Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 24

“Jipe Moyo!”

“Jipe Moyo!”

Paulo anusurika kifo na anajitetea mbele ya Feliksi

Matendo 23:11–24:27

1, 2. Kwa nini Paulo hashangazwi na mateso anayokabili jijini Yerusalemu?

 BAADA ya kuokolewa kutoka kwenye umati wenye hasira kali jijini Yerusalemu, Paulo awekwa kizuizini tena. Mateso anayokabili katika jiji la Yerusalemu hayamshangazi mtume huyo mwenye bidii. Aliambiwa atazamie ‘kufungwa gerezani na kupatwa na dhiki’ katika jiji hilo. (Mdo. 20:22, 23) Ijapokuwa Paulo hajui kitakachompata, anajua kwamba atateseka kwa ajili ya jina la Yesu.​—Mdo. 9:16.

2 Hata manabii Wakristo walimwonya Paulo kwamba atafungwa na kutiwa “mikononi mwa watu wa mataifa.” (Mdo. 21:4, 10, 11) Siku chache zilizotangulia, umati wa Wayahudi ulijaribu kumuua, na muda mfupi baadaye, washiriki wa Sanhedrini karibu ‘wangemrarua-rarua’ walipokuwa wakibishana kwa sababu ya mambo aliyosema. Sasa mtume huyo ni mfungwa chini ya ulinzi wa askari jeshi Waroma, akikabili kesi na mashtaka mengi. (Mdo. 21:31; 23:10) Bila shaka, mtume Paulo anahitaji kutiwa moyo!

3. Sisi hutiwa moyo jinsi gani kuendelea kuhubiri?

3 Katika siku hizi za mwisho, tunajua kwamba “wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Tim. 3:12) Mara kwa mara, sisi pia tunahitaji kutiwa moyo ili tuendelee katika kazi yetu ya kuhubiri. Tunathamini sana maneno yenye kutia moyo na yenye kufariji tunayopata kwa wakati unaofaa, kupitia machapisho na mikutano inayotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”! (Mt. 24:45) Yehova ametuhakikishia kwamba hakuna adui wa habari njema atakayefanikiwa. Hawawezi kuwaangamiza watumishi wake wakiwa kikundi wala kukomesha kazi yao ya kuhubiri. (Isa. 54:17; Yer. 1:19) Namna gani mtume Paulo? Je, alitiwa moyo kuendelea kutoa ushahidi kamili licha ya upinzani? Ikiwa ndivyo, alitiwa moyo jinsi gani, naye alifanya nini?

‘Hila Iliyofungwa kwa Kiapo’ Yazimwa (Mdo. 23:11-34)

4, 5. Paulo alitiwa moyo jinsi gani, na kwa nini alitiwa moyo kwa wakati unaofaa?

4 Mtume Paulo alitiwa moyo sana usiku uliofuata, baada ya kuokolewa kutoka kwa Sanhedrini. Masimulizi yaliyoongozwa na roho yanasema: “Bwana akasimama kando yake na kumwambia: ‘Jipe moyo! Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi kamili kunihusu katika Yerusalemu, ndivyo utakavyotoa ushahidi huko Roma pia.’” (Mdo. 23:11) Maneno hayo ya Yesu yanayotia moyo yalimhakikishia Paulo kwamba atakombolewa. Alijua kwamba atafika Roma na kutoa ushahidi kumhusu Yesu.

“Wanaume zaidi ya 40 kati yao walio tayari kumvizia.”—Matendo 23:21

5 Paulo alitiwa moyo kwa wakati unaofaa. Siku iliyofuata, wanaume Wayahudi zaidi ya 40, “wakafanya hila na kujifunga kwa kiapo cha laana, wakisema hawatakula wala kunywa mpaka watakapomuua Paulo.” ‘Hila iliyofungwa kwa kiapo,’ ilionyesha jinsi Wayahudi hao walivyoazimia kabisa kumuua mtume huyo. Waliamini kwamba, ikiwa hawangefanikiwa katika hila yao, basi wangestahili kulaaniwa, au kupatwa na mabaya. (Mdo. 23:12-15) Wakiwa na kibali cha wakuu wa makuhani na wazee, walipanga Paulo arudishwe mbele ya mahakama ya Sanhedrini ili kujibu maswali zaidi, kana kwamba kuna mambo yanayomhusu ambayo wanataka kuhakikisha. Hata hivyo, lengo lao lilikuwa kumvizia Paulo akiwa njiani na kumuua.

6. Njama ya kumuua Paulo ilifunuliwaje, na vijana wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa mpwa wa Paulo?

6 Hata hivyo, mpwa wa Paulo alipata habari kuhusu njama hiyo, naye akamjulisha Paulo. Kisha, Paulo akamwagiza kijana huyo amwambie Klaudio Lisia, kiongozi wa jeshi la Roma. (Mdo. 23:16-22) Bila shaka, Yehova anawapenda vijana ambao, kama mpwa huyo wa Paulo, hutanguliza kwa ujasiri hali njema ya watu wa Mungu na kufanya kwa uaminifu yote wawezayo ili kuendeleza kazi ya Ufalme.

7, 8. Klaudio Lisia alifanya nini ili kuhakikisha usalama wa Paulo?

7 Mara tu baada ya kuambiwa kuhusu njama iliyopangwa dhidi ya Paulo, Klaudio Lisia, aliyekuwa akisimamia askari 1,000, akaamuru kikosi cha askari 470—askari jeshi, wenye mikuki, na wapanda farasi—kiende Yerusalemu usiku huo na kumsindikiza Paulo mpaka Kaisaria. Akiwa huko alipaswa kufikishwa mbele ya Gavana Feliksi. a Jiji la Kaisaria lilikuwa kituo cha serikali ya Roma katika mkoa wa Yudea. Kulikuwa na Wayahudi wengi, lakini wakaaji wengi zaidi walikuwa Watu wa Mataifa. Mkoa huo ulikuwa tofauti kabisa na Yerusalemu, ambako watu wengi walionyesha chuki ya kidini na kusababisha ghasia. Kaisaria lilikuwa pia makao makuu ya majeshi ya Roma katika mkoa wa Yudea.

8 Kupatana na sheria za Roma, Lisia alimtumia Feliksi barua kumweleza mashtaka yaliyotolewa. Lisia alitaja kwamba alipojua Paulo ni raia wa Roma, alimwokoa ili ‘asiuawe’ na Wayahudi. Lisia alisema kwamba hakumpata Paulo na hatia yoyote ya ‘kustahili kifo au kufungwa gerezani,’ lakini kwa sababu ya hila iliyopangwa dhidi ya Paulo, alimtuma kwa Feliksi ili awasikilize wanaomshtaki na kutoa hukumu.​—Mdo. 23:25-30.

9. (a) Haki za Paulo akiwa raia wa Roma zilikiukwa jinsi gani? (b) Kwa nini huenda tukahitaji kutumia haki zetu tukiwa raia wa nchi?

9 Je, mambo yote ambayo Lisia aliandika yalikuwa kweli? Hapana. Inaonekana alikuwa anajitafutia sifa. Ukweli ni kwamba hakumwokoa Paulo kwa kuwa alijua kwamba mtume huyo ni raia wa Roma. Isitoshe, Lisia hakutaja kwamba alikuwa ameamuru Paulo “afungwe kwa minyororo miwili” na baadaye alitoa amri Paulo “ahojiwe huku akipigwa mijeledi.” (Mdo. 21:30-34; 22:24-29) Lisia alikuwa amekiuka haki za Paulo akiwa raia wa Roma. Leo, Shetani hutumia wapinzani wa kidini kuchochea mateso, na huenda uhuru wetu wa ibada ukavurugwa. Hata hivyo, kama Paulo alivyofanya, watu wa Mungu wanaweza kutumia haki zao wakiwa raia wa nchi ili kutafuta ulinzi wa kisheria.

“Nami Nafurahi Kujitetea Mbele Yako” (Mdo. 23:35–24:21)

10. Paulo alishtakiwa mambo gani mazito?

10 Akiwa Kaisaria, Paulo ‘aliwekwa chini ya ulinzi katika jumba la kifalme la Herode’ akingojea waliomshtaki wafike kutoka Yerusalemu. (Mdo. 23:35) Siku tano baadaye, wakafika—Kuhani Mkuu Anania, wakili anayeitwa Tertulo, na kikundi cha wazee. Tertulo alianza kwa kumsifu Feliksi kwa mambo aliyokuwa akiwafanyia Wayahudi, huenda ili apate kibali chake. b Kisha, akianza mashtaka yake, Tertulo alisema kwamba Paulo ni “msumbufu, akichochea uasi miongoni mwa Wayahudi wote katika dunia yote inayokaliwa, naye ni kiongozi wa madhehebu ya Wanazareti. Pia alijaribu kulichafua hekalu, basi tukamkamata.” Wale Wayahudi wengine “wakajiunga katika shambulio hilo, wakisisitiza kwamba mambo hayo ni ya kweli.” (Mdo. 24:5, 6, 9) Kuchochea uasi, kuongoza madhehebu hatari, na kulichafua hekalu—hayo yalikuwa mashtaka mazito ambayo yangeweza kufanya mtu ahukumiwe kifo.

11, 12. Paulo alikanushaje mashtaka yaliyoletwa dhidi yake?

11 Kisha, Paulo akaruhusiwa azungumze. Akasema hivi: “Nami nafurahi kujitetea mbele yako.” Kisha, akakanusha mashtaka hayo. Mtume huyo hakuwa amelichafua hekalu, wala kujaribu kuchochea uasi. Alisema kwamba hata hakuwa Yerusalemu kwa “miaka kadhaa” na kwamba alikuwa amefika kuleta “zawadi za rehema”​—michango kwa ajili ya Wakristo ambao walikuwa maskini kwa sababu ya njaa na mateso. Paulo alisisitiza kwamba kabla ya kuingia hekaluni, alikuwa ‘ametakaswa kisherehe’ naye aliazimia “kudumisha dhamiri safi mbele za Mungu na wanadamu.”​—Mdo. 24:10-13, 16-18.

12 Paulo alikiri kwamba alikuwa akitoa utumishi mtakatifu kwa Mungu wa mababu zake “kulingana na njia wanayoiita madhehebu.” Hata hivyo, alisisitiza kwamba anaamini “mambo yote yaliyo katika Sheria na yaliyoandikwa katika Manabii.” Na kama washtaki wake, alikuwa na tumaini la “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Kisha, Paulo akawataka washtaki wake watoe uthibitisho wa madai yao: “Uwaambie watu walio hapa waseme wenyewe kosa walilopata nilipokuwa nimesimama mbele ya Sanhedrini, isipokuwa jambo hili moja nililosema kwa sauti kubwa nilipokuwa nimesimama kati yao: ‘Mimi ninahukumiwa leo mbele yenu kwa sababu ya ufufuo wa wafu!’”​—Mdo. 24:14, 15, 20, 21.

13-15. Ni kwa njia gani Paulo alituwekea mfano mzuri wa kutoa ushahidi kwa ujasiri tunaposhtakiwa?

13 Paulo alituwekea mfano mzuri tunaoweza kufuata ikiwa tutashtakiwa kwa sababu ya ibada yetu na tukishtakiwa kuwa wachochezi, waasi, au washiriki wa “madhehebu hatari.” Paulo hakujaribu kujipendekeza mbele ya gavana, akimsifu kama alivyofanya Tertulo. Paulo alikuwa mtulivu na mwenye heshima. Kwa busara, alitoa ushahidi wenye kusadikisha na wa kweli. Paulo alitaja kwamba “Wayahudi fulani kutoka mkoa wa Asia” waliodai kwamba alichafua hekalu hawako, na kulingana na sheria wanapaswa kuwapo ili wathibitishe mashtaka yao.​—Mdo. 24:18, 19.

14 Zaidi ya yote, Paulo hakuogopa kutoa ushahidi kuhusu imani yake. Kwa ujasiri mtume alitaja tena na tena imani yake katika ufufuo, suala ambalo lilisababisha vurugu alipokuwa mbele ya Sanhedrini. (Mdo. 23:6-10) Alipokuwa akijitetea, Paulo alikazia tumaini la ufufuo. Kwa nini? Kwa sababu Paulo alikuwa akitoa ushahidi kumhusu Yesu na ufufuo wake—jambo ambalo wapinzani hao hawakukubali. (Mdo. 26:6-8, 22, 23) Vurugu zilizotokea zilitokana na suala la ufufuo, imani katika Yesu na ufufuo wake.

15 Kama Paulo alivyofanya, tunaweza kutoa ushahidi kwa ujasiri, nasi tunaweza kutiwa moyo na maneno ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu. Lakini yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” Je, tunapaswa kuhangaikia tutakalosema? Hapana, kwa kuwa Yesu alitoa uhakikisho huu: “Watakapokuwa wakiwapeleka kuwashtaki, msihangaike kuhusu jambo mtakalosema; bali semeni jambo mtakalopewa saa hiyo, kwa maana si ninyi mnaosema, bali ni roho takatifu.”​—Marko 13:9-13.

“Feliksi Akaogopa” (Mdo. 24:22-27)

16, 17. (a) Feliksi alishughulikia jinsi gani kesi ya Paulo? (b) Huenda ni kwa nini Feliksi aliogopa, hata hivyo ni kwa nini aliendelea kukutana na Paulo?

16 Hiyo haikuwa mara ya kwanza Gavana Feliksi kusikia kuhusu imani ya Kikristo. Masimulizi hayo yanasema: “Feliksi, akiwa anajua vizuri ukweli kuhusu Njia hii [jina lililotumiwa kufafanua Ukristo wa mapema], akaahirisha kesi yao kwa kusema: ‘Lisia kamanda wa jeshi atakapokuja, nitaamua mambo haya yanayowahusu.’ Naye akamwagiza ofisa wa jeshi kwamba mtu huyo awekwe chini ya kizuizi lakini apewe uhuru fulani, na watu wake waruhusiwe kumhudumia.”​—Mdo. 24:22, 23.

17 Siku kadhaa baadaye, Feliksi na mke wake Myahudi, Drusila, waliwatuma watu wamwite Paulo ili ‘wamsikilize akizungumza kuhusu imani katika Kristo Yesu.’ (Mdo. 24:24) Hata hivyo, Paulo alipozungumzia “uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja, Feliksi akaogopa,” huenda kwa sababu dhamiri yake ilimsumbua kwa kuwa alijua anaishi maisha mapotovu. Kwa hiyo akamruhusu Paulo aondoke na kumwambia: “Kwa sasa unaweza kwenda, lakini nitakapopata nafasi nitakuita tena.” Baada ya hapo Feliksi alikutana na Paulo mara nyingi, si kwa sababu alitaka kujua kweli, lakini kwa sababu alitumaini kwamba Paulo atampa rushwa.​—Mdo. 24:25, 26.

18. Kwa nini Paulo alizungumza na Feliksi na mke wake kuhusu “uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja”?

18 Kwa nini Paulo alizungumza na Feliksi na mke wake kuhusu “uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja”? Kumbuka, walitaka kujua “imani katika Kristo Yesu” inahusisha nini. Kwa kuwa Paulo alijua kwamba walikuwa wakiishi maisha mapotovu, walikuwa wakatili, na wasiotenda haki, aliwaonyesha wazi kinachohitajika ili kuwa wafuasi wa Yesu. Mambo ambayo Paulo alisema yalionyesha tofauti kubwa kati ya viwango vya Mungu vya uadilifu na mwenendo wa Feliksi na mke wake. Hayo yangewasaidia kuona kwamba wanadamu wote wanawajibika mbele ya Mungu kuhusu wanavyofikiri, kusema, na kutenda na kwamba jambo muhimu zaidi kuliko hukumu ambayo Paulo anakabili ni hukumu watakayokabili mbele za Mungu. Ndiyo sababu Feliksi ‘aliogopa’!

19, 20. (a) Tunapohubiri, tunapaswa kushughulika jinsi gani na watu wanaoonekana kana kwamba wanapendezwa na kweli, lakini wana sababu za kibinafsi? (b) Tunajuaje kwamba Feliksi hakuwa rafiki ya Paulo?

19 Tunapohubiri, huenda tukawapata watu walio kama Feliksi. Mwanzoni wanaweza kuonekana wanapendezwa na kweli, lakini labda wakawa na sababu za kibinafsi. Tunapaswa kuwa waangalifu tunaposhughulika nao. Hata hivyo, kama Paulo alivyofanya, tunaweza kutumia busara kuwaambia kuhusu viwango vya Mungu vya uadilifu. Huenda kweli ikagusa mioyo yao. Lakini, tukiona wazi kwamba hawana nia ya kuacha njia zao mbaya, tunawaacha na kutafuta wale wanaoitafuta sana kweli.

20 Nia ya Feliksi inaonekana wazi kutokana na maneno haya: “Miaka miwili ilipokwisha, Porkio Festo alichukua nafasi ya Feliksi; na kwa sababu Feliksi alitamani kukubaliwa na Wayahudi, akamwacha Paulo akiwa amefungwa.” (Mdo. 24:27) Feliksi hakuwa rafiki wa kweli wa Paulo. Feliksi alijua kwamba wafuasi wa “Ile Njia” hawakuwa wachochezi wala wafanya mapinduzi. (Mdo. 19:23) Pia, alijua kwamba Paulo hakuwa amevunja sheria yoyote ya Roma. Hata hivyo, Feliksi alimtia mtume huyo kifungoni ili ‘akubaliwe na Wayahudi.’

21. Ni nini kilichompata Paulo baada ya Porkio Festo kuwa gavana, na ni nini kilichoendelea kumwimarisha Paulo?

21 Kama tunavyoona katika mstari wa mwisho wa Matendo sura ya 24, bado Paulo alikuwa gerezani Porkio Festo alipoanza kutawala baada ya Feliksi. Kukawa na mfululizo wa kesi, naye Paulo akapelekwa kutoka kwa ofisa mmoja hadi mwingine. Kwa kweli, mtume huyo mwenye ujasiri ‘alipelekwa mbele ya wafalme na magavana.’ (Luka 21:12) Kama tutakavyoona, baadaye alitoa ushahidi mbele ya mtawala mwenye nguvu zaidi wa siku zake. Wakati wote huo, imani ya Paulo haikuyumba kamwe. Bila shaka, aliendelea kuimarishwa na maneno ya Yesu: “Jipe moyo!”

a Ona sanduku lenye kichwa, “ Feliksi—Gavana wa Mkoa wa Yudea.”

b Tertulo alimshukuru Feliksi kwa “amani nyingi” aliyoileta katika taifa hilo. Hata hivyo, ukweli ni kwamba amani iliyokuwa Yudea Feliksi akiwa gavana, ilikuwa ndogo ukilinganisha na amani nyingi iliyokuwako wakati wa wale magavana wengine waliotangulia mpaka uasi dhidi ya Roma ulipotokea. Pia, hakusema kweli alipotaja kwamba Wayahudi walitoa “shukrani nyingi sana” kwa marekebisho ambayo Feliksi alikuwa amefanya. Ukweli ni kwamba Wayahudi wengi walimchukia Feliksi kwa sababu ya kuwakandamiza na kuwatendea kikatili walipoasi.​—Mdo. 24:2, 3.