “Acheni kupiga kelele, kwa maana yuko hai.” Paulo amemfufua Eutiko!—Mdo. 20:10.

3 Tukio hilo linaonyesha nguvu za roho takatifu ya Mungu. Paulo hakusababisha kifo cha Eutiko. Hata hivyo, hakutaka kifo cha kijana huyo kivuruge pindi hiyo muhimu au kumkwaza mtu yeyote kiroho. Kwa kumfufua Eutiko, Paulo aliliacha kutaniko likiwa limefarijiwa na likiwa tayari kuendeleza huduma yao. Ni wazi kwamba Paulo alithamini uhai wa wengine. Kumbuka alivyosema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote.” (Mdo. 20:26) Acheni tuone jinsi mfano wa Paulo unavyoweza kutusaidia.

“Akaanza Safari Yake ya Kwenda Makedonia” (Mdo. 20:1, 2)

4. Paulo alikabili hali gani yenye kuogopesha?

4 Kama tulivyoona katika sura ya 20, Paulo alikuwa amekabili hali yenye kuogopesha. Huduma yake katika jiji la Efeso ilisababisha mvurugo. Mafundi wa fedha ambao biashara yao ilitegemea ibada ya Artemi ndio waliochochea mvurugo huo! “Baada ya ghasia kutulia,” andiko la Matendo 20:1 linasema, “Paulo akatuma watu wawaite wanafunzi, akawatia moyo na kuwaaga, kisha akaanza safari yake ya kwenda Makedonia.”

5, 6. (a) Huenda Paulo alikaa Makedonia kwa muda gani, na aliwafanyia nini akina ndugu huko? (b) Paulo aliwaonaje waamini wenzake?

5 Alipokuwa akielekea Makedonia, Paulo alifika katika bandari ya Troa na kukaa huko kidogo. Paulo alitazamia kukutana na Tito, aliyekuwa ametumwa Korintho. (2 Kor. 2:12, 13) Hata hivyo, alipoona kwamba Tito hafiki, Paulo akaenda Makedonia, ambako yaelekea alikaa kwa mwaka mmoja hivi na “kuwatia moyo kwa maneno mengi.” a (Mdo. 20:2) Mwishowe, Tito alijiunga na Paulo huko Makedonia, na kumweleza habari njema kuhusu jinsi Wakorintho walivyoitikia barua ya kwanza ya Paulo. (2 Kor. 7:5-7) Hilo lilimchochea Paulo kuwaandikia barua nyingine, ambayo leo twaijua kama Barua ya Pili kwa Wakorintho.

6 Luka anatumia maneno “akawatia moyo,” na “kuwatia moyo,” anapofafanua ziara ya Paulo kwa akina ndugu wa Efeso na Makedonia. Maneno hayo yanaonyesha vizuri jinsi Paulo alivyowaona waamini wenzake! Tofauti na Mafarisayo, waliowadharau watu, Paulo aliwaona kondoo hao kuwa wafanyakazi wenzake. (Yoh. 7:47-49; 1 Kor. 3:9) Paulo alikuwa na maoni hayo sikuzote, hata wakati ambapo alilazimika kuwapa shauri kali.​—2 Kor. 2:4.

7. Wazee Wakristo wanaweza kuigaje mfano wa Paulo?

7 Leo, wazee wa kutaniko na waangalizi wa mzunguko hujitahidi kuiga mfano wa Paulo. Hata wanapotoa karipio, lengo lao ni kuwatia nguvu wale wanaohitaji msaada. Wazee na waangalizi huwahangaikia wengine na kujitahidi kuwatia moyo badala ya kuwashutumu. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema hivi: “Ndugu na dada zetu wengi wanataka kufanya yaliyo sawa, lakini mara nyingi wao huvunjika moyo, huogopa na huhisi kwamba hawajui jambo la kufanya.” Wazee wanaweza kuwatia nguvu waamini wenzao wanaokabili hali kama hizo.​—Ebr. 12:12, 13.

‘Walitunga Hila Dhidi Yake’ (Mdo. 20:3, 4)

8, 9. (a) Ni nini kilichokatiza safari ya Paulo kuelekea Siria? (b) Huenda ni nini kilichochochea chuki ya Wayahudi dhidi ya Paulo?

8 Alipotoka Makedonia, Paulo alienda Korintho. b Baada ya kukaa miezi mitatu huko, alitamani kwenda Kenkrea, ambapo angepanda mashua hadi Siria. Akiwa huko angeweza kwenda Yerusalemu na kuwapa msaada ndugu wenye uhitaji. c (Mdo. 24:17; Rom. 15:25, 26) Lakini, mambo yasiyotazamiwa yalibadili mipango yake. Andiko la Matendo 20:3 linasema hivi: “Wayahudi walikuwa wametunga hila dhidi yake”!

9 Si ajabu kwamba Wayahudi walimchukia Paulo kwa kuwa walimwona kuwa mwasi imani. Mwanzoni, Paulo alipohubiri Korintho, alimsaidia Krispo kuwa mwamini. Krispo alikuwa kiongozi katika sinagogi. (Mdo. 18:7, 8; 1 Kor. 1:14) Pindi nyingine, Wayahudi waliokuwa Korintho walimshtaki Paulo kwa Galio, liwali wa Akaya. Hata hivyo, Galio aliyatupilia mbali mashtaka hayo na kusema kwamba hayana msingi. Uamuzi huo uliwakasirisha sana adui za Paulo. (Mdo. 18:12-17) Huenda Wayahudi waliokuwa Korintho walijua au walidhani kwamba karibuni Paulo angesafiri kutoka Kenkrea, hivyo wakapanga njama ya kumvamia. Paulo angefanya nini?

10. Eleza kwa nini Paulo hakutenda kwa woga alipoamua kutoenda Kenkrea.

10 Akihangaikia usalama wake—na ili kuhakikisha kwamba michango aliyokabidhiwa iko salama—Paulo aliamua kurudi Makedonia badala ya kwenda Kenkrea. Ni kweli kwamba kusafiri barabarani kulikuwa na hatari nyingi. Mara nyingi wezi waliwaibia watu barabarani. Hata nyumba za wageni hazikuwa salama. Hata hivyo, Paulo aliamua kwamba yote hayo ni afadhali kuliko yaliyokuwa yakimsubiri huko Kenkrea. Jambo zuri ni kwamba hakusafiri peke yake. Katika safari hiyo ya umishonari, aliandamana na Aristarko, Gayo, Sekundo, Sopatro, Timotheo, Trofimo, na Tikiko.​—Mdo. 20:3, 4.

11. Ni kwa njia gani Wakristo leo huchukua hatua zinazohitajika ili kujilinda, na Yesu aliwawekea mfano mzuri jinsi gani?

11 Kama alivyofanya Paulo, Wakristo leo huchukua hatua zinazohitajika ili kujilinda wanapokuwa katika huduma. Katika maeneo fulani, wao huhubiri wakiwa vikundi—au angalau wawili—badala ya kwenda peke yao. Namna gani mateso? Wakristo wanatambua kwamba hawawezi kuepuka mateso. (Yoh. 15:20; 2 Tim. 3:12) Hata hivyo, hawajiweki katika hali ya hatari. Fikiria mfano wa Yesu. Pindi moja, wapinzani wake katika jiji la Yerusalemu walipookota mawe ili wampige, ‘Yesu alijificha na kuondoka hekaluni.’ (Yoh. 8:59) Baadaye, Wayahudi walipopanga njama ya kumuua, “Yesu hakutembea tena hadharani kati ya Wayahudi, bali alienda katika eneo lililo karibu na nyika.” (Yoh. 11:54) Yesu alichukua hatua zinazohitajika ili kujilinda, maadamu kufanya hivyo hakukupingana na mapenzi ya Mungu. Wakristo pia hufanya hivyo leo.​—Mt. 10:16.

“Wakafarijika Sana” (Mdo. 20:5-12)

12, 13. (a) Ufufuo wa Eutiko ulikuwa na matokeo gani kutanikoni? (b) Ni tumaini gani linalopatikana katika Biblia ambalo huwafariji wale wanaofiwa leo?

12 Baada ya kupita Makedonia, Paulo na wenzake waligawanyika na kwenda sehemu tofauti. Yaonekana kwamba kikundi hicho kilikutana tena Troa. d Masimulizi yanasema: “Siku tano baadaye tukawafikia huko Troa.” e (Mdo. 20:6) Wakiwa Troa ndipo yule kijana Eutiko alipofufuliwa, kama tulivyosoma mwanzoni mwa sura hii. Wazia jinsi akina ndugu walivyohisi walipomwona mwenzao Eutiko akifufuliwa! Masimulizi hayo yanasema kwamba ‘walifarijika sana.’​—Mdo. 20:12.

13 Bila shaka, miujiza kama hiyo haitokei leo. Hata hivyo, wale ambao wamefiwa ‘hufarijiwa sana’ na tumaini la ufufuo linalopatikana katika Biblia. (Yoh. 5:28, 29) Fikiria hili: Kwa kuwa Eutiko hakuwa mkamilifu, alikufa tena baadaye. (Rom. 6:23) Hata hivyo, watakaofufuliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu wana tumaini la kuishi milele! Isitoshe, wale wanaofufuliwa wakatawale pamoja na Yesu huko mbinguni huvikwa kutoweza kufa. (1 Kor. 15:51-53) Wakristo leo—iwe ni watiwa mafuta au ni “kondoo wengine”​—wana sababu nzuri ya ‘kufarijiwa sana.’​—Yohana 10:16.

“Hadharani na Nyumba kwa Nyumba” (Mdo. 20:13-24)

14. Paulo aliwaambia nini wazee wa Efeso walipokutana naye huko Mileto?

14 Paulo na wenzake walisafiri kutoka Troa hadi Aso, kisha wakaenda Mitilene, Kio, Samo, na Mileto. Paulo alikusudia kufika Yerusalemu kabla ya Sherehe ya Pentekoste. Kwa kuwa alikuwa na haraka ya kurudi Yerusalemu kabla ya Pentekoste, huenda ndiyo sababu aliamua kutopitia Efeso. Hata hivyo, kwa kuwa Paulo alitaka kuongea na wazee wa Efeso, aliwaomba wakutane naye Mileto. (Mdo. 20:13-17) Walipofika, Paulo aliwaambia hivi: “Mnajua vema jinsi nilivyotenda kati yenu tangu siku ya kwanza niliyokanyaga mkoa wa Asia, nilivyomtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote na machozi na majaribu yaliyonipata kupitia hila za Wayahudi, nami sikuepuka kuwaambia ninyi jambo lolote lenye faida na kuwafundisha hadharani na nyumba kwa nyumba. Lakini nilitoa ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.”​—Mdo. 20:18-21.

15. Kwa nini sisi huhubiri nyumba kwa nyumba?

15 Leo, kuna njia nyingi za kuwahubiria watu habari njema. Kama alivyofanya Paulo, sisi hujitahidi kwenda mahali ambapo watu wanapatikana, iwe ni katika vituo vya mabasi, barabara zenye watu wengi, au sokoni. Hata hivyo, njia kuu inayotumiwa na Mashahidi wa Yehova ni kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba kuhubiri nyumba kwa nyumba huwapa watu wote nafasi ya kutosha kuusikia ujumbe wa Ufalme kwa ukawaida, na hilo huonyesha wazi kwamba Mungu hana ubaguzi. Pia, tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunaweza kuwasaidia kibinafsi watu wanaopendezwa na ujumbe wetu. Tena, kufanya hivyo hutusaidia kuimarisha imani yetu na kusitawisha sifa ya uvumilivu. Wakristo wa kweli wanajulikana kwa bidii yao katika kuhubiri “hadharani na nyumba kwa nyumba.”

16, 17. Paulo alionyesha ujasiri wake jinsi gani, na Wakristo leo wanawezaje kufuata mfano wake?

16 Paulo aliwaeleza wazee wa Efeso kwamba hajui hatari ambazo angepata baada ya kurudi Yerusalemu. Aliwaambia hivi: “Hata hivyo, sioni uhai wangu kuwa muhimu kwangu, mradi tu nimalize mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” (Mdo. 20:24) Paulo hakuogopa wala kuruhusu hali yoyote—iwe ni afya mbaya au upinzani mkali—imzuie kutimiza mgawo wake.

17 Leo pia, Wakristo huvumilia hali nyingi ngumu. Katika nchi fulani wamepigwa marufuku na kuteswa. Wengine hupambana kwa ujasiri na magonjwa ya kimwili au kihisia. Vijana Wakristo hushinikizwa na marafiki shuleni. Vyovyote vile, Mashahidi wa Yehova huonyesha ushikamanifu, kama alivyofanya Paulo. Wameazimia “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema.”

“Jiangalieni Wenyewe na Kundi Lote” (Mdo. 20:25-38)

18. Paulo aliepuka hatia ya damu jinsi gani, nao wazee wa Efeso wangeweza kufuata mfano wake kwa njia gani?

18 Paulo aliwahimiza wazee wa Efeso, akitumia mfano wake mwenyewe. Kwanza aliwaambia kwamba huenda hawatamwona tena. Kisha akasema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote, kwa maana sikukosa kuwaambia mashauri yote ya Mungu.” Wazee wa Efeso wangeweza kufuata mfano wa Paulo kwa kuepuka hatia ya damu jinsi gani? Paulo aliwaambia: “Jiangalieni wenyewe na kundi lote, ambalo kati yake roho takatifu imewaweka ninyi rasmi muwe waangalizi, mlichunge kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Mdo. 20:26-28) Paulo alionya kwamba “mbwamwitu wenye kukandamiza” wangeingia kutanikoni na “kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” Wazee hao walipaswa kufanya nini? Paulo aliwahimiza hivi: “Endeleeni kukesha, na kukumbuka kwamba kwa miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mmoja kwa machozi.”​—Mdo. 20:29-31.

19. Ni uasi imani gani uliotokea kufikia mwishoni mwa karne ya kwanza, nao ulitokeza nini katika karne zilizofuata?

19 “Mbwamwitu wenye kukandamiza” walianza kutokea mwishoni mwa karne ya kwanza. Mwaka wa 98 hivi W.K., mtume Yohana aliandika: “Hata sasa wapinga-Kristo wengi wametokea . . .  Waliondoka miongoni mwetu, lakini hawakuwa wa namna yetu; kwa maana kama wangekuwa wa namna yetu, wangebaki pamoja nasi.” (1 Yoh. 2:18, 19) Kufikia karne ya tatu, uasi imani ulitokeza makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, na katika karne ya nne, Maliki Konstantino akaidhinisha rasmi “Ukristo” huo bandia. Viongozi wa dini ‘walisema mambo yaliyopotoka’ kwa kuchukua mazoea ya kipagani na kuyafanya yaonekane kuwa ya “Kikristo.” Hata leo hii, matokeo ya uasi imani huo yanaonekana katika mafundisho na desturi ya dini zinazodai kuwa za Kikristo.

20, 21. Paulo alionyeshaje roho ya kujidhabihu, nao wazee Wakristo wanaweza kufuata mfano wake kwa njia gani leo?

20 Maisha ya Paulo yalikuwa tofauti kabisa na ya wale ambao baadaye walilitumia kundi vibaya. Alifanya kazi ya kimwili na kujitegemeza ili asiwe mzigo kutanikoni. Paulo aliwatumikia ndugu zake na hakutarajia kupata pesa kutoka kwao. Aliwahimiza wazee wa Efeso waonyeshe roho ya kujidhabihu. Aliwaambia hivi: “Lazima mwasaidie walio dhaifu, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, aliposema: ‘Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.’”​—Mdo. 20:35.

21 Kama alivyofanya Paulo, wazee Wakristo hujidhabihu. Tofauti na makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, wanaofilisi makundi yao, wale walio na jukumu la ‘kulichunga kutaniko la Mungu’ hufanya hivyo bila ubinafsi. Watu wenye kiburi na wanaojitakia makuu hawana nafasi yoyote katika kutaniko la Kikristo. Wale wanaotafuta ‘utukufu wao wenyewe’ mwishowe wataambulia patupu. (Met. 25:27) Sikuzote, kimbelembele huleta aibu.​—Met. 11:2.

“Wote wakalia sana.”—Matendo 20:37

22. Kwa nini wazee wa Efeso walimpenda sana Paulo?

22 Kwa kuwa Paulo aliwapenda akina ndugu kikweli, ndugu hao walimpenda sana. Kwa kweli, wakati wake wa kuondoka ulipofika, ‘wote walilia sana, nao wakamkumbatia Paulo na kumbusu kwa upendo.’ (Mdo. 20:37, 38) Wakristo huwathamini na kuwapenda ndugu ambao, kama alivyofanya Paulo, hujitoa wenyewe bila ubinafsi kwa manufaa ya kundi. Unapotafakari mfano mzuri wa Paulo, je, hukubali kwamba hakuwa akijisifu wala kutilia chumvi aliposema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote”?​—Mdo. 20:26.

a Ona sanduku lenye kichwa “ Barua Ambazo Paulo Aliandika Alipokuwa Makedonia.”

b Inawezekana Paulo aliandika barua yake kwa Waroma alipokuwa Korintho.

c Ona sanduku lenye kichwa “ Paulo Apeleka Misaada.”

d Maneno ya Luka katika Matendo 20:5, 6 yanadokeza kwamba Luka aliungana tena na Paulo huko Filipi. Mapema Paulo alimwacha Luka huko.​—Mdo. 16:10-17, 40.

e Safari ya kutoka Filipi hadi Troa iliwachukua siku tano. Yawezekana kwamba kulikuwa na upepo mkali, kwa sababu awali safari hiyo iliwachukua siku mbili tu.​—Mdo. 16:11.